Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Mkristo anaweza kumpa mfanyakazi wa serikali bakshishi au zawadi kwa huduma yake, au kufanya hivyo ni kutoa rushwa?

Nyakati zote Wakristo hujiendesha kwa hekima kupatana na desturi za mahali wanapoishi, wakikumbuka kwamba jambo linalokubalika na ambalo ni halali mahali pamoja huenda lisikubalike au hata lisiwe halali kwingineko. (Methali 2:6-9) Bila shaka, Mkristo anapaswa kuzingatia kwamba yeyote anayetaka kuwa “mgeni katika hema” la Yehova anapaswa kujiepusha na rushwa.—Zaburi 15:1, 5; Methali 17:23.

Rushwa ni nini? Kulingana na Kamusi ya Kiswahili Sanifu (Toleo la 1981), “rushwa ni fedha au kitu chochote . . . cha thamani kinachotolewa na kupewa mtu mwenye madaraka ya jambo fulani ili apate kupendelea au kutoa haki au kitu kwa asiyestahiki.” Hivyo, kumpa hakimu au polisi pesa ili apotoshe haki au apuuze kosa au ukiukaji fulani wa sheria ni kutoa rushwa, haidhuru mtu anaishi wapi. Pia ukimpa mtu zawadi ili akufanyie hisani, kama vile kutanguliza jina lako katika orodha ya watu wanaosubiri kuhudumiwa au kumpa zawadi ili akutangulize katika foleni, ni kutoa rushwa. Kufanya hivyo ni kukosa upendo.—Mathayo 7:12; 22:39.

Lakini je, kumpa mtumishi wa umma zawadi au bakshishi ili akuhudumie kwa njia halali au ili kuepuka kuhangaishwa ni kutoa rushwa? Kwa mfano, katika nchi fulani, huenda maofisa fulani wakasita kuwaandikisha watoto katika shule, kumhudumia mgonjwa, au kupiga muhuri vyeti vya usafiri kabla ya kupewa bakshishi. Au huenda wakachelewesha maombi fulani ya kupata leseni au vibali vipya.

Kwa kawaida desturi za kutoa bakshishi na maoni ya watu hutofautiana katika nchi mbalimbali. Mahali ambapo kutoa bakshishi ni jambo la kawaida, huenda Wakristo fulani wakaona kwamba maadamu hawavunji sheria, hawakiuki kanuni za Biblia wanapompa mtumishi wa umma bakshishi ili afanye kazi yake. Katika nchi fulani huenda watu wakaiona bakshishi kuwa zawadi kwa mtumishi wa umma ambaye hupata mshahara wa chini. Kumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kumpa mtu zawadi kwa ajili ya huduma halali na kutoa rushwa ili kufanyiwa jambo lisilo halali.

Kwa upande mwingine, baadhi ya Mashahidi wa Yehova hawatoi bakshishi kwa wakaguzi, maofisa wa forodha au wengineo, wanapofanyiwa utumishi halali hata ikiwa ni kawaida kufanya hivyo. Hiyo ni kwa sababu katika maeneo hayo msimamo wa Mashahidi unajulikana wazi, nao hutambuliwa kwa unyoofu wao na hivyo hupata huduma ambazo wengine hutoa bakshishi ili wafanyiwe.—Methali 10:9; Mathayo 5:16.

Kwa muhtasari, kila mtumishi wa Yehova anapaswa kujiamulia mwenyewe ikiwa atatoa bakshishi kwa huduma halali au kuepuka kuhangaishwa. Zaidi ya yote, anapaswa kujiendesha kwa njia ambayo itamwacha akiwa na dhamiri nzuri, ambayo haitamletea Yehova suto wala kuwakwaza wengine.—Mathayo 6:9; 1 Wakorintho 10:31-33; 2 Wakorintho 6:3; 1 Timotheo 1:5.