Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ingawa Mimi Ni Dhaifu, Nina Nguvu

Ingawa Mimi Ni Dhaifu, Nina Nguvu

Simulizi la Maisha

Ingawa Mimi Ni Dhaifu, Nina Nguvu

LIMESIMULIWA NA LEOPOLD ENGLEITNER

Ofisa mmoja wa Hitler alichomoa bastola yake, akaiweka kwenye kichwa changu, na kuniuliza: “Je, uko tayari kufa? Nitakupiga risasi kwa sababu wewe ni bure kabisa.” Kisha nikajibu kwa sauti imara, “Niko tayari.” Nilijitayarisha, nikafunga macho, na kungoja afyatue risasi, lakini hakufanya hivyo. “Mpumbavu wewe, hata unataka kufa!” akapiga kelele, huku akiondoa bastola kwenye kichwa changu. Ilikuwaje nikajikuta katika hali hiyo hatari?

NILIZALIWA Julai 23, 1905, katika mji wa Aigen-Voglhub, kwenye Milima ya Alps huko Austria. Baba yangu alikuwa mfanyakazi wa kiwanda cha kupasulia mbao, naye mama alikuwa binti ya mkulima. Mimi ndiye niliyekuwa mtoto wa kwanza. Wazazi wangu walikuwa maskini lakini walikuwa wafanyakazi wenye bidii. Katika miaka yangu ya utotoni, niliishi huko Bad Ischl, karibu na Salzburg, katikati ya maziwa na milima yenye kuvutia sana.

Nilipokuwa mtoto, nilifikiri mara nyingi kuhusu ukosefu wa haki maishani, si kwa sababu tu wazazi wangu walikuwa maskini, bali pia kwa sababu nilizaliwa na tatizo la uti wa mgongo. Hali hiyo ilisababisha maumivu ya mgongo na ilikuwa vigumu kwangu kusimama wima. Shuleni, sikuruhusiwa kufanya mazoezi ya mwili na hivyo nilidhihakiwa sana na wanafunzi wenzangu.

Mwishoni mwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, muda mfupi tu kabla ya kufikia umri wa miaka 14, niliamua kutafuta kazi ili kuepuka umaskini. Niliumwa na njaa mara nyingi, na nilikuwa dhaifu wakati fulani kwa sababu ya homa kali iliyosababishwa na homa ya Hispania, ambayo iliua mamilioni ya watu. Nilipoomba kazi, wakulima wengi walikuwa wakiniambia: “Hatuna kazi kwa ajili ya mtu dhaifu kama wewe.” Hata hivyo, mkulima mmoja alinipa kazi.

Kuchochewa na Upendo wa Mungu

Hata ingawa Mama alikuwa Mkatoliki mwenye bidii, sikwenda kanisani mara nyingi, hasa kwa sababu baba yangu hakushikilia sana mambo ya dini. Kwa upande wangu nilikasirishwa na ibada ya sanamu, ambayo ilifanywa waziwazi katika Kanisa Katoliki.

Siku moja mnamo Oktoba 1931, rafiki mmoja aliniomba niandamane naye kwenye mkutano fulani wa kidini uliofanywa na Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Kwenye mkutano huo, nilipata majibu ya Biblia kuhusu maswali muhimu, kama vile: Je, ibada ya sanamu inampendeza Mungu? (Kutoka 20:4, 5) Je, kuna moto wa mateso? (Mhubiri 9:5) Je, wafu watafufuliwa?—Yohana 5:28, 29.

Nilivutiwa sana na wazo la kwamba Mungu haungi mkono vita vya kikatili vya wanadamu, hata ikiwa vinapiganwa kwa jina Lake. Nilijifunza kwamba “Mungu ni upendo” na kwamba ana jina tukufu, yaani, Yehova. (1 Yohana 4:8; Zaburi 83:18) Nilichochewa kujua kwamba kupitia Ufalme wa Yehova, wanadamu wataweza kuishi milele kwa furaha katika paradiso itakayoenea duniani pote. Pia nilijifunza kuhusu tazamio zuri linalotolewa kwa wanadamu fulani wasio wakamilifu ambao wamechaguliwa na Mungu ili watawale pamoja na Yesu katika Ufalme wa Mungu huko mbinguni. Nilikuwa tayari kufanya yote niwezayo kwa ajili ya Ufalme huo. Hivyo, mnamo Mei 1932, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Ilihitaji ujasiri ili kubatizwa kwa sababu kulikuwa na chuki ya kidini katika nchi ya Austria, ambako dini ya Katoliki ndiyo tu iliyokubaliwa.

Kukabili Dharau na Upinzani

Wazazi wangu walishtuka sana nilipoacha kanisa, naye kasisi akafanya haraka kueneza habari hiyo jukwaani. Majirani walikuwa wakitema mate chini mbele yangu ili kunionyesha dharau. Hata hivyo, niliazimia kuwa mhudumu wa wakati wote, nami nikaanza upainia mnamo Januari 1934.

Kwa kuwa chama cha Nazi kiliendelea kuwa na uvutano mkubwa katika jimbo letu, hali ya kisiasa ilizidi kuwa mbaya. Nilipokuwa painia huko Styria katika Bonde la Enns, sikuzote nilifuatwa na polisi, na ilinibidi “kujihadhari kama nyoka.” (Mathayo 10:16) Tangu mwaka wa 1934 hadi 1938, niliteswa mara nyingi. Ijapokuwa sikuwa na kazi, nilinyimwa malipo yanayopewa watu wasio na kazi, na kwa sababu ya kazi yangu ya kuhubiri nilifungwa gerezani mara kadhaa kwa muda mfupi na pia nikafungwa kwa muda mrefu mara nne.

Vikosi vya Hitler Vyateka Austria

Mnamo Machi 1938, vikosi vya Hitler vilivamia Austria. Baada ya siku chache tu, watu zaidi ya 90,000, yaani asilimia 2 hivi ya watu wazima walioshtakiwa kwa kupinga utawala wa Nazi, walikamatwa na kutiwa gerezani au kupelekwa kwenye kambi za mateso. Kwa kadiri fulani, Mashahidi wa Yehova walikuwa tayari kwa ajili ya yale ambayo yangetukia. Katika kiangazi cha 1937, washiriki kadhaa wa kutaniko letu walisafiri kwa baiskeli kilometa 350 kwenda Prague ili kuhudhuria kusanyiko la kimataifa. Kwenye kusanyiko hilo walisikia kuhusu ukatili ambao waamini wenzao walikuwa wakitendewa huko Ujerumani. Kwa wazi, sasa ilikuwa zamu yetu.

Tangu vikosi vya Hitler vivamie Austria, mikutano na kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova ilifanywa kwa siri. Ingawa vichapo vya Biblia viliingizwa kwa siri kupitia mpaka wa Uswisi, havikutosha kwa kila mtu. Hivyo, Wakristo wenzetu huko Vienna walichapisha vichapo kwa siri. Mara nyingi nilifanya kazi ya kuwapelekea Mashahidi wengine vichapo.

Napelekwa Kwenye Kambi ya Mateso

Aprili 4, 1939, mimi na Wakristo wenzangu watatu tulikamatwa na askari wa Gestapo tulipokuwa tukiadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo huko Bad Ischl. Sote tulisafirishwa kwa gari hadi kwenye kituo kikuu cha polisi huko Linz. Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kusafiri kwa gari, lakini nilikuwa na wasiwasi hivi kwamba sikuweza kufurahia safari hiyo. Huko Linz, nilihojiwa kwa ukali, lakini sikuikana imani yangu. Baada ya miezi mitano, nilipelekwa mbele ya hakimu huko Upper Austria. Bila kutarajia, mashtaka ya uhalifu yaliondolewa. Hata hivyo, huo haukuwa mwisho wa mateso yangu. Wenzangu watatu walipelekwa kwenye kambi ya mateso ambako walikufa wakiwa waaminifu.

Niliwekwa chini ya ulinzi, na Oktoba 5, 1939, nilijulishwa kwamba ningepelekwa kwenye kambi ya mateso ya Buchenwald huko Ujerumani. Gari-moshi la pekee lilikuwa likitungoja kwenye kituo cha Linz. Mabehewa yake yalikuwa na vyumba vilivyotosha watu wawili tu. Nilikuwa katika chumba kimoja na Dakt. Heinrich Gleissner, aliyekuwa gavana wa Upper Austria.

Mimi na Dakt. Gleissner tulianza kuongea mambo yenye kupendeza. Alihangaikia sana hali yangu mbaya na alisikitika kwamba hata wakati alipokuwa gavana, Mashahidi wa Yehova walikabili matatizo mengi ya kisheria katika jimbo lake. Aliniambia hivi kwa kusikitika: “Bwana Engleitner, maji yakimwagika hayazoleki, lakini naomba msamaha. Inaonekana kwamba serikali yetu ilikuwa na hatia ya kupotosha haki. Mkihitaji msaada wowote, nitakuwa tayari kuwasaidia.” Tulikutana tena baada ya vita. Alinisaidia kupata malipo ya uzeeni kutoka kwa serikali kwa ajili ya watu walioathiriwa na chama cha Nazi.

“Nitakupiga Risasi”

Oktoba 9, 1939, nilifika kwenye kambi ya mateso ya Buchenwald. Muda mfupi baadaye, msimamizi wa kambi alijulishwa kwamba Shahidi mmoja alikuwa kati ya wafungwa waliofika, nami nikawa shabaha yake. Alinipiga sana. Kisha, baada ya kutambua kwamba hangeweza kunifanya nikane imani yangu, aliniambia: “Engleitner, nitakupiga risasi. Lakini kabla ya kufanya hivyo, ninakuruhusu uwaandikie wazazi wako kadi ya kuwaaga.” Nilifikiria maneno ya kufariji ambayo ningeweza kuwaandikia wazazi wangu, lakini kila nilipojaribu kuandika, alinigonga mkono na kufanya nisiweze kuandika vizuri. Alinidhihaki hivi: “Mpumbavu huyu! Hata hajui kuandika vizuri. Lakini hiyo haimzuii asiisome Biblia.”

Baadaye, msimamizi huyo alichomoa bastola yake, akaiweka kwenye kichwa changu, na kunifanya niamini kwamba alikuwa tayari kunipiga risasi, kama nilivyoeleza mwanzoni mwa simulizi hili. Kisha akanilazimisha kuingia ndani ya chumba kidogo cha gereza, ambacho kilijaa watu kupita kiasi. Nililazimika kusimama usiku kucha. Vyovyote vile, singeweza kulala kwa kuwa nilikuwa na maumivu katika mwili wote. “Ni upumbavu kufa kwa ajili ya dini fulani ya kijinga!” Hivyo ndivyo wafungwa wenzangu “walivyonifariji.” Dakt. Gleissner alikuwa katika chumba kilichokuwa karibu na changu. Alisikia yale yaliyotukia naye akasema kwa kusikitika: “Mateso ya Wakristo yametokea tena!”

Katika mwaka wa 1940, wafungwa wote waliamuriwa kwenda kwenye machimbo ya mawe Jumapili fulani, hata ingawa kwa kawaida hatukufanya kazi Jumapili. Hatua hiyo ilikuwa ya kulipiza kisasi kwa sababu ya “makosa” ya wafungwa fulani. Tuliamuriwa kubeba mawe makubwa kutoka kwenye machimbo hayo hadi kambini. Wafungwa wawili walijaribu kunitwika jiwe kubwa mgongoni, na nilikuwa karibu kuanguka kwa sababu ya uzito wa jiwe hilo. Hata hivyo, bila kutarajia, Arthur Rödl, msimamizi wa kambi aliyeogopwa sana, aliniokoa. Alipoona jinsi ilivyokuwa vigumu kwangu kubeba jiwe hilo, aliniambia: “Hutaweza kubeba jiwe hilo mgongoni hadi kambini! Liweke chini mara moja!” Nilifurahia kutii amri hiyo. Kisha Rödl akanionyesha jiwe dogo zaidi, na kusema: “Chukua hilo, na ulipeleke kambini. Si zito sana!” Baadaye, aligeuka na kumwamuru msimamizi wetu hivi: “Acha Wanafunzi wa Biblia warudi kambini. Wamefanya kazi ya kutosha leo!”

Mwishoni mwa kila siku ya kazi, nilikuwa mwenye furaha kushirikiana na familia yetu ya kiroho. Tulifanya mipango ya kugawa chakula cha kiroho. Ndugu fulani alikuwa akiandika andiko la Biblia kwenye karatasi ndogo na kuipitisha kwa wengine. Biblia pia iliingizwa kambini kwa siri. Iligawanywa katika vitabu mbalimbali. Kwa miezi mitatu nilikabidhiwa kitabu cha Ayubu. Nilikificha ndani ya soksi zangu. Simulizi la Ayubu lilinisaidia kubaki imara.

Mwishowe, Machi 7, 1941, nilijiunga na msafara mrefu wa watu waliohamishwa kwenda kwenye kambi ya mateso ya Niederhagen. Afya yangu iliendelea kuwa mbaya siku baada ya siku. Siku moja, mimi na ndugu wawili tuliamuriwa tupakie vifaa fulani ndani ya masanduku. Baada ya kufanya kazi hiyo, tulirudi kambini pamoja na kikundi kingine cha wafungwa. Askari mmoja wa Hitler aliona kwamba nilikuwa nimebaki nyuma ya wengine. Alikasirika sana, na bila kuniarifu akanipiga teke kali kutoka nyuma na kuniumiza sana. Nilihisi maumivu makali sana, lakini licha ya maumivu hayo nilienda kufanya kazi siku iliyofuata.

Nawekwa Huru Bila Kutarajia

Mnamo Aprili 1943, mwishowe wafungwa wa kambi ya Niederhagen walihamishwa. Kwa sababu hiyo, nilipelekwa kwenye kambi ya kifo ya Ravensbrück. Kisha, mnamo Juni 1943, bila kutarajia niliruhusiwa kuondoka katika kambi ya mateso. Mara hii, sikulazimishwa kukana imani yangu kwanza kabla ya kuachiliwa huru. Ilinibidi tu kukubali kufanya kazi ngumu shambani maisha yangu yote. Nilikuwa tayari kufanya kazi hiyo ili kuepuka ukatili kambini. Nilienda kumwona daktari wa kambi ili kufanyiwa uchunguzi wa mwisho. Daktari alishangaa kuniona. Alisema: “Ala! Bado wewe ni Shahidi wa Yehova!” “Ndiyo, Daktari Herr,” nikajibu. “Basi sioni kwa nini tukuache uende. Kwa upande mwingine, ni heri tukuweke huru kwa sababu wewe ni dhaifu.”

Kwa kusema hivyo, hakuwa akitia chumvi. Kwa kweli, afya yangu ilikuwa mbaya sana. Ngozi yangu ilikuwa imeliwa na chawa, na kwa sababu ya kupigwa, sikio langu moja halikuwa likisikia. Mwili wangu wote ulijaa vidonda vyenye usaha. Baada ya miezi 46 ya hali ngumu, njaa, na kazi ngumu, nilikuwa na uzito wa kilogramu 28 tu. Nikiwa katika hali hiyo, niliachiliwa kutoka katika kambi ya Ravensbrück Julai 15, 1943.

Nilirudishwa nyumbani kwa gari-moshi bila kuwa na mlinzi wa kuandamana nami, na nilienda kujitambulisha kwenye kituo kikuu cha Gestapo huko Linz. Ofisa wa Gestapo alinipa hati ya kuniruhusu kurudi nyumbani, naye akanionya hivi: “Ikiwa unafikiri kwamba tunakuweka huru ili uendelee na kazi yako kwa siri, unajidanganya sana! Mungu akusaidie tukikupata tena ukihubiri.”

Mwishowe, nilifika nyumbani. Mama hakubadili chochote ndani ya chumba changu tangu nifungwe mara ya kwanza, Aprili 4, 1939. Hata Biblia yangu ilikuwa wazi karibu na meza yangu! Nilipiga magoti na kutoa sala ya shukrani kutoka moyoni.

Punde baada ya hapo, nilipewa kazi kwenye shamba moja milimani. Mwenye shamba hilo alikuwa rafiki yangu tangu utotoni, naye alinilipa mshahara mdogo, ingawa haikuwa lazima kufanya hivyo. Kabla ya vita, rafiki huyo aliniruhusu kuficha baadhi ya vichapo vya Biblia kwenye shamba lake. Nilifurahi kutumia vizuri depo hiyo ndogo ya vichapo ili kujiimarisha kiroho. Mahitaji yangu yote yalitoshelezwa, nami niliazimia kuvumilia huko shambani hadi mwisho wa vita.

Najificha Milimani

Hata hivyo, siku hizo tulivu za kuwa huru zilikuwa fupi sana. Katikati ya Agosti 1943, niliamuriwa kwenda kumwona daktari wa jeshi kwa ajili ya uchunguzi wa kitiba. Kwanza, alisema kwamba sikustahili kufanya kazi jeshini kwa sababu ya matatizo yangu ya mgongo. Hata hivyo, juma moja baadaye daktari huyohuyo alirekebisha ripoti yake naye akaandika: “Anastahili kufanya kazi jeshini kwenye mstari wa mbele vitani.” Kwa muda, jeshi halikuweza kunipata, lakini Aprili 17, 1945, muda mfupi kabla ya vita kwisha, jeshi lilinipata. Nililazimishwa kuingia jeshini na kuwekwa kwenye mstari wa mbele vitani.

Nikiwa na nguo, chakula kidogo, na Biblia moja nilijificha katika milima ya karibu. Kwanza, nililala nje, lakini hali ya hewa ikawa mbaya sana, na theluji yenye kina cha sentimeta 50 ikaanguka. Nilikuwa nimelowa kabisa. Nilifaulu kufika kwenye kibanda kimoja milimani kilichokuwa karibu meta 1,200 juu ya usawa wa bahari. Nikiwa ninatetemeka, niliwasha moto, nikajipasha joto na kukausha mavazi yangu. Kwa sababu ya uchovu, nililala kwenye kiti kirefu mbele ya moto. Punde si punde, niliamshwa kwa ghafula na maumivu makali. Mavazi yangu yalikuwa yanaungua. Nilijiviringisha kwenye sakafu ili kuzima moto huo. Mgongo wangu wote ulijaa vipele vya moto.

Kwa sababu ya kuogopa kukamatwa, nilienda tena kujificha shambani huko milimani kabla ya mapambazuko, lakini mke wa yule mkulima aliogopa sana naye akaniambia niondoke, huku akinieleza kwamba nilikuwa nikitafutwa. Hivyo nikaenda kwa wazazi wangu. Mwanzoni, hata wazazi wangu walisita kunikaribisha, lakini mwishowe wakaniacha nilale ndani ya ghala la kuwekea nyasi kavu, na Mama akasafisha vidonda vyangu. Hata hivyo, siku mbili baadaye, wazazi wangu walikuwa na wasiwasi sana, hivyo nikaamua kwenda kujificha tena milimani.

Mei 5, 1945, niliamshwa na sauti kubwa. Niliona ndege za majeshi ya Muungano zikiruka chini-chini. Wakati huo, nilijua kwamba utawala wa Hitler ulikuwa umepinduliwa! Roho ya Yehova iliniimarisha kuvumilia mateso makali sana. Niliona ukweli wa maneno ya Zaburi 55:22, ambayo yalinifariji sana mwanzoni mwa majaribu yangu. ‘Nilimtupia Yehova mzigo wangu,’ na ingawa nilikuwa dhaifu kimwili, alinitegemeza nilipokuwa nikitembea katika “bonde lenye kivuli kizito.”—Zaburi 23:4.

Nguvu za Yehova “Zinakamilishwa Katika Udhaifu”

Baada ya vita, maisha yalirudi kuwa shwari pole kwa pole. Mwanzoni, nilipata kazi ya kibarua huko milimani kwenye shamba la yule rafiki yangu. Ilikuwa tu baada ya majeshi ya Marekani kuingia mnamo Aprili 1946 kwamba niliwekwa huru nisifanye kazi ya kulima ya kulazimishwa maisha yangu yote.

Mwishoni mwa vita, ndugu Wakristo huko Bad Ischl na wa wilaya ya karibu walianza kufanya mikutano kwa ukawaida. Walianza kuhubiri kwa bidii. Nilipewa kazi ya kuwa mlinzi wa usiku katika kiwanda fulani na hilo liliniwezesha kuendelea na upainia. Mwishowe, nilienda kuishi katika eneo la St. Wolfgang, na mnamo 1949, nikafunga ndoa na Theresia Kurz, aliyekuwa na binti mmoja katika ndoa yake ya kwanza. Tuliishi pamoja kwa miaka 32 hadi mke wangu mpendwa alipokufa mnamo 1981. Nilikuwa nimemtunza kwa zaidi ya miaka saba.

Baada ya kifo cha Theresia, nilianza tena utumishi wa painia, ambao ulinisaidia kuvumilia huzuni ya kufiwa na mke wangu. Kwa sasa ninatumika nikiwa painia na mzee katika kutaniko letu la Bad Ischl. Kwa kuwa ninalazimika kutumia kiti cha magurudumu, mimi hutoa vichapo vya Biblia na kuzungumza na watu kuhusu tumaini la Ufalme kwenye bustani ya Bad Ischl au mbele ya nyumba yangu. Mazungumzo mazuri ya Biblia pamoja na watu hunipa shangwe kubwa.

Ninapofikiria miaka ya nyuma, ninaweza kusema kwamba mambo ya kuogopesha sana ambayo nililazimika kuvumilia hayakunitia uchungu. Bila shaka, nyakati fulani nilishuka moyo kwa sababu ya majaribu. Hata hivyo, uhusiano wangu mchangamfu pamoja na Yehova Mungu ulinisaidia kukabiliana na nyakati hizo ngumu. Pia shauri hili la Bwana kwa Paulo, “Nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu,” lilithibitika kuwa kweli katika maisha yangu. Sasa, nikiwa na umri wa karibu miaka 100, ninaweza kujiunga na mtume Paulo kusema: “Napendezwa na udhaifu, na matusi, na hali za uhitaji, na mateso na magumu, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.”—2 Wakorintho 12:9, 10.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nakamatwa na askari wa Gestapo, Aprili 1939

Hati ya Gestapo yenye mashtaka, Mei 1939

[Hisani]

Both images: Privatarchiv; B. Rammerstorfer

[Picha katika ukurasa wa 26]

Milima niliyoikimbilia

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 23]

Foto Hofer, Bad Ischl, Austria