Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, mtume Paulo alikana imani yake ya Kikristo aliposema mbele ya Sanhedrini: “Mimi ni Farisayo”?

Ili kuelewa maneno ya Paulo, kwenye Matendo 23:6, tunahitaji kufikiria muktadha wake.

Baada ya kushambuliwa na umati wa Wayahudi huko Yerusalemu, Paulo alizungumza na umati huo. Alitaja kwamba ‘alielimishwa jijini Yerusalemu miguuni pa Gamalieli na alikuwa amefundishwa kwa usahihi kabisa Sheria ya mababu wake.’ Ingawa umati ulisikiliza kwa muda mfupi Paulo alipojitetea, mwishowe walipokasirika, kiongozi wa kijeshi alimchukua Paulo na kumsindikiza hadi kwenye makao ya askari-jeshi. Walipotaka kumpiga mijeledi, Paulo aliwauliza: “Je, ni halali kwa ninyi watu kumpiga mijeledi mtu ambaye ni Mroma na ambaye hajahukumiwa kuwa mwenye hatia?”—Matendo 21:27–22:29.

Siku iliyofuata, kiongozi wa kijeshi alimpeleka Paulo mbele ya Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi. Paulo aliwakazia macho naye akatambua kwamba Sanhedrini ilikuwa na Masadukayo na Mafarisayo. Kisha akasema: “Wanaume, akina ndugu, mimi ni Farisayo, mwana wa Mafarisayo. Ninahukumiwa juu ya tumaini la ufufuo wa wafu.” Kwa hiyo, mtengano ukatokea kati ya Mafarisayo na Masadukayo, “kwa maana Masadukayo husema hakuna ufufuo wala malaika wala roho, lakini Mafarisayo huyatangaza yote hadharani.” Baadhi ya wale waliokuwa wa madhehebu ya Mafarisayo wakapinga kwa hasira: “Sisi hatuoni kosa lolote katika mtu huyu.”—Matendo 23:6-10.

Kwa kuwa alijulikana kuwa Mkristo mwenye bidii, Paulo hangeweza kusadikisha Sanhedrini kwamba alikuwa Farisayo mwenye kutenda. Mafarisayo waliokuwapo hawangemkubali Farisayo yeyote ambaye hakuamini mafundisho yao yote. Hivyo, Paulo aliposema kwamba alikuwa Farisayo hakumaanisha hivyo hasa, na bila shaka Mafarisayo waliokuwapo walielewa maneno yake katika maana hiyo.

Kwa kusema kwamba alikuwa akihukumiwa juu ya tumaini la ufufuo wa wafu, kwa wazi Paulo alimaanisha kwamba kuhusiana na tumaini hilo alikuwa kama Mafarisayo. Hivyo, katika mabishano yoyote kuhusu ufufuo, Paulo angehusianishwa na Mafarisayo wala si Masadukayo, ambao hawakuamini ufufuo.

Imani ya Paulo akiwa Mkristo haikupingana na ile ya Mafarisayo kuhusu ufufuo, malaika, na mambo mengine yaliyohusu Sheria. (Wafilipi 3:5) Hivyo, katika mambo hayo, Paulo angeweza kuwaunga mkono Mafarisayo, na wale waliokuwapo katika Sanhedrini walielewa maneno yake kwa njia hiyo. Kwa hiyo, alikuwa akitumia malezi yake ya Kiyahudi ili kukabiliana na ubaguzi wa mahakama kuu ya Kiyahudi.

Hata hivyo, uthibitisho mkubwa zaidi unaoonyesha kuwa Paulo hakuikana imani yake ni kwamba aliendelea kukubaliwa na Yehova. Usiku huo baada ya Paulo kusema kwamba alikuwa Farisayo, Yesu alimwambia: “Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili katika Yerusalemu juu ya mambo yanayonihusu, vivyo hivyo utatoa ushahidi katika Roma pia.” Kwa kuwa Paulo alikubaliwa na Mungu, tunapaswa kufikia mkataa kwamba hakuikana imani yake ya Kikristo.—Matendo 23:11.