Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uvutano wa Yesu Ulimwenguni Pote

Uvutano wa Yesu Ulimwenguni Pote

Uvutano wa Yesu Ulimwenguni Pote

“YALE yote ambayo vitabu vya injili huripoti kwamba Yesu alisema faraghani na hadharani, huenda aliyasema kwa saa mbili,” akaandika mtafsiri wa Biblia, Edgar Goodspeed. “Hata hivyo, mafundisho hayo machache yaliwachochea watu sana hivi kwamba tunaweza kusema kuwa hakuna mtu mwingine yeyote ambaye amekuwa na uvutano mkubwa sana ulimwenguni kama yeye.”

Alipomaliza huduma yake duniani katika mwaka wa 33 W.K., Yesu Kristo alikuwa na wafuasi wanaume na wanawake angalau 120 hivi. (Matendo 1:15) Leo, zaidi ya watu bilioni mbili hudai kuwa Wakristo. Mamia ya mamilioni ya wengine humtambua Yesu kuwa nabii. Kwa kweli, mafundisho yake yamekuwa na uvutano mkubwa kwa wanadamu.

Uvutano wa Yesu ulimwenguni pote umetambuliwa hata na viongozi wa dini zisizo za Kikristo. Kwa mfano, rabi Myahudi Hyman Enelow aliandika hivi: “Yesu amekuwa mtu mashuhuri sana, mtu ambaye watu wamejifunza mengi sana juu yake, mtu mwenye uvutano mkubwa zaidi katika historia ya kidini ya wanadamu.” Enelow alisema hivi pia: “Ni nani anayeweza kukisia uvutano ambao Yesu amekuwa nao juu ya wanadamu? Upendo ambao amechochea, faraja ambayo ametoa, wema ambao ameleta, tumaini na shangwe ambayo amechochea—mambo hayo yote hayana kifani katika historia ya wanadamu. Kati ya watu mashuhuri na wazuri ambao wamepata kuishi, hakuna hata mmoja ambaye amemkaribia Yesu kwa kuwa na uvutano na mamlaka ulimwenguni pote. Amekuwa mtu mwenye kuvutia zaidi katika historia.” Naye kiongozi Mhindu, Mohandas K. Gandhi alisema: “Simjui mtu mwingine yeyote ambaye amewafanyia wanadamu mengi kama Yesu. Kwa kweli, Ukristo hauna ubaya wowote.” Hata hivyo, aliongezea kusema: “Ninyi Wakristo ndio wenye tatizo. Maisha yenu hayapatani hata kidogo na mafundisho yenu wenyewe.”

Wale wanaojidai kuwa Wakristo wameshindwa kabisa kuishi kupatana na mafundisho ya Yesu. Mwanahistoria wa Ukristo, Cecil John Cadoux, alisema kwamba “ongezeko la hatua kwa hatua la ulegevu fulani wa maadili katika Kanisa lote lilitambuliwa na viongozi Wakristo mapema . . . mwaka wa 140 W.K.” Alisema: “Kulegea huko kwa maadili kwa kawaida kungefanya iwe rahisi kwa watu kufuata njia za ulimwengu.”

Kulegea huko kwa maadili kulienea katika karne ya nne, wakati Maliki Mroma Konstantino alipokuwa Mkristo. Cadoux aliandika: “Wanahistoria wametambua hilo na baadhi yao wameshutumu jinsi Kanisa lilivyolegeza msimamo wake kabisa kwa kuungana na Konstantino.” Katika karne zilizofuata, wale wanaojidai kuwa Wakristo wamefanya mambo mengi ya aibu ambayo hulivunjia heshima jina la Kristo.

Basi, maswali yanayotuhangaisha ni: Kwa kweli, Yesu alifundisha nini? Nayo mafundisho yake yanapaswa kuwa na uvutano gani juu yetu?

[Picha katika ukurasa wa 3]

“Simjui mtu mwingine yeyote ambaye amewafanyia wanadamu mengi kama Yesu.”—Mohandas K. Gandhi

[Picha katika ukurasa wa 3]

“Hakuna mtu mwingine yeyote ambaye amekuwa na uvutano mkubwa sana ulimwenguni kama yeye.”—Edgar Goodspeed

[Hisani]

Culver Pictures