Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha Neno la Mungu Liangaze Barabara Yako

Acha Neno la Mungu Liangaze Barabara Yako

Acha Neno la Mungu Liangaze Barabara Yako

“Neno lako ni . . . nuru kwa barabara yangu.”—ZABURI 119:105.

1, 2. Ni katika hali gani neno la Yehova litaangaza barabara yetu?

NENO la Yehova litaangaza barabara yetu tukiliruhusu lifanye hivyo. Ili kunufaika na nuru hiyo ya kiroho, lazima tujifunze kwa bidii na kufuata shauri la Neno la Mungu lililoandikwa. Hilo tu ndilo litakalotuwezesha kuwa na hisia kama hizi za mtunga-zaburi: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.”—Zaburi 119:105.

2 Sasa tuzungumzie Zaburi 119:89-176. Mistari hiyo ina habari nyingi sana zilizopangwa katika beti 11, nayo inaweza kutusaidia kudumu katika barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Mathayo 7:13, 14.

Kwa Nini Ulipende Neno la Mungu?

3. Zaburi 119:89, 90 inaonyeshaje kwamba tunaweza kulitegemea neno la Mungu?

3 Tukilipenda neno la Yehova tutakuwa imara kiroho. (Zaburi 119:89-96) Mtunga-zaburi aliimba: “Mpaka wakati usio na kipimo, Ee Yehova, neno lako limesimama mbinguni. . . . Umeiweka dunia imara, ili ipate kuendelea kusimama.” (Zaburi 119:89, 90) Kwa neno la Mungu, yaani, ‘sheria zake za mbingu,’ jua, mwezi, na nyota husonga katika mizunguko yake pasipo kugongana, nayo dunia imewekwa imara milele. (Ayubu 38:31-33; Zaburi 104:5) Tunaweza kulitegemea kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova kwa sababu kila asemalo “hakika litafanikiwa” katika kutimizwa kwa kusudi lake.—Isaya 55:8-11.

4. Kulipenda neno la Mungu huwasaidiaje watumishi wake wanaoteseka?

4 Mtunga-zaburi ‘angaliangamia katika mateso yake kama asingaliipenda sheria ya Mungu.’ (Zaburi 119:92) Hakuteswa na wageni, bali aliteswa na Waisraeli wenye kuvunja sheria ambao walimchukia. (Mambo ya Walawi 19:17) Lakini hilo halikumfadhaisha, kwa kuwa aliipenda sheria ya Mungu iliyomtegemeza. Huko Korintho, mtume Paulo alikuwa “katika hatari za katikati ya ndugu wa uwongo,” ambao labda walitia ndani wale ‘mitume walio bora sana’ waliotafuta jambo ili wamshtaki. (2 Wakorintho 11:5, 12-14, 26) Lakini Paulo alinusurika kiroho kwa sababu alilipenda neno la Mungu. Kwa kuwa sisi tunalipenda Neno la Yehova lililoandikwa na tunafuata vile linavyosema, tunawapenda ndugu zetu. (1 Yohana 3:15) Hata chuki ya ulimwengu haiwezi kufanya tusahau agizo lolote la Mungu. Tunaendelea kufanya mapenzi yake kwa umoja na kwa upendo pamoja na ndugu zetu, huku tukingojea kumtumikia Yehova milele na kwa shangwe.—Zaburi 119:93.

5. Mfalme Asa alimtafutaje Yehova?

5 Ili kuonyesha kwamba tumejitoa kwa Yehova, huenda tukasali hivi: “Mimi ni wako. Uniokoe, kwa sababu nimeyatafuta maagizo yako.” (Zaburi 119:94) Mfalme Asa alimtafuta Mungu na kuondolea mbali uasi-imani huko Yuda. Kwenye kusanyiko moja kubwa katika mwaka wa 15 wa utawala wake (963 K.W.K.), wakaaji wa Yuda ‘waliingia katika agano ili kumtafuta Yehova.’ Mungu “aliwaruhusu wampate,” naye “akaendelea kuwapa pumziko kuzunguka pande zote.” (2 Mambo ya Nyakati 15:10-15) Mfano huo wapaswa kumtia moyo yeyote ambaye amekengeuka na kuliacha kutaniko la Kikristo amtafute Mungu tena. Yeye atawabariki na kuwalinda wale ambao wanaanza tena kushirikiana na watu wake.

6. Ni hatua gani itakayotulinda tusipate madhara ya kiroho?

6 Neno la Yehova hutupa hekima inayoweza kutulinda tusipate madhara ya kiroho. (Zaburi 119:97-104) Amri za Mungu hutufanya tuwe wenye hekima zaidi ya adui zetu. Kufuata vikumbusho vyake hutupa ufahamu, na ‘kushika maagizo yake hutuwezesha kujiendesha kwa uelewaji mwingi kuliko wanaume wazee.’ (Zaburi 119:98-100) Ikiwa maneno ya Yehova ni ‘laini katika kaakaa yetu kuliko asali kinywani mwetu,’ tutachukia na kuepuka “kila njia ya uwongo.” (Zaburi 119:103, 104) Jambo hilo litatulinda tusipate madhara ya kiroho tunapokutana na watu wenye kiburi, wakatili, na wasiomwogopa Mungu katika siku hizi za mwisho.—2 Timotheo 3:1-5.

Taa ya Miguu Yetu

7, 8. Kupatana na Zaburi 119:105, tunahitaji kufanya nini?

7 Neno la Mungu ni chanzo cha nuru ya kiroho yenye kutegemeka. (Zaburi 119:105-112) Tuwe Wakristo waliotiwa mafuta au “kondoo wengine,” tunatangaza hivi: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.” (Yohana 10:16; Zaburi 119:105) Neno la Mungu ni kama taa inayoangaza njia yetu, ili tusijikwae na kuanguka kiroho. (Methali 6:23) Hata hivyo, lazima kila mmoja aruhusu neno la Yehova liwe taa kwa miguu yake.

8 Tunahitaji kuwa imara kama mtungaji wa Zaburi ya 119. Aliazimia kutoondoka katika maagizo ya Mungu. Alisema: “Nimetoa ahadi yenye kiapo, nami nitaitimiza, kuyashika maamuzi yako [ya Yehova] ya hukumu ya uadilifu.” (Zaburi 119:106) Hatupaswi kamwe kupuuza manufaa ya kujifunza Biblia kwa ukawaida na kushiriki kwenye mikutano ya Kikristo.

9, 10. Tunajuaje kwamba watu waliojiweka wakfu kwa Yehova wanaweza ‘kuondoka katika maagizo yake,’ na tunawezaje kuepuka jambo hilo?

9 Mtunga-zaburi ‘hakuondoka katika maagizo ya Mungu,’ lakini hata mtu aliyejiweka wakfu kwa Yehova anaweza kufanya hivyo. (Zaburi 119:110) Mfalme Sulemani aliondoka katika maagizo ya Mungu, ingawa mwanzoni alitenda kupatana na hekima aliyopewa na Mungu na alikuwa raia wa taifa lililowekwa wakfu kwa Yehova. “Wake wa kigeni walimfanya hata yeye atende dhambi” walipomshawishi aabudu miungu ya uwongo.—Nehemia 13:26; 1 Wafalme 11:1-6.

10 Shetani ni “mwindaji wa ndege,” naye hutega mitego mingi. (Zaburi 91:3) Kwa mfano, mtu aliyeacha kumwabudu Yehova anaweza kutushawishi tuondoke katika njia yenye nuru ya kiroho na kuingia katika giza la uasi-imani. Kati ya Wakristo wa Thiatira, kulikuwa na “yule mwanamke Yezebeli,” ambaye yaelekea alifananisha kikundi cha wanawake waliowafundisha wengine kuabudu sanamu na kufanya uasherati. Yesu hakuvumilia maovu hayo, nasi hatupaswi kuyavumilia. (Ufunuo 2:18-22; Yuda 3, 4) Kwa hiyo, na tumwombe Yehova msaada ili tusiondoke katika maagizo yake bali tudumu katika nuru yake.—Zaburi 119:111, 112.

Neno la Mungu Hututegemeza

11. Kulingana na Zaburi 119:119, Mungu huwaonaje waovu?

11 Mungu atatutegemeza tusipoondoka katika masharti yake. (Zaburi 119:113-120) Sisi hatupendezwi na watu “wenye moyo nusu nusu,” kama vile Yesu asivyopendezwa na watu walio vuguvugu wanaojidai kuwa Wakristo leo. (Zaburi 119:113; Ufunuo 3:16) Kwa kuwa tunamtumikia Yehova kwa moyo wote, yeye ni ‘mahali petu pa kujificha’ naye atatutegemeza. ‘Atawarusha mbali wale wote wanaoondoka katika masharti yake’ wanapoanza kutumia ujanja na uwongo. (Zaburi 119:114, 117, 118; Methali 3:32) Yeye huwaona waovu hao kama “takataka,” yaani, uchafu unaoondolewa kwenye vyuma vyenye thamani kama vile fedha na dhahabu. (Zaburi 119:119; Methali 17:3) Tunapaswa kuvipenda vikumbusho vya Mungu sikuzote, kwa kuwa hatungependa kuharibiwa na kutupwa kama takataka pamoja na waovu.

12. Kwa nini ni muhimu kumwogopa Yehova?

12 Mtunga-zaburi alisema, “Mwili wangu umetetemeka kwa sababu ya kukuhofu [wewe Yehova].” (Zaburi 119:120) Ili Mungu atutegemeze tukiwa watumishi wake, ni muhimu kuwa na hofu inayofaa kumwelekea, ambayo inaonyeshwa kwa kuepuka mambo anayokataa. Ayubu alikuwa mwadilifu katika maisha yake kwa sababu alimwogopa na kumheshimu Mungu. (Ayubu 1:1; 23:15) Kumwogopa Mungu kunaweza kutusaidia tuendelee kufanya yale yanayompendeza licha ya hali ambazo ni lazima tuvumilie. Hata hivyo, tunahitaji kusali kwa bidii na kwa imani ili tuvumilie.—Yakobo 5:15.

Sali kwa Imani

13-15. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba sala zetu zitajibiwa? (b) Ni nini kinachoweza kutukia ikiwa hatujui la kusema katika sala? (c) Onyesha jinsi Zaburi 119:121-128 inavyoweza kuwakilisha ‘kuugua kwetu kusikotamkwa’ katika sala.

13 Tunaweza kusali tukiwa na uhakika kwamba Mungu atatusaidia. (Zaburi 119:121-128) Kama mtunga-zaburi tuna uhakika kwamba sala zetu zitajibiwa. Kwa nini? Kwa sababu tunazipenda amri za Mungu “kuliko dhahabu, naam, dhahabu safi.” Isitoshe, ‘tunayaona maagizo yote ya Mungu juu ya mambo yote kuwa ni sawa.’—Zaburi 119:127, 128.

14 Yehova husikiliza maombi yetu kwa sababu sisi husali kwa imani na pia hufuata kwa makini maagizo yake. (Zaburi 65:2) Lakini, vipi ikiwa nyakati nyingine matatizo yetu ni tata sana hivi kwamba hatujui la kusema katika sala? Basi, “roho yenyewe hutuombea pamoja na kuugua kusikotamkwa.” (Waroma 8:26, 27) Nyakati hizo, Mungu hukubali maneno yaliyo katika Neno lake yawakilishe yale ambayo tungesema.

15 Katika Maandiko, kuna sala na mawazo mengi yanayoweza kuwakilisha ‘kuugua kwetu kusikotamkwa.’ Kwa mfano, fikiria Zaburi 119:121-128. Huenda mambo yanayotajwa katika mistari hiyo yakafanana na hali zetu. Kwa mfano, ikiwa tunaogopa kupunjwa, huenda kama mtunga-zaburi tukamwomba Mungu atusaidie. (Mstari wa 121-123) Tuseme tunataka kufanya uamuzi mgumu. Basi huenda tukasali ili roho ya Yehova itusaidie kukumbuka na kutumia vikumbusho vyake. (Mstari wa 124, 125) Ingawa ‘tunaichukia kila njia ya uwongo,’ huenda tukahitaji kumwomba Mungu atusaidie ili tusishindwe na kishawishi fulani na kuvunja sheria yake. (Mstari 126-128) Tukiisoma Biblia kila siku, huenda tukakumbuka mistari inayofaa kama hiyo tunaposali kwa Yehova.

Vikumbusho vya Yehova Hutusaidia

16, 17. (a) Kwa nini tunahitaji vikumbusho vya Mungu, nasi tuvioneje? (b) Huenda wengine wakatuonaje, lakini ni jambo gani la maana hasa?

16 Ili sala zetu zisikilizwe na tukubaliwe na Mungu, ni lazima tusikilize vikumbusho vyake. (Zaburi 119:129-136) Kwa kuwa sisi ni wasahaulifu, tunahitaji vikumbusho vya Yehova ambavyo hutukumbusha maagizo na amri zake. Bila shaka, tunashukuru kwa ajili ya nuru ya kiroho inayotokana na uelewaji mpya wa maneno ya Mungu. (Zaburi 119:129, 130) Pia, tunashukuru kwamba Yehova ‘ametuangazia uso wake’ kwa kutukubali, ingawa ‘vijito vya maji vinatiririka kutoka machoni petu’ kwa sababu wengine wanavunja sheria yake.—Zaburi 119:135, 136; Hesabu 6:25.

17 Tuna uhakika kwamba Mungu ataendelea kutuonyesha kibali tukifuata vikumbusho vyake vya uadilifu. (Zaburi 119:137-144) Tukiwa watumishi wa Yehova, tunakubali kwamba yeye ana haki ya kutupa vikumbusho vyake vya uadilifu vikiwa sheria anazotarajia tuzitii. (Zaburi 119:138) Kwa kuwa mtunga-zaburi alitii amri za Mungu, kwa nini alisema: “Mimi ni mnyonge na wa kudharaulika”? (Zaburi 119:141) Yaelekea alikuwa akizungumzia jinsi adui zake walivyomwona. Huenda wengine wakatudharau tukidumisha msimamo imara kuhusiana na uadilifu. Lakini jambo la maana hasa ni kwamba Yehova hutukubali kwa sababu tunaishi kupatana na vikumbusho vyake vya uadilifu.

Tuko Salama na Wenye Amani

18, 19. Tunapata matokeo gani tunaposhika vikumbusho vya Mungu?

18 Kushika vikumbusho vya Mungu hutusaidia kuwa na uhusiano wa karibu naye. (Zaburi 119:145-152) Kwa kuwa tunazingatia vikumbusho vya Yehova, tunajihisi huru kusali kwake kwa moyo wote, tukitarajia kwamba atatusikiliza. Huenda tukaamka “mapema wakati wa mapambazuko ya asubuhi” na kulilia msaada. Huo ni wakati mzuri kama nini wa kusali! (Zaburi 119:145-147) Mungu yu karibu nasi kwa sababu sisi huepuka mwenendo mpotovu na, kama Yesu, huliona neno lake kuwa kweli. (Zaburi 119:150, 151; Yohana 17:17) Uhusiano wetu na Yehova hututegemeza katika ulimwengu huu wenye misukosuko na utatusaidia kuokoka vita vyake vikuu vya Har–Magedoni.—Ufunuo 7:9, 14; 16:13-16.

19 Tunafurahia usalama wa kweli kwa sababu tunaliheshimu sana neno la Mungu. (Zaburi 119:153-160) Tofauti na waovu, sisi ‘hatujaondoka katika vikumbusho vya Yehova.’ Tunayapenda maagizo ya Mungu, kwa hiyo sisi tuko salama katika fadhili zake zenye upendo. (Zaburi 119:157-159) Vikumbusho vya Yehova huchochea akili zetu ili kukumbuka yale anayotaka tufanye katika hali fulani. Kwa upande mwingine, maagizo ya Mungu ni miongozo, na tunakubali kwa utayari kwamba Muumba ana haki ya kutuongoza. Kwa kuwa tunajua kwamba ‘kiini cha neno la Mungu ni kweli’ na kwamba hatuwezi kuongoza hatua zetu bila kumtegemea, tunakubali mwongozo wake kwa furaha.—Zaburi 119:160; Yeremia 10:23.

20. Kwa nini tuna “amani nyingi”?

20 Kupenda sheria ya Yehova hutuletea amani nyingi. (Zaburi 119:161-168) Mateso hayatunyang’anyi “amani ya Mungu” ambayo haina kifani. (Wafilipi 4:6, 7) Kwa kuwa tunayathamini sana maamuzi ya hukumu ya Yehova, sisi humsifu mara nyingi—“mara saba wakati wa mchana.” (Zaburi 119:161-164) Mtunga-zaburi aliimba: “Wale wanaoipenda sheria yako wana amani nyingi, na hakuna kitu cha kuwakwaza.” (Zaburi 119:165) Ikiwa sisi binafsi tunaipenda sheria ya Yehova, hatutakwazwa kiroho na matendo ya wengine au na jambo lingine lolote.

21. Kuna mifano gani ya Kimaandiko inayoonyesha kwamba hatupaswi kukwazika matatizo yanapotokea kutanikoni?

21 Watu wengi wanaotajwa katika Biblia hawakuruhusu chochote kiendelee kuwakwaza. Kwa mfano, mwanamume Mkristo Gayo hakukwazwa bali ‘aliendelea kutembea katika kweli’ licha ya mwenendo mwovu wa Diotrefe. (3 Yohana 1-3, 9, 10) Paulo aliwahimiza wanawake Wakristo Euodia na Sintike “wawe na akili moja katika Bwana,” labda kwa sababu kulikuwa na matatizo kati yao. Yaonekana walisaidiwa kutatua tatizo lao na waliendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. (Wafilipi 4:2, 3) Kwa hiyo, si lazima tukwazike matatizo fulani yanapotokea kutanikoni. Acheni tuzingatie kuyashika maagizo ya Yehova na kukumbuka kwamba ‘njia zetu zote ziko mbele yake.’ (Zaburi 119:168; Methali 15:3) Hivyo, hakuna kitu chochote kitakachotunyang’anya kabisa ‘amani yetu nyingi.’

22. (a) Tunaweza kupata pendeleo gani tukimtii Mungu? (b) Tuwaoneje wale ambao wametanga-tanga na kuliacha kutaniko la Kikristo?

22 Tukimtii Yehova sikuzote, tutakuwa na pendeleo la kuendelea kumsifu. (Zaburi 119:169-176) Kwa kuishi kupatana na masharti ya Mungu, sisi hufurahia usalama wa kiroho na pia ‘midomo yetu huendelea kububujika sifa ya Yehova.’ (Zaburi 119:169-171, 174) Hilo ndilo pendeleo kuu zaidi tunaloweza kupata katika siku hizi za mwisho. Mtunga-zaburi alitaka kuendelea kuishi na kumsifu Yehova, lakini kwa njia ambayo haijatajwa, ‘alitanga-tanga kama kondoo aliyepotea.’ (Zaburi 119:175, 176) Huenda wengine ambao wametanga-tanga na kuliacha kutaniko la Kikristo bado wanampenda Mungu na wangependa kumsifu. Kwa hiyo, na tufanye yote tuwezayo kuwasaidia ili wapate usalama wa kiroho na shangwe ya kumsifu Yehova pamoja na watu wake.—Waebrania 13:15; 1 Petro 5:6, 7.

Nuru Itakayoangaza Barabara Yetu Milele

23, 24. Umepata manufaa gani kwa kuichunguza Zaburi ya 119?

23 Zaburi ya 119 inaweza kutunufaisha kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, inaweza kutufanya tumtegemee Mungu zaidi, kwa kuwa inaonyesha kwamba furaha ya kweli hutokana na ‘kutembea katika sheria ya Yehova.’ (Zaburi 119:1) Mtunga-zaburi anatukumbusha kwamba ‘kiini cha neno la Mungu ni kweli.’ (Zaburi 119:160) Bila shaka, jambo hilo linapaswa kutusaidia tuthamini zaidi Neno lote la Mungu lililoandikwa. Kutafakari Zaburi ya 119 kunapaswa kutuchochea kujifunza Maandiko kwa bidii. Mtunga-zaburi alimsihi Mungu tena na tena hivi: “Unifundishe masharti yako.” (Zaburi 119:12, 68, 135) Pia alimsihi hivi: “Unifundishe wema, kuwa na akili na ujuzi, kwa maana nimeonyesha imani katika amri zako.” (Zaburi 119:66) Tunapaswa kusali vivyo hivyo.

24 Mafundisho ya Yehova hutuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Mtunga-zaburi anajiita mtumishi wa Mungu tena na tena. Hata anazungumza na Yehova kwa maneno haya yenye kugusa moyo: “Mimi ni wako.” (Zaburi 119:17, 65, 94, 122, 125; Waroma 14:8) Ni pendeleo kubwa sana kumtumikia na kumsifu Yehova tukiwa Mashahidi wake! (Zaburi 119:7) Je, unamtumikia Mungu kwa shangwe ukiwa mhubiri wa Ufalme? Ikiwa ndivyo, uwe na uhakika kwamba Yehova ataendelea kukutegemeza na kukubariki katika kazi hiyo ya pekee ikiwa utategemea neno lake sikuzote na kuliacha liwe nuru kwa barabara yako.

Ungejibuje?

• Kwa nini tulipende neno la Mungu?

• Tunategemezwaje na neno la Mungu?

• Vikumbusho vya Yehova vinatusaidia katika njia zipi?

• Kwa nini watu wa Yehova wana amani na usalama?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Neno la Mungu ni chanzo cha nuru ya kiroho

[Picha katika ukurasa wa 17]

Ikiwa tunapenda vikumbusho vya Yehova, yeye hatatuona kamwe kama “takataka”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tukiisoma Biblia kila siku, tunaweza kukumbuka kwa urahisi mistari inayofaa tunaposali