Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watoto Wetu Ni Urithi Wenye Thamani

Watoto Wetu Ni Urithi Wenye Thamani

Watoto Wetu Ni Urithi Wenye Thamani

“Tazama! Wana ni urithi kutoka kwa Yehova; uzao wa tumbo ni thawabu.”—ZABURI 127:3.

1. Mtoto wa kwanza wa kibinadamu alitokeaje?

HEBU wazia matukio ya ajabu ambayo Yehova Mungu alifanya yawezekane kwa kumuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza. Adamu na Hawa, waliungana na kuanzisha chembe ambayo ilikua ndani ya tumbo la uzazi la Hawa na kuwa mtu mpya—mtoto wa kwanza wa kibinadamu. (Mwanzo 4:1) Hadi leo hii, kutungwa mimba na kuzaliwa kwa mtoto ni jambo la ajabu ambalo wengi huliita muujiza.

2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba jinsi mtoto anavyokua katika tumbo la mwanamke mjamzito ni muujiza?

2 Kwa siku 270 hivi, yai la mama lililotungishwa mimba, hukua na kuwa mtoto mwenye matrilioni ya chembe. Chembe ya kwanza, ina maagizo yanayohitajiwa ili kufanyiza chembe za aina zaidi ya 200. Chembe hizo za ajabu hufuata maagizo hayo ya ajabu ambayo wanadamu hawawezi kuelewa, na hukua kwa utaratibu sana katika njia inayofaa ili kufanyiza mtu mpya anayeishi!

3. Kwa nini watu wengi wanakubali kwamba Mungu ndiye anayewezesha kuzaliwa kwa mtoto?

3 Unafikiri mtoto huyo ametoka wapi hasa? Bila shaka, ni kwa Yule aliyeuanzisha uhai. Mtunga-zaburi wa Biblia aliimba hivi: “Jueni kwamba Yehova ni Mungu. Yeye ndiye aliyetufanya, wala si sisi wenyewe.” (Zaburi 100:3) Ninyi wazazi, mnajua vizuri kwamba hamkumtokeza mtoto huyo kwa uwezo wenu. Ni Mungu tu mwenye hekima isiyo na kikomo anayeweza kufanya muujiza wa kumuumba mtu. Kwa maelfu ya miaka, watu wengi hawana shaka kwamba mtoto aliye ndani ya tumbo la uzazi la mama yake aliumbwa na Muumba Mtukufu. Vipi wewe?—Zaburi 139:13-16.

4. Ni udhaifu gani walio nao wanadamu ambao Yehova hana?

4 Hata hivyo, je, Yehova ni Muumba tu asiye na hisia ambaye aliwapa wanaume na wanawake uwezo wa kuzaa watoto? Baadhi ya wanadamu hawana hisia, lakini sivyo alivyo Yehova. (Zaburi 78:38-40) Biblia inasema hivi kwenye Zaburi 127:3: “Tazama! Wana [na binti pia] ni urithi kutoka kwa Yehova; uzao wa tumbo ni thawabu.” Urithi ni nini, nao huthibitisha nini? Na tuone.

Urithi na Thawabu

5. Kwa nini watoto ni urithi?

5 Urithi ni kama zawadi. Mara nyingi wazazi hufanya kazi kwa bidii ili kuwaachia watoto wao urithi. Huenda urithi huo ukawa pesa, mali, au kitu fulani kinachothaminiwa sana. Vyovyote vile, urithi ni uthibitisho wa upendo wa wazazi. Biblia inasema kwamba watoto ni urithi ambao Mungu amewapa wazazi. Urithi huo ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Ikiwa wewe ni mzazi, je, matendo yako yanathibitisha kwamba unawaona watoto wako kuwa zawadi ambayo Muumba wa ulimwengu amekukabidhi?

6. Kwa nini Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuzaa watoto?

6 Yehova alipowapa wazazi zawadi hiyo, alikusudia wazao wa Adamu na Hawa waijaze dunia. (Mwanzo 1:27, 28; Isaya 45:18) Yehova hakumuumba mwanadamu mmoja-mmoja kama alivyowaumba mamilioni ya malaika. (Zaburi 104:4; Ufunuo 4:11) Badala yake, Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuzaa watoto ambao wanafanana nao. Ni pendeleo kubwa sana kwa mama na baba kumzaa na kumtunza mtoto! Je, ninyi wazazi, mnamshukuru Yehova kwa kuwakabidhi urithi huo wenye thamani?

Iga Mfano wa Yesu

7. Tofauti na jinsi wazazi fulani hufanya, Yesu alionyeshaje kwamba anawapenda na kuwajali “wana wa binadamu”?

7 Inasikitisha kwamba wazazi fulani hawawaoni watoto wao kuwa zawadi. Wengi hawawajali watoto wao. Wazazi hao hawamwigi Yehova wala Mwana wake. (Zaburi 27:10; Isaya 49:15) Ona mtazamo ambao Yesu alikuwa nao kuwaelekea watoto. Hata kabla ya Yesu kuja duniani—alipokuwa malaika mwenye nguvu huko mbinguni—Biblia inasema kwamba ‘vitu alivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.’ (Methali 8:31) Aliwapenda sana wanadamu hivi kwamba alikuwa tayari kutoa uhai wake ukiwa fidia ili tupate uzima wa milele.—Mathayo 20:28; Yohana 10:18.

8. Yesu aliwawekeaje wazazi mfano mzuri?

8 Alipokuwa duniani, Yesu aliwawekea wazazi mfano mzuri sana. Fikiria alilofanya. Alitumia wakati pamoja na watoto, hata alipokuwa na shughuli nyingi au mfadhaiko. Aliwatazama wakicheza sokoni na katika mafundisho yake alitaja baadhi ya mambo aliyoona wakifanya. (Mathayo 11:16, 17) Wakati wa safari yake ya mwisho kwenda Yerusalemu, Yesu alijua kwamba angeteseka na kuuawa. Kwa hiyo, watu walipowaleta watoto wamwone, wanafunzi wa Yesu, walijaribu kuwazuia wasimkaribie. Labda walifanya hivyo ili Yesu asipate mfadhaiko zaidi. Lakini Yesu aliwakemea wanafunzi wake. Ili kuonyesha kwamba ‘aliwapenda sana’ watoto, alisema hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.”—Marko 10:13, 14.

9. Kwa nini mambo tunayofanya ni muhimu hata kuliko yale tunayosema?

9 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yesu? Watoto wanapotujia, tunatendaje—hata ikiwa tuna shughuli nyingi? Je, tunatenda kama alivyotenda Yesu? Mambo ambayo watoto wanahitaji hasa kutoka kwa wazazi wao ni wakati na usikivu, na Yesu alikuwa tayari kuwapa mambo hayo. Maneno kama vile “nakupenda” ni muhimu. Hata hivyo, matendo huwa na matokeo zaidi kuliko maneno. Upendo wako hautaonekana kupitia mambo unayoyasema tu bali utaonekana hata zaidi kupitia mambo unayofanya. Unaweza kuonyesha kwamba unawapenda watoto wako kwa kutumia wakati pamoja nao, kuwahangaikia, na kuwatunza. Hata hivyo, huenda wazazi wasione mara moja matokeo ya kazi yao hata baada ya kufanya mambo hayo yote. Subira inahitajiwa. Tunaweza kujifunza kuwa na subira kwa kuiga jinsi Yesu alivyowatendea wanafunzi wake.

Subira na Upendo wa Yesu

10. Yesu aliwafundishaje wanafunzi wake unyenyekevu, naye alipata matokeo gani mwanzoni?

10 Yesu alijua kwamba wanafunzi wake walikuwa wakishindana kupata umashuhuri na sifa. Siku moja, baada ya kufika Kapernaumu aliwauliza wanafunzi wake hivi: “‘Mlikuwa mkibishania nini barabarani?’ Wakakaa kimya, kwa maana barabarani walikuwa wamebishana wenyewe, ni nani aliye mkuu zaidi.” Badala ya kuwakemea kwa ukali, Yesu aliwafundisha maana ya unyenyekevu kwa kuwapa mfano. (Marko 9:33-37) Je, alipata matokeo aliyotarajia? Ilichukua muda. Miezi sita baadaye, Yakobo na Yohana walimhimiza mama yao amwombe Yesu awape cheo mashuhuri katika Ufalme. Tena, Yesu akawarekebisha kwa subira.—Mathayo 20:20-28.

11. (a) Mitume walikosa kufanya utumishi gani wa kidesturi baada ya kufika katika chumba cha juu pamoja na Yesu? (b) Yesu alifanya nini, je, jitihada zake zilifanikiwa wakati huo?

11 Punde si punde, wakati wa Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. ukafika, naye Yesu akakutana faraghani na mitume wake ili kuisherehekea. Alipoingia katika chumba cha juu, hakuna hata mmoja kati ya mitume wake 12 aliyejitolea kuwaosha wengine miguu kama ilivyokuwa desturi. Kwa kawaida, hiyo ilionwa kuwa kazi ya hali ya chini iliyofanywa na mtumishi au mwanamke. (1 Samweli 25:41; 1 Timotheo 5:10) Lazima Yesu awe alihuzunika sana kuwaona wanafunzi wake wakiendelea kujitafutia cheo na umashuhuri! Kwa hiyo, Yesu akamwosha kila mmoja wao miguu na kuwasihi wamwige kwa kuwatumikia wengine. (Yohana 13:4-17) Je, walifanya hivyo? Biblia inasema kwamba baadaye jioni hiyohiyo “kukatokea pia bishano kali kati yao juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote.”—Luka 22:24.

12. Wazazi wanawezaje kumwiga Yesu katika jitihada za kuwazoeza watoto wao?

12 Watoto wenu wasipofuata mashauri yenu, je, ninyi wazazi mnaelewa jinsi Yesu alivyohisi? Kumbuka kwamba Yesu aliendelea kuwasaidia mitume wake bila kukata tamaa licha ya kwamba walichukua muda mrefu kurekebisha makosa yao. Mwishowe subira yake ilikuwa na matokeo. (1 Yohana 3:14, 18) Wazazi mnapaswa kuiga upendo na subira ya Yesu. Msikate tamaa kamwe na kuacha kujitahidi kuwazoeza watoto wenu.

13. Kwa nini mzazi hapaswi kumkemea kwa ukali mtoto anapouliza swali?

13 Watoto wanapaswa kuhisi kwamba wazazi wao wanawapenda na kuwajali. Kwa kuwa Yesu alitaka kujua maoni ya wanafunzi wake, aliwasikiliza walipouliza maswali. Aliwauliza maoni yao kuhusu mambo fulani. (Mathayo 17:25-27) Naam, njia bora ya kufundisha inatia ndani kusikiliza kwa makini na kupendezwa kikweli. Mtoto anapouliza swali, mzazi anapaswa kuepuka mwelekeo wowote wa kumfukuza kwa kumkemea kwa ukali na kumwambia: “Ondoka! Huoni nina kazi?” Ikiwa kwa kweli mzazi ana kazi, anapaswa kumwambia mtoto kwamba watazungumzia jambo hilo baadaye. Kisha wazazi wanapaswa kuhakikisha kwamba wanalizungumzia. Akifanya hivyo, mtoto ataona kwamba kwa kweli mzazi anapendezwa naye, na itakuwa rahisi zaidi kwake kumfunulia mzazi yaliyo moyoni mwake.

14. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yesu kuhusu kuwaonyesha watoto wao upendo?

14 Je, inafaa wazazi kuwaonyesha watoto wao upendo kwa kuwakumbatia? Wazazi wanaweza tena kumwiga Yesu kwa kufanya hivyo. Biblia inasema kwamba ‘alichukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.’ (Marko 10:16) Unafikiri watoto walihisije? Bila shaka, walichangamka na kuvutiwa na Yesu! Wazazi, ikiwa kuna upendo wa kweli kati yenu na watoto, watakubali kwa urahisi nidhamu na mafundisho yenu.

Suala la Wakati

15, 16. Ni dhana gani imezuka kuhusu kulea watoto, na huenda imetokana na nini?

15 Watu fulani wanadai kwamba watoto hawahitaji wakati mwingi na upendo kutoka kwa wazazi wao. Dhana fulani imezuka kwamba wazazi wanahitaji tu kuutumia vizuri wakati wanaopata wa kuwa pamoja na watoto wao. Wanaoiunga mkono dhana hiyo wanasema kwamba wazazi hawahitaji kutumia wakati mwingi na watoto wao maadamu wazazi wanafanya matayarisho na mipango mizuri na kuutumia vilivyo wakati wanaopata. Je, unakubaliana na maoni hayo, na je, yanazingatia hali bora ya watoto?

16 Mwandishi mmoja ambaye alikuwa amezungumza na watoto wengi alisema kwamba kile ambacho “watoto wanahitaji sana ni kutumia wakati mwingi pamoja na wazazi wao,” pasipo “vikengeusha fikira.” Profesa mmoja alisema hivi: “Dhana ya kuutumia vizuri wakati imetokana na wazazi wanaohisi kwamba hawatimizi jukumu lao. Watu walikuwa wakitafuta udhuru wa kutumia wakati mchache zaidi na zaidi pamoja na watoto wao.” Wazazi wanapaswa kutumia kiasi gani cha wakati pamoja na watoto wao?

17. Watoto wanahitaji nini kutoka kwa wazazi wao?

17 Biblia haitaji. Hata hivyo, wazazi Waisraeli walihimizwa wazungumze na watoto wao nyumbani mwao, wanapotembea barabarani, wanapolala, na wanapoamka. (Kumbukumbu la Torati 6:7) Ni wazi kwamba wazazi wanapaswa kuzungumza na watoto na kuwafundisha daima kila siku.

18. Yesu alitumiaje kila nafasi kuwafundisha wanafunzi wake, na wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

18 Yesu alifaulu kuwafundisha wanafunzi wake alipokuwa akila pamoja nao, akisafiri pamoja nao, na hata kupumzika pamoja nao. Kwa hiyo, alitumia vizuri kila nafasi aliyopata ili kuwafundisha. (Marko 6:31, 32; Luka 8:1; 22:14) Vivyo hivyo, wazazi Wakristo wanapaswa kuwa tayari kutumia kila nafasi kukuza na kudumisha mawasiliano mazuri kati yao na watoto wao na kuwafundisha njia za Yehova.

Mambo ya Kufundisha na Jinsi ya Kufundisha

19. (a) Mbali na kutumia wakati pamoja na watoto ni nini kingine kinachohitajiwa? (b) Ni mambo gani hasa ambayo wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao?

19 Ili kufanikiwa kuwalea watoto, mengi zaidi yanahitajiwa kuliko tu kutumia wakati pamoja nao na kuwafundisha. Mambo wanayofundishwa ni muhimu pia. Ona jinsi Biblia inavyokazia mambo ambayo watoto wanapaswa kufundishwa. Inasema: ‘Maneno haya ninayokuamuru leo lazima uyakazie kwa mwana wako.’ Ni “maneno” gani hayo ambayo watoto wanapaswa kufundishwa? Haikosi ni maneno haya yaliyotoka tu kutajwa: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5-7) Yesu alisema kwamba hiyo ndiyo amri iliyo kuu kati ya amri zote za Mungu. (Marko 12:28-30) Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao kumhusu Yehova hasa na kuwaeleza ni kwa nini ni yeye peke yake tunayepaswa kumpenda na kufanya mapenzi yake kwa nafsi yote.

20. Mungu aliwaagiza wazazi wa zamani wawafundishe watoto wao nini?

20 Hata hivyo, “maneno” ambayo wazazi wanahimizwa wawafundishe watoto wao yanatia ndani mengi zaidi ya kumpenda Mungu kwa nafsi yao yote. Utaona kwamba katika sura inayotangulia ya kitabu cha Kumbukumbu la Torati, Musa anataja tena zile sheria ambazo Mungu aliandika kwenye mabamba ya mawe—zile Amri Kumi. Sheria hizo zinatia ndani amri kama vile usiseme uwongo, usiibe, usiue, na usifanye uzinzi. (Kumbukumbu la Torati 5:11-22) Kwa hiyo, wazazi wa zamani walikaziwa umuhimu wa kuwafundisha watoto wao maadili mazuri. Wazazi Wakristo leo wanapaswa kuwafundisha vivyo hivyo watoto wao ili wawe na wakati ujao ulio salama, na wenye furaha.

21. Agizo la wazazi ‘kuyakazia’ maneno ya Mungu kwa watoto wao linamaanisha nini?

21 Ona kwamba wazazi wanaelezwa jinsi ya kuwafundisha watoto wao “maneno” au amri hizo: “Lazima uyakazie kwa mwana wako.” Neno linalotafsiriwa ‘-kazia’ linamaanisha “kufundisha na kukazia jambo kwa kurudia-rudia au kuhimiza: kuchochea au kukaza akilini.” Kwa hiyo, ni kana kwamba Mungu anawaambia wazazi wawe na mpango wa kuwafundisha watoto wao Biblia, mpango ambao kusudi lake la pekee ni kukazia mambo ya kiroho katika akili za watoto wao.

22. Wazazi wa Israeli waliambiwa wafanye nini ili kuwafundisha watoto wao, na hilo linamaanisha nini?

22 Wazazi wanahitaji kujitahidi ili kuwa na mpango mzuri wa kuwafundisha watoto wao. Biblia inasema: “Nawe uyafunge [“maneno,” au amri za Mungu] kama ishara kwenye mkono wako, na yawe kama utepe wa kipaji katikati ya macho yako; nawe uyaandike juu ya miimo ya mlango wa nyumba yako na juu ya malango yako.” (Kumbukumbu la Torati 6:8, 9) Hiyo haimaanishi kwamba wazazi wanapaswa kuandika kihalisi sheria za Mungu katika miimo ya milango na malango au kufunga nakala ya sheria hizo kwenye mikono ya watoto wao au katikati ya macho yao. Badala yake, inamaanisha kwamba wazazi wanapaswa kuwakumbusha daima watoto wao mafundisho ya Mungu. Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto kwa ukawaida sana hivi kwamba ni kana kwamba mafundisho ya Mungu yako mbele ya watoto wao nyakati zote.

23. Ni mambo gani yatakayozungumziwa katika funzo la juma lijalo?

23 Ni mambo gani muhimu ambayo wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao? Kwa nini watoto wanapaswa kufundishwa na kuzoezwa kujilinda leo? Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi kuwafundisha watoto wao ifaavyo leo? Maswali hayo pamoja na mengine yanayowahangaisha wazazi wengi yatazungumziwa katika makala inayofuata.

Ungejibuje?

• Kwa nini wazazi wanapaswa kuwaona watoto wao kuwa wenye thamani?

• Wazazi na watu wengine wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yesu?

• Wazazi wanapaswa kutumia kiasi gani cha wakati pamoja na watoto wao?

• Watoto wanapaswa kufundishwa nini, na jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na njia ya Yesu ya kufundisha?

[Picha katika ukurasa wa 11]

Wazazi Waisraeli walipaswa kuwafundisha watoto wao wakati gani na jinsi gani?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wazazi wanapaswa kuweka mafundisho ya Mungu mbele ya watoto wao