Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi, Ulindeni Urithi Wenu Wenye Thamani

Wazazi, Ulindeni Urithi Wenu Wenye Thamani

Wazazi, Ulindeni Urithi Wenu Wenye Thamani

“Hekima ni ulinzi . . . huwahifadhi hai waliyo nayo.”—MHUBIRI 7:12.

1. Kwa nini wazazi wanapaswa kuwaona watoto wao kuwa zawadi?

WAZAZI huzaa watoto wanaofanana nao, wenye sifa na utu kama wao. Biblia inawaita watoto hao “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zaburi 127:3) Kwa kweli Yehova ndiye Mpaji-Uhai, hivyo anawakabidhi wazazi mali yake. (Zaburi 36:9) Wazazi mnaionaje zawadi hiyo yenye thamani kutoka kwa Mungu?

2. Manoa alitendaje alipoambiwa kwamba atapata mtoto?

2 Kwa kweli, zawadi hiyo inapaswa kuthaminiwa sana. Zaidi ya miaka 3,000 iliyopita, Mwisraeli aliyeitwa Manoa alifanya hivyo mke wake alipoambiwa na malaika kwamba atazaa mtoto. Baada ya kusikia habari hizo njema, Manoa alisali hivi: “Nakuomba radhi, Yehova. Tafadhali, yule mtu wa Mungu wa kweli ambaye ulimtuma na arudi kwetu tena, atufundishe yale tunayopaswa kumtendea huyo mtoto atakayezaliwa.” (Waamuzi 13:8) Wazazi, mnaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Manoa?

Kwa Nini Wazazi Wanahitaji Msaada wa Mungu Leo?

3. Kwa nini wazazi wanahitaji msaada wa Mungu katika kulea watoto wao hasa leo?

3 Leo hasa, wazazi wanahitaji msaada wa Yehova katika kuwalea watoto wao. Kwa nini? Shetani Ibilisi na malaika zake wametupwa duniani kutoka mbinguni. Biblia inaonya hivi: “Ole wa dunia . . . kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:7-9, 12) Biblia inasema kwamba Shetani ni “kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Kwa kawaida simba huwinda wanyama walio dhaifu, hasa walio wachanga. Basi, wazazi Wakristo wenye hekima humtegemea Yehova awafundishe jinsi ya kuwalinda watoto wao. Unajitahidi kadiri gani kuwalinda watoto wako?

4. (a) Wazazi wangetendaje ikiwa wangejua kwamba kuna simba anayetembea-tembea mtaani? (b) Watoto wanahitaji nini ili wawe salama?

4 Ikiwa ungejua kwamba kuna simba anayetembea-tembea mtaani, jambo la kwanza ambalo ungefanya ni kuwalinda watoto wako. Shetani ni mwindaji hatari. Yeye hujaribu kuwapotosha watu wa Mungu, na hivyo kuwafanya wakose kibali cha Mungu. (Ayubu 2:1-7; 1 Yohana 5:19) Watoto ni mawindo rahisi. Ili waepuke mitego ya Ibilisi, lazima watoto wamjue na kumtii Yehova. Wanahitaji ujuzi wa Biblia. Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Isitoshe, watoto wanahitaji hekima, yaani, uwezo wa kuelewa na kutumia mambo wanayojifunza. Kwa kuwa “hekima huwahifadhi hai waliyo nayo,” ninyi wazazi mnahitaji kuingiza kweli mioyoni mwa watoto wenu. (Mhubiri 7:12) Mnawezaje kufanya hivyo?

5. (a) Wazazi wanawezaje kuwafundisha watoto wao ili wawe na hekima? (b) Methali inaelezaje thamani ya hekima?

5 Unaweza na unapaswa kuwasomea watoto wako Neno la Mungu. Lakini mengi zaidi yanahitajiwa ili kuwasaidia kumpenda na kumtii Yehova. Wanahitaji uelewaji. Kwa mfano: Mtoto anaweza kuambiwa asivuke barabara kabla ya kuangalia upande wa kushoto na wa kulia. Hata hivyo, watoto fulani hawatii. Kwa nini? Kwa sababu huenda hawakuambiwa tena na tena matokeo ya kugongwa na gari au hawakuelezwa kwa njia ambayo itawasaidia kuelewa vizuri hatari yenyewe na hivyo kuepuka “ujinga” unaoweza kuwafanya wagongwe na gari. Ili kuwafundisha watoto kuwa na hekima, wazazi wanahitaji wakati na subira nyingi. Hata hivyo, hekima ni yenye thamani sana! Biblia inasema, “njia zake ni njia za uzuri, na barabara zake zote ni amani. Ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika sana wataitwa wenye furaha.”—Methali 3:13-18; 22:15.

Njia Bora ya Kuwafundisha Watoto Kuwa na Hekima

6. (a) Kwa nini mara nyingi watoto hutenda kipumbavu? (b) Ni vita gani vinavyoendelea?

6 Mara nyingi watoto hufanya kosa, si kwa sababu hawajafundishwa lililo sawa, bali kwa sababu mafundisho hayo hayajaingia moyoni mwao. Ibilisi anajitahidi sana kuipotosha mioyo ya vijana. Anajaribu kuwanasa kwa kutumia uvutano wa kilimwengu. Pia hujaribu kutumia mielekeo yao yenye dhambi ili kuwashawishi kutenda maovu. (Mwanzo 8:21; Zaburi 51:5) Wazazi wanapaswa kutambua kwamba kuna vita vikali vya kuipotosha mioyo ya watoto wao.

7. Kwa nini haitoshi tu kumwambia mtoto yaliyo mema au mabaya?

7 Kwa kawaida wazazi humwambia mtoto yaliyo mema na mabaya, wakiamini kwamba wamemfundisha kanuni fulani ya maadili. Huenda wakamwambia mtoto kwamba ni kosa kusema uwongo, kuiba, au kufanya ngono na mtu yeyote ambaye si mwenzi wake wa ndoa. Hata hivyo, kuambiwa tu na wazazi wake jambo la kufanya hakutoshi kumchochea mtoto kutii. Hizo ni sheria za Yehova. Mtoto anapaswa kujua kwamba ni jambo la hekima kutii amri za Mungu.—Methali 6:16-19; Waebrania 13:4.

8. Ni njia gani ya kufundisha inayoweza kuwasaidia watoto watende kwa hekima?

8 Mtoto anaweza kusaidiwa kuelewa kuwapo kwa Muumba mwenye hekima kutokana na mambo kama vile maajabu ya ulimwengu, aina mbalimbali za viumbe, na mabadiliko ya majira. (Waroma 1:20; Waebrania 3:4) Isitoshe, mtoto anapaswa kufundishwa kwamba Mungu anampenda na amefanya mpango wa kumpa uzima wa milele kupitia dhabihu ya Mwana Wake na kwamba anaweza kumfurahisha Mungu kwa kumtii. Huenda kufanya hivyo kutamchochea mtoto aamue kumtumikia Yehova zijapokuwa jitihada za Ibilisi za kujaribu kumzuia.—Methali 22:6; 27:11; Yohana 3:16.

9. (a) Ni ufundishaji gani unaookoa uhai? (b) Akina baba wanaagizwa wafanye nini, na hilo linatia ndani nini?

9 Ili kumpa mtoto mafundisho yanayomlinda na kumchochea kufanya yaliyo sawa, mzazi anahitaji kutumia wakati, kuwa msikivu, na kufanya mipango mizuri. Wazazi wanapaswa kukubali mwongozo wa Mungu. Biblia inasema: “Nanyi, akina baba, . . . endeleeni kuwalea [watoto wenu] katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Hilo linamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mwongozo wa akilini” linatoa wazo la “kuingiza akili [nyingine] ndani ya.” Kwa hiyo, akina baba wanahimizwa waingize akili ya Yehova ndani ya watoto wao. Huo utakuwa ulinzi ulioje! Ikiwa maoni ya Mungu na njia yake ya kufikiri itakaziwa katika akili za watoto, watalindwa wasipatwe na mabaya.

Tamaa Inayochochewa na Upendo

10. Ili kumfundisha mtoto wako ifaavyo, ni muhimu kujua nini?

10 Hata hivyo, ili ufanikiwe kumlea mtoto wako kwa njia inayofaa, unapaswa kuchochewa na upendo. Mojawapo ya mambo muhimu ni kuwa na mawasiliano mazuri. Mwelewe mtoto wako na ujue maoni yake. Mchochee kwa busara mtoto wako ajieleze katika hali yenye kustarehesha. Wakati mwingine huenda ukashangaa kusikia anayosema. Dhibiti hisia zako. Msikilize kwa makini.

11. Mzazi anawezaje kuingiza akili ya Mungu ndani ya mtoto?

11 Ni kweli kwamba huenda umemsomea mtoto wako sheria za Mungu zinazokataza uasherati katika Biblia. Huenda hata umefanya hivyo mara kadhaa. (1 Wakorintho 6:18; Waefeso 5:5) Huenda watoto wako wanaelewa mambo yanayompendeza Yehova na yale yasiyompendeza. Hata hivyo, unahitaji kufanya mengi zaidi ili kuingiza akili ya Yehova ndani ya mtoto. Watoto wanahitaji kusaidiwa ili wajue umuhimu wa sheria za Yehova. Wanahitaji kusadikishwa kwamba sheria zake ni nzuri na zenye manufaa na kwamba wanapaswa kuzitii. Unapowafundisha watoto wako, wasaidie waelewe sababu za Kimaandiko na kukubali maoni ya Mungu. Ukifanya hivyo, basi utakuwa ukiingiza akili ya Yehova ndani yao.

12. Mzazi anawezaje kumsaidia mtoto wake awe na maoni yanayofaa kuhusu ngono?

12 Unapozungumza kuhusu ngono, unaweza kumuuliza, “Je, unafikiri kutii sheria ya Mungu inayokataza kufanya ngono kabla ya ndoa kunamnyima mtu furaha?” Mtie moyo mtoto wako afafanue jibu lake. Baada ya kuzungumzia utaratibu wa Mungu wa kutokeza mtoto, unaweza kumuuliza: “Je, unafikiri Mungu wetu mwenye upendo angetunga sheria ili kutuzuia tusifurahie maisha? Au unafikiri sheria hizo zimekusudiwa kutufanya tuwe na furaha na kutulinda?” (Zaburi 119:1, 2; Isaya 48:17) Jitahidi kujua maoni ya mtoto wako kuhusu jambo hilo. Kisha unaweza kumsimulia mifano inayoonyesha jinsi mwenendo mpotovu katika ngono umesababisha maumivu na matatizo. (2 Samweli 13:1-33) Kwa kumsaidia mtoto wako aelewe na kukubali maoni ya Mungu, utakuwa umejitahidi sana kuingiza akili ya Mungu ndani yake. Hata hivyo, kuna jambo lingine unaloweza kufanya.

13. Mtoto anaweza kuchochewa kumtii Yehova akielewa nini hasa?

13 Mbali na kumfundisha mtoto wako matokeo mabaya ya kutomtii Yehova, ni jambo la hekima kumweleza jinsi Yehova anavyohisi kuhusu mwenendo wetu maishani. Mwonyeshe mtoto wako katika Biblia kwamba tunaweza kumtia Yehova uchungu tusipofanya mapenzi yake. (Zaburi 78:41) Huenda ukamuuliza, “Kwa nini hungependa kumtia Yehova uchungu?” Kisha mweleze: “Adui ya Mungu, Shetani anadai kwamba tunamtumikia Mungu kwa sababu ya ubinafsi wala si kwa sababu tunampenda.” Kisha mweleze jinsi Ayubu alivyomfurahisha Yehova kwa kuwa mwaminifu na hivyo kupinga mashtaka ya uwongo ya Shetani. (Ayubu 1:9-11; 27:5) Mtoto wako anahitaji kuelewa kwamba mwenendo wake unaweza kumfurahisha Yehova au kumhuzunisha. (Methali 27:11) Watoto wanaweza kufundishwa mambo hayo muhimu na mengine mengi kwa kutumia kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. *

Matokeo Yenye Kuridhisha

14, 15. (a) Ni mambo gani yaliyo katika kitabu Mwalimu ambayo yamewachochea watoto? (b) Umepata matokeo gani mazuri kwa kutumia kitabu hicho? (Pia ona sanduku kwenye ukurasa wa 18-19.)

14 Babu mmoja huko Kroatia ambaye humsomea mjukuu wake mwenye umri wa miaka saba kitabu Mwalimu, anasema kwamba mtoto huyo alimwambia yafuatayo: “Mama aliniambia nifanye jambo fulani, lakini sikutaka kulifanya. Kisha nikakumbuka sura yenye kichwa ‘Utii Unakulinda Wewe,’ na hivyo nikarudi na kumwambia kwamba nitamtii.” Kuhusu ile sura yenye kichwa “Kwa Nini Hatupaswi Kusema Uwongo,” wenzi fulani wa ndoa huko Florida, Marekani walisema hivi: “Ina maswali yanayowachochea watoto waeleze yaliyo moyoni mwao na kukubali makosa ambayo huenda hawangeyakubali.”

15 Kitabu Mwalimu kina picha zaidi ya 230, pia kuna maelezo, au ufafanuzi, kwenye kila picha au picha kadhaa. Mama mmoja anayethamini kitabu hicho alisema: “Mara nyingi mwana wangu akiona picha huiangalia kwa muda mrefu na hataki ukurasa mwingine ufunguliwe. Mbali na kuvutia, picha hizo hufundisha na kuwachochea watoto waulize maswali. Mwanangu alipoona ile picha inayoonyesha mtoto akitazama televisheni kwenye chumba chenye giza, aliuliza, ‘Mama, huyu mvulana anafanya nini?’ kwa sauti inayoonyesha kwamba anaelewa kuna tatizo.” Kando ya picha hiyo kuna swali: “Ni nani anayeweza kuona kila kitu tunachofanya?”

Elimu Muhimu Leo

16. Ni jambo gani muhimu ambalo watoto wanapaswa kufundishwa leo na kwa nini?

16 Watoto wanapaswa kujua matumizi yanayofaa na yasiyofaa ya viungo vyao vya siri. Hata hivyo, kuzungumzia mambo hayo si rahisi. Mwandishi wa gazeti moja alisema kwamba alipokuwa mchanga ilikuwa mwiko kutaja viungo vya uzazi. Aliandika hivi kuhusu kuwafundisha watoto wake: “Lazima nishinde aibu yangu.” Kwa kweli, wazazi wanapoepuka kuzungumzia masuala ya ngono kwa sababu ya aibu, hawawalindi watoto wao. Watu wanaowatendea vibaya kingono watoto hutumia kwa faida yao kutojua kwa watoto. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu huzungumzia mambo hayo kwa staha na heshima. Kuwajulisha watoto juu ya ngono hakutawafanya wajiingize katika mambo hayo bali kunaweza kuwalinda na kuwaepusha na hatari.

17. Kitabu Mwalimu kinawasaidiaje wazazi kuwafundisha watoto wao mambo yanayohusu ngono?

17 Mnapozungumzia sura ya 10 kuhusu malaika waovu waliokuja duniani na kuzaa watoto, kuna swali ambalo mtoto anatakiwa ajibu, “Ngono ni nini?” Kitabu Mwalimu kinajibu kwa njia rahisi na yenye heshima. Baadaye, sura ya 32 inaeleza jinsi watoto wanavyoweza kulindwa kutokana na watu wanaotaka kuwatendea vibaya kingono. Watu wengi wameandika barua kusema kwamba mafundisho hayo ni muhimu. Mama mmoja aliandika: “Mwanangu Javan alipoenda kumwona daktari juma lililopita, daktari huyo aliniuliza ikiwa tumezungumza naye kuhusu matumizi yanayofaa ya viungo vya uzazi. Alifurahi sana kujua kwamba tulifanya hivyo tukitumia kitabu chetu kipya.”

18. Kitabu Mwalimu kinasema nini kuhusu kuheshimu nembo za kitaifa?

18 Sura nyingine inazungumzia masimulizi ya Biblia ya wale vijana watatu Waebrania, Shadraka, Meshaki, na Abednego ambao walikataa kuiinamia sanamu iliyowakilisha Serikali ya Babiloni. (Danieli 3:1-30) Huenda wengine wasione uhusiano kati ya kuabudu sanamu na kuisalimu bendera, kama kitabu Mwalimu kinavyosema. Hata hivyo, fikiria alivyosema mhariri Edward Gaffney, katika gazeti la U.S. Catholic. Alitaja kwamba binti yake alipomwambia amejifunza “sala mpya shuleni” siku ya kwanza, alimwomba amkaririe. Gaffney asema: “Aliuweka mkono wake kifuani na kusema hivi kwa fahari, ‘Naapa kwamba nitakuwa mwaminifu kwa bendera . . . ’” Mhariri huyo aendelea kusema: “Papo hapo nikaelewa. Mashahidi wa Yehova hawakuwa wamekosea. Tangu wakiwa na umri mchanga, watoto wanafundishwa kuabudu na kuwa waaminifu kabisa kwa taifa.”

Fanya Yote Uwezayo

19. Kuwafundisha watoto huleta thawabu gani?

19 Kwa kweli, unapaswa kufanya yote uwezayo ili kuwafundisha watoto wako. Mama mmoja huko Kansas, Marekani, alitokwa na machozi baada ya kupokea barua kutoka kwa mwanaye. Aliandika hivi: “Nafurahi sana kwamba malezi yangu yamenisaidia kuwa mtulivu na mwenye usawaziko. Bila shaka, wewe na Baba mnastahili pongezi.” (Methali 31:28) Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kinaweza kuwasaidia wazazi wengi zaidi waulinde urithi wao wenye thamani kwa kuwafundisha watoto wao.

20. Wazazi wanapaswa kukumbuka nini sikuzote, na hilo linapaswa kuwa na matokeo gani kwao?

20 Watoto wetu wanastahili wakati, usikivu, na jitihada zote tunazoweza kutoa. Hawatakuwa watoto milele. Tumia vizuri kila nafasi ili kuwa nao na kuwasaidia. Hutajuta kamwe kwa kufanya hivyo. Watakupenda sana. Kumbuka sikuzote kwamba watoto wako ni zawadi kutoka kwa Mungu. Nao ni urithi wenye thamani sana! (Zaburi 127:3-5) Kwa hiyo, watunze kana kwamba Mungu atakutoza hesabu, kwa kuwa kwa kweli, una wajibu mbele za Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Ona sura ya 40, yenye kichwa, “Jinsi ya Kumfurahisha Mungu.”

Ungejibuje?

• Kwa nini wazazi wanapaswa kuwalinda watoto wao leo hasa?

• Ni njia gani ya kufundisha inayoweza kuwafanya watoto wawe na hekima?

• Ni mambo gani muhimu ambayo unapaswa kuzungumzia pamoja na watoto wako leo?

• Kitabu Mwalimu kimewasaidiaje wazazi kuwafundisha watoto wao?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18, 19]

Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote

Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu kimekusudiwa kuwasaidia wazazi au watu wengine wazima wasome na kuzungumzia mafundisho ya Yesu Kristo pamoja na watoto. Hata hivyo, watu wazima ambao wamesoma kitabu hicho wametoa shukrani zao kwa yale ambayo wamejifunza.

Mwanamume mmoja huko Texas, Marekani, alisema: “Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu ni rahisi na chenye kuvutia, kinachochea watu wa umri mbalimbali, hata walio na umri wa miaka 76, kama mimi. Asanteni sana. Kutoka kwa mtu ambaye amemtumikia Yehova tangu utotoni.”

Mtu mmoja huko London, Uingereza ambaye alikisoma alisema: “Hapana shaka kwamba picha zake maridadi zinawavutia wazazi na watoto vilevile. Maswali yamepangwa vizuri sana, kinapendeza pia kwa kuwa kinazungumzia masuala muhimu sana, kama inavyoonyeshwa katika sura ya 32, yenye kichwa ‘Jinsi Yesu Alivyolindwa.’” Anamalizia hivi: “Ingawa kitabu hiki kimekusudiwa hasa watoto wa Mashahidi wa Yehova, nafikiri walimu na watu wengine pia watafurahi sana kuwa nacho. Natazamia kukitumia sasa na wakati ujao.”

Mwanamke mmoja huko Massachusetts, Marekani, alivutiwa na picha zake nyingi “zilizofikiriwa vizuri.” Aliandika: “Ingawa kitabu hicho kimekusudiwa watoto, nimeona kwamba mambo kinayozungumzia yanaweza pia kutusaidia sisi watu wazima kufikiria uhusiano wetu pamoja na Yehova.”

Mwanamke mmoja huko Maine, Marekani, alisema hivi kwa furaha: “Lo! Ni kitabu kizuri wee! Si cha watoto tu bali chetu sote tukiwa watoto wa Mungu. Kimenigusa moyo sana, kimechochea hisia zangu na kunituliza na sasa nina amani. Nahisi kuwa karibu sana na Yehova kama Baba yangu. Ameniondolea maumivu mengi ambayo nimekuwa nayo kwa miaka mingi na nimeelewa kusudi lake vizuri zaidi.” Alimalizia hivi: “Namwambia kila mtu, ‘Tafadhali kisome.’”

Mwanamke mmoja huko Kyoto, Japani, alisema kwamba alipokuwa akiwasomea wajukuu wake, waliuliza maswali kama: “‘Mvulana huyu anafanya nini? Kwa nini msichana huyu anagombezwa? Huyu mama anafanya nini? Na huyu simba je?’ Kitabu hicho kinafundisha mambo tunayopenda, kwa hiyo nakipenda sana kuliko kitabu kingine chochote katika maktaba.”

Baba mmoja huko Calgary, Kanada, alisema kwamba mara tu alipokipokea kitabu hicho, alianza kumsomea binti yake wa miaka sita na mwana wake wa miaka tisa. Anasema: “Matokeo yalikuwa mazuri sana. Watoto wangu walikuwa wakisikiliza kwa makini na kujibu maswali kutoka moyoni. Walishiriki funzo na walikuwa na nafasi ya kujieleza. Wamesisimuka sana, na binti yangu anasema kwamba anataka kujifunza kitabu hicho kipya kila jioni.”

Siku moja baada ya kujifunza, baba huyo alisema: “Nilizungumza na mwanangu kwa saa nyingi sana kumhusu Yehova na makusudi yake. Alikuwa na maswali mengi sana kutokana na kitabu hicho. Nilitokwa na machozi aliponiaga kabla ya kulala na kuniuliza: ‘Baba, tutasoma lini tena? Nina maswali mengi sana, na ninataka kujua kila kitu kumhusu Yehova.’”

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wazazi, mnaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Manoa?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Watoto, mnaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa wale Waebrania watatu?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Picha na maelezo katika kitabu “Mwalimu” yana mafunzo muhimu

Anania anamdanganya Petro kuhusu nini?

Ni nani anayeweza kuona kila kitu tunachofanya?