Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Imani Yako Inakuchochea Kutenda?

Je, Imani Yako Inakuchochea Kutenda?

Je, Imani Yako Inakuchochea Kutenda?

OFISA fulani wa jeshi hakuwa na shaka kwamba Yesu angemponya mtumwa wake aliyekuwa na ugonjwa wa kupooza. Lakini ofisa huyo hakumwalika Yesu nyumbani kwake, pengine kwa sababu alijihisi kwamba hafai au kwa sababu hakuwa Myahudi. Badala yake, aliwatuma wazee fulani Wayahudi wazungumze na Yesu na kumwambia: “Bwana, mimi sistahili hivi kwamba wewe uingie chini ya paa yangu, lakini sema neno tu na mtumishi wangu atapona.” Yesu alipotambua kwamba ofisa huyo anaamini kuwa yeye anaweza kuponya hata kutoka mbali, aliuambia hivi umati uliomfuata: “Ninawaambia ninyi kweli, Sijapata yeyote katika Israeli mwenye imani kubwa kama hii.”—Mathayo 8:5-10; Luka 7:1-10.

Kisa hicho kinaweza kutusaidia kukazia fikira jambo fulani muhimu kuhusu imani. Imani ya kweli huonyeshwa kwa matendo. Mwandikaji wa Biblia Yakobo alieleza: “Imani, ikiwa haina matendo, imekufa yenyewe.” (Yakobo 2:17) Jambo hilo linaeleweka hata zaidi tunapofikiria mfano halisi wa yale yanayoweza kutukia imani inapokuwa bila matendo.

Katika mwaka wa 1513 K.W.K., agano la Sheria liliunganisha taifa la Israeli pamoja na Yehova Mungu. Musa, mpatanishi wa agano hilo, aliwaeleza Waisraeli neno la Mungu kwa kusema hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mtakapokuwa . . . taifa takatifu.” (Kutoka 19:3-6) Naam, utakatifu wa Waisraeli ulitegemea utii.

Karne nyingi baadaye, Wayahudi walianza kuona kujifunza Sheria kuwa jambo la maana kuliko kufuata kanuni za Sheria hiyo. Katika kitabu chake The Life and Times of Jesus the Messiah, Alfred Edersheim aliandika hivi: “Kwa muda mrefu [marabi], ‘watu mashuhuri wa ulimwengu,’ walikuwa wamekata kauli kwamba kujifunza sheria ni muhimu kuliko matendo.”

Kwa kweli, Waisraeli wa kale waliamuriwa kujifunza kwa bidii matakwa ya Mungu. Mungu mwenyewe alisema: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.” (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Lakini je, kuna wakati ambapo Yehova alionyesha kwamba kujifunza Sheria ni muhimu kuliko matendo yanayopatana na Sheria hiyo? Na tuone.

Kujifunza ili Kuelimika Tu

Huenda Waisraeli walikazia kupita kiasi umuhimu wa kujifunza Sheria kwa sababu mapokeo fulani ya Kiyahudi yalionyesha kwamba kila siku Mungu mwenyewe alijifunza Sheria kwa muda wa saa tatu. Basi unaelewa kwa nini huenda Wayahudi fulani walifikiri hivi: ‘Ikiwa Mungu anajifunza Sheria kwa ukawaida, je, viumbe wake walio duniani hawapaswi kufanya vivyo hivyo?’

Kufikia karne ya kwanza W.K., maoni ya warabi yalikuwa yamepotoka kabisa kwa sababu walijishughulisha sana na uchanganuzi na ufasiri wa Sheria. “Waandishi na Mafarisayo . . . husema lakini hawatendi,” Yesu akasema. “Wao hufunga mizigo mizito na kuiweka juu ya mabega ya watu, lakini wao wenyewe hawataki kuisogeza kwa kidole chao.” (Mathayo 23:2-4) Viongozi hao wa kidini walitunga sheria na kanuni nyingi zilizowalemea watu wa kawaida, lakini kwa unafiki walibuni njia ambazo zingewaepusha kufuata sheria hizo. Isitoshe, watu hao waliojishughulisha sana na utafiti ‘walipuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.’—Mathayo 23:16-24.

Inashangaza kwamba katika jitihada zao za kujionyesha kuwa waadilifu, waandishi na Mafarisayo waliivunja Sheria ileile waliyodai kuifuata! Mijadala kuhusu maneno na mambo madogo-madogo ya Sheria iliyoendelea kwa karne nyingi haikuwasaidia kumkaribia Mungu. Matokeo yake yalifanana na kukengeuka kunakosababishwa na kile ambacho mtume Paulo alikiita “maneno matupu,” “maneno yanayopingana,” na “ujuzi” wa uwongo. (1 Timotheo 6:20, 21) Hata hivyo, tatizo lingine zito ni jinsi walivyoathiriwa na utafiti huo usiokoma. Hawakuwa na imani ambayo iliwachochea kutenda mema.

Wenye Akili, Lakini Wasio na Imani

Kufikiri kwa viongozi wa dini ya Kiyahudi kulikuwa tofauti sana na kufikiri kwa Mungu. Muda mfupi kabla ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Musa aliwaambia: “Tieni mioyo yenu katika maneno yote ninayosema kwa kuwaonya ninyi leo, ili muwaamuru wana wenu wawe waangalifu kufanya maneno yote ya sheria hii.” (Kumbukumbu la Torati 32:46) Ni wazi kwamba watu wa Mungu hawakupaswa tu kujifunza Sheria bali kuifuata.

Hata hivyo, mara kwa mara, taifa la Israeli lilikosa uaminifu kwa Yehova. Badala ya kutenda mambo yanayofaa, Waisraeli ‘hawakumwamini wala hawakuisikiliza sauti yake.’ (Kumbukumbu la Torati 9:23; Waamuzi 2:15, 16; 2 Mambo ya Nyakati 24:18, 19; Yeremia 25:4-7) Mwishowe, Wayahudi walitenda tendo baya zaidi la ukosefu wa uaminifu walipokataa kwamba Yesu ndiye Masihi. (Yohana 19:14-16) Kwa sababu hiyo, Yehova Mungu aliwakataa Waisraeli na kuwageukia watu wa mataifa.—Matendo 13:46.

Kwa kweli, tunahitaji kuwa waangalifu ili tusiangukie mtego huo, yaani, kufikiri kwamba tunaweza kumwabudu Mungu kwa kutegemea akili tu bila kuwa na imani. Hiyo inamaanisha kwamba hatupaswi kujifunza Biblia ili kupata ujuzi tu. Ujuzi sahihi unapaswa kugusa mioyo yetu na kutunufaisha. Ingekuwa na manufaa gani kujifunza kulima ikiwa hatupandi chochote? Kwa kweli, tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu kulima, lakini hatutavuna ikiwa hatupandi chochote. Vivyo hivyo, watu wanaojifunza matakwa ya Mungu kupitia funzo la Biblia wanapaswa kuacha mbegu za kweli zifikie moyo ili zikue na kuwachochea kutenda.—Mathayo 13:3-9, 19-23.

“Iweni Watendaji wa Neno”

Mtume Paulo alisema kwamba “imani hufuata jambo lililosikiwa.” (Waroma 10:17) Kusikia Neno la Mungu kisha kumwamini Mwana wake Yesu Kristo, hutupa taraja la kupata uzima wa milele. Naam, mengi zaidi yanahitajiwa kuliko kusema tu, ‘Ninamwamini Mungu na Kristo.’

Yesu aliwahimiza wafuasi wake wawe na imani ambayo ingewachochea kutenda: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi na kujionyesha kuwa wanafunzi wangu.” (Yohana 15:8) Baadaye, Yakobo, ndugu-nusu wa Yesu aliandika hivi: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.” (Yakobo 1:22) Hata hivyo, tunawezaje kujua yale tunayopaswa kufanya? Kwa maneno na kwa matendo, Yesu alionyesha yale tunayohitaji kufanya ili kumpendeza Mungu.

Alipokuwa duniani, Yesu alijitahidi sana kuendeleza mambo ya Ufalme na kulitukuza jina la Baba yake. (Yohana 17:4-8) Kwa njia gani? Huenda watu wengi wakakumbuka miujiza ya Yesu ya kuponya wagonjwa na viwete. Lakini Injili ya Mathayo inaonyesha wazi njia kuu zaidi ambayo Yesu alitumia ili kuendeleza mambo ya Ufalme: “Yesu akaondoka ili kutembelea majiji na vijiji vyote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme.” Ona kwamba, katika huduma yake Yesu hakuzungumza tu na marafiki wachache au majirani. Alijitahidi kabisa na kutumia kila njia ili kuwatembelea watu “katika Galilaya yote.”—Mathayo 4:23, 24; 9:35.

Yesu aliwaagiza pia wafuasi wake kushiriki kazi ya kufanya wanafunzi. Kwa kweli, aliwawekea mfano bora ili waige. (1 Petro 2:21) Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake waaminifu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20.

Ni kweli kwamba, kazi ya kuhubiri si rahisi. Yesu mwenyewe alisema: “Tazama! Ninawatuma ninyi kama wana-kondoo katikati ya mbwa-mwitu.” (Luka 10:3) Tunapokabili upinzani, ni kawaida kutaka kurudi nyuma ili tusipatwe na huzuni au mahangaiko yasiyo ya lazima. Hilo ndilo lililotukia jioni ile Yesu alipokamatwa. Mitume walikimbia baada ya kuzidiwa na woga. Baadaye jioni hiyo, Petro alimkana Yesu mara tatu.—Mathayo 26:56, 69-75.

Isitoshe, huenda ukashangaa kujua kwamba hata mtume Paulo alisema kuwa alijitahidi sana ili kuhubiri habari njema. Aliliandikia hivi kutaniko la Thesalonike: “Tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu ili kuwaambia ninyi habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.”—1 Wathesalonike 2:1, 2.

Paulo na mitume wenzake walishinda woga wa kuwaeleza wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. Wewe pia unaweza kufanya hivyo. Jinsi gani? Hatua iliyo muhimu zaidi ni kumtegemea Yehova. Ikiwa tunamwamini Yehova kabisa, imani hiyo itatuchochea kutenda, nasi tutaweza kufanya mapenzi yake.—Matendo 4:17-20; 5:18, 27-29.

Utapata Thawabu kwa Kazi Yako

Yehova anajua vizuri jitihada tunayofanya ili kumtumikia. Kwa mfano, anajua wakati tunapokuwa wagonjwa au wachovu. Anajua tunapokuwa na shaka na kukosa kujiamini. Tunaposumbuliwa na matatizo ya kifedha, au afya yetu au hisia zetu zinapotukatisha tamaa, sikuzote Yehova hutambua hali yetu.—2 Mambo ya Nyakati 16:9; 1 Petro 3:12.

Yehova anafurahi sana anapoona imani inatuchochea kutenda licha ya magumu na hali yetu ya kutokamilika. Hisia nyororo za Yehova kuelekea watumishi wake waaminifu si hisia tu zisizo na maana, bali zinaonyeshwa kupitia ahadi fulani. Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.”—Waebrania 6:10.

Unaweza kuitumaini Biblia inapomtaja Yehova kuwa “Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki,” na “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Kumbukumbu la Torati 32:4; Waebrania 11:6) Kwa mfano, mwanamke mmoja huko California, Marekani, anasema: “Baba yangu alitumika akiwa mhudumu wa wakati wote kwa miaka kumi kabla ya kuwa na familia. Nilipendezwa na habari alizonieleza kuhusu jinsi Yehova alivyomtegemeza katika kazi ya kuhubiri. Mara nyingi alitumia pesa zote kununua petroli ili aende kuhubiri. Aliporudi nyumbani, mara nyingi bila kutarajia alipata chakula mlangoni.”

Mbali na kututegemeza kimwili, “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote” hututegemeza kihisia na kiroho. (2 Wakorintho 1:3) Shahidi mmoja aliyevumilia majaribu mengi kwa miaka mingi anasema hivi: “Kumtegemea Yehova kunaridhisha kihisia. Kunakupa nafasi ya kumtegemea na kuona jinsi anavyokusaidia.” Unaweza kusali kwa unyenyekevu kwa “Msikiaji wa sala,” ukiwa na uhakika kwamba atasikiliza mahangaiko yako.—Zaburi 65:2.

Tunapata baraka na thawabu nyingi tukiwa wafanyakazi katika mavuno ya kiroho. (Mathayo 9:37, 38) Kushiriki katika kazi ya kuhubiri kumewanufaisha wengi kiafya, na huenda hata wewe ukanufaika. Hata hivyo, lililo muhimu zaidi ni kwamba kuwahubiria wengine hutusaidia kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Mungu.—Yakobo 2:23.

Endelea Kutenda Mema

Ingekuwa kosa kwa mtumishi wa Mungu kukata kauli kwamba Yehova hafurahi ikiwa ugonjwa au uzee unamzuia asitimize yote ambayo angependa kutimiza katika huduma. Pia ingekuwa kosa kukata kauli hiyohiyo kuhusu wale walio na afya mbaya, madaraka ya familia, au hali nyingine.

Kumbuka kwamba mtume Paulo alipohisi kwamba anazuiwa na ugonjwa au kikwazo fulani, ‘mara tatu alimsihi Bwana kwamba kikwazo hicho kiondoke.’ Badala ya kumponya Paulo ili atimize mengi zaidi katika utumishi wake, Yehova alimwambia: “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha wewe; kwa maana nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu.” (2 Wakorintho 12:7-10) Hivyo, uwe na uhakika kwamba licha ya hali zozote ngumu ambazo huenda ikawa unavumilia, Baba yako wa mbinguni anathamini chochote unachofanya kuhusiana na mapenzi yake.—Waebrania 13:15, 16.

Muumba wetu mwenye upendo hataki tufanye zaidi ya uwezo wetu. Anataka tu tuwe na imani ambayo inatuchochea kutenda.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, ilitosha tu kujifunza Sheria?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Imani yetu inahitaji kuwa yenye matendo