Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mlinunuliwa Kwa Bei”

“Mlinunuliwa Kwa Bei”

“Mlinunuliwa Kwa Bei”

“Mlinunuliwa kwa bei. Kwa vyovyote, mtukuzeni Mungu.” —1 Wakorintho 6:20.

1, 2. (a) Kulingana na Sheria ya Musa, watumwa Waisraeli wangepaswa kutendewaje? (b) Mtumwa aliyempenda bwana wake angeweza kufanya uamuzi gani?

“UTUMWA ulienea sana na kukubaliwa katika ulimwengu wa kale,” chasema kitabu Holman Illustrated Bible Dictionary. Kinaongeza kusema: “Uchumi wa Misri, Ugiriki, na Roma ulitegemea kazi iliyofanywa na watumwa. Katika karne ya kwanza ya Kikristo, mtu mmoja kati ya watu watatu huko Italia alikuwa mtumwa na kwingineko, mmoja kati ya watano.”

2 Ingawa utumwa ulikuwepo katika Israeli la kale, Sheria ya Musa ilihakikisha kwamba watumwa Waebrania walilindwa. Kwa mfano, Sheria ilisema kwamba Mwisraeli hangetumikia akiwa mtumwa kwa zaidi ya miaka sita. Katika mwaka wa saba, aliruhusiwa ‘kuondoka kama mtu aliyewekwa huru bila malipo.’ Lakini masharti kuhusu namna ya kuwatendea watumwa yalikuwa ya haki na yenye huruma sana hivi kwamba kulikuwa na maandalizi haya katika Sheria ya Musa: “Ikiwa mtumwa huyo atasisitiza kusema, ‘Nampenda bwana wangu kwelikweli, mke wangu na wanangu; sitaki kuondoka kama mtu aliyewekwa huru,’ basi bwana wake atamleta karibu na Mungu wa kweli naye atamleta kwenye mlango au kwenye mwimo wa mlango; naye bwana wake atalichoma sikio lake na kulitoboa kwa sindano, naye atakuwa mtumwa wake mpaka wakati usio na kipimo.”—Kutoka 21:2-6; Mambo ya Walawi 25:42, 43; Kumbukumbu la Torati 15:12-18.

3. (a) Wakristo wa karne ya kwanza walikubali utumwa wa aina gani? (b) Ni nini hutuchochea kumtumikia Mungu?

3 Mpango wa utumwa wa kujitolea ulionyesha kimbele utumwa ambao Wakristo wa kweli wako chini yake. Kwa mfano, waandikaji wa Biblia Paulo, Yakobo, Petro, na Yuda walijitambulisha wenyewe kuwa watumwa wa Mungu na wa Kristo. (Tito 1:1; Yakobo 1:1; 2 Petro 1:1; Yuda 1) Paulo aliwakumbusha Wakristo Wathesalonike kwamba walikuwa ‘wamemgeukia Mungu kutoka kwenye sanamu zao ili wamtumikie Mungu aliye hai na wa kweli.’ (1 Wathesalonike 1:9) Ni nini kilichowachochea Wakristo hao wawe watumwa wa Mungu? Kwa kweli, ni nini kilichomchochea mtumwa Mwisraeli akatae kuwekwa huru? Kwa sababu alimpenda bwana wake. Utumwa wa Kikristo unategemea kumpenda Mungu. Tunapomjua na kumpenda Mungu wa kweli na aliye hai, tunachochewa kumtumikia ‘kwa moyo wetu wote na kwa nafsi yetu yote.’ (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Hata hivyo, kuwa mtumwa wa Mungu na wa Kristo kunatia ndani nini? Kunaathirije maisha yetu ya kila siku?

“Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”

4. Tunakuwaje watumwa wa Mungu na wa Kristo?

4 Mtumwa ni “mtu ambaye kulingana na sheria ni mali ya mtu mwingine au wengine naye anapaswa kuonyesha utii kamili.” Kulingana na sheria, tunakuwa mali ya Yehova tunapoweka maisha yetu wakfu kwake na kubatizwa. “Ninyi si mali yenu wenyewe, kwa maana mlinunuliwa kwa bei,” akaeleza mtume Paulo. (1 Wakorintho 6:19, 20) Bila shaka, bei hiyo ni dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, kwa sababu ni kupitia kwa dhabihu hiyo Mungu anatukubali kuwa watumishi wake, iwe sisi ni Wakristo watiwa-mafuta au waandamani wao walio na tumaini la kidunia. (Waefeso 1:7; 2:13; Ufunuo 5:9) Hivyo, tangu wakati tulipobatizwa, “sisi ni wa Yehova.” (Waroma 14:8) Kwa kuwa tumenunuliwa kwa damu yenye thamani ya Yesu Kristo, tunakuwa pia watumwa wake na tunakuwa na wajibu wa kushika amri zake.—1 Petro 1:18, 19.

5. Tukiwa watumwa wa Yehova, tuna wajibu gani wa msingi, nasi tunaweza kuutimizaje?

5 Lazima watumwa wamtii bwana wao. Utumwa wetu ni wa kujitolea nao huchochewa na kumpenda Bwana wetu. Andiko la 1 Yohana 5:3 linasema: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” Kwa hiyo, utii wetu huthibitisha upendo na pia ujitiisho wetu. Unaonekana wazi katika yote tunayofanya. Paulo alisema, “kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Katika maisha ya kila siku, hata katika mambo madogo, tunataka kuonyesha kwamba ‘tunamtumikia Yehova.’—Waroma 12:11.

6. Kuwa watumwa wa Mungu huathirije maamuzi tunayofanya maishani? Toa mfano wa kuonyesha jambo hilo.

6 Kwa mfano, tunapofanya maamuzi, tungependa kufikiria kwa makini mapenzi ya Bwana wetu wa mbinguni, Yehova. (Malaki 1:6) Maamuzi magumu yanaweza kujaribu utii wetu kwa Mungu. Je, basi tutatii shauri lake badala ya kufuata maelekeo ya moyo wetu ambao ni “wenye hila” na “hatari”? (Yeremia 17:9) Melisa, Mkristo mseja, alikuwa amebatizwa kwa muda mfupi tu wakati mwanamume mmoja kijana alipoanza kuvutiwa naye kimapenzi. Alionekana kuwa mtu mwenye tabia nzuri, naye tayari alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, mzee mmoja aliongea na Melisa kuhusu hekima ya kufuata amri ya Yehova ya kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39; 2 Wakorintho 6:14) “Haikuwa rahisi kwangu kufuata shauri hilo,” Melisa anakiri. “Lakini niliamua kwamba kwa kuwa nilikuwa nimejiweka wakfu kwa Mungu kufanya mapenzi yake, ningetii maagizo yake yaliyo wazi.” Akifikiria mambo yaliyotokea, anasema: “Ninafurahi sana kwamba nilifuata shauri hilo. Punde si punde, mwanamume huyo aliacha kujifunza. Ikiwa ningeendelea na uhusiano huo, sasa ningekuwa nimeolewa na mtu asiyeamini.”

7, 8. (a) Kwa nini hatupaswi kuhangaika sana kuhusu kuwapendeza wanadamu? (b) Onyesha jinsi tunavyoweza kushinda woga wa wanadamu.

7 Kwa kuwa sisi ni watumwa wa Mungu, hatupaswi kuwa watumwa wa wanadamu. (1 Wakorintho 7:23) Ni kweli, kila mmoja wetu hutaka kupendwa na watu, lakini tunapaswa kukumbuka kwamba Wakristo wana viwango vilivyo tofauti na ulimwengu. Paulo aliuliza hivi: “Je, ninatafuta kuwapendeza wanadamu?” Alikata kauli hii: “Kama ningekuwa bado ninawapendeza wanadamu, mimi singekuwa mtumwa wa Kristo.” (Wagalatia 1:10) Hatupaswi kuacha marika wetu watusonge na kufanya tuwapendeze wanadamu. Basi, tunaweza kufanya nini tunapokabili msongo huo?

8 Fikiria mfano wa Elena, Mkristo mchanga anayeishi Hispania. Wanafunzi kadhaa katika darasa lake walikuwa wakijitolea kutoa damu. Walijua kwamba Elena ambaye ni Shahidi wa Yehova, hangekubali kutoa au kutiwa damu mishipani. Alipopata nafasi ya kueleza darasa zima maoni yake, Elena alijitolea kutoa hotuba. Elena anasema: “Kwa kweli, nilikuwa na wasiwasi mwingi kuhusu jambo hilo. Lakini nilijitayarisha vizuri, na matokeo yalikuwa yenye kushangaza. Wanafunzi wengi waliniheshimu, naye mwalimu akaniambia kwamba alipendezwa na kazi niliyokuwa nikifanya. Zaidi ya yote, niliridhika kwamba nilikuwa nimetetea jina la Yehova na kueleza waziwazi sababu za msimamo wangu wa Kimaandiko.” (Mwanzo 9:3, 4; Matendo 15:28, 29) Naam, tukiwa watumwa wa Mungu na wa Kristo, sisi ni tofauti. Hata hivyo, huenda watu wakatuheshimu ikiwa tutakuwa tayari kutetea imani yetu kwa heshima.—1 Petro 3:15.

9. Tunajifunza nini kutokana na malaika aliyemtokea mtume Yohana?

9 Kukumbuka kwamba sisi ni watumwa wa Mungu kunaweza kutusaidia pia tuwe wanyenyekevu. Pindi moja, mtume Yohana alivutiwa sana na maono yenye kutokeza ya Yerusalemu wa kimbingu hivi kwamba aliinama ili kuabudu mbele ya miguu ya malaika aliyetumika kuwa mnenaji wa Mungu. Malaika huyo alimwambia: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa mwenzako tu na wa ndugu zako walio manabii na wa wale wanaoshika maneno ya kitabu hiki cha kukunjwa. Mwabudu Mungu.” (Ufunuo 22:8, 9) Bila shaka, malaika huyo aliwawekea watumwa wote wa Mungu kielelezo kizuri. Huenda Wakristo fulani wakawa na madaraka ya pekee kutanikoni. Hata hivyo, Yesu alisema: “Yeyote anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu, na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza katikati yenu lazima awe mtumwa wenu.” (Mathayo 20:26, 27) Tukiwa wafuasi wa Yesu, sisi sote ni watumwa.

“Jambo Ambalo Tumefanya Ndilo Tulilopaswa Kufanya”

10. Toa vielelezo vya Kimaandiko kuonyesha kwamba haikuwa rahisi sikuzote kwa watumishi waaminifu wa Mungu kufanya mapenzi yake.

10 Si rahisi sikuzote kwa wanadamu wasio wakamilifu kufanya mapenzi ya Mungu. Nabii Musa alisita kutii Yehova alipomwamuru aende kuwatoa wana wa Israeli kutoka utumwani Misri. (Kutoka 3:10, 11; 4:1, 10) Alipopokea mgawo wa kuwatangazia watu wa Ninawi ujumbe wa hukumu, Yona ‘alisimama na kukimbia kwenda Tarshishi kutoka mbele za Yehova.’ (Yona 1:2, 3) Baruku, mwandishi wa nabii Yeremia, alilalamika kwamba alikuwa amechoka. (Yeremia 45:2, 3) Tunapaswa kufanya nini wakati tamaa au mapendezi yetu yanapopingana na kufanya mapenzi ya Mungu? Tunapata jibu kutokana na mfano fulani ambao Yesu alitoa.

11, 12. (a) Eleza kifupi mfano ambao Yesu alitoa kwenye Luka 17:7-10. (b) Tunajifunza jambo gani kutokana na mfano wa Yesu?

11 Yesu alizungumza kuhusu mtumwa ambaye alikuwa akichunga kondoo wa bwana wake kondeni siku yote. Aliporudi nyumbani akiwa amechoka kutokana na kazi ngumu aliyofanya kwa muda wa saa 12 hivi, bwana wake hakumwalika aketi na kula chakula kitamu cha jioni. Badala yake, bwana huyo alisema: “Nitayarishie kitu ili nipate mlo wangu wa jioni, nawe jifunge unihudumie mpaka niwe nimemaliza kula na kunywa, kisha unaweza kula na kunywa.” Mtumwa huyo angeweza tu kushughulikia mahitaji yake baada ya kumtumikia bwana wake. Yesu alimalizia mfano huo kwa kusema: “Ndivyo na ninyi, pia, wakati mmefanya mambo yote mliyoagizwa, semeni, ‘Sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Jambo ambalo tumefanya ndilo tulilopaswa kufanya.’”—Luka 17:7-10.

12 Yesu hakutoa mfano huo ili kuonyesha kwamba Yehova hathamini utumishi tunaomtolea. Biblia inasema hivi waziwazi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Waebrania 6:10) Badala yake, jambo tunalojifunza kutokana na mfano wa Yesu ni kwamba mtumwa hawezi kujipendeza au kushughulikia starehe zake. Tulipojiweka wakfu kwa Mungu na kuchagua kuwa watumwa wake, tulikubali kutanguliza mapenzi yake. Tunapaswa kutanguliza mapenzi ya Mungu badala ya mapenzi yetu.

13, 14. (a) Ni katika hali gani huenda ikatubidi tushinde maelekeo yetu? (b) Kwa nini tunapaswa kutanguliza mapenzi ya Mungu?

13 Huenda tukahitaji kujitahidi sana ili kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida pamoja na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45) Huenda ikawa hivyo hasa ikiwa hatupendi kusoma au ikiwa kichapo kinazungumzia “mambo mazito ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10) Ingawa hivyo, je, hatupaswi kuwa na ratiba ya funzo la kibinafsi? Huenda tukahitaji kujitia nidhamu ili kukaa na kujifunza kichapo fulani kwa makini. Hata hivyo, tusipojitia nidhamu jinsi hiyo, tutasitawishaje tamaa ya “chakula kigumu [ambacho] ni cha watu wakomavu”?—Waebrania 5:14.

14 Namna gani tukirudi nyumbani tukiwa tumechoka sana baada ya shughuli nyingi za siku? Huenda ikabidi tujitahidi kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Au huenda lisiwe jambo la kawaida kwetu kuwahubiria watu tusiowafahamu. Paulo mwenyewe alitambua kwamba huenda pindi fulani tukatangaza habari njema ‘kinyume cha kupenda kwetu.’ (1 Wakorintho 9:17) Hata hivyo, tunafanya mambo hayo kwa sababu Yehova, Bwana wetu wa mbinguni ambaye tunampenda anatuambia kwamba tunapaswa kuyafanya. Lakini je, sikuzote hatujihisi kwamba tunaridhika na kuburudishwa tunapojitahidi kujifunza, kuhudhuria mikutano na kuhubiri?—Zaburi 1:1, 2; 122:1; 145:10-13.

Usitazame “Mambo Yaliyo Nyuma”

15. Yesu aliwekaje kielelezo cha kujitiisha kwa Mungu?

15 Yesu Kristo alionyesha ujitiisho kwa Baba yake wa mbinguni katika njia bora zaidi. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.” (Yohana 6:38) Alipokuwa na maumivu makali katika shamba la Gethsemane, alisali hivi: “Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki na kipitilie mbali kutoka kwangu. Lakini, si kulingana na mapenzi yangu, bali kulingana na mapenzi yako.”—Mathayo 26:39.

16, 17. (a) Tunapaswa kuyaonaje mambo tuliyoacha nyuma? (b) Eleza jinsi Paulo alivyoonyesha usawaziko kuhusu namna alivyoona matarajio yake ya kilimwengu kuwa “takataka nyingi.”

16 Yesu Kristo anataka tuendelee kuwa waaminifu katika uamuzi wetu wa kuwa watumwa wa Mungu. Alisema: “Hakuna mtu ambaye ameweka mkono wake kwenye jembe la ng’ombe na kutazama mambo yaliyo nyuma anayefaa kwa ajili ya ufalme wa Mungu.” (Luka 9:62) Bila shaka, haifai kuendelea kufikiria mambo tuliyoacha nyuma tunapomtumikia Mungu. Badala yake, tunapaswa kuthamini mambo ambayo tumepata kwa kuamua kuwa watumwa wa Mungu. Paulo aliwaandikia Wafilipi hivi: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo.”—Wafilipi 3:8.

17 Fikiria mambo yote ambayo Paulo aliyaona kuwa takataka na kuyaacha ili kupata thawabu akiwa mtumwa wa Mungu. Hakuacha tu starehe za ulimwengu bali pia uwezekano wa kuwa kiongozi wa dini ya Wayahudi. Ikiwa Paulo angeendelea kufuatilia dini ya Wayahudi, labda angekuwa na cheo kama kile cha Simeoni, mwana wa Gamalieli, mwalimu wa Paulo. (Matendo 22:3; Wagalatia 1:14) Simeoni alipata kuwa kiongozi wa Mafarisayo naye alitimiza fungu muhimu—licha ya kuwa na shaka— katika uasi wa Wayahudi dhidi ya Roma mwaka wa 66 hadi 70 W.K. Alikufa katika vita hivyo, kwa kuuawa ama na Wayahudi wenye siasa kali ama na jeshi la Roma.

18. Toa mfano ili kuonyesha jinsi ambavyo mafanikio ya kiroho huleta thawabu.

18 Mashahidi wengi wa Yehova wamefuata kielelezo cha Paulo. “Miaka michache baada ya kuacha shule, nilipata kazi ya kuwa sekretari wa mwana-sheria mashuhuri huko London,” asema Jean. “Nilifurahia kazi yangu na nilipata mshahara mzuri, lakini nilijua moyoni mwangu kwamba ningeweza kufanya mengi zaidi ili kumtumikia Yehova. Mwishowe, niliandika barua ya kuacha kazi na nikaanza upainia. Ninashukuru sana kwamba nilichukua hatua hiyo karibu miaka 20 iliyopita. Utumishi wangu wa wakati wote umefanya maisha yangu yawe yenye kuridhisha zaidi kuliko kazi yoyote ya sekretari. Hakuna jambo linaloridhisha zaidi kuliko kuona Neno la Yehova likibadili maisha ya mtu. Inafurahisha sana kuchangia katika jambo hilo. Tunapata mengi zaidi kutoka kwa Yehova kuliko yale tunayompa.”

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na kwa nini?

19 Huenda hali zetu zikabadilika kadiri wakati unavyopita. Hata hivyo, wakfu wetu kwa Mungu haubadiliki. Sisi bado ni watumwa wa Yehova, naye huturuhusu tuamue jinsi tutakavyotumia wakati, nguvu, vipawa, na mali zetu nyingine. Hivyo, maamuzi tunayofanya kuhusiana na mambo hayo yanaweza kuonyesha upendo wetu kwa Mungu. Pia yanaweza kuonyesha kadiri tunavyojidhabihu. (Mathayo 6:33) Bila kujali hali zetu, je, hatupaswi kuazimia kumpa Yehova kilicho bora zaidi? Paulo aliandika hivi: “Ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho, si kulingana na kile ambacho mtu hana.”—2 Wakorintho 8:12.

“Mnapata Tunda Lenu”

20, 21. (a) Watumwa wa Mungu hutokeza matunda gani? (b) Yehova huwathawabishaje wale wanaompa kilicho bora zaidi?

20 Kuwa watumwa wa Mungu si jambo lenye kukandamiza. Badala yake, kunatuweka huru na utumwa wenye kukandamiza ambao hufanya tusiwe na furaha. Paulo aliandika: “Kwa sababu mliwekwa huru kutoka katika dhambi lakini mkawa watumwa kwa Mungu, mnapata tunda lenu katika utakatifu, na mwisho ni uzima wa milele.” (Waroma 6:22) Kumtumikia Mungu hutokeza tunda katika utakatifu katika maana ya kwamba sisi hupata manufaa ya kuwa na mwenendo mtakatifu, au safi kiadili. Isitoshe, kutaongoza kwenye uzima wa milele wakati ujao.

21 Yehova ni mkarimu kwa watumwa wake. Tunapofanya yote tuwezayo katika utumishi wake, yeye hutufungulia “malango ya mbinguni” na kutumwagia “baraka hata kusiwe na uhitaji tena.” (Malaki 3:10) Tutafurahia kuendelea kumtumikia Yehova tukiwa watumwa wake kwa umilele wote.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini sisi huwa watumwa wa Mungu?

• Sisi huonyeshaje ujitiisho wetu kwa mapenzi ya Mungu?

• Kwa nini tunapaswa kuwa tayari kutanguliza mapenzi ya Yehova badala ya mapenzi yetu?

• Kwa nini hatupaswi ‘kutazama mambo yaliyo nyuma’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Mpango wa utumwa wa kujitolea katika Israeli ulionyesha kimbele utumwa ambao Wakristo wako chini yake

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tunakuwa watumwa wa Mungu tunapobatizwa

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wakristo hutanguliza mapenzi ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Musa alisita kukubali mgawo wake