Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Ujuzi Sasa na Milele

Kupata Ujuzi Sasa na Milele

Kupata Ujuzi Sasa na Milele

DAKTARI mmoja Mjerumani anayeitwa Ulrich Strunz aliandika mfululizo wa vitabu fulani (vinavyoitwa Forever Young). Katika vitabu hivyo anasema kwamba mtu anaweza kuwa na afya njema na kuishi muda mrefu akifanya mazoezi, akila vizuri, na kuishi maisha mazuri. Lakini, daktari huyo hasemi kwamba wasomaji wake wanaweza kuishi milele wanapofuata mashauri yake.

Hata hivyo, kuna ujuzi fulani unaowahakikishia watu kwamba watapata uzima wa milele. Ukiishi milele, unaweza kujifunza mambo yenye faida milele. Yesu alisema hivi aliposali kwa Mungu: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Hebu kwanza tufafanue “uzima wa milele” kisha tuzungumzie ujuzi huo na jinsi tunavyoweza kuupata.

Biblia inasema kwamba hivi karibuni Muumba atafanya dunia iwe paradiso halisi, na kuwawezesha watu kuishi kwa muda mrefu. Hatua kubwa, kama ile iliyochukuliwa wakati wa Gharika ya siku za Noa, itahitaji kuchukuliwa ili kuleta Paradiso hiyo. Kwenye Mathayo sura ya 24, mstari wa 37 hadi 39, Yesu alilinganisha wakati wetu na “siku za Noa,” ambapo watu “hawakujali” hali yao hatari. Pia, walipuuza ujumbe ambao Noa alihubiri. Kisha “siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina” ikafika, nayo Gharika ikawaharibu wote waliokataa ujuzi huo. Noa na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya safina waliokoka.

Yesu alionyesha kwamba “siku” kama hiyo itakuja katika wakati wetu. Wale wanaozingatia ujuzi unaohusiana na tukio hilo wataokoka na kuwa na tumaini la kuishi milele. Isitoshe, wafu walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa na inawezekana wasife tena. (Yohana 5:28, 29) Ona jinsi Yesu alivyozungumzia mambo hayo mawili. Alipokuwa akizungumza na Martha kuhusu ufufuo wa wafu, Yesu alisema hivi: “Yule anayeniamini, hata akifa, atarudi kwenye uzima; na kila mtu aliye hai na ananiamini hatakufa kamwe.” Uthibitisho wote unaonyesha kwamba “siku” hiyo iko karibu sana, na hiyo inamaanisha kwamba huenda ‘usife kamwe.’—Yohana 11:25-27.

Yesu pia alimuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Naye akamjibu: “Ndiyo, Bwana.” Ikiwa Yesu angekuuliza swali hilo leo, ungemjibuje? Huenda ungeona ni vigumu kuamini kwamba inawezekana usife kamwe. Lakini hata ikiwa ungehisi hivyo, hapana shaka kwamba ungependa kuamini jambo hilo. Hebu wazia mambo ambayo ungejifunza ikiwa ‘hungekufa kamwe’! Wazia ukifurahia mambo ambayo huwezi kujifunza na kufanya kwa sasa kwa sababu huna wakati. Na hebu fikiria jinsi utakavyohisi utakapoungana tena na wapendwa wako ambao wamekufa! Ni ujuzi gani utakaokuwezesha kufurahia mambo hayo, nawe unaweza kuupataje?

Tunaweza Kupata Ujuzi Unaoongoza Kwenye Uzima

Je, ni vigumu kupata ujuzi juu ya Mungu na Kristo? La. Ni kweli kwamba ujuzi kuhusu kazi za Muumba hauna kikomo. Lakini Yesu hakuwa akizungumza kuhusu elimu ya nyota au elimu nyingine ya kisayansi alipohusianisha “ujuzi” na “uzima wa milele.” Andiko la Methali sura ya 2, mstari wa 1 na wa 5 linaonyesha kwamba “maneno” na “amri” zinazopatikana katika Biblia ndiyo mambo ya msingi katika “kumjua Mungu.” Na kumhusu Yesu, andiko la Yohana 20:30, 31 linasema kwamba mambo yaliyoandikwa yanatosha ili ‘tupate kuwa na uzima.’

Hivyo, ujuzi unaopatikana katika Biblia kumhusu Yehova na Yesu Kristo unatosha kukuonyesha jinsi ya kupata uzima wa milele. Biblia ni kitabu cha pekee. Muumba aliwatumia wanadamu waiandike kwa njia inayowawezesha watu wasio na elimu na wasio na uwezo wa kuipata wajifunze mambo ya kutosha ili wapate uzima wa milele. Vilevile, mtu mwenye akili chapuchapu, mwenye wakati mwingi, na aliye na njia za kujipatia elimu, anaweza kujifunza mambo mapya katika Maandiko. Kwa kuwa unasoma makala hii, hiyo inaonyesha kwamba una uwezo wa kujifunza. Lakini, unapaswa kuutumia jinsi gani?

Mifano ya watu ulimwenguni pote imeonyesha kwamba njia bora ya kupata ujuzi huo ni kujifunza Biblia na mtu ambaye tayari anaielewa. Kama vile Noa alivyowafundisha watu wa siku zake, Mashahidi wa Yehova wako tayari kuja nyumbani kwako ili wazungumze pamoja nawe kuhusu Biblia. Huenda wakatumia broshua yenye kichwa Mungu Anataka Tufanye Nini? au kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. * Hata ukiona ni vigumu kuamini kwamba katika dunia Paradiso watu waaminifu ‘hawatakufa kamwe,’ mazungumzo hayo ya Biblia yanaweza kukusaidia kusadiki ahadi hiyo. Kwa hiyo, unapaswa kufanya nini ikiwa unataka kuishi milele au unataka tu kujua kama inawezekana kuishi milele? Basi, kubali kujifunza Biblia.

Funzo hilo la Biblia litachukua muda gani? Broshua hiyo iliyotajwa yenye kurasa 32, inapatikana katika lugha nyingi, nayo ina masomo mafupi 16. Au ikiwa unaweza kutenga saa moja kila juma, itakuchukua miezi michache tu kujifunza habari muhimu za Biblia ukitumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Vichapo hivyo vimewasaidia watu wengi kupata ujuzi mwingi na kumpenda Mungu sana. Muumba atawapa thawabu wale wanaompenda kwelikweli kwa kuwawezesha kupata uzima wa milele.

Ni kweli kwamba tunaweza kupata ujuzi unaoongoza kwenye uhai, nao unapatikana kwa urahisi. Biblia nzima au sehemu fulani zake zimetafsiriwa katika lugha zaidi ya 2,000. Mashahidi wa Yehova katika nchi 235 wako tayari kukusaidia na kukuletea vichapo vinavyoifafanua Biblia ili uongeze ujuzi wako.

Funzo la Kibinafsi

Uhusiano wako na Mungu ni jambo la kibinafsi kati yako na Muumba. Ni wewe tu unayeweza kuudumisha na kuuimarisha, na ni yeye tu anayeweza kukupatia uzima wa milele. Hivyo, unapaswa kuendelea kujifunza kibinafsi Neno lake lililoandikwa. Ukikubali mtu fulani akutembelee nyumbani kwa ukawaida ili ajifunze nawe, huenda ikawa rahisi kwako kutenga wakati kwa ajili ya funzo.

Kwa kuwa Biblia na vichapo vinavyoifafanua vinaweza kukusaidia “kumjua Mungu,” ni muhimu kuvitunza. (Methali 2:5) Ukifanya hivyo utavitumia kwa miaka mingi. Ikiwa unaishi katika nchi inayoendelea, huenda hukutumia vitabu vingi shuleni bali ulijifunza kwa kusikiliza na kutazama tu. Kwa mfano, kuna lugha zaidi ya 50 huko Benin. Si ajabu kuwasikia watu fulani wakizungumza lugha nne au tano vizuri, ijapokuwa hawajawahi kusoma vitabu vya lugha hizo. Umebarikiwa kuwa na uwezo wa kujifunza kwa kusikiliza, kutazama, na kukaza fikira. Lakini bado unaweza kujifunza mengi sana kwa kutumia vitabu.

Hata ikiwa unaishi katika nyumba ndogo, jitahidi kuweka Biblia na vichapo vinavyoifafanua mahali panapofaa. Viweke mahali unapoweza kuvipata kwa urahisi na ambapo havitaharibika.

Funzo la Familia

Ikiwa wewe ni mzazi, inafaa uwasaidie watoto wako kujifunza mambo yaleyale unayojifunza. Katika nchi zinazoendelea, mara nyingi wazazi huwafundisha watoto wao kazi nyingi ambazo watafanya maishani. Kazi hizo zinatia ndani kupika, kukusanya kuni, kuchota maji, kulima, kuvua samaki, na kuuza bidhaa sokoni. Elimu hiyo huwasaidia maishani. Lakini wazazi wengi hawawasaidii watoto wao kupata ujuzi unaoweza kuongoza kwenye uzima wa milele.

Hata hali yako iweje, huenda unahisi kwamba huna wakati mwingi. Muumba anatambua jambo hilo pia. Ona yale aliyosema zamani kuhusu jinsi ya kuwafundisha watoto njia zake: “Uyakazie kwa mwana wako [au binti yako] na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.” (Kumbukumbu la Torati 6:7) Kwa kutumia maneno hayo, jitahidi kupanga ratiba ya kuwafundisha watoto wako, kama hii inayoonyeshwa hapa:

1. “Unapoketi katika nyumba yako”: Jitahidi kuzungumza na watoto wako kwa ukawaida kuhusu Biblia mnapokuwa nyumbani, labda kila juma, sawa na vile mtu fulani alivyojifunza nawe. Mashahidi wa Yehova hutoa vichapo vinavyoifafanua Biblia ili kuwafundisha watoto wa umri wowote ule.

2. “Unapotembea barabarani”: Zungumza na watoto wako kumhusu Yehova kwa njia ya kirafiki sawa na vile unavyowafundisha mambo muhimu maishani au kuwapa mwongozo.

3. “Unapolala”: Sali na watoto wako kila jioni.

4. “Unapoamka”: Familia nyingi zimenufaika kwa kuchunguza andiko moja la Biblia kila asubuhi. Mashahidi wa Yehova hufanya hivyo kwa kutumia kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. *

Katika nchi zinazoendelea, wazazi wengi hujitahidi sana kuhakikisha kwamba watoto wao wanapata elimu bora. Kwa njia hiyo, watoto wataweza kuwatunza wazazi wao watakapokuwa wazee. Hata hivyo, ukijifunza Biblia na kuwasaidia watoto wako kufanya hivyo pia, utapata ujuzi ambao utakuwezesha wewe na familia yako yote kuishi milele.

Je, kuna wakati ambapo tutajua kila kitu? La. Kadiri dunia yetu inavyoendelea kusonga, ndivyo tutakavyoendelea kujifunza. Andiko la Mhubiri 3:11 linasema: “[Mungu] amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” Tutaendelea kufurahia kujifunza milele.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Vyote vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 23 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi . . . ”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Saidia familia yako kupata ujuzi sasa na milele