Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fundisho la Ufufuo Linakuhusu

Fundisho la Ufufuo Linakuhusu

Fundisho la Ufufuo Linakuhusu

“Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—MATENDO 24:15.

1. Ufufuo ulipataje kuwa suala la kujadiliwa mbele ya Sanhedrini?

MTUME Paulo alikuwa Yerusalemu mwishoni mwa safari yake ya tatu ya umishonari mwaka wa 56 W.K. Baada ya kukamatwa na Waroma, aliruhusiwa kwenda mbele ya Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi. (Matendo 22:29, 30) Paulo alipowatazama washiriki wa mahakama hiyo, aliona Masadukayo na Mafarisayo. Kulikuwa na tofauti moja kubwa sana kati ya vikundi hivyo viwili. Mafarisayo waliamini kuna ufufuo, nao Masadukayo walisema hakuna ufufuo. Ili kuonyesha msimamo wake kuhusu suala hilo, Paulo alisema: “Wanaume, akina ndugu, mimi ni Farisayo, mwana wa Mafarisayo. Ninahukumiwa juu ya tumaini la ufufuo wa wafu.” Maneno hayo ya Paulo yalisababisha mvurugo katika mahakama hiyo!—Matendo 23:6-9.

2. Kwa nini Paulo alikuwa tayari kutetea imani yake kuhusu ufufuo?

2 Miaka kadhaa awali, alipokuwa njiani kwenda Damasko, Paulo aliona maono na kusikia sauti ya Yesu. Paulo hata alimuuliza Yesu: “Nitafanya nini, Bwana?” Yesu akamjibu: “Simama, ondoka uende Damasko, na huko utaambiwa kila kitu ambacho umewekewa kufanya.” Paulo alipofika Damasko, Anania, mwanafunzi Mkristo mwenye kujali, alimtafuta Paulo na kumweleza hivi: “Mungu wa mababu zetu amekuchagua upate kujua mapenzi yake na kumwona yule Aliye mwadilifu [Yesu aliyefufuliwa] na kuisikia sauti ya kinywa chake.” (Matendo 22:6-16) Basi, haishangazi kwamba Paulo alikuwa tayari kutetea imani yake kuhusu ufufuo.—1 Petro 3:15.

Atangaza Waziwazi Tumaini la Ufufuo

3, 4. Paulo aliliteteaje fundisho la ufufuo kwa uthabiti, na mfano wake unaweza kutufunza nini?

3 Baadaye, Paulo alipelekwa mbele ya Gavana Feliksi. Pindi hiyo, Tertulo, “msemaji wa hadharani” aliyewasilisha kesi ya Wayahudi dhidi ya Paulo, alimshtaki kuwa mchochezi wa uasi na kiongozi wa madhehebu fulani. Kwa kujibu, Paulo alitangaza hivi waziwazi: “Ninakiri jambo hili kwako, kwamba, kulingana na ile njia wanayoiita ‘madhehebu,’ kwa namna hii mimi ninatoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa mababu zangu.” Kisha akaeleza suala kuu lililohusika kwa kusema: “Nina tumaini kwa Mungu, tumaini ambalo watu hawa pia wanalo, kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 23:23, 24; 24:1-8, 14, 15.

4 Miaka miwili hivi baadaye, Porkio Festo, aliyekuwa Gavana baada ya Feliksi, alimwalika Mfalme Herode Agripa ajiunge naye kumhoji Paulo, aliyekuwa mfungwa. Festo alieleza kwamba wale waliomshtaki Paulo walikataa dai lake kwamba “mtu fulani anayeitwa Yesu aliyekuwa amekufa . . . alikuwa hai.” Paulo alijitetea kwa kuuliza hivi: “Kwa nini mnaamua kwamba ni jambo lisiloaminika kwamba Mungu hufufua wafu?” Kisha akasema: “Kwa sababu nimeupata msaada kutoka kwa Mungu ninaendelea mpaka leo kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia, lakini bila kusema lolote ila mambo ambayo Manabii na vilevile Musa walisema yatatukia, kwamba Kristo angeteseka na, akiwa wa kwanza kufufuliwa kutoka kwa wafu, angetangaza nuru kwa watu hawa na pia kwa mataifa.” (Matendo 24:27; 25:13-22; 26:8, 22, 23) Paulo alikuwa mteteaji thabiti sana wa tumaini la ufufuo. Kama Paulo, sisi pia tunaweza kutangaza kwa uhakika kwamba kutakuwa na ufufuo. Lakini tunaweza kutazamia watu waitikieje? Yaelekea itikio litakuwa sawa na lile ambalo Paulo alipata.

5, 6. (a) Watu waliitikiaje mitume walipotetea tumaini la ufufuo? (b) Tunapoendelea kuwaeleza watu kuhusu tumaini letu katika ufufuo, ni jambo gani lililo muhimu?

5 Fikiria mambo yaliyotukia mapema katika safari ya pili ya Paulo ya umishonari (yapata mwaka wa 49-52 W.K.) alipotembelea jiji la Athene. Alijadiliana na watu walioamini katika miungu mingi na kuwahimiza wafikirie kusudi la Mungu la kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye Amemweka rasmi. Mwanamume huyo ni Yesu. Paulo alieleza kwamba Mungu alitoa uhakikisho wa jambo hilo kwa kumfufua Yesu. Watu waliitikiaje? Tunasoma hivi: “Basi, waliposikia juu ya ufufuo wa wafu, wengine kati yao wakaanza kudhihaki, huku wengine wakisema: ‘Tutakusikiliza tena juu ya jambo hili wakati mwingine.’”—Matendo 17:29-32.

6 Watu hao waliitikia kama wale waliowasikiliza Petro na Yohana muda mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K. Kwa mara nyingine tena, Masadukayo walihusika sana katika ubishi huo. Andiko la Matendo 4:1-4 linaeleza kilichotukia: “Sasa hao wawili walipokuwa wakisema na watu, wakuu wa makuhani na kapteni wa hekalu na Masadukayo wakawajia, wakiwa wameudhika kwa sababu walikuwa wakiwafundisha watu na walikuwa wakiutangaza waziwazi ufufuo kutoka kwa wafu kwa kisa cha Yesu.” Hata hivyo, wengine waliitikia vizuri. “Wengi kati ya wale waliokuwa wamesikiliza maneno hayo wakaamini, na hesabu ya wanaume ikawa karibu elfu tano.” Tunaweza kutazamia watu waitikie kwa njia tofauti-tofauti tunapowaeleza kuhusu tumaini la ufufuo. Kwa hiyo, ni muhimu tuimarishe imani yetu katika fundisho hilo.

Imani na Ufufuo

7, 8. (a) Kama inavyoonyeshwa katika barua iliyoandikiwa kutaniko la Korintho katika karne ya kwanza, imani inawezaje kuwa bure? (b) Kulielewa tumaini la ufufuo kwa usahihi hutofautishaje Wakristo wa kweli na wa uwongo?

7 Si Wakristo wote katika karne ya kwanza W.K. waliokubali kwa urahisi tumaini la ufufuo. Baadhi ya Wakristo hao walikuwa katika kutaniko la Korintho. Paulo aliwaandikia hivi: “Niliwapa ninyi, kati ya mambo ya kwanza, yale niliyopokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko.” Kisha Paulo akathibitisha jambo hilo kwa kusema kwamba Kristo aliyefufuliwa “aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano,” naye akaongeza kwamba wengi wao bado walikuwa hai. (1 Wakorintho 15:3-8) Paulo pia alitoa hoja hii: “Ikiwa Kristo anahubiriwa kwamba amefufuliwa kutoka kwa wafu, kwa nini wengine kati yenu wanasema hakuna ufufuo wa wafu? Ikiwa, kwa kweli, hakuna ufufuo wa wafu, basi Kristo hakufufuliwa. Lakini ikiwa Kristo hakufufuliwa, hakika kuhubiri kwetu ni bure, na imani yetu ni bure.”—1 Wakorintho 15:12-14.

8 Kwa kweli, fundisho la ufufuo ni muhimu sana hivi kwamba imani ya Kikristo ni bure ikiwa ufufuo haukubaliwi kuwa jambo halisi. Naam, kuuelewa ufufuo kwa usahihi hutofautisha Wakristo wa kweli na wa uwongo. (Mwanzo 3:4; Ezekieli 18:4) Kwa hiyo, Paulo anataja ufufuo kuwa sehemu ya “fundisho la msingi” la Ukristo. Na tuazimie ‘kusonga mbele kuelekea ukomavu.’ Paulo anatuhimiza hivi: “Na hili tutalifanya, ikiwa kwa kweli Mungu ataruhusu.”—Waebrania 6:1-3.

Tumaini la Ufufuo

9, 10. Biblia inamaanisha nini inapotaja ufufuo?

9 Ili kuimarisha imani yetu katika ufufuo, acheni tuchunguze maswali haya: Biblia inamaanisha nini inapotaja ufufuo? Fundisho la ufufuo huonyeshaje kwamba Yehova ana upendo mwingi sana? Majibu ya maswali hayo yatatusaidia kuwafundisha wengine na pia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.—2 Timotheo 2:2; Yakobo 4:8.

10 “Ufufuo” ni tafsiri ya neno la Kigiriki ambalo kihalisi linamaanisha “kusimama tena.” Neno hilo linahusisha nini? Kulingana na Biblia, tumaini la ufufuo ni usadikisho kwamba mtu aliyekufa anaweza kuishi tena. Pia Biblia inaonyesha kwamba mtu hufufuliwa akiwa na mwili wa kibinadamu ikiwa ana tumaini la kuishi duniani, au mwili wa roho ikiwa ana tumaini la kuishi mbinguni. Tunavutiwa na upendo, hekima, na nguvu ambazo Yehova anaonyesha katika tumaini hili zuri la ufufuo.

11. Watumishi wa Mungu watiwa-mafuta wanaweza kutazamia nini kuhusiana na ufufuo?

11 Kama vile Yesu, ndugu zake watiwa-mafuta hupewa mwili wa roho wanapofufuliwa ambao unafaa kwa utumishi wao mbinguni. (1 Wakorintho 15:35-38, 42-53) Yesu na ndugu zake watiwa-mafuta watatawala katika Ufalme wa Kimasihi ambao utaifanya dunia kuwa Paradiso. Watiwa-mafuta wanakuwa ukuhani wa kifalme chini ya Yesu, Kuhani Mkuu. Watatumia faida za dhabihu yake ya fidia kwa ajili ya wanadamu katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Waebrania 7:25, 26; 9:24; 1 Petro 2:9; Ufunuo 22:1, 2) Sasa Wakristo watiwa-mafuta ambao bado wako duniani wanatamani kuendelea kuwa na kibali cha Mungu. Wanapokufa, wanapokea “thawabu” yao kwa kufufuliwa ili waishi mbinguni wakiwa viumbe wa roho wasioweza kufa. (2 Wakorintho 5:1-3, 6-8, 10; 1 Wakorintho 15:51, 52; Ufunuo 14:13) Paulo aliandika: “Ikiwa tumeungana pamoja naye katika mfano wa kifo chake, hakika sisi pia tutaunganishwa pamoja naye katika mfano wa ufufuo wake.” (Waroma 6:5) Lakini vipi wale ambao watafufuliwa kuishi tena duniani wakiwa wanadamu? Tumaini la ufufuo linawezaje kuwasaidia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu? Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wa Abrahamu.

Ufufuo na Urafiki Pamoja na Yehova

12, 13. Abrahamu alikuwa na sababu gani nzuri sana ya kuamini katika ufufuo?

12 Abrahamu, anayetajwa kuwa “rafiki ya Yehova,” alikuwa na imani ya pekee. (Yakobo 2:23) Paulo alitaja imani ya Abrahamu mara tatu alipowataja wanaume na wanawake wenye imani katika sura ya 11 ya kitabu cha Waebrania. (Waebrania 11:8, 9, 17) Anapomtaja Abrahamu mara ya tatu anakazia imani ambayo Abrahamu alionyesha wakati ambapo, kwa utii, alimtayarisha mwanawe Isaka ili amtoe akiwa dhabihu. Abrahamu alisadiki kwamba Yehova hangekosa kutimiza ahadi yake ya kumpa uzao kupitia Isaka. Hata kama Isaka angekufa kwa kutolewa akiwa dhabihu, Abrahamu “alifikia uamuzi kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumfufua hata kutoka kwa wafu.”

13 Hivyo, Yehova alipoona imani yenye nguvu ya Abrahamu, aliandaa mnyama atolewe akiwa dhabihu badala ya Isaka. Hata hivyo, kisa cha Isaka kinatoa mfano wa ufufuo, kama Paulo alivyoeleza: “Kutoka huko [Abrahamu] alimpokea [Isaka] pia kwa njia ya mfano.” (Waebrania 11:19) Isitoshe, tayari Abrahamu alikuwa na sababu nzuri sana ya kuamini ufufuo. Je, Yehova hakurudisha nguvu za uzazi za Abrahamu wakati yeye na mke wake Sara walipompata mwana wao Isaka wakiwa wazee?—Mwanzo 18:10-14; 21:1-3; Waroma 4:19-21.

14. (a) Kulingana na Waebrania 11:9, 10, Abrahamu alingojea nini? (b) Ni jambo gani ambalo ni lazima litukie kwa Abrahamu ili apate baraka za Ufalme katika ulimwengu mpya? (c) Tunawezaje kupata baraka za Ufalme?

14 Paulo alitaja kwamba Abrahamu alikuwa mkaaji mgeni, aliyeishi katika mahema “akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.” (Waebrania 11:9, 10) Hilo ni jiji la mfano, wala si jiji halisi kama Yerusalemu, ambako hekalu la Mungu lilikuwa. Jiji hilo ni Ufalme wa mbinguni wa Mungu ambao mtawala wake ni Kristo Yesu na watawala wenzake 144,000. Wanapokuwa katika utukufu wao mbinguni, watawala hao 144,000 pia wanaitwa “jiji takatifu, Yerusalemu Jipya,” “bibi-arusi” wa Kristo. (Ufunuo 21:2) Katika mwaka wa 1914, Yehova alimtawaza Yesu kuwa Mfalme wa Kimasihi wa Ufalme wa mbinguni na kumwamuru atawale katikati ya adui zake. (Zaburi 110:1, 2; Ufunuo 11:15) Ili kupata baraka za utawala wa Ufalme, lazima Abrahamu, “rafiki ya Yehova,” aishi tena. Vivyo hivyo, ili tupate baraka za Ufalme, lazima tuwe hai katika ulimwengu mpya wa Mungu tukiwa sehemu ya umati mkubwa utakaookoka Har–Magedoni au wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu. (Ufunuo 7:9, 14) Lakini ni nini msingi wa tumaini la ufufuo?

Upendo wa Mungu Ndio Msingi wa Tumaini la Ufufuo

15, 16. (a) Unabii wa kwanza katika Biblia hutuwekeaje msingi wa kuwa na tumaini la ufufuo? (b) Imani katika ufufuo hutuwezeshaje kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova?

15 Kwa sababu ya uhusiano wetu wa karibu pamoja na Baba yetu mwenye upendo wa mbinguni, imani yetu yenye nguvu kama ile ya Abrahamu, na utii wetu kwa amri za Mungu, Yehova hututangaza kuwa waadilifu na kutuona kuwa rafiki zake. Hilo hutuwezesha kunufaika na utawala wa Ufalme. Naam, unabii wa kwanza kabisa kuandikwa katika Neno la Mungu, kwenye Mwanzo 3:15, hutuwekea msingi wa kuwa na tumaini la ufufuo na urafiki pamoja na Mungu. Unabii huo unataja kupondwa kwa kichwa cha Shetani na pia kutiwa jeraha kwa kisigino cha Uzao wa mwanamke wa Mungu. Yesu alitiwa jeraha kwa njia ya mfano alipokufa kwenye mti wa mateso. Ufufuo wake katika siku ya tatu uliponya kidonda hicho na kumwezesha kuchukua hatua madhubuti dhidi ya “yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi.”—Waebrania 2:14.

16 Paulo anatukumbusha kwamba “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Waroma 5:8) Kuthamini fadhili hizo zisizostahiliwa hutuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yesu na Baba yetu wenye upendo wa mbinguni.—2 Wakorintho 5:14, 15.

17. (a) Ayubu alikuwa na tumaini gani? (b) Andiko la Ayubu 14:15 linafunua nini kumhusu Yehova, na jambo hilo linakufanya uhisije?

17 Ayubu, mtu mwaminifu aliyeishi kabla ya Ukristo, alitarajia kufufuliwa pia. Shetani alimtesa sana. Ayubu alikuwa tofauti na rafiki zake wa uwongo ambao hawakutaja ufufuo kamwe. Alifarijiwa na tumaini hilo la ufufuo na kuuliza: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Akijibu swali lake mwenyewe, Ayubu alisema: “Mimi nitangojea siku zote za kazi yangu ya kulazimishwa, mpaka kitulizo changu kije.” Alipozungumza na Mungu wake Yehova, Ayubu alisema hivi: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.” Kuhusu hisia za Muumba wetu mwenye upendo, Ayubu alisema: “Utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Naam, Yehova anatazamia kwa hamu wakati ambapo waaminifu watakuwa hai tena kupitia ufufuo. Kwa kweli, jambo hilo hutuvuta kwake tunapotafakari kuhusu upendo na fadhili zisizostahiliwa ambazo yeye hutuonyesha ingawa sisi si wakamilifu!—Waroma 5:21; Yakobo 4:8.

18, 19. (a) Danieli ana tazamio gani la kuishi tena? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

18 Nabii Danieli, ambaye alitajwa na malaika wa Mungu kuwa “mtu mwenye kutamanika sana,” alimtumikia Mungu kwa uaminifu kwa muda mrefu. (Danieli 10:11, 19) Alidumisha utimilifu wake kwa Yehova tangu apelekwe uhamishoni mwaka wa 617 K.W.K., hadi alipokufa muda fulani baada ya kupata maono mwaka wa 536 K.W.K., ambao ulikuwa mwaka wa tatu wa utawala wa Koreshi, mfalme wa Uajemi. (Danieli 1:1; 10:1) Wakati fulani katika mwaka huo wa tatu wa utawala wa Koreshi, Danieli aliona maono kuhusu mfuatano wa serikali za ulimwengu ambao utakoma wakati wa dhiki kuu inayokuja. (Danieli 11:1–12:13) Kwa kuwa hakuweza kuelewa maono hayo kikamili, Danieli alimuuliza hivi malaika aliyetumwa kumwonyesha maono hayo: “Ee bwana wangu, mwisho wa mambo hayo utakuwa nini?” Malaika huyo alimjibu kwa kutaja “wakati wa mwisho” ambapo “wale walio na ufahamu wataelewa.” Danieli mwenyewe alikuwa na tazamio gani? Malaika huyo alimwambia: “Utapumzika, lakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa zile siku.” (Danieli 12:8-10, 13) Danieli atarudi “katika ufufuo wa walio waadilifu,” wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo.—Luka 14:14.

19 Tunaishi katika umalizio wa wakati wa mwisho na sasa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo uko karibu zaidi kuanza kutawala kuliko wakati tulipoanza kuamini. Kwa hiyo, lazima tujiulize, ‘Je, nitakuwapo katika dunia mpya ili kuungana na Abrahamu, Ayubu, Danieli, na wanaume na wanawake wengine waaminifu?’ Tutakuwapo ikiwa tutaendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kutii amri zake. Katika makala yetu inayofuata, tutachunguza tumaini la ufufuo kwa undani zaidi ili tupate kujua ni nani watakaofufuliwa.

Je, Unakumbuka?

• Watu waliitikiaje Paulo alipotangaza tumaini lake katika ufufuo?

• Kwa nini tumaini la ufufuo hutofautisha Wakristo wa kweli na wa uwongo?

• Tunajuaje kwamba Abrahamu, Ayubu, na Danieli waliamini ufufuo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Paulo alitangaza tumaini la ufufuo kwa uhakika alipopelekwa mbele ya Gavana Feliksi

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kwa nini Abrahamu aliamini ufufuo?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ayubu alifarijiwa na tumaini la ufufuo

[Picha katika ukurasa wa 12]

Danieli atafufuliwa wakati wa ufufuo wa waadilifu