Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sayansi na Biblia—Je, Kweli Zinapingana?

Sayansi na Biblia—Je, Kweli Zinapingana?

Sayansi na Biblia—Je, Kweli Zinapingana?

DHANA iliyoanzisha ubishi kati ya Galileo na Kanisa Katoliki ilianza zamani kabla ya Copernicus na Galileo kuzaliwa. Dhana ya kwamba dunia ndiyo kitovu cha ulimwengu ilikubaliwa na Wagiriki wa kale na kusambazwa na mwanafalsafa Aristotle (384-322 K.W.K.) na Ptolemy, mtaalamu wa nyota aliyekuwa pia mnajimu (karne ya pili W.K.). *

Dhana ya Aristotle kuhusu ulimwengu ilitegemea maoni ya mwanahisabati na mwanafalsafa Mgiriki, Pythagoras (karne ya sita K.W.K.). Akifuata maoni ya Pythagoras ya kwamba duara na tufe ni maumbo kamili, Aristotle aliamini kwamba mbingu zina matabaka kama ya kitunguu. Kila tabaka lilifanyizwa kwa fuwele, dunia ikiwa katikati kabisa. Nyota zilizunguka kwenye tabaka la juu, chanzo cha nguvu za kimungu. Aristotle aliamini pia kwamba jua na vitu vingine vya angani vilikuwa kamili, havikuwa na doa au kasoro yoyote wala havingeweza kubadilika.

Nadharia ya Aristotle ilitokana na falsafa wala si sayansi. Kwa maoni yake, wazo la kwamba dunia inazunguka halikupatana na akili. Pia alikataa dhana ya kwamba dunia iko katika nafasi tupu na hivyo aliamini kwamba pasipo na nguvu zinazoisukuma daima, ingepunguza mwendo wake na kuacha kuzunguka kwa sababu ya msuguano. Kwa miaka 2,000 hivi watu waliamini nadharia ya Aristotle kwa kuwa ilionekana kuwa inapatana na akili wakati huo. Hata kufikia karne ya 16, mwanafalsafa Mfaransa Jean Bodin, alisema hivi kuhusu nadharia hiyo: “Hakuna mtu mwenye akili au aliye na ujuzi kidogo wa fizikia, anaweza kufikiri kwamba dunia ambayo ni kubwa na nzito . . . , huyumba-yumba . . . huzunguka katika mhimili wake na kulizunguka jua; kwa kuwa dunia ikisogea kidogo tu, majiji na ngome, miji na milima itaporomoka.”

Kanisa Lakubali Nadharia ya Aristotle

Ubishi mwingine kati ya Galileo na kanisa ulitokea katika karne ya 13 na ulihusisha Mkatoliki maarufu, Thomas Aquinas (1225-1274). Aquinas alimheshimu sana Aristotle, hata alimwita Mwanafalsafa Mkuu. Kwa miaka mitano Aquinas alijitahidi sana kupatanisha falsafa ya Aristotle na mafundisho ya kanisa. Katika kitabu chake (Galileo’s Mistake), Wade Rowland aliandika kwamba kufikia wakati wa Galileo, “mchanganyiko wa nadharia ya Aristotle na mafundisho ya Aquinas ulikuwa fundisho la msingi katika Kanisa Katoliki.” Pia, kumbuka kwamba nyakati hizo hakukuwa na tofauti kati ya wanasayansi na wanadini. Dini ndiyo iliyosimamia elimu. Kwa kawaida dini ndiyo iliyoamua masuala ya kidini na ya kisayansi.

Huo ndio uliokuwa mwanzo wa ubishi kati ya kanisa na Galileo. Hata kabla ya kujihusisha na elimu ya nyota, Galileo alikuwa ameandika makala rasmi kuhusu mwendo. Alitilia shaka dhana nyingi za Aristotle. Hata hivyo, Galileo alifikishwa mbele ya Baraza la Kuhukumu Wazushi mwaka wa 1633 kwa sababu ya kusisitiza kuwa nadharia ya kwamba jua ndilo kitovu cha ulimwengu inapatana na Maandiko.

Alipokuwa akijitetea, Galileo alisisitiza kuwa anaamini kabisa kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho. Pia alisema kwamba Maandiko yaliandikwa kwa ajili ya watu wa kawaida na mistari ya Biblia inayozungumzia kuzunguka kwa jua haipaswi kufasiriwa kihalisi. Hata hivyo, hakufanikiwa. Kwa kuwa Galileo alikataa ufasiri wa Maandiko uliotegemea falsafa za Kigiriki, alihukumiwa! Katika mwaka wa 1992 ndipo Kanisa Katoliki lilipokubali rasmi kuwa lilikosea katika kumhukumu Galileo.

Mambo Tunayoweza Kujifunza

Tunaweza kujifunza nini kutokana na matukio hayo? Kwanza kabisa, Galileo hakuipinga Biblia. Badala yake, alitilia shaka mafundisho ya kanisa. Mwandishi mmoja wa mambo ya kidini aliandika: “Inaonekana kwamba jambo tunaloweza kujifunza kutokana na kisa cha Galileo si kwamba Kanisa lilishikamana sana na kweli za Biblia; bali kwamba halikushikamana nazo vya kutosha.” Kwa kuruhusu falsafa ya Kigiriki iathiri mafundisho yake, kanisa lilifuata mapokeo badala ya mafundisho ya Biblia.

Yote hayo yanatukumbusha onyo hili la Biblia: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Wakolosai 2:8.

Hadi leo hii, Wakristo wengi wanaendelea kushikilia nadharia na falsafa zinazoipinga Biblia. Kwa mfano, wengi wanaiamini nadharia ya mageuzi ya Darwin badala ya masimulizi ya uumbaji katika kitabu cha Mwanzo. Kwa kufanya hivyo, ni kana kwamba makanisa yanamfanya Darwin kuwa Aristotle wa leo na mageuzi kuwa fundisho la msingi la dini. *

Sayansi ya Kweli Inapatana na Biblia

Haimaanishi kwamba hatupaswi kupendezwa na sayansi. Biblia inatutia moyo tujifunze kutokana na uumbaji wa Mungu na kuona sifa zake za ajabu. (Isaya 40:26; Waroma 1:20) Bila shaka, Biblia si kitabu cha sayansi. Badala yake, inafunua viwango vya Mungu, mambo mbalimbali kuhusu utu wake ambayo uumbaji peke yake hauwezi kutufundisha, pamoja na kusudi lake kwa wanadamu. (Zaburi 19:7-11; 2 Timotheo 3:16) Hata hivyo, Biblia inapozungumzia mambo ya asili, nyakati zote huwa sahihi. Galileo mwenyewe alisema: “Maandiko Matakatifu na mambo ya asili yanatokana na Mungu . . . Kweli mbili haziwezi kupingana kamwe.” Fikiria mifano ifuatayo.

Jambo la msingi hata zaidi kuliko mwendo wa nyota na sayari ni kwamba kila kitu ulimwenguni huongozwa na sheria, kama vile nguvu za uvutano. Mbali na Biblia, Pythagoras ndiye mtu wa kwanza kurejelea sheria za asili, naye aliamini kwamba ulimwengu ungeweza kufafanuliwa kwa hesabu. Hatimaye, miaka 2,000 baadaye, Galileo, Kepler, na Newton walithibitisha kwamba kila kitu huongozwa na sheria.

Katika Biblia, sheria ya asili inatajwa katika kitabu cha Ayubu. Karibu mwaka wa 1600 K.W.K., Mungu alimuuliza Ayubu: “Je, umepata kujua sheria za mbingu?” (Ayubu 38:33) Kitabu cha Yeremia kilichoandikwa katika karne ya saba K.W.K., kinamtaja Yehova kuwa Muumba wa “sheria za mwezi na nyota” na “sheria za mbingu na dunia.” (Yeremia 31:35; 33:25) Kuhusiana na taarifa hizo, mchanganuzi wa Biblia G. Rawlinson alisema: “Waandishi wa Biblia na sayansi ya kisasa wanathibitisha kabisa kwamba kuna sheria zinazoongoza ulimwengu.”

Maneno ya Ayubu yaliandikwa miaka 1,000 hivi kabla Pythagoras hajaandika kuhusu sheria zinazoongoza ulimwengu. Kumbuka kwamba kusudi la Biblia si kufundisha mambo ya asili bali ni kutusaidia kuelewa kwamba Yehova ni Muumba wa vitu vyote—ndiye aliyeumba sheria za asili.—Ayubu 38:4, 12; 42:1, 2.

Mfano mwingine tunaoweza kufikiria ni kwamba maji yote duniani hufuata mzunguko unaoitwa mzunguko wa maji. Kwa ufupi, maji ya bahari huwa mvuke na kufanyiza mawingu kisha hunyesha juu ya nchi na hatimaye hurudi baharini. Mbali na Biblia, habari za kale zaidi zinazorejelea mzunguko huo ni za karne ya nne K.W.K. Hata hivyo, Biblia ilizungumzia mzunguko huo mamia ya miaka mapema. Kwa mfano, katika karne ya 11 K.W.K., Mfalme Sulemani wa Israeli aliandika: “Mito yote hutiririkia baharini, lakini bahari kamwe haijai; huko ambako mito hutiririkia ndiko huko inakotoka tena.”—Mhubiri 1:7, Biblia Habari Njema.

Vivyo hivyo, karibu mwaka wa 800 K.W.K., nabii Amosi, aliyekuwa mchungaji na mkulima tu, aliandika kwamba ni Yehova “ambaye anaita maji ya bahari, ili ayamwage kwenye uso wa dunia.” (Amosi 5:8) Bila kutumia maneno magumu, Sulemani na Amosi walifafanua kwa usahihi na kwa njia tofauti mzunguko wa maji.

Biblia pia inasema kwamba Mungu ‘ameitundika dunia pasipo na kitu.’ (Ayubu 26:7) Kupatana na habari zilizojulikana kufikia mwaka wa 1600 K.W.K., wakati ambao maneno hayo yaliandikwa, ingekuwa vigumu sana kwa mtu kusema kwa uhakika kwamba kitu fulani kingeweza kuning’inia katika nafasi tupu pasipo kutegemezwa na chochote. Kama tulivyotaja awali, Aristotle mwenyewe alipinga dhana ya kuwepo kwa nafasi tupu, naye aliishi zaidi ya miaka 1,200 baadaye!

Je, haishangazi kwamba Biblia inataja mambo kwa usahihi sana, hasa unapozingatia kwamba watu wengi walioishi wakati huo walikuwa na maoni tofauti na yasiyo sahihi? Kwa walio wengi, hilo ni mojawapo ya mambo yanayothibitisha kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu. Basi, si jambo la hekima kukengeushwa na mafundisho au nadharia yoyote inayopinga Neno la Mungu. Kama historia inavyoonyesha tena na tena, falsafa za wanadamu hata walioelimika sana hazidumu, lakini “neno la Yehova linadumu milele.”—1 Petro 1:25.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Katika karne ya tatu K.W.K., Mgiriki aliyeitwa Aristarchus kutoka Samos alianzisha nadharia ya kwamba jua ndilo kitovu cha ulimwengu, lakini maoni yake yalikataliwa na yale ya Aristotle yakakubaliwa.

^ fu. 12 Unaweza kupata habari zaidi katika sura ya 15 “Why Do Many Accept Evolution? ya kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Maoni ya Waprotestanti

Viongozi wa Marekebisho Makubwa ya Kidini pia walipinga nadharia ya kwamba jua ndilo kitovu cha ulimwengu. Baadhi yao ni, Martin Luther (1483-1546), Philipp Melanchthon (1497-1560), na John Calvin (1509-1564). Luther alisema hivi kumhusu Copernicus: “Mpumbavu huyu anataka kugeuza sayansi ya nyota.”

Wanaharakati hao walidai kwamba maandiko fulani yalipaswa kueleweka kihalisi, kama vile masimulizi ya Yoshua sura ya 10 yanayotaja kwamba jua na mwezi ‘vilisimama tuli.’ * Kwa nini wanaharakati hao waliamini hivyo? Kitabu kimoja (Galileo’s Mistake) kinaeleza kwamba ingawa Waprotestanti walijitenga na Kanisa Katoliki, walishindwa “kuacha mafundisho” ya Aristotle na Thomas Aquinas, ambayo “yalikubaliwa na Wakatoliki na Waprotestanti vilevile.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 28 Kisayansi si sahihi kusema kwamba jua “huchomoza” na “kutua.” Hata hivyo, katika mazungumzo ya kila siku maneno hayo hukubalika na ni sahihi kupatana na maoni yetu hapa duniani. Vivyo hivyo, Yoshua hakuwa akizungumzia sayansi ya nyota, alikuwa tu akieleza matukio jinsi alivyoyaona.

[Picha]

Luther

Calvin

[Hisani]

▲ From the book Servetus and Calvin, 1877

[Picha katika ukurasa wa 4]

Aristotle

[Hisani]

◀ From the book A General History for Colleges and High Schools, 1900

[Picha katika ukurasa wa 5]

Thomas Aquinas

[Hisani]

From the book Encyclopedia of Religious Knowledge, 1855

[Picha katika ukurasa wa 6]

Isaac Newton

[Picha katika ukurasa wa 7]

Zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Biblia ilizungumzia mzunguko wa maji