Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msaada Mkubwa wa Kutafsiri

Msaada Mkubwa wa Kutafsiri

Msaada Mkubwa wa Kutafsiri

MTUNGAJI wa Biblia, Yehova Mungu, anatamani kwamba habari njema kuhusu Ufalme wake zitangazwe kwa “kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufunuo 14:6) Anataka wanadamu wote wajue Neno lake lililoandikwa. Ili kufikia lengo hilo, Biblia imetafsiriwa katika lugha nyingi kuliko kitabu kingine chochote ulimwenguni. Watafsiri wengi wametumia wakati na jitihada nyingi ili kutafsiri mawazo ya Mungu katika lugha nyingine.

Lakini Biblia si kitabu cha kutafsiriwa tu. Mara nyingi, Biblia yenyewe imetumiwa kutafsiri maandishi mengine. Watafsiri wengi wamelinganisha jinsi ambavyo maneno ya Biblia yametafsiriwa katika lugha mbalimbali ili wapate tafsiri inayofaa ya maneno fulani. Sasa Biblia inatumiwa ili kuiwezesha kompyuta itafsiri.

Kwa kweli, ni vigumu kufanya kompyuta itokeze tafsiri nzuri. Wataalamu fulani hata wamehisi kwamba kompyuta haiwezi kutafsiri. Kwa nini? Kwa kuwa lugha si kupanga maneno tu. Kila lugha ina mpangilio wake wa maneno, kanuni, maneno na miundo isiyofuata kanuni hizo, misemo, na semi za mfano. Jitihada za kuingiza mambo yote hayo ndani ya kompyuta hazijafanikiwa. Karibu tafsiri zote ambazo zimefanywa na kompyuta zimekuwa ngumu sana kueleweka.

Hata hivyo, Franz Josef Och, mtaalamu mashuhuri wa tafsiri ya kompyuta, anasema kwamba sasa wataalamu wanatafuta njia mpya za kuziwezesha kompyuta kutafsiri. Tuseme unataka kutafsiri Kihindi katika Kiswahili. Kwanza, chukua maandishi fulani ambayo tayari yanapatikana katika lugha hizo mbili. Kisha ingiza maandishi hayo katika kompyuta. Kompyuta italinganisha maandishi ya lugha hizo mbili. Kwa mfano, kompyuta inapopata neno lilelile la Kihindi katika sehemu kadhaa, na kila mara inapotafuta neno au fungu la maneno linalofanana na hilo inapata neno la Kiswahili “nyumba,” kompyuta itatambua kwamba neno hilo la Kihindi ndiyo tafsiri ya neno “nyumba.” Na yaelekea kwamba maneno yaliyo karibu na nomino hiyo ni vivumishi kama vile “kubwa,” “ndogo,” “-a zamani,” au “mpya.” Hivyo, inaorodhesha tafsiri ya maneno na vifungu vya maneno. Baada ya kuingiza maneno ya kutosha, labda kwa siku chache au majuma machache, kompyuta inaweza kutumia maneno hayo kutafsiri maneno mengine. Ingawa tafsiri hiyo huenda ikawa ya hali ya chini kisarufi na katika muundo, kwa kawaida inaeleweka na inaeleza maana na mambo makuu.

Ubora wa tafsiri unategemea hasa wingi na ubora wa maandishi yaliyoingizwa ndani ya kompyuta. Kwa upande huo Biblia imekuwa msaada mkubwa. Imetafsiriwa kwa makini katika lugha nyingi, inapatikana kwa urahisi, nayo ina maandishi mengi sana. Hivyo, watafiti waliingiza maneno ya Biblia kwanza walipoitayarisha kompyuta kutafsiri lugha mpya.