Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Wanaomsifu Yehova Huboresha Maisha Yao

Vijana Wanaomsifu Yehova Huboresha Maisha Yao

“Msaada Wangu Unatoka Kwa Yehova”

Vijana Wanaomsifu Yehova Huboresha Maisha Yao

“NATAKA kuwa na vitu vizuri maishani!” Hivyo ndivyo mvulana mmoja tineja alivyoeleza matarajio yake. Lakini kijana anawezaje kupata vitu vizuri maishani? Biblia inatoa jibu lililo wazi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako.”—Mhubiri 12:1, Union Version.

Si watu wazima tu humsifu na kumtumikia Yehova. Samweli, mwana wa Elkana na Hana alikuwa mchanga sana alipomtumikia Yehova kwenye maskani. (1 Samweli 1:19, 20, 24; 2:11) Msichana Mwebrania mwenye umri mdogo alionyesha imani thabiti katika Yehova alipodokeza kwamba Naamani, mkuu wa jeshi la Siria aende kwa nabii Elisha ili aponywe ukoma wake. (2 Wafalme 5:2, 3) Kwenye Zaburi 148:7, 12, wote, wavulana kwa wasichana wanaamriwa wamsifu Yehova. * Alipokuwa na umri wa miaka 12 tu, Yesu alipendezwa sana na kumtumikia Baba yake. (Luka 2:41-49) Kwa sababu walifundishwa Maandiko, wavulana fulani walipaaza sauti hivi walipomwona Yesu hekaluni: “Mwokoe Mwana wa Daudi, tunaomba!”—Mathayo 21:15, 16.

Kumsifu Yehova Leo

Leo, vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova hujivunia mafundisho yao nao huwaambia wengine kwa ujasiri juu ya mafundisho hayo wakiwa shuleni na kwingineko. Fikiria mifano miwili.

Huko Uingereza, wanadarasa wa Stephanie, mwenye umri wa miaka 18 walikuwa wakizungumzia utoaji-mimba na masuala mengine ya maadili. Mwalimu alisema kwamba sasa utoaji-mimba unakubaliwa na kwamba mwanamke yeyote kijana hana msingi wa kupinga zoea hilo. Wanafunzi wote walipokubaliana na maoni hayo, Stephanie alitaka sana kutetea msimamo wake unaotegemea Biblia. Nafasi ilijitokeza mwalimu alipomwuliza Stephanie maoni yake. Ingawa alikuwa na wasiwasi mwanzoni, Stephanie alitumia nafasi hiyo kueleza maoni ya Biblia. Alitaja andiko la Kutoka 21:22-24 na kueleza kwamba ikiwa lilikuwa kosa kumuumiza mtoto aliye tumboni, basi bila shaka, utoaji-mimba ungekuwa kinyume cha mapenzi ya Mungu.

Mwalimu wake ambaye pia alikuwa kasisi, hakuwa amewahi kusoma mistari hiyo. Kwa sababu ya kuhubiri kwa ujasiri, Stephanie alikuwa na mazungumzo mengi yenye kupendeza na wanadarasa wenzake kuhusu mambo mbalimbali. Sasa msichana mmoja hupokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida, nao wasichana wengine wawili walihudhuria kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova ili kumwona Stephanie akionyesha wakfu wake kwa Mungu kwa kubatizwa.

Vareta, mwenye umri wa miaka sita ambaye anaishi Suriname, huko Amerika Kusini, alipata nafasi ya kumsifu Mungu mwalimu wake alipohitaji faraja kutoka kwenye Maandiko. Aliporudi shuleni baada ya siku tatu, mwalimu huyo aliwauliza wanafunzi wake ikiwa walijua kwa nini hakuja shuleni siku hizo tatu. Walijibu, “Ulikuwa mgonjwa, sivyo?” “La,” akajibu mwalimu. “Dada yangu alikufa, nami nina huzuni sana. Kwa hiyo, sitaki kelele.”

Alasiri hiyo, mama yake alipokuwa akipumzika, Vareta alipekua-pekua magazeti ya zamani huko akisoma vichwa vyake. Alipata gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2001, lenye kichwa “Je, Kuna Uhai Baada ya Kifo?” Akiwa na shauku nyingi, alimwamsha mama yake na kusema, “Mama, Mama, tazama! Nimepata gazeti kuhusu kifo ambalo nitampa mwalimu wangu!” Mwalimu huyo alitumiwa gazeti hilo pamoja na barua ya Vareta. Aliandika: “Gazeti hili ni lako hasa. Utamwona tena dada yako katika Paradiso kwa sababu Yehova hasemi uwongo. Ameahidi kuleta paradiso, si mbinguni, bali hapa duniani.” Mwalimu huyo alithamini sana faraja kutoka kwenye Biblia aliyopata katika makala hizo.

Kujitayarisha kwa Ajili ya Wakati Ujao

Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” naye anataka vijana wawe na furaha. (1 Timotheo 1:11) Neno lake linasema hivi: ‘Furahia ujana wako. Uchangamke wakati ungali kijana.’ (Mhubiri 11:9, Biblia Habari Njema) Yehova haangalii matokeo ya sasa tu bali yeye huona matokeo ya wakati ujao ya mwenendo mzuri au mbaya. Kwa sababu hiyo, Neno lake linawashauri vijana hivi: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako, kabla siku zenye msiba hazijaja, au miaka iwe imefika wakati utasema: ‘Sipendezwi nayo.’”—Mhubiri 12:1.

Naam, Yehova anataka vijana wafurahie kikamili zawadi ya uhai ambayo ni yenye thamani sana. Vijana wanaweza kuwa na maisha yenye kusudi na yenye kuridhisha kwa kumkumbuka Mungu na kumsifu. Hata wanapokabili magumu, wanaweza kusema hivi kwa uhakika: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”—Zaburi 121:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona Kalenda ya mwaka wa 2005 ya Mashahidi wa Yehova, Machi/Aprili.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Msifuni Yehova kutoka duniani, . . . enyi vijana, nanyi mabikira pia.”—ZABURI 148:7, 12

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

YEHOVA HUWATEGEMEZA VIJANA

“Wewe ni tumaini langu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova, tegemeo langu tangu ujana wangu.”—Zaburi 71:5.

‘Mungu anaushibisha muda wote wa maisha yako kwa mambo mema; ujana wako unajifanya upya kama ule wa tai.’—Zaburi 103:5.