Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Watakaofufuliwa?

Ni Nani Watakaofufuliwa?

Ni Nani Watakaofufuliwa?

“Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” —YOHANA 5:28, 29.

1. Ni maneno gani ya ajabu ambayo Musa alisikia kwenye mti wa miiba uliokuwa ukiwaka moto, na ni nani aliyeyarudia baadaye?

JAMBO fulani la ajabu sana lilitukia miaka zaidi ya 3,500 iliyopita. Musa alikuwa akichunga kondoo za Yethro, mzee wa ukoo, karibu na Mlima Horebu, wakati malaika wa Yehova alipomtokea katika mwali wa moto katikati ya mti wa miiba. Kitabu cha Kutoka kinasema: “Alipoendelea kuangalia, tazama, ule mti wa miiba ulikuwa ukiwaka moto lakini haukuwa ukiteketea.” Kisha sauti ikamwita kutoka kwenye mti huo na kumwambia: “Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.” (Kutoka 3:1-6) Baadaye katika karne ya kwanza W.K., maneno hayo yalirudiwa na Yesu, Mwana wa Mungu.

2, 3. (a) Abrahamu, Isaka, na Yakobo wanangojea thawabu gani? (b) Ni maswali gani yanayotokea?

2 Yesu alikuwa akizungumza na Masadukayo fulani ambao hawakuamini ufufuo. Yesu alisema: “Hata Musa alifunua kwamba wafu watafufuliwa, katika masimulizi juu ya ule mti wa miiba, anapomwita Yehova ‘Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ Yeye ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, hao wote wako hai.” (Luka 20:27, 37, 38) Kwa kusema hivyo, Yesu alithibitisha kwamba kulingana na maoni ya Mungu, bado Abrahamu, Isaka, na Yakobo, waliokufa zamani, wako hai katika kumbukumbu ya Mungu. Kama Ayubu, wanangojea ‘kazi yao ya kulazimishwa’ iishe, yaani, kulala usingizi katika kifo. (Ayubu 14:14) Watafufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu.

3 Lakini, itakuwaje kwa mabilioni ya watu ambao wamekufa katika historia yote ya mwanadamu? Je, wao pia watafufuliwa? Kabla ya kujibu swali hilo kwa njia yenye kuridhisha, na tuone kulingana na Neno la Mungu watu huenda wapi wanapokufa.

Wafu Wako Wapi?

4. (a) Watu huenda wapi wanapokufa? (b) Sheoli ni nini?

4 Biblia inasema kwamba wafu “hawajui lolote kamwe.” Baada ya kifo, wanadamu hawateswi katika moto wala hawangoji kwa muda mrefu chini ya hali ngumu katika Ahera, bali wao hurudi mavumbini. Kwa hiyo, Neno la Mungu linawashauri hivi walio hai: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi [“Sheoli,” maelezo ya chini], mahali unapokwenda.” (Mhubiri 9:5, 10; Mwanzo 3:19) Hapa neno “Kaburi” ni tafsiri ya neno la Kiebrania “Sheoli.” Dini nyingi hufundisha kwamba wafu bado wako hai, lakini kama vile Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linavyoonyesha, wale walio katika Sheoli wamekufa, hawana fahamu yoyote. Sheoli ni kaburi.

5, 6. Yakobo alienda wapi alipokufa, naye alijiunga na nani huko?

5 Katika Biblia, neno “Sheoli” linapatikana kwa mara ya kwanza katika Mwanzo 37:35. Baada ya kufikiri kwamba mwanawe mpendwa Yosefu alikuwa amekufa, mzee wa ukoo Yakobo alikataa kufarijiwa na kusema: “Nitashuka kuingia katika [Sheoli] nikimwombolezea mwanangu!” Kwa kuamini kwamba mwanawe alikuwa amekufa, Yakobo alitamani kufa na kwenda katika Sheoli. Baadaye, wana tisa wa Yakobo, waliokuwa na umri mkubwa, walitaka kwenda na mwanawe mdogo, Benyamini, huko Misri ili kutafuta chakula kwa sababu ya njaa. Hata hivyo, Yakobo alikataa na kusema: “Mwanangu hatashuka kwenda nanyi, kwa sababu ndugu yake amekufa naye amebaki peke yake. Tukio lenye kufisha likimpata katika njia mtakayoiendea, basi bila shaka mtazishusha mvi zangu kwa huzuni mpaka katika [Sheoli].” (Mwanzo 42:36, 38) Maandiko hayo mawili yanahusianisha kifo na Sheoli, bali si hali ya kuendelea kuishi baada ya kufa.

6 Masimulizi ya kitabu cha Mwanzo yanaonyesha kwamba Yosefu alikuwa msimamizi wa chakula huko Misri. Hivyo, Yakobo alienda huko ili akaungane kwa furaha na Yosefu. Baadaye, Yakobo aliishi katika nchi hiyo hadi alipokufa akiwa na umri mkubwa wa miaka 147. Kulingana na mapendekezo yake kabla ya kufa, wanawe waliusafirisha mwili wake na kuuzika katika pango la Makpela katika nchi ya Kanaani. (Mwanzo 47:28; 49:29-31; 50:12, 13) Kwa hiyo, Yakobo alijiunga na Isaka baba yake, na Abrahamu babu yake.

‘Walikusanywa kwa Mababu Zao’

7, 8. (a) Abrahamu alienda wapi alipokufa? Eleza. (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba wengine walienda katika Sheoli walipokufa?

7 Awali, Yehova alipohalalisha agano lake na Abrahamu na kumwahidi kwamba uzao wake ungekuwa mwingi, alimweleza jambo ambalo lingempata. Yehova alimwambia hivi: “Lakini wewe, utaenda kwa mababu zako kwa amani; utazikwa katika uzee mwema.” (Mwanzo 15:15) Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Andiko la Mwanzo 25:8 linasema: “Kisha Abrahamu akakata pumzi, akafa katika umri mwema wa uzee, akiwa mzee na mwenye kutosheka, naye akakusanywa kwa watu wake.” Hao ni akina nani? Andiko la Mwanzo 11:10-26 linataja mababu zake wote kuanzia Shemu, mwana wa Noa. Kwa hiyo alipokufa, Abrahamu alikusanywa na kujiunga na watu hao ambao tayari walikuwa wanalala katika Sheoli.

8 Maneno ‘kukusanywa kwa watu wake’ yametajwa mara nyingi katika Maandiko ya Kiebrania. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba Ishmaeli, mwana wa Abrahamu, na Haruni, ndugu ya Musa, walienda katika Sheoli walipokufa, nao wanangojea ufufuo wakiwa huko. (Mwanzo 25:17; Hesabu 20:23-29) Musa pia alienda katika Sheoli, ingawa hakuna mtu aliyejua mahali kaburi lake lilipokuwa. (Hesabu 27:13; Kumbukumbu la Torati 34:5, 6) Vivyo hivyo, Yoshua, ambaye alikuwa kiongozi wa Waisraeli baada ya Musa, pamoja na kizazi kizima cha watu, walienda katika Sheoli walipokufa.—Waamuzi 2:8-10.

9. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba neno la Kiebrania “Sheoli” na neno la Kigiriki “Hadesi” hurejelea mahali palepale? (b) Kuna tazamio gani kwa wale walio katika Sheoli, au Hadesi?

9 Karne kadhaa baadaye, Daudi akawa mfalme wa makabila 12 ya Israeli. Alipokufa, ‘alilala na mababu zake.’ (1 Wafalme 2:10) Je, yeye pia alikuwa katika Sheoli? Katika siku ya Pentekoste 33 W.K., mtume Petro alitaja kifo cha Daudi na kunukuu andiko la Zaburi 16:10, linalosema: “Hutaiacha nafsi yangu katika [Sheoli].” Baada ya kutaja kwamba Daudi bado alikuwa katika kaburi lake, Petro alitumia maneno hayohayo kumhusu Yesu, naye akasema kwamba Daudi “aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika [“Hadesi,” maelezo ya chini] wala mwili wake haukuona uharibifu. Yesu huyo Mungu alimfufua, uhakika ambao sisi sote ni mashahidi.” (Matendo 2:29-32) Hapa Petro alitumia neno la Kigiriki “Hadesi,” ambalo lina maana sawa na neno la Kiebrania “Sheoli.” Hivyo, hali ya wale wanaosemwa kwamba wako katika Hadesi ni sawa na ya wale wanaosemwa kwamba wako katika Sheoli. Wanalala huku wakingojea ufufuo.

Je, Kuna Watu Wasio Waadilifu Katika Sheoli?

10, 11. Kwa nini tunaweza kusema kwamba watu fulani wasio waadilifu huenda katika Sheoli, au Hadesi, wanapokufa?

10 Baada ya Musa kuliongoza taifa la Israeli kutoka Misri, kulitokea uasi nyikani. Musa aliwaambia watu wajitenge na Kora, Dathani, na Abiramu, viongozi wa uasi huo. Watu hao wangekufa ghafula na kwa uchungu mwingi. Musa alieleza: “Ikiwa watu hawa watakufa kifo cha wanadamu wote na kwamba adhabu iletwe juu yao kulingana na adhabu ya wanadamu wote, basi si Yehova aliyenituma mimi. Lakini ikiwa ni kitu fulani kilichoumbwa ambacho Yehova ataumba, nayo nchi ifungue kinywa chake na kuwameza na kila kitu kilicho chao, nao washuke chini wakiwa hai mpaka katika [Sheoli], ndipo hakika mtajua kwamba watu hawa wamemtendea Yehova bila heshima.” (Hesabu 16:29, 30) Hivyo, wawe walimezwa na dunia iliyofunguka au wawe waliteketezwa kwa moto, kama ilivyokuwa katika kisa cha Kora na Walawi 250 waliomuunga mkono, waasi hao wote walienda katika Sheoli, au Hadesi.—Hesabu 26:10.

11 Shimei, ambaye alimlaani Mfalme Daudi, aliadhibiwa na Sulemani aliyekuwa Mfalme baada ya Daudi. Daudi aliamuru: “Usimwache bila adhabu, kwa maana wewe ni mtu mwenye hekima na unajua vema jinsi unavyopaswa kumtendea, nawe lazima ushushe katika [Sheoli] mvi zake kwa damu.” Sulemani alimwagiza Benaya atekeleze hukumu hiyo. (1 Wafalme 2:8, 9, 44-46) Mtu mwingine aliyeuawa na Benaya ni Yoabu, aliyekuwa mkuu wa jeshi la Israeli. Mvi zake ‘hazikushuka kwa amani katika Sheoli.’ (1 Wafalme 2:5, 6, 28-34) Mifano hiyo miwili inaonyesha kwamba wimbo ambao Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kuimba ni wa kweli: “Watu waovu watarudi katika [Sheoli], naam, mataifa yote yanayomsahau Mungu.”—Zaburi 9:17.

12. Ahithofeli alikuwa nani, naye alienda wapi alipokufa?

12 Ahithofeli alikuwa mshauri wa kibinafsi wa Daudi. Shauri lake lilionwa kuwa muhimu, kana kwamba lilitoka kwa Yehova mwenyewe. (2 Samweli 16:23) Kwa kusikitisha, mtumishi huyo mwenye kutegemewa alimsaliti Daudi na alihusika katika mapinduzi yaliyoongozwa na Absalomu, mwana wa Daudi. Yaonekana Daudi aliurejelea usaliti huo alipoandika: “Sikushutumiwa na adui; kama ndivyo ningaliweza kuvumilia hilo. Si mtu anayenichukia vikali aliyejivuna sana dhidi yangu; kama ndivyo ningaliweza kujificha kutoka kwake.” Daudi aliongeza: “Ukiwa na uwe juu yao! Na washuke katika [Sheoli] wakiwa hai; kwa maana wakati wao wa kukaa ugenini mambo mabaya yamekuwa ndani yao.” (Zaburi 55:12-15) Walipokufa, Ahithofeli na wenzake walienda katika Sheoli.

Ni Nani Walio Katika Gehena?

13. Kwa nini Yuda anaitwa “mwana wa maangamizi”?

13 Linganisha hali ya Daudi na ile iliyompata Daudi Mkuu, Yesu. Kama Ahithofeli, Yuda Iskariote, mmoja kati ya mitume 12 wa Kristo, alibadilika akawa msaliti. Usaliti wake ulikuwa mbaya kuliko ule wa Ahithofeli. Yuda alimsaliti Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. Aliposali mwishoni mwa huduma yake duniani, Mwana wa Mungu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Nilipokuwa pamoja nao nilikuwa nikiwalinda kwa sababu ya jina lako ambalo umenipa; nami nimewatunza, na hata mmoja wao hakuangamizwa ila yule mwana wa maangamizi, ili andiko lipate kutimizwa.” (Yohana 17:12) Kwa kutaja kwamba Yuda alikuwa “mwana wa maangamizi,” Yesu alionyesha kwamba Yuda alipokufa, hakuwa na tumaini lolote la kufufuliwa. Hakubaki katika kumbukumbu ya Mungu. Hivyo, hakuenda katika Sheoli, bali alienda katika Gehena. Gehena ni nini?

14. Gehena inafananisha nini?

14 Yesu aliwashutumu viongozi wa dini wa siku zake kwa sababu walimfanya kila mmoja wa wanafunzi wao “astahili Gehena.” (Mathayo 23:15) Wakati huo, watu walilijua Bonde la Hinomu, lililotumiwa kama mahali pa kutupia takataka ambako pia watu walitupa miili ya wahalifu waliouawa ambao walionwa kuwa hawastahili mazishi yanayofaa. Awali, Yesu mwenyewe alikuwa ametaja Gehena katika Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo 5:29, 30) Wasikilizaji wake walielewa maana ya mfano ya Gehena. Hiyo inafananisha kuharibiwa kabisa bila tumaini la ufufuo. Mbali na Yuda Iskariote wa siku za Yesu, je, kuna wengine ambao, baada ya kufa, wameenda katika Gehena badala ya kwenda katika Sheoli, au Hadesi?

15, 16. Ni nani walioenda katika Gehena walipokufa, na kwa nini walienda huko?

15 Wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, waliumbwa wakiwa wakamilifu. Walifanya dhambi kimakusudi. Wangeweza kuchagua uzima wa milele au kifo. Lakini wakamwasi Mungu na kumuunga mkono Shetani. Walipokufa, hawakuwa na tazamio lolote la kufaidika na dhabihu ya fidia ya Kristo. Hivyo, walienda katika Gehena.

16 Kaini, mwana wa kwanza wa Adamu, alimuua ndugu yake Abeli na baadaye akawa mkimbizi. Mtume Yohana alimtaja Kaini kuwa mtu “aliyetokana na yule mwovu.” (1 Yohana 3:12) Ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba Kaini alienda katika Gehena alipokufa, sawa na wazazi wake. (Mathayo 23:33, 35) Hali hiyo ni tofauti sana na ya Abeli mwadilifu. Paulo alieleza: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu, Mungu akitoa ushahidi kuhusu zawadi zake.” Kisha akaongeza: “Na kupitia hiyo yeye, ijapokuwa alikufa, bado anasema.” (Waebrania 11:4) Naam, kwa sasa Abeli yuko katika Sheoli akingojea ufufuo.

Ufufuo wa “Kwanza” na Ufufuo “Ulio Bora”

17. (a) Ni nani wanaoenda katika Sheoli ‘wakati huu wa mwisho’? (b) Kuna matazamio gani kwa wale walio katika Sheoli na wale walio katika Gehena?

17 Wengi watakaosoma makala hii watataka kujua kuhusu hali ya wale wanaokufa ‘wakati huu wa mwisho.’ (Danieli 8:19) Sura ya 6 ya kitabu cha Ufunuo inaeleza kuhusu wapanda-farasi wanne wanaoendesha farasi wakati huu. Mpanda-farasi wa mwisho anaitwa Kifo, naye anafuatwa na Hadesi. Hivyo, wengi wanaokufa mapema kwa sababu ya matukio na hali zinazofananishwa na wapanda-farasi wanaotangulia, wanaingia katika Hadesi. Huko wanangojea ufufuo katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Ufunuo 6:8) Hivyo basi, kuna matazamio gani kwa wale walio katika Sheoli (Hadesi) na wale walio katika Gehena? Kwa ufupi, kuna tazamio la ufufuo kwa wale walio katika Sheoli (Hadesi), lakini kwa wale walio katika Gehena kuna tazamio la uharibifu wa milele, yaani, kutokuwapo tena.

18. Wale wanaofufuliwa katika “ufufuo wa kwanza” wana tazamio gani?

18 Mtume Yohana aliandika: “Mwenye furaha na mtakatifu ni yeyote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; kifo cha pili hakina mamlaka juu ya hao, bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.” Wale watakaotawala pamoja na Kristo wanafufuliwa katika “ufufuo wa kwanza.” Lakini wanadamu wengine wana tazamio gani?—Ufunuo 20:6.

19. Wengine hunufaikaje na “ufufuo ulio bora”?

19 Tangu siku za watumishi wa Mungu, Eliya na Elisha, muujiza wa ufufuo uliwawezesha watu kuwa hai tena. Paulo aliandika hivi: “Wanawake waliwapokea wafu wao kwa ufufuo; lakini watu wengine waliteswa kwa sababu hawakukubali kuachiliwa huru kupitia fidia fulani, ili waupate ufufuo ulio bora.” Naam, watu hao waaminifu waliodumisha utimilifu walitazamia ufufuo ambao ungewawezesha kuishi milele, wala si kuishi kwa miaka kadhaa kisha wafe tena! Kwa kweli, huo utakuwa “ufufuo ulio bora.”—Waebrania 11:35.

20. Makala inayofuata itazungumzia nini?

20 Iwapo tutakufa tukiwa waaminifu kabla ya Yehova kuangamiza mfumo huu mwovu, tuna tumaini hakika la kupata “ufufuo ulio bora,” katika maana ya kwamba tukifufuliwa tutakuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. Yesu aliahidi: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Makala inayofuata itazungumzia zaidi kusudi la ufufuo. Itaonyesha jinsi ambavyo tumaini la ufufuo hutuimarisha ili kudumisha utimilifu wetu na kutusaidia kusitawisha roho ya kujitolea.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Yehova anatajwa kuwa Mungu “wa walio hai”?

• Wale walio katika Sheoli wako katika hali gani?

• Kuna tazamio gani kwa wale walio katika Gehena?

• Wengine watanufaikaje na “ufufuo ulio bora”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama Abrahamu, kuna tazamio la ufufuo kwa wale wanaoenda katika Sheoli

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kwa nini Adamu na Hawa, Kaini, na Yuda Iskariote walienda katika Gehena?