Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo Ana Uvutano Gani Juu Yako?

Yesu Kristo Ana Uvutano Gani Juu Yako?

Yesu Kristo Ana Uvutano Gani Juu Yako?

KWA kuzingatia yale ambayo tulizungumzia katika makala iliyopita, hakuna shaka kwamba mafundisho ya Yesu yana uvutano mkubwa ulimwenguni pote. Hata hivyo, swali ambalo kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza ni hili, “Mafundisho ya Yesu yana uvutano gani juu yangu mimi binafsi?”

Mafundisho ya Yesu yalitia ndani mambo mengi. Mambo muhimu ambayo alifundisha yanaweza kuathiri kila sehemu ya maisha yako. Acheni tukazie fikira yale ambayo Yesu alifundisha kuhusu kupanga mambo ya kutangulizwa maishani, kusitawisha urafiki pamoja na Mungu, kusitawisha uhusiano mzuri pamoja na wengine, kutatua matatizo, na kujiepusha na matendo ya jeuri.

Panga Mambo ya Kutangulizwa Maishani

Ulimwengu wa leo wenye hekaheka huchukua wakati na nguvu zetu nyingi sana hivi kwamba hatupati wakati wa kufanya mambo ya kiroho. Fikiria mfano wa mwanamume mmoja aliye na miaka 20 na kitu ambaye tutamwita Jerry. Ingawa Jerry hufurahia kuzungumzia mambo ya kiroho na huthamini sana yale anayojifunza, yeye analalamika hivi: “Sina wakati wa kuzungumzia mambo hayo kwa ukawaida. Mimi hufanya kazi siku sita kwa juma. Jumapili tu ndiyo siku yangu ya kupumzika. Na baada ya kufanya mambo ninayopaswa kufanya, mimi huwa nimechoka sana.” Ukijikuta katika hali kama hiyo, unaweza kunufaika na yale ambayo Yesu alifundisha katika Mahubiri ya Mlimani.

Yesu aliuambia hivi umati uliokuwa umekusanyika kumsikiliza: “Acheni kuhangaika juu ya nafsi zenu kuhusu kile mtakachokula au kile mtakachokunywa, au juu ya miili yenu kuhusu kile mtakachovaa. Je, nafsi haimaanishi zaidi ya chakula na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao? . . . Kwa hiyo msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mathayo 6:25-33) Maneno hayo yanatufunza nini?

Yesu hakuwa akisema kwamba tunapaswa kupuuza mahitaji yetu ya kimwili na yale ya washiriki wa familia zetu. “Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake,” Biblia inasema, “ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, Yesu aliahidi kwamba tukipanga mambo yanayopaswa kutangulizwa na kutanguliza mambo ya kiroho, Mungu atahakikisha kwamba tunatimiziwa mahitaji yale mengine. Jambo kuu hapa ni kuhusu mambo tunayopaswa kutanguliza. Kufuata shauri hilo huleta furaha, kwa kuwa “wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Sitawisha Urafiki Pamoja na Mungu

Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho huona umuhimu wa kusitawisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Tunasitawishaje uhusiano mzuri pamoja na mtu fulani? Ni kwa kujitahidi kumjua vizuri mtu huyo. Lazima tuchukue wakati kujua maoni na mitazamo yake, yale ambayo ametimiza, uwezo wake, mambo anayopenda na yale anayochukia. Ndivyo ilivyo na kusitawisha urafiki pamoja na Mungu. Tunahitaji kuwa na ujuzi sahihi kumhusu. Alipokuwa akisali kwa Mungu kuhusu wanafunzi wake, Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Naam, ili tusitawishe urafiki pamoja na Mungu, tunahitaji kumjua. Ujuzi huo unapatikana tu katika Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (2 Timotheo 3:16) Ni lazima tutenge wakati wa kujifunza Biblia.

Hata hivyo, ujuzi pekee hautoshi. Katika sala hiyohiyo, Yesu alisema: “[Wanafunzi wake] wamelishika neno lako.” (Yohana 17:6) Hatupaswi tu kupata ujuzi kumhusu Mungu bali pia tunapaswa kutenda kupatana na ujuzi huo. Hatuwezi kuwa rafiki za Mungu tusipofanya hivyo. Je, urafiki wetu na mtu mwingine unaweza kukua ikiwa tutatenda kimakusudi kinyume cha maoni na kanuni za mtu huyo? Hivyo basi, maoni na kanuni za Mungu zinapaswa kuongoza hatua zetu zote maishani. Ona jinsi ambavyo kanuni zake mbili zinaweza kutumiwa katika mahusiano yetu na wanadamu wengine.

Sitawisha Uhusiano Mzuri na Wengine

Pindi moja, Yesu alisimulia hadithi fupi ili kufundisha jambo muhimu kuhusu mahusiano ya kibinadamu. Alizungumza kuhusu mfalme aliyetaka kufanya hesabu pamoja na watumishi wake. Hata hivyo, mmoja wa watumishi hao alikuwa na deni kubwa, naye hakuwa na uwezo wa kulilipa. Bwana huyo aliagiza mtu huyo, mke wake, na watoto wake wauzwe na malipo yatolewe. Mtumishi huyo alianguka chini na kumsihi hivi: “Uwe na subira kwangu nami nitakulipa kila kitu.” Kwa kumsikitikia, bwana huyo alifuta deni lake. Lakini mtumwa huyo alienda zake na akamkuta mmoja wa watumwa wenzake aliyekuwa na deni lake dogo, na akadai amlipe. Ingawa mtumwa mwenzake alimsihi amhurumie, mtumwa wa kwanza aliagiza atupwe gerezani mpaka alipe deni lake lote. Mfalme aliposikia jambo hilo, alikasirika sana. “Haikukupasa wewe . . . kuwa na rehema juu ya mtumwa mwenzako, kama mimi pia nilivyokuwa na rehema juu yako?” akamuuliza. Naye akaagiza mtumwa huyo asiye na rehema afungwe mpaka alipe deni lake lote. Ili kufundisha jambo kuu katika hadithi hiyo, Yesu alisema: “Vivyo hivyo Baba yangu wa mbinguni atashughulika nanyi pia ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni mwake.”—Mathayo 18:23-35.

Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, tuna kasoro nyingi. Hatuwezi kamwe kumlipa Mungu deni kubwa ambalo tumerundika kwa sababu ya kumkosea. Jambo tunaloweza kufanya tu ni kumwomba msamaha. Naye Yehova Mungu yuko tayari kutusamehe makosa yetu yote mradi tu tunawasamehe ndugu zetu makosa ambayo wametutendea. Hilo ni somo lenye nguvu kama nini! Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.”—Mathayo 6:12.

Tatua Kisababishi cha Tatizo

Yesu alikuwa stadi wa kuelewa utu wa kibinadamu. Alishauri watu watatue kisababishi cha matatizo. Fikiria mifano miwili ifuatayo.

“Ninyi mlisikia kwamba watu wa kale waliambiwa, ‘Usiue; lakini yeyote yule anayeua atatoa hesabu mahakamani,’” Yesu akasema. “Hata hivyo, ninawaambia ninyi kwamba kila mtu anayeendelea kuwa na ghadhabu na ndugu yake atatoa hesabu mahakamani.” (Mathayo 5:21, 22) Hapa Yesu alionyesha kwamba chanzo cha tatizo la kuua kinahusisha mengi zaidi ya tendo hilo la jeuri. Ni mtazamo unaokua ndani ya moyo wa muuaji. Ikiwa watu hawangeruhusu kinyongo au hasira ikue, basi tendo hilo la jeuri lililopangwa kimbele halingekuwako. Umwagaji mwingi wa damu ungeepukwa ikiwa fundisho hilo lingefuatwa.

Ona jinsi Yesu anavyoshughulikia kisababishi cha tatizo lingine ambalo husababisha huzuni nyingi. Aliuambia umati: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake. Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe.” (Mathayo 5:27-29) Yesu alifundisha kwamba tatizo halikuwa tu mwenendo usio wa adili. Tatizo linasababishwa na kitu kinachotangulia mwenendo huo, yaani, tamaa ya mambo yasiyo ya adili. Ikiwa mtu atakataa kufikiria tamaa zisizofaa na ‘kuzing’oa akilini mwake, basi atashinda tatizo la mwenendo usio wa adili.

“Rudisha Upanga Wako Mahali Pake”

Usiku ambao Yesu alisalitiwa na kukamatwa, mmoja wa wanafunzi wake alitoa upanga wake ili kumlinda. Yesu alimwamuru hivi: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Asubuhi iliyofuata, Yesu alimwambia hivi Pontio Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Je, Yesu alikuwa akifundisha jambo lisilo la hekima?

Wakristo wa mapema walikuwa na mtazamo gani kuhusu yale ambayo Yesu alifundisha juu ya kutojihusisha na jeuri? Kitabu The Early Christian Attitude to War kinasema: ‘Kwa kuwa mafundisho ya Yesu yalikataza jeuri na mambo yote ambayo huwaumiza wengine kwa kuwa ni kinyume cha sheria, ni wazi kwamba si halali kwenda vitani. Wakristo wa mapema walitii maneno ya Yesu, nao walielewa kwamba mafundisho yake yalimaanisha kuwa walipaswa kuwa wapole na kujiepusha kihalisi na jeuri. Walihusianisha dini yao na amani; walishutumu vikali vita kwa sababu vilisababisha umwagaji mwingi wa damu.’ Mambo yangekuwa tofauti kama nini ikiwa wale wote waliodai kuwa Wakristo wangefuata fundisho hilo!

Unaweza Kunufaika na Mafundisho Yote ya Yesu

Mafundisho ya Yesu ambayo tumezungumzia ni mazuri, rahisi, na yenye nguvu. Wanadamu wanaweza kunufaika na mafundisho yake ikiwa watayafahamu na kuyatumia. *

Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia uone jinsi unavyoweza kunufaika na mafundisho yenye hekima ambayo hayajawahi kutamkwa na mwanadamu yeyote. Tunakualika kwa uchangamfu uwasiliane nao au uwaandikie ukitumia mojawapo ya anwani zilizo kwenye ukurasa wa 2 wa gazeti hili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 22 Ili ujifunze hatua kwa hatua mafundisho ya Yesu, ona kitabu, Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

“Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mafundisho ya Yesu yanaweza kuwa na uvutano mzuri maishani mwako