Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa kuwa Daudi na wanaume wake walikula mikate ya toleo, je, hilo linaonyesha kwamba mtu anaweza kuvunja sheria ya Mungu chini ya hali ngumu naye asiadhibiwe?—1 Samweli 21:1-6.

Kulingana na Mambo ya Walawi 24:5-9, mikate ya toleo ambayo ilibadilishwa kila Sabato ilipaswa kuliwa na makuhani. Kanuni iliyowaongoza makuhani kufanya hivyo ni kwamba mikate hiyo ilikuwa mitakatifu nayo ilipaswa kuliwa tu na wanaume waliokuwa katika utumishi wa Mungu, yaani, makuhani. Bila shaka, lingekuwa kosa kumpa mfanyakazi wa kawaida au kuila ili kujifurahisha. Hata hivyo, kuhani Ahimeleki hakutenda dhambi yoyote alipompa Daudi na wanaume wake mkate wa wonyesho.

Yaonekana Daudi alikuwa katika mgawo wa pekee aliopewa na Mfalme Sauli. Daudi na wanaume wake walikuwa na njaa. Ahimeleki alikata kauli kwamba walikuwa safi kidesturi. Ingawa kulingana na sheria walikosea kwa kula mikate ya toleo, kufanya hivyo kulipatana na matumizi ya msingi ya mkate wa wonyesho. Kwa kufikiria jambo hilo, Ahimeleki aliwaruhusu kula mikate hiyo. Yesu Kristo mwenyewe alitumia tukio hilo kuonyesha jinsi Mafarisayo walivyokosea katika kufafanua sheria ya Sabato na kuifuata kwa njia isiyofaa.—Mathayo 12:1-8.

Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba sheria ya Mungu inaweza kuvunjwa hali zinapokuwa ngumu. Kwa mfano, hali iliyoonekana kuwa mbaya ilitokea wakati mashujaa wa vita Waisraeli walipopigana na Wafilisti. Mfalme Sauli alikuwa amesema hivi: “Alaaniwe mtu yeyote atakayekula mkate kabla ya jioni na mpaka niwe nimejilipiza kisasi juu ya adui zangu!” Biblia inasema: “Siku hiyo wakaendelea kuwapiga Wafilisti.” Kwa sababu ya mapigano hayo, askari-jeshi walikuwa wamechoka nao walikuwa na njaa, ‘na watu wakaanza kuwachinja wanyama juu ya nchi, nao wakaanza kula pamoja na damu.’ (1 Samweli 14:24, 31-33) Walimtendea Yehova dhambi kwa kuvunja sheria yake kuhusu damu. Matendo yao hayakupatana na matumizi pekee ya damu ambayo Mungu alikubali, yaani, ‘kufanya upatanisho’ kwa ajili ya dhambi. (Mambo ya Walawi 17:10-12; Mwanzo 9:3, 4) Kwa rehema, Yehova alikubali dhabihu za pekee zilizotolewa kwa niaba ya wale waliotenda dhambi.—1 Samweli 14:34, 35.

Naam, Yehova anatarajia tutii sheria zake chini ya hali zote. Mtume Yohana anasema hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.”—1 Yohana 5:3.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Mikate mipya ya toleo iliwekwa ndani ya Maskani kila Sabato