Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Samsoni Ashinda kwa Nguvu za Yehova!

Samsoni Ashinda kwa Nguvu za Yehova!

Samsoni Ashinda kwa Nguvu za Yehova!

WALIPIZA-KISASI waliomkamata wayang’oa macho yake na kumfanyiza kazi ngumu. Kisha wanamtoa nje ya nyumba ya gereza na kumwingiza katika hekalu la kipagani ili autumbuize umati. Wanamlazimisha kutembea mbele ya maelfu ya watazamaji nao wanamdhihaki. Mfungwa huyo si mhalifu wala kamanda wa jeshi la adui. Yeye ni mwabudu wa Yehova naye ametumika akiwa mwamuzi katika Israeli kwa miaka 20.

Samsoni, mwanamume mwenye nguvu zaidi za kimwili aliyepata kuishi, alijikutaje katika hali hiyo yenye kuabisha? Je, nguvu zake zisizo za kawaida zingemwokoa? Nguvu za Samsoni zilitoka wapi? Je, kuna jambo lolote tunaloweza kujifunza kutokana na simulizi la maisha yake?

‘Ataongoza Katika Kuokoa Israeli’

Wana wa Israeli waliacha ibada ya kweli mara nyingi. Hivyo ‘walipoanza tena kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, Yehova akawatia mkononi mwa Wafilisti kwa miaka 40.’—Waamuzi 13:1.

Simulizi la Samsoni lilianza wakati malaika wa Yehova alipomtokea mke tasa wa mwanamume Mwisraeli aliyeitwa Manoa na kumwambia kwamba angezaa mwana. Malaika huyo alimwagiza hivi: “Na wembe wowote usipite juu ya kichwa chake, kwa maana mtoto huyo atakuwa Mnadhiri wa Mungu tangu atakapotoka tumboni; naye ndiye atakayeongoza katika kuokoa Israeli kutoka mkononi mwa Wafilisti.” (Waamuzi 13:2-5) Kabla ya kutungwa kwa mimba ya Samsoni, Yehova aliamua kwamba Samsoni angekuwa na mgawo hususa. Tangu kuzaliwa kwake, alipaswa kuwa Mnadhiri, yaani, mtu aliyechaguliwa kwa ajili ya utumishi mtakatifu wa aina ya pekee.

Ndiye “Anayestahili Kabisa Machoni Pangu”

Samsoni alipoendelea kukua, ‘Yehova aliendelea kumbariki.’ (Waamuzi 13:24) Siku moja, Samsoni aliwaendea baba na mama yake na kuwaambia: “Nimemwona mwanamke mmoja huko Timna kati ya binti za Wafilisti, basi sasa mniletee mwanamke huyo awe mke wangu.” (Waamuzi 14:2) Hebu wazia jinsi walivyoshangaa. Badala ya kuwakomboa Waisraeli kutoka mikononi mwa wakandamizaji wao, mwana wao alitaka kufanya mapatano ya ndoa pamoja nao. Kumwoa mwanamke ambaye alikuwa mwabudu wa miungu ya kipagani kulikuwa kinyume cha Sheria ya Mungu. (Kutoka 34:11-16) Hivyo, wazazi wake walikataa na kumwambia: “Je, hakuna mwanamke yeyote kati ya binti za ndugu zako na kati ya watu wangu wote, hivi kwamba uende kumchukua mwanamke kutoka kwa Wafilisti wasiotahiriwa?” Lakini bado Samsoni alisisitiza hivi: “Nileteeni huyo, kwa maana ndiye anayestahili kabisa machoni pangu.”—Waamuzi 14:3.

Mwanamke huyo Mfilisti alikuwaje mwenye ‘kustahili kabisa’ machoni pa Samsoni? Si katika maana ya kwamba alikuwa “mrembo na mwenye kuvutia,” chasema kichapo Cyclopedia cha McClintock na Strong, “bali alistahili katika maana ya kwamba angeweza kumsaidia kutimiza lengo lake.” Kutimiza lengo gani? Andiko la Waamuzi 14:4 linaeleza kwamba Samsoni “alikuwa akitafuta nafasi ya kuwapiga Wafilisti.” Samsoni alipendezwa na mwanamke huyo kwa lengo hilo. Samsoni alipokuwa mtu mzima, ‘roho ya Yehova ilianza kumchochea,’ au ilimsukuma kutenda. (Waamuzi 13:25) Kwa hiyo, roho ya Yehova ndiyo iliyomchochea Samsoni kufanya ombi lisilo la kawaida la kupewa mke na pia ndiyo iliyomchochea muda wote aliotumika akiwa mwamuzi juu ya Israeli. Je, Samsoni alipata nafasi aliyokuwa akitafuta? Kwanza, acheni tuone jinsi Yehova alivyomhakikishia kwamba angemtegemeza.

Samsoni alikuwa akisafiri kuelekea Timna, jiji la yule ambaye angekuwa mke wake. Simulizi la Biblia linasema: “Alipofika katika mashamba ya mizabibu ya Timna, tazama! mwana-simba mwenye manyoya shingoni akamngurumia alipokutana naye. Ndipo roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu yake, naye akampasua vipande viwili.” Samsoni alipata nguvu hizo zisizo za kawaida alipokuwa peke yake. Hakukuwa na mashahidi wowote. Je, hiyo ilikuwa njia ya Yehova ya kumhakikishia Samsoni kwamba akiwa Mnadhiri angeweza kutimiza kazi aliyopewa na Mungu? Biblia haielezi jambo lolote, lakini bila shaka Samsoni alitambua kwamba nguvu hizo zisizo za kawaida hazikuwa zake. Lazima ziwe zilitoka kwa Mungu. Angeweza kumtegemea Yehova amsaidie kutimiza kazi iliyokuwa mbele yake. Akiwa ameimarishwa na kisa hicho cha simba, Samsoni ‘aliendelea kushuka, akaanza kusema na yule mwanamke; na huyo mwanamke alikuwa bado ni mwenye kustahili machoni pake.’—Waamuzi 14:5-7.

Baadaye, Samsoni aliporudi ili kumchukua mwanamke huyo na kumpeleka nyumbani kwake, ‘aligeuka kando kuuangalia ule mzoga wa simba, na tazama, kulikuwa na bumba la nyuki ndani ya huo mzoga wa simba, na asali.’ Akikumbuka hilo, Samsoni alitega kitendawili hiki kwa Wafilisti 30, rafiki za bwana-arusi kwenye arusi yake: “Katika mwenye kula kilitoka kitu fulani cha kula, na katika mwenye nguvu kilitoka kitu fulani kitamu.” Kama wangetegua kitendawili hicho, Samsoni angewapa mavazi ya ndani na nguo 30. Kama wangeshindwa, wangempa vitu hivyo. Wafilisti walitatanishwa na kitendawili hicho kwa muda wa siku tatu. Siku ya nne, waliamua kumtisha mwanamke huyo. Walimwambia hivi: “Mdanganye mume wako ili atutegulie kitendawili hicho. Kama sivyo tutakuteketeza kwa moto wewe na nyumba ya baba yako.” Huo ni ukatili ulioje! Ikiwa Wafilisti waliwatendea watu wao katika njia hiyo, hebu fikiria masaibu ya Waisraeli waliokandamizwa!—Waamuzi 14:8-15.

Mwanamke huyo aliyekuwa ameogopa sana alimsonga Samsoni amwambie jibu. Akionyesha ukosefu wa upendo na ushikamanifu kwa Samsoni, alienda mara moja kuwajulisha rafiki za bwana-arusi. Walitegua kitendawili hicho, naye Samsoni alijua jinsi walivyofanikiwa. Aliwaambia hivi: “Kama hamngelima na ng’ombe wangu mchanga, hamngekitegua kitendawili changu.” Nafasi ambayo Samsoni alikuwa akingojea sasa ilikuwa imejitokeza. “Roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu yake, kisha akashuka Ashkeloni, akawapiga watu 30 kati yao, akachukua mavazi aliyowavua, akawapa mavazi hayo wale wasemaji wa kile kitendawili.”—Waamuzi 14:18, 19.

Je, tendo la Samsoni huko Ashkeloni lilichochewa na tamaa ya kulipiza kisasi? La. Hilo lilikuwa tendo la Mungu kupitia mtu aliyemchagua kuwa mkombozi. Kupitia Samsoni, Yehova alianzisha vita dhidi ya watu waliowakandamiza watu wake kwa ukatili. Kampeni hiyo ingeendelea. Nafasi nyingine ilijitokeza Samsoni alipoenda kumtembelea mke wake.

Apigana Akiwa Peke Yake

Aliporudi Timna, Samsoni aligundua kwamba baba ya mke wake alimwoza kwa mwanamume mwingine, akiamini kwamba Samsoni alimchukia binti yake. Samsoni alionekana kuwa ameudhika. Aliwakamata mbweha 300, akawafunga wawili-wawili, na kuweka mwenge katikati ya mikia yao. Alipowaachilia, waliwasha moto mashamba ya nafaka, mizabibu, na mizeituni, na kuharibu mazao makuu matatu ya Wafilisti ya mwaka huo. Wafilisti wenye hasira walitenda kikatili. Waliona kwamba mke wa Samsoni na baba yake ndio waliosababisha jambo hilo na hivyo wakawateketeza kwa moto. Ukatili wao wa kulipiza kisasa ulitimiza lengo la Samsoni. Naye, akawapiga kwa mauaji makubwa.—Waamuzi 15:1-8.

Je, Waisraeli walielewa kwamba Yehova Mungu alikuwa akimbariki Samsoni na hivyo kuungana naye ili kukomesha utawala wa Wafilisti? La. Ili kuepuka matatizo, watu wa Yuda waliwatuma wanaume 3,000 wamkamate kiongozi aliyechaguliwa na Mungu na kumtoa kwa maadui wake. Hata hivyo, ukosefu huo wa ushikamanifu wa Waisraeli ulimpa Samsoni nafasi ya kuwapiga tena maadui wake. Alipokuwa karibu kutolewa kwa Wafilisti, “roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu yake, na zile kamba zilizokuwa kwenye mikono yake zikawa kama nyuzi za kitani ambazo zimeunguzwa kwa moto, nazo pingu zake zikayeyuka kutoka kwenye mikono yake.” Kisha akachukua mfupa mbichi wa taya ya punda na kuutumia kuwapiga maadui elfu moja.—Waamuzi 15:10-15.

Akimsihi Yehova, Samsoni alisema: “Wewe ndiye uliyetia wokovu huu mkubwa mkononi mwa mtumishi wako, na je, sasa nife kutokana na kiu, na je, nianguke mkononi mwa wasiotahiriwa?” Yehova alisikia sala ya Samsoni na kuijibu. “Mungu akapasua shimo lenye umbo la kinu . . . , na maji yakaanza kutoka ndani yake, naye akanywa, kisha roho yake ikarudi na nguvu zikamrudia.”—Waamuzi 15:18, 19.

Samsoni alikuwa ameazimia kufuatia lengo lake, yaani, kupigana na Wafilisti. Samsoni alikaa katika nyumba ya kahaba huko Gaza akiwa na lengo la kuwapiga maadui wa Mungu. Samsoni alihitaji mahali pa kulala usiku huo katika jiji la adui, na mahali hapo pangeweza kupatikana katika nyumba ya kahaba. Samsoni hakufikiria kufanya tendo lisilo la adili. Aliondoka nyumbani kwa mwanamke huyo katikati ya usiku, akakamata milango ya lango la jiji na miimo yake miwili, na kuibeba mpaka kwenye kilele cha mlima uliokuwa karibu na Hebroni, jiji lililokuwa umbali wa kilometa 60 hivi. Alifanya hivyo kwa sababu alikuwa na kibali na nguvu alizopewa na Mungu.—Waamuzi 16:1-3.

Roho takatifu ilitenda kwa njia ya pekee katika kisa cha Samsoni kwa sababu ya hali zisizo za kawaida. Watumishi waaminifu wa Mungu leo wanaweza kuitegemea roho hiyo hiyo iwape nguvu. Yesu aliwahakikishia wafuasi wake kwamba Yehova ‘atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.’—Luka 11:13.

Kwa Nini Yehova ‘Alimwacha Samsoni’?

Ikawa kwamba Samsoni alimpenda mwanamke fulani aliyeitwa Delila. Wakuu watano wa muungano wa Wafilisti walitaka sana kumwangamiza Samsoni, kwa hiyo walitafuta msaada wa Delila. Walimwendea Delila na kumwambia: “Mdanganye ili uone nguvu zake nyingi zinatokana na nini, na kile tunachoweza kutumia ili kumshinda.” Ili kumhonga, kila mmoja wa wakuu hao watano aliahidi kumpa “vipande elfu moja na mia moja vya fedha.”—Waamuzi 16:4, 5.

Ikiwa vipande vya fedha vilikuwa shekeli, hongo ya shekeli 5,500 ilikuwa kubwa sana. Abrahamu alilipa shekeli 400 kwa ajili ya mahali pa kumzikia mke wake, naye mtumwa aliuzwa kwa shekeli 30 tu. (Mwanzo 23:14-20; Kutoka 21:32) Huenda Delila alikuwa mwanamke Mwisraeli kwa kuwa wakuu, yaani, watawala wa majiji matano ya Wafilisti walimhonga badala ya kumwambia awasaidie kwa sababu ya ushikamanifu wake kwa taifa lake. Vyovyote vile, Delila alikubali fedha hizo.

Mara tatu Samsoni alimpa Delila majibu yasiyo ya kweli, naye Delila alimsaliti mara tatu kwa kujaribu kumtoa kwa maadui wake. Lakini “ikawa kwamba kwa sababu mwanamke huyo alimkaza kwa maneno yake wakati wote na kuendelea kumsihi, nafsi yake ikakosa subira kufikia hatua ya kutaka kufa.” Mwishowe, Samsoni alifunua ukweli, yaani, nywele zake hazikuwa zimewahi kunyolewa. Kama angenyolewa, angekuwa dhaifu na kuwa kama wanadamu wengine wote.—Waamuzi 16:6-17.

Kufunua siri hiyo kulisababisha kuanguka kwa Samsoni. Delila alipanga njama na kufanya Samsoni anyolewe. Hata hivyo, kwa kweli nguvu za Samsoni hazikuwa katika nywele zake. Nywele zake ziliwakilisha tu uhusiano wake wa pekee pamoja na Mungu akiwa Mnadhiri. Samsoni alipojiruhusu awe katika hali ambayo iliathiri Unadhiri wake kwa kunyolewa kichwa chake, ‘Yehova alimwacha.’ Sasa Wafilisti walimshinda nguvu Samsoni, wakampofusha, na kumtia gerezani.—Waamuzi 16:18-21.

Kisa hicho kinatufunza jambo muhimu sana. Je, hatupaswi kuona uhusiano wetu pamoja na Yehova kuwa kitu chenye thamani sana? Tukilegeza kwa njia yoyote wakfu wetu kwa Mungu tukiwa Wakristo, tunawezaje kutarajia Mungu aendelee kutubariki?

“Nafsi Yangu na Ife Pamoja na Wafilisti”

Wafilisti wenye furaha nyingi walimshukuru mungu wao Dagoni kwa kumshinda Samsoni. Ili kusherehekea ushindi wao, walimpeleka mateka wao kwenye hekalu la Dagoni. Lakini Samsoni alijua vizuri sababu ya kuanguka kwake. Alijua sababu iliyofanya Yehova amwache, naye alitubu kwa kosa lake. Samsoni alipokuwa katika nyumba ya gereza, nywele zake zilianza kukua sana. Kwa kuwa sasa alikuwa mbele ya maelfu ya Wafilisti, angefanya nini?

Samsoni alisali hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, tafadhali nikumbuke, tafadhali unitie nguvu, mara hii moja tu, Ee Mungu wa kweli, ili nijilipize kisasi juu ya Wafilisti kwa ajili ya jicho langu moja kati ya macho yangu mawili.” Ndipo akajiinamisha kwa zile nguzo mbili za katikati za jengo hilo, naye “akajiinamisha kwa nguvu.” Matokeo yakawaje? “Nyumba ile ikawaangukia wale wakuu wa muungano na watu wote waliokuwamo ndani, hivi kwamba wafu alioua wakati wa kifo chake wakawa wengi kuliko wale alioua wakati wa maisha yake.”—Waamuzi 16:22-30.

Samsoni ndiye aliyekuwa mwanadamu mwenye nguvu nyingi zaidi za kimwili. Kwa kweli, matendo yake makuu yalijulikana. Lakini jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba Neno la Yehova humtaja Samsoni kuwa miongoni mwa watu wenye imani yenye nguvu.—Waebrania 11:32-34.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nguvu za Samsoni zilitoka wapi?