Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tegemea Neno la Yehova

Tegemea Neno la Yehova

Tegemea Neno la Yehova

“Nimelitegemea neno lako.”—Zaburi 119:42.

1. Unajua nini kuhusu mwandikaji wa Zaburi ya 119 na mtazamo wake?

MTUNGAJI wa Zaburi ya 119 alilipenda sana neno la Yehova. Huenda mtungaji huyo alikuwa Hezekia, mwana wa mfalme wa Yuda. Hisia zinazoonyeshwa katika wimbo huu ulioongozwa na roho ya Mungu zinapatana na mtazamo wa Hezekia ambaye, alipokuwa mfalme wa Yuda, ‘aliendelea kushikamana na Yehova.’ (2 Wafalme 18:3-7) Zaburi hiyo inaonyesha wazi kwamba yule aliyeitunga alitambua uhitaji wake wa kiroho.—Mathayo 5:3.

2. Zaburi ya 119 inakazia nini, na wimbo huo umepangwaje?

2 Zaburi ya 119 inakazia umuhimu wa neno la Mungu, au ujumbe wake. * Yaelekea ili aweze kuikumbuka, mwandikaji aliitunga kama wimbo uliopangwa kialfabeti. Hivyo, alipanga mistari yake 176 kulingana na mfuatano wa herufi za Kiebrania. Katika Kiebrania cha awali, kila ubeti kati ya beti 22 za zaburi hiyo una mistari 8 inayoanza kwa herufi ileile. Zaburi hiyo inataja neno la Mungu, sheria, vikumbusho, njia, maagizo, masharti, amri, maamuzi ya hukumu, na maneno yake. Katika makala hii na ile inayofuata, Zaburi ya 119 itazungumziwa kulingana na tafsiri sahihi ya maandishi ya Kiebrania ya Biblia. Kutafakari mambo yaliyowapata watumishi wa Yehova wakati uliopita na sasa kwapaswa kuongeza ufahamu wetu kuhusu wimbo huo ulioongozwa na roho ya Mungu, na kufanya tuwe wenye shukrani zaidi kwa Neno la Mungu lililoandikwa, Biblia.

Tii Neno la Mungu Upate Furaha

3. Eleza na utoe mfano kuhusu maana ya kuwa bila kosa.

3 Ili tuwe na furaha ya kweli, tunahitaji kutembea katika sheria ya Mungu. (Zaburi 119:1-8) Tukifanya hivyo, Yehova atatuona kuwa ‘wasio na kosa katika njia yetu.’ (Zaburi 119:1) Kuwa wasio na kosa hakumaanishi kwamba sisi ni wakamilifu, lakini kunaonyesha kwamba tunajitahidi sana kufanya mapenzi ya Yehova Mungu. Noa “alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake,” kama mtu ‘aliyetembea pamoja na Mungu wa kweli.’ Mzee huyo mwaminifu wa ukoo pamoja na familia yake waliokoka Gharika kwa sababu aliishi kupatana na mapenzi ya Yehova. (Mwanzo 6:9; 1 Petro 3:20) Vivyo hivyo, tutaokoka mwisho wa ulimwengu huu ikiwa ‘tutashika kwa uangalifu maagizo ya Mungu’ na kufanya mapenzi yake.—Zaburi 119:4.

4. Tunahitaji kufanya nini ili kupata furaha na mafanikio?

4 Yehova hatatuacha kamwe ikiwa ‘tutamsifu kwa unyoofu wa moyo na kuendelea kushika masharti yake.’ (Zaburi 119:7, 8) Mungu hakumwacha Yoshua, kiongozi wa Waisraeli, ambaye alifuata shauri la ‘kukisoma kitabu cha sheria mchana na usiku ili aweze kufanya yote yaliyoandikwa ndani yake.’ Kwa kufanya hivyo, alifanikiwa naye akatenda kwa hekima. (Yoshua 1:8) Alipokaribia kufa, Yoshua alikuwa bado akimsifu Mungu, naye aliwakumbusha Waisraeli jambo hili: “Mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi.” (Yoshua 23:14) Kama vile Yoshua na mwandikaji wa Zaburi ya 119, tunaweza kupata furaha na mafanikio tunapomsifu Yehova na kulitegemea neno lake.

Neno la Yehova Hutusafisha

5. (a) Eleza jinsi tunavyoweza kuwa safi kiroho. (b) Kijana aliyefanya dhambi nzito anaweza kusaidiwaje?

5 Tunaweza kuwa safi kiroho tukijilinda kulingana na neno la Mungu. (Zaburi 119:9-16) Tunaweza kufanya hivyo hata kama wazazi wetu hawatuwekei mfano mzuri. Ingawa baba ya Hezekia alikuwa mwabudu wa sanamu, Hezekia ‘alisafisha njia yake’ labda ili asiathiriwe na ibada ya sanamu. Tuseme kijana anayemtumikia Mungu leo anafanya dhambi nzito. Toba, sala, msaada wa wazazi wake, na pia msaada wenye upendo wa wazee Wakristo unaweza kumsaidia awe kama Hezekia na ‘kusafisha njia yake na kujilinda.’—Yakobo 5:13-15.

6. Ni wanawake gani ‘waliosafisha njia yao na kujilinda kulingana na neno la Mungu’?

6 Rahabu na Ruthu ‘walisafisha njia yao’ ingawa waliishi muda mrefu kabla ya Zaburi ya 119 kutungwa. Rahabu alikuwa kahaba Mkanaani, lakini alipata kujulikana kwa sababu ya imani yake akiwa mwabudu wa Yehova. (Waebrania 11:30, 31) Ruthu Mmoabu, aliacha miungu yake, akamtumikia Yehova, na kufuata Sheria aliyowapa Waisraeli. (Ruthu 1:14-17; 4:9-13) Wanawake hao wawili wasio Waisraeli ‘walijilinda kulingana na neno la Mungu’ na walipata pendeleo zuri la kuwa nyanya za Yesu Kristo.—Mathayo 1:1, 4-6.

7. Danieli na vijana wengine watatu Waebrania walituwekea mfano gani mzuri katika kudumisha usafi wa kiroho?

7 “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea,” lakini vijana wanaweza kuwa na mwenendo safi, hata katika ulimwengu huu uliopotoka na ambao unatawaliwa na Shetani. (Mwanzo 8:21; 1 Yohana 5:19) Danieli na vijana wengine watatu Waebrania ‘walijilinda kulingana na neno la Mungu’ walipokuwa uhamishoni Babiloni. Kwa mfano, hawakujitia unajisi “kwa vyakula vitamu vya mfalme.” (Danieli 1:6-10) Wababiloni walikula wanyama wasio safi ambao hawakupaswa kuliwa kulingana na Sheria ya Musa. (Mambo ya Walawi 11:1-31; 20:24-26) Halikuwa jambo la kawaida kwao kutoa damu walipochinja wanyama, nao walivunja sheria ya Mungu kuhusu damu kwa kula nyama isiyotolewa damu. (Mwanzo 9:3, 4) Basi haishangazi kwamba wale Waebrania wanne hawakula vyakula vitamu vya mfalme! Vijana hao waliomwogopa Mungu walidumisha usafi wa kiroho na kutuwekea mfano mzuri.

Neno la Mungu Hutusaidia Kuwa Waaminifu

8. Tunahitaji kuwa na mtazamo na ujuzi gani ili tuielewe na kuifuata sheria ya Mungu?

8 Kulipenda neno la Mungu ni muhimu ili kuendelea kuwa waaminifu kwake. (Zaburi 119:17-24) Ikiwa sisi ni kama yule mtunga-zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu, tutatamani sana kuelewa “mambo ya ajabu” ya sheria ya Mungu. Daima ‘tutatamani maamuzi ya Yehova ya hukumu’ na kuonyesha kwamba ‘tunavipenda vikumbusho vyake.’ (Zaburi 119:18, 20, 24) Hata kama tulijiweka wakfu kwa Yehova hivi karibuni, je, ‘tumekuza tamaa kwa ajili ya maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno’? (1 Petro 2:1, 2) Tunahitaji kujua mafundisho ya msingi ya Biblia ili tuweze kuielewa na kuifuata sheria ya Mungu.

9. Tufanyeje iwapo matakwa ya wanadamu yanapingana na sheria ya Mungu?

9 Huenda ikawa tunavipenda vikumbusho vya Mungu, lakini tutafanyaje “wakuu” wakisema dhidi yetu kwa sababu fulani? (Zaburi 119:23, 24) Leo, mara nyingi wenye mamlaka hujaribu kutulazimisha kutanguliza sheria za kibinadamu badala ya sheria za Mungu. Tufanyeje iwapo matakwa ya wanadamu yanapingana na mapenzi ya Mungu? Kulipenda neno la Mungu kutatusaidia kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova. Kama mitume wa Yesu Kristo walioteswa, tutasema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

10, 11. Onyesha jinsi tunavyoweza kudumisha utimilifu wetu kwa Yehova katika hali ngumu sana.

10 Tunaweza kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova hata katika hali ngumu sana. (Zaburi 119:25-32) Ili tufaulu kudumisha utimilifu wetu kwa Mungu, tunapaswa kuwa tayari kufundishwa na kusali kwa bidii ili tupate maagizo yake. Lazima pia tuchague “njia ya uaminifu.”—Zaburi 119:26, 30.

11 Hezekia, ambaye huenda ndiye aliyeandika Zaburi ya 119, alichagua “njia ya uaminifu.” Ijapokuwa huenda alidharauliwa na watu wa nyumba ya mfalme na alizungukwa na waabudu wa uwongo, Hezekia alichagua kufuata njia hiyo. Yaelekea ‘nafsi yake ilikosa usingizi kwa sababu ya huzuni’ iliyotokana na hali hiyo. (Zaburi 119:28) Lakini Hezekia alimtegemea Mungu, alikuwa mfalme mzuri, na alifanya “yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova.” (2 Wafalme 18:1-5) Kwa kumtegemea Mungu, sisi pia tunaweza kuvumilia majaribu na kudumisha utimilifu wetu kwake.—Yakobo 1:5-8.

Neno la Yehova Hutupa Ujasiri

12. Unawezaje kutumia andiko la Zaburi 119:36, 37 katika maisha yako?

12 Kufuata mwongozo wa neno la Mungu hutupa ujasiri tunaohitaji ili kukabiliana na majaribu maishani. (Zaburi 119:33-40) Sisi hutafuta maagizo ya Yehova kwa unyenyekevu ili tuweze kushika sheria yake “kwa moyo wote.” (Zaburi 119:33, 34) Kama vile mtunga-zaburi, sisi humwomba Mungu hivi: “Uelekeze moyo wangu kwa vikumbusho vyako, wala si kwa faida,” yaani, faida isiyo ya haki. (Zaburi 119:36) Kama vile mtume Paulo, ‘tunajiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.’ (Waebrania 13:18) Mwajiri wetu akitaka tufanye jambo fulani la udanganyifu, tutajipa ujasiri na kufuata mwongozo wa Yehova, naye atabariki hatua hiyo. Yeye pia hutusaidia kudhibiti tamaa zetu mbovu. Kwa hiyo, acheni tusali hivi: “Uyafanye macho yangu yapite ili yasione jambo lisilofaa.” (Zaburi 119:37) Hatungependa kamwe kutamani jambo lolote lisilofaa ambalo Mungu anachukia. (Zaburi 97:10) Baadhi ya mambo ambayo sala hiyo hutusaidia kuepuka ni ponografia na kuwasiliana na roho waovu.—1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8.

13. Wanafunzi wa Yesu walioteswa walipataje ujasiri waliohitaji ili kuhubiri?

13 Ujuzi sahihi wa neno la Mungu hutupa uhakika wa kuhubiri kwa ujasiri. (Zaburi 119:41-48) Tunahitaji ujasiri ili ‘kumjibu yeye anayetushutumu.’ (Zaburi 119:42) Nyakati nyingine, huenda hali yetu ikafanana na ya wanafunzi wa Yesu walioteswa, ambao walisali: ‘Yehova, wawezeshe watumwa wako kuendelea kusema neno lako kwa ujasiri wote.’ Ilikuwaje waliposali? ‘Wote walijazwa roho takatifu na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri.’ Vivyo hivyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu hutupa ujasiri wa kusema neno lake.—Matendo 4:24-31.

14. Ni nini hutusaidia kuhubiri kwa ujasiri kama Paulo?

14 Ikiwa tunalipenda “neno la kweli” na ‘kuishika sheria ya Mungu daima,’ tutakuwa na ujasiri unaohitajiwa ili kuhubiri bila kuogopa kuaibika. (Zaburi 119:43, 44) Kujifunza kwa bidii Neno la Mungu lililoandikwa hutusaidia ‘kusema juu ya vikumbusho vyake mbele ya wafalme.’ (Zaburi 119:46) Sala na roho ya Yehova hutusaidia pia kusema mambo yanayofaa kwa njia inayofaa. (Mathayo 10:16-20; Wakolosai 4:6) Kwa ujasiri, Paulo aliwaeleza watawala wa karne ya kwanza vikumbusho vya Mungu. Kwa mfano, alimhubiria Feliksi, Gavana Mroma, ambaye ‘alimsikiliza juu ya imani katika Kristo Yesu.’ (Matendo 24:24, 25) Paulo pia alimhubiria Gavana Festo na Mfalme Agripa. (Matendo 25:22–26:32) Kwa msaada wa Yehova, sisi pia tunaweza kuhubiri kwa ujasiri, bila ‘kuionea aibu kamwe habari njema.’—Waroma 1:16.

Neno la Mungu Hutufariji

15. Neno la Mungu linawezaje kutufariji tunapodharauliwa na wengine?

15 Neno la Yehova hutufariji sikuzote. (Zaburi 119:49-56) Kuna nyakati ambazo tunahitaji sana kufarijiwa. Ingawa sisi husema kwa ujasiri tukiwa Mashahidi wa Yehova, nyakati nyingine watu “wenye kimbelembele,” yaani, wale wanaotenda kwa kimbelembele kuelekea Mungu, ‘hutudharau kupindukia.’ (Zaburi 119:51) Hata hivyo, tunaposali tunaweza kukumbuka mambo yenye kutia moyo yanayotajwa katika Neno la Mungu, na hivyo ‘kujipatia faraja.’ (Zaburi 119:52) Katikati ya sala, huenda tukakumbuka sheria au kanuni fulani ya Kimaandiko inayotupa faraja na ujasiri tunaohitaji katika hali ngumu.

16. Watumishi wa Mungu wamekataa kufanya nini licha ya mateso?

16 Watu wenye kimbelembele waliomdharau mtunga-zaburi ni Waisraeli, watu wa taifa lililowekwa wakfu kwa Mungu. Hiyo ni aibu iliyoje! Hata hivyo, tofauti nao, na tuazimie kutoiacha kamwe sheria ya Mungu. (Zaburi 119:51) Licha ya kuteswa na Wanazi na kupatwa na mateso mengine katika miaka iliyopita, maelfu ya watumishi wa Mungu wamekataa kuacha sheria na kanuni za Neno la Mungu. (Yohana 15:18-21) Si jambo gumu kumtii Yehova, kwa kuwa masharti yake ni kama muziki wenye kutufariji.—Zaburi 119:54; 1 Yohana 5:3.

Onyesha Shukrani kwa Ajili ya Neno la Yehova

17. Kuthamini neno la Mungu hutuchochea kufanya nini?

17 Sisi huonyesha shukrani kwa ajili ya neno la Mungu kwa kulifuata. (Zaburi 119:57-64) Mtunga-zaburi ‘aliahidi kushika maneno ya Yehova,’ na hata ‘aliamka katikati ya usiku ili kumshukuru Mungu kwa ajili ya maamuzi Yake ya hukumu ya uadilifu.’ Tukiamka usiku, huo ni wakati mzuri sana wa kumshukuru Mungu katika sala. (Zaburi 119:57, 62) Kuthamini neno la Mungu hutuchochea kutafuta mafundisho yake na hutufanya kuwa ‘wenzi wa wale wanaomwogopa Yehova,’ watu wanaomcha Mungu na kumheshimu. (Zaburi 119:63, 64) Hao tu ndio watu wazuri zaidi tunaoweza kushirikiana nao.

18. Yehova hujibuje sala zetu ‘kamba za waovu zinapotuzingira’?

18 Tunaposali kwa moyo wetu wote na kumwomba Yehova kwa unyenyekevu atufundishe, ‘tunautuliza uso wake’ ili atukubali. Tunahitaji kusali hasa wakati ‘kamba za waovu zinapotuzingira.’ (Zaburi 119:58, 61) Yehova anaweza kukata kamba za adui na kutuweka huru ili tuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Amefanya hivyo mara nyingi katika nchi ambako kazi yetu imepigwa marufuku.

Uwe na Imani Katika Neno la Mungu

19, 20. Inawezaje kuwa vema kuteseka?

19 Kuwa na imani katika Mungu na neno lake hutusaidia kuvumilia magumu na kufanya mapenzi yake. (Zaburi 119:65-72) Ingawa watu wenye kimbelembele ‘walimpaka uwongo,’ mtunga-zaburi aliimba: “Ni vema kwamba nimeteseka.” (Zaburi 119:66, 69, 71) Inawezaje kuwa vema kwa mtumishi yeyote wa Yehova kuteseka?

20 Tunapoteseka, bila shaka sisi humwomba Yehova kwa bidii, na hivyo kumkaribia zaidi. Huenda tukatumia wakati mwingi zaidi kujifunza Neno la Mungu lililoandikwa na kujitahidi zaidi kulifuata. Jambo hilo hutuletea furaha zaidi. Lakini vipi ikiwa tutaonyesha tabia zisizofaa, kama vile kuwa na kiburi na kukosa subira tunapopatwa na matatizo? Tukisali kwa bidii na kupata msaada wa Neno la Mungu na roho yake, tunaweza kushinda kasoro hizo na ‘kujivika utu mpya’ kwa ukamili zaidi. (Wakolosai 3:9-14) Isitoshe, imani yetu huimarishwa tunapovumilia matatizo. (1 Petro 1:6, 7) Paulo alinufaika kutokana na dhiki zilizompata kwa sababu zilifanya amtegemee Yehova zaidi. (2 Wakorintho 1:8-10) Je, sisi huacha mateso yatunufaishe?

Mtegemee Yehova Sikuzote

21. Ni nini ambacho hutokea Mungu anapowatia aibu wenye kimbelembele?

21 Neno la Mungu hutupa sababu nzuri ya kumtegemea. (Zaburi 119:73-80) Tukimtegemea Muumba wetu kikweli, hatutakuwa na sababu ya kuaibika. Hata hivyo, kwa sababu ya matendo ya wengine, tunahitaji faraja na huenda tukahisi kwamba tunataka kusali hivi: “Wenye kimbelembele na waone aibu.” (Zaburi 119:76-78) Yehova anapowatia aibu watu hao, hilo hufunua njia zao mbovu na hutakasa jina lake takatifu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba wale wanaowatesa watu wa Mungu hawapati manufaa yoyote. Kwa mfano, hawawezi wala hawataweza kuwamaliza Mashahidi wa Yehova ambao humtegemea Mungu kwa moyo wao wote.—Methali 3:5, 6.

22. Ni katika maana gani mtunga-zaburi alikuwa “kama kiriba katika moshi”?

22 Neno la Mungu hufanya tumtegemee zaidi tunapoteswa. (Zaburi 119:81-88) Kwa sababu wenye kimbelembele walimtesa, mtunga-zaburi alihisi “kama kiriba katika moshi.” (Zaburi 119:83, 86) Nyakati za Biblia, viriba vilivyotengenezwa kwa ngozi ya wanyama vilitumiwa kuweka maji, divai, au vitu vingine vya majimaji. Wakati ambapo havitumiwi, viriba hivyo vinaweza kuwa vidogo vinapowekwa karibu na moto katika chumba kilichojaa moshi. Je, magumu au mateso hukufanya uhisi “kama kiriba katika moshi”? Ikiwa ndivyo, mtegemee Yehova na kusali: “Unihifadhi hai kulingana na fadhili zako zenye upendo, ili nipate kushika kikumbusho cha kinywa chako.”—Zaburi 119:88.

23. Tumejifunza nini kwa kuipitia Zaburi 119:1-88, nasi tunaweza kujiuliza nini tunapongojea kujifunza Zaburi 119:89-176?

23 Mambo ambayo tumezungumzia katika sehemu ya kwanza ya Zaburi ya 119 yanadhihirisha kwamba Yehova huwaonyesha watumishi wake fadhili zenye upendo kwa sababu wanalitegemea neno lake na wanapenda sheria, vikumbusho, na amri zake. (Zaburi 119:16, 47, 64, 70, 77, 88) Yeye hufurahi kwamba wale ambao wamejitoa kwake hujilinda kulingana na neno lake. (Zaburi 119:9, 17, 41, 42) Unapongojea kujifunza sehemu inayobaki ya zaburi hii nzuri, unaweza kujiuliza, ‘Je, mimi huacha neno la Yehova liangaze barabara yangu?’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kinachozungumziwa hapa ni ujumbe wa Yehova, bali si Biblia nzima, yaani, Neno la Mungu.

Ungejibuje?

• Tunahitaji kufanya nini ili kupata furaha ya kweli?

• Neno la Yehova hutusaidiaje kuwa safi kiroho?

• Neno la Mungu hutupa ujasiri na faraja katika njia zipi?

• Kwa nini tuwe na imani katika Yehova na neno lake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ruthu, Rahabu, na wale vijana Waebrania ambao walikuwa uhamishoni Babiloni ‘walijilinda kulingana na neno la Mungu’

[Picha katika ukurasa wa 12]

Paulo ‘alisema juu ya vikumbusho vya Mungu mbele ya wafalme’ kwa ujasiri