Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Mambo Mengi Sana ya Kujifunza?

Je, Kuna Mambo Mengi Sana ya Kujifunza?

Je, Kuna Mambo Mengi Sana ya Kujifunza?

Mume na mke ambao ni wamishonari walikuwa wameketi ufuoni huko Afrika Magharibi wakitazama mwezi mwangavu. Kisha mume akamuuliza mke wake hivi: “Mwanadamu anajua mambo mengi kadiri gani kuhusu mwezi, na ni mambo gani ambayo hajui?”

Mke akamjibu: “Hebu wazia ikiwa tungeweza kutazama dunia ikisonga polepole kama mwezi. Tayari watu wamejifunza mambo mengi kuhusu dunia na kuna mengine mengi ambayo hawajui. Wazia hili pia! Dunia inazunguka jua, na mfumo wote wa jua unasonga. Hiyo inamaanisha kwamba hatutarudi mahali tulipo sasa ulimwenguni. Isitoshe, tunajua mahali tulipo kwa kutegemea mahali ambapo jua na nyota zipo. Tunajua mengi sana kuhusu vitu fulani, lakini hatujui mahali tulipo!”

MANENO hayo yana ukweli fulani muhimu. Kuna mambo mengi sana ya kujifunza. Sote hujifunza mambo mapya kila siku. Lakini hata tujifunze mambo mengi kadiri gani hatuwezi kujifunza yote tunayotaka kujua.

Ni kweli kwamba, mbali na uwezo wa kujifunza mambo mapya, uwezo wa kuhifadhi habari umeongezeka sana kwa sababu ya teknolojia. Sasa diski za kompyuta zina uwezo mkubwa sana wa kuhifadhi habari hivi kwamba maneno mapya ya hesabu yametungwa ili kufafanua uwezo huo. Diski ya kawaida tu ya CD-ROM inaweza kuhifadhi habari chungu nzima kwani uwezo wake unafikia megabaiti 680 au zaidi. Uwezo wa kuhifadhi habari wa diski ya kawaida ya DVD unazidi kwa karibu mara saba ule wa CD-ROM, na nyingine zenye uwezo mkubwa zaidi zinatengenezwa.

Sisi hustaajabia njia za kisasa ambazo mwanadamu anatumia kuwasilisha habari. Kuna mashine ambazo huchapisha magazeti na vitabu haraka sana. Mtu anayetumia mtandao wa Intaneti anaweza kupata habari nyingi sana kwa kubonyeza tu kidude fulani cha kompyuta. Mifano hiyo inaonyesha kwamba habari zinatayarishwa haraka sana hivi kwamba ni vigumu kuzisoma zote. Kuna msemo unaosema elimu ni bahari. Tunahitaji kujifunza kuogelea katika bahari hiyo kubwa tusije tukazama. Kwa kuwa kuna habari nyingi sana, ni lazima tuzichague kwa uangalifu.

Pia, tunapaswa kuwa waangalifu tunapochagua habari kwa sababu nyingi hazina faida sana. Kwa kweli, baadhi ya habari hizo hazifai na hakuna haja ya kuzijua. Kumbuka kwamba ujuzi unahusisha kupata habari, ziwe mbaya au nzuri, ziwe zenye faida au hazina faida. Isitoshe, habari nyingi zinazoonekana kuwa za kweli huwa si sahihi. Mara nyingi, kauli za wataalamu wenye kuheshimika zimethibitishwa kuwa zenye kasoro, au zisizo za kweli. Kwa mfano, fikiria kisa cha yule karani wa jiji la kale la Efeso, ambaye alionwa kuwa ofisa mwenye ujuzi. Alisema hivi: “Kwa kweli ni nani kati ya wanadamu ambaye hajui kwamba jiji la Efeso ndilo mtunza-hekalu wa Artemi mkuu na wa sanamu iliyoanguka kutoka mbinguni?” (Matendo 19:35, 36) Watu wengi walifikiri, na hata kushikilia kwamba sanamu hiyo ilikuwa imeanguka kutoka mbinguni, lakini huo ulikuwa uwongo. Hiyo ndiyo sababu Biblia Takatifu huwaonya Wakristo wajihadhari na “ule unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi.’”—1 Timotheo 6:20.

Tunapaswa kuchagua kwa uangalifu mambo tunayojifunza kwa sababu nyingine ya maana sana. Maisha yetu ni mafupi sana. Hata uwe na miaka mingapi, kuna mambo mengi ambayo ungependa kujifunza, lakini unatambua kwamba huwezi kufanya hivyo kwa sababu maisha ni mafupi.

Je, tatizo hilo litakwisha? Je, kuna ujuzi ambao unaweza kumsaidia mwanadamu aishi kwa muda mrefu, hata milele? Je, ujuzi huo unapatikana? Ikiwa ndivyo, je, watu wote wanaweza kuupata? Je, kuna wakati ambapo ujuzi wote utakaopatikana utakuwa wa kweli? Wale wenzi wa ndoa wamishonari waliotajwa juu wamepata majibu yenye kuridhisha kwa maswali hayo, nawe pia unaweza kuyapata. Tafadhali soma makala inayofuata kwani itakuonyesha jinsi unavyoweza kujifunza milele.