Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutosheleza Uhitaji Huko Makedonia

Kutosheleza Uhitaji Huko Makedonia

Kutosheleza Uhitaji Huko Makedonia

“VUKA uingie Makedonia utusaidie.” (Matendo 16:9) Maneno hayo ya mtu mmoja aliyemtokea mtume Paulo katika maono yanaonyesha uhitaji wa kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu katika maeneo mengine, yaani, katika majiji ambayo sasa yako Ugiriki.

Katika Makedonia ya leo, kuna Shahidi 1 wa Yehova kwa kila wakaaji 1,840 wa nchi hiyo. Watu wengi hawajasikia kumhusu Yehova Mungu. Naam, watu wa nchi hiyo wanahitaji sana kusikia ujumbe wa amani.—Mathayo 24:14.

Mungu amefungua njia ya kutosheleza uhitaji huo. Siku moja katika Novemba 2003, akina ndugu katika ofisi ya Mashahidi wa Yehova huko Skopje, Makedonia, walipigiwa simu isiyotarajiwa. Simu hiyo ilitoka kwenye Kituo cha Ushirikiano wa Kimataifa cha Makedonia ambacho kilipanga kufanya maonyesho ya siku tatu kuanzia Novemba 20. Mashahidi walikaribishwa kuwa na kibanda chao ili kueleza imani yao kwenye maonyesho hayo. Hiyo ilikuwa nafasi ya pekee sana ya kuwafikia maelfu ya watu ambao hawakuwa wamesikia habari njema za Ufalme!

Mashahidi walifanya kazi kwa bidii ili kutayarisha na kupanga mahali pa kuonyeshea vichapo vyao katika lugha ya Makedonia. Baadhi ya vichapo hivyo vilionyeshwa waziwazi ili wageni waweze kuvichukua wakitaka. Jambo hilo liliwapa wengi nafasi ya kupata maji ya kiroho bure.—Ufunuo 22:17.

Wageni walitaka vichapo ambavyo vilihusu maisha yao, kama vile kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na Siri ya Kupata Furaha ya Familia. * Watu 98 walitoa anwani zao na kuomba watembelewe na Mashahidi wa Yehova. Wengi wao walisifu kazi nzuri ya Mashahidi wa Yehova na vichapo vyao.

Mtu mmoja alifika kwenye kibanda hicho huku akiushika mkono wa mwana wake mdogo. Mtu huyo aliuliza ikiwa kuna vitabu vya watoto. Mashahidi walimwonyesha Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. * Alikichunguza na kuuliza kwa uchangamfu bei yake. Aliposikia kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuwaelimisha watu inaendeshwa kwa michango ya hiari, alisisimuka zaidi. (Mathayo 10:8) Alimwonyesha mwana wake kitabu hicho na kusema: “Ni kitabu kizuri sana! Nitakusomea hadithi moja kila siku!”

Profesa mmoja wa falsafa alifika kwenye kibanda hicho. Alipendezwa sana na dini kwa ujumla na hasa mafundisho ya Mashahidi wa Yehova. Alipochunguza kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, * profesa huyo alisema hivi: “Kitabu hiki kinawasilisha hoja zake vizuri sana! Hivyo ndivyo mambo yanavyopaswa kufafanuliwa.” Baadaye baadhi ya wanafunzi wake walikuja kwenye kibanda hicho na kuomba kitabu kama kile ambacho profesa huyo alichukua. Walitaka kusoma kitabu hichohicho kwa kuwa walifikiri kwamba atakitumia anapofundisha.

Watu wengine walisikia kweli za Biblia kwa mara ya kwanza kwenye maonyesho hayo. Vijana fulani wasioweza kusikia walitembelea kibanda hicho. Shahidi mmoja alizungumza nao kifupi huku msichana mmoja akitafsiri katika lugha ya ishara. Akitumia picha za kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, * Shahidi huyo alieleza kwamba Yesu aliwaponya wagonjwa, kutia ndani watu wasioweza kusikia. Walifurahi “kusikia” ahadi ya Biblia inayosema kwamba hivi karibuni Yesu atawaponya watu wanaoishi duniani. Baadhi yao walichukua vichapo vinavyoifafanua Biblia, na mipango ikafanywa ili watembelewe na Shahidi anayejua lugha ya ishara.

Mbali na lugha ya Makedonia, vichapo vya Kialbania, Kiingereza, na Kituruki vilikuwepo. Mtu mmoja ambaye hakujua Kimakedonia aliomba vichapo vya Kiingereza. Alipopokea magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, alisema kwamba anazungumza Kituruki. Mtu huyo alipoonyeshwa vichapo vya lugha yake, alishangaa sana! Alitambua kwamba Mashahidi wa Yehova wanataka kuwasaidia watu wote.

Ushahidi mzuri ulitolewa wakati huo, na inatia moyo sana kuona jinsi watu wengi wanavyopendezwa na kweli za Biblia! Naam, Yehova alifungua njia ya kueneza habari njema za Ufalme huko Makedonia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Vyote vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 7 Vyote vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova

^ fu. 8 Vyote vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova

^ fu. 9 Vyote vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

MAENDELEO MAKUBWA!

Katika Mei 17, 2003, hatua kubwa ilipigwa katika kazi ya kueneza habari njema za Ufalme wa Mungu. Ofisi ya Mashahidi wa Yehova iliwekwa wakfu huko Skopje. Ujenzi wa ofisi hiyo ulichukua miaka miwili, na ukubwa wake ni mara nne zaidi ya ofisi ya zamani.

Kuna majengo matatu tofauti-tofauti ambayo yana ofisi za usimamizi na tafsiri, vyumba vya kulala, jiko, na mahali pa kuoshea nguo. Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alitoa hotuba ya wakfu. Wageni kutoka nchi kumi walihudhuria programu hiyo. Wote walisisimuka walipoona majengo hayo mapya yenye kupendeza.

[Ramani katika ukurasa wa 8, 9]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

BULGARIA

MAKEDONIA

Skopje

ALBANIA

UGIRIKI

[Picha katika ukurasa wa 8]

Skopje, Makedonia