Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumaini la Ufufuo Linamaanisha Nini Kwako?

Tumaini la Ufufuo Linamaanisha Nini Kwako?

Tumaini la Ufufuo Linamaanisha Nini Kwako?

“Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” —Zaburi 145:16.

1-3. Wengine wana tumaini gani la wakati ujao? Eleza.

SIKU moja asubuhi, Christopher mwenye umri wa miaka tisa na ndugu yake, binamu zao wawili, pamoja na mjomba na shangazi yao, walienda kuhubiri nyumba kwa nyumba karibu na mji wa Manchester, huko Uingereza. Gazeti letu la Amkeni! linaeleza yaliyotukia. “Alasiri, walisafiri pamoja kwenda kutazama mandhari huko Blackpool, eneo la watalii lililo karibu na kwao. Wote 6 walikuwa kati ya watu 12 waliokufa papo hapo kwenye msiba wa barabarani, ambao ulifafanuliwa na polisi kuwa ‘maafa makubwa.’”

2 Usiku uliotangulia msiba huo, familia ya akina Christopher ilikuwa imehudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko, ambako kifo kilizungumziwa. Babake alisema: “Christopher alikuwa mvulana mwenye kutafakari sana. Usiku huo alizungumza waziwazi kuhusu ulimwengu mpya na tumaini lake la wakati ujao. Mazungumzo yalipokuwa yakiendelea, Christopher alisema hivi kwa ghafula: ‘Faida ya kuwa Shahidi wa Yehova ni kwamba ingawa kifo huumiza, tunajua kwamba siku moja tutaonana tena duniani.’ Hatukutambua kwamba maneno hayo yangetugusa moyo sana baadaye.” *

3 Katika mwaka wa 1940, Shahidi mmoja wa Austria anayeitwa Franz alijua kwamba angekatwa kichwa kwa sababu ya ushikamanifu wake kwa Yehova. Franz alimwandikia mamake hivi kutoka gerezani huko Berlin: “Kwa yale niliyojua, ikiwa ningalikula kiapo [cha kijeshi], ningalitenda dhambi inayostahili kifo. Huo ungekuwa uovu kwangu. Nisingepata ufufuo. . . . Na sasa, Mama yangu mpendwa na ndugu na dada zangu wote, leo niliambiwa hukumu yangu, na msiogopeshwe, ni kifo, nami nitauawa kesho asubuhi. Nina nguvu yangu kutoka kwa Mungu, sawa na ilivyokuwa sikuzote kwa Wakristo wote wa kweli huko nyuma. . . . Ikiwa mtasimama imara hadi kifo, tutaonana tena kwenye ufufuo. . . . Hadi tutakapoonana tena.” *

4. Unahisije baada ya kusoma visa vilivyosimuliwa hapa, na tutazungumzia nini?

4 Tumaini la ufufuo lilikuwa na maana kubwa kwa Christopher na Franz. Ufufuo ulikuwa halisi kwao. Bila shaka, masimulizi hayo yanatugusa moyo! Ili tuwe na uthamini mkubwa zaidi kwa Yehova na kuimarisha tumaini letu katika ufufuo, acheni tuone kwa nini kutakuwa na ufufuo na jinsi jambo hilo linavyoweza kumchochea kila mmoja wetu.

Maono Kuhusu Ufufuo wa Watakaoishi Duniani

5, 6. Maono ambayo mtume Yohana aliandika kwenye Ufunuo 20:12, 13 yanafunua nini?

5 Katika maono kuhusu mambo yatakayotukia wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo Yesu, mtume Yohana aliona ufufuo wa wale watakaoishi duniani. ‘Niliwaona wafu, wakubwa kwa wadogo,’ akasema. “Na bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na [Hadesi] vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake.” (Ufunuo 20:12, 13) Hata wawe wa cheo gani, wawe “wakubwa” au “wadogo,” wote ambao ni mateka katika Hadesi (Sheoli), yaani, kaburi, wataachiliwa. Pia wale waliofia baharini watakuwa hai tena wakati huo. Tukio hilo zuri ni sehemu ya kusudi la Yehova.

6 Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo utakapoanza, Shetani atafungwa na kutupwa katika abiso. Hakuna yeyote kati ya wale watakaofufuliwa au watakaookoka dhiki kuu atakayepotoshwa na Shetani wakati wa utawala huo, kwa kuwa hatakuwa anatenda. (Ufunuo 20:1-3) Huenda ukafikiri kwamba miaka elfu ni muda mrefu, lakini Yehova huiona “kama siku moja.”—2 Petro 3:8.

7. Hukumu itategemea nini wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo?

7 Kulingana na maono hayo, Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo utakuwa wakati wa hukumu. Mtume Yohana aliandika: ‘Niliwaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya kile kiti cha ufalme, na vitabu vya kukunjwa vikafunguliwa. Lakini kitabu kingine cha kukunjwa kikafunguliwa; hicho ni kitabu cha uzima. Na wafu wakahukumiwa kutokana na mambo yale yaliyoandikwa katika vile vitabu kulingana na matendo yao. Nao walihukumiwa kila mmoja kulingana na matendo yake.’ (Ufunuo 20:12, 13) Ona kwamba hukumu hiyo haitategemea mambo ambayo watu hao walitenda kabla ya kufa. (Waroma 6:7) Badala yake, inahusiana na “vitabu vya kukunjwa” vitakavyofunguliwa. Kuandikwa kwa jina la mtu katika “kitabu cha kukunjwa cha uzima” kutategemea jinsi atakavyotenda baada ya kujifunza mambo yaliyo katika vitabu hivyo.

“Ufufuo wa Uzima” au “Ufufuo wa Hukumu”

8. Wale watakaofufuliwa watapata mojawapo ya mambo gani mawili?

8 Mapema katika maono ya Yohana, Yesu anatajwa kuwa na “funguo za kifo na za [Hadesi].” (Ufunuo 1:18) Yeye ndiye ‘Wakili Mkuu wa Yehova wa uzima,’ ambaye amepewa mamlaka ya kuhukumu “walio hai na wafu.” (Matendo 3:15; 2 Timotheo 4:1) Atafanyaje hivyo? Kwa kuwafufua wale waliolala usingizi katika kifo. Yesu aliuambia hivi umati ambao aliuhubiria: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” Kisha akaongeza: “Wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:28-30) Kwa hiyo, wanaume na wanawake waaminifu wa kale wana tazamio gani la wakati ujao?

9. (a) Wengi watajifunza nini baada ya kufufuliwa? (b) Ni kazi gani kubwa ya kuelimisha itakayoanza?

9 Wakati watu hao waaminifu wa kale watakapofufuliwa, watatambua upesi kwamba ahadi walizotumaini zimetimia. Watatamani sana kujua Uzao wa mwanamke wa Mungu anayetajwa katika unabii wa kwanza wa Biblia kwenye Mwanzo 3:15! Watafurahi kama nini kusikia kwamba Yesu, Masihi huyo aliyeahidiwa, alikuwa mwaminifu hadi kifo, na hivyo kutoa uhai wake ukiwa dhabihu ya fidia! (Mathayo 20:28) Wale watakaowakaribisha baada ya kufufuliwa watafurahia sana kuwasaidia waelewe kwamba fidia hiyo ni wonyesho wa rehema na fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Bila shaka, wale watakaofufuliwa watamsifu Yehova sana watakapotambua yale ambayo Ufalme wa Mungu unafanya ili kutimiza kusudi lake kuihusu dunia. Watakuwa na nafasi ya kutosha kuonyesha ushikamanifu wao kwa Baba yao mpendwa wa mbinguni na Mwana wake. Wakati huo, kila mtu atafurahia kazi kubwa ya kuwaelimisha mabilioni ya watu watakaofufuliwa, ambao pia watahitaji kukubali maandalizi ya Mungu ya fidia.

10, 11. (a) Ile Miaka Elfu itawaandalia nafasi gani wote watakaokuwa duniani? (b) Hilo linapaswa kutuchochea kufanya nini?

10 Abrahamu atakapofufuliwa atafarijiwa sana na jinsi maisha yatakavyokuwa katika utawala wa “jiji” alilotazamia. (Waebrania 11:10) Ayubu mwaminifu aliyeishi zamani atafurahi sana kujua kwamba maisha yake yaliwaimarisha watumishi wengine wa Yehova ambao utimilifu wao ulijaribiwa! Naye Danieli atatamani sana kujua ikiwa unabii ambao roho ya Mungu ilimwongoza kuandika ulitimia!

11 Naam, wote watakaopata uhai katika ulimwengu mpya wenye uadilifu, iwe ni kupitia ufufuo au kuokoka dhiki kuu, watajifunza mengi juu ya kusudi la Yehova kuihusu dunia na wakaaji wake. Bila shaka, tazamio la kuishi milele na kumsifu Yehova milele na milele litafanya programu ya elimu ya Miaka Elfu iwe yenye kufurahisha sana. Hata hivyo, jambo la maana zaidi ni matendo yetu binafsi baada ya kujifunza mambo yaliyo katika vitabu vya kukunjwa. Je, matendo yetu yatapatana na yale tutakayojifunza? Je, tutatafakari na kutenda kupatana na habari muhimu ambazo zitatuimarisha kushinda jaribu la mwisho la Shetani la kutukengeusha kutoka katika kweli?

12. Ni nini kitakachomsaidia kila mmoja kushiriki kikamili katika kazi ya kuwaelimisha watu na kuigeuza dunia kuwa paradiso?

12 Hatupaswi kupuuza baraka zitakazotokana na kutumia faida za dhabihu ya fidia ya Kristo. Wale watakaofufuliwa hawatakuwa na ulemavu au magonjwa yanayowapata watu leo. (Isaya 33:24) Kwa sababu watakuwa na mwili wenye afya na tazamio la kuwa na afya kamilifu, wakaaji wote wa ulimwengu mpya wataweza kushiriki kikamili katika kazi ya kuwaelimisha mabilioni ya watu watakaofufuliwa kuhusu njia ya uzima. Pia wakaaji hao watashiriki katika kazi kubwa zaidi kuwahi kufanywa duniani, yaani, kuigeuza dunia yote kuwa paradiso na kumletea Yehova sifa.

13, 14. Shetani ataachiliwa kwa kusudi gani wakati wa lile jaribu la mwisho, na huenda mtu mmoja-mmoja akapatwa na nini?

13 Shetani atakapoachiliwa kutoka katika abiso kwa ajili ya jaribu la mwisho, atajaribu kuwapotosha wanadamu tena. Kulingana na Ufunuo 20:7-9, mataifa yote au vikundi vya watu ‘watakaopotoshwa’ kwa kuvutwa na ushawishi mwovu wa Shetani, watahukumiwa uharibifu: ‘Moto utashuka kutoka mbinguni na kuwateketeza.’ Kwa habari ya wale watakaofufuliwa wakati wa kipindi cha ile Miaka Elfu, uharibifu huo utafanya ufufuo wao uwe wa hukumu. Tofauti na hao, wale watakaodumisha utimilifu baada ya ufufuo watapokea zawadi ya uzima wa milele. Kwa kweli, ufufuo wao utakuwa “ufufuo wa uzima.”—Yohana 5:29.

14 Tumaini la ufufuo linawezaje kutufariji hata sasa? Naam, tunapaswa kufanya nini ili kuhakikisha kwamba tutanufaika na ufufuo wakati ujao?

Mambo ya Kutilia Maanani Sasa

15. Imani katika ufufuo inawezaje kutusaidia sasa?

15 Huenda umefiwa na mpendwa wako hivi majuzi, na huenda unakabiliana na mabadiliko makubwa yanayosababishwa na hali hiyo. Tumaini la ufufuo linakusaidia kupata amani ya akili na nguvu ambazo wale wasiojua kweli hawapati. Paulo aliwafariji hivi Wathesalonike: “Hatutaki mkose kujua kuhusu wale walalao usingizi katika kifo; ili msiwe na huzuni kama wale watu wengine wasio na tumaini.” (1 Wathesalonike 4:13) Je, unajiona ukiwa katika ulimwengu mpya, ukishuhudia ufufuo? Pata faraja sasa kwa kutafakari juu ya tazamio la kukutana tena na wapendwa wako.

16. Huenda utahisije ufufuo utakapotokea?

16 Huenda kwa sasa wewe ni mgonjwa kwa sababu ya matokeo ya kuasi kwa Adamu. Usiruhusu huzuni inayotokana na hali hiyo ikufanye usahau tazamio lenye kufurahisha la kufufuliwa na kuishi tena ukiwa na afya nzuri na nguvu katika ulimwengu mpya. Bila shaka, utakapofungua macho na kuona watu wenye furaha na hamu ya kushangilia pamoja nawe ufufuo wako, utamshukuru Mungu kwa fadhili zake zenye upendo.

17, 18. Ni mambo gani mawili tunayopaswa kutilia maanani?

17 Kwa sasa, fikiria mambo mawili ambayo tunapaswa kutilia maanani. Jambo la kwanza ni umuhimu wa kumtumikia Yehova kwa nafsi yote sasa. Kwa kumwiga Bwana wetu, Kristo Yesu, maisha yetu ya kujitolea huonyesha tunampenda Yehova na jirani zetu. Upinzani au mateso yakitukosesha riziki au uhuru, sisi huazimia kuendelea kuwa na imani thabiti hata tupatwe na majaribu ya aina gani. Wapinzani wakitisha kutuua, tumaini la ufufuo hutufariji na kutuimarisha kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova na Ufalme wake. Naam, kuhubiri na kufanya wanafunzi kwa bidii hutupa tazamio la kupata baraka za milele ambazo Yehova atawapa waadilifu.

18 Jambo la pili linahusiana na jinsi tunavyoweza kukabili majaribu yanayosababishwa na mwili wenye dhambi. Kujua tumaini la ufufuo na kuthamini fadhili zisizostahiliwa za Yehova huimarisha azimio letu la kudumisha imani thabiti. Mtume Yohana alionya: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. Zaidi ya hayo, ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:15-17) Vitu vya kimwili ambavyo ulimwengu hutumia kutushawishi havitakuwa vyenye kuvutia sana tunapovilinganisha na “uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 6:17-19) Tukishawishiwa kufanya jambo fulani chafu kiadili, tutakataa katakata. Tunajua kwamba tukiendelea kufanya mambo yasiyompendeza Yehova kisha tufe kabla ya Har–Magedoni, tunaweza kupoteza tazamio la ufufuo.

19. Ni pendeleo gani kubwa tusilopaswa kupuuza?

19 Zaidi ya yote, hatupaswi kupuuza pendeleo kubwa sana la kuufanya moyo wa Yehova ushangilie, sasa na milele. (Methali 27:11) Uaminifu wetu hadi kifo au kudumisha utimilifu wetu hadi mwisho wa mfumo huu mwovu humwonyesha Yehova tuko upande gani kuhusiana na suala la enzi kuu ya ulimwengu wote. Itakuwa shangwe iliyoje kuishi katika dunia Paradiso kwa kuokoka dhiki kuu au kupitia muujiza wa ufufuo!

Kutosheleza Tamaa Zetu

20, 21. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kuwa waaminifu hata ingawa kuna maswali ambayo hayajajibiwa kuhusu ufufuo? Eleza.

20 Mazungumzo yetu kuhusu ufufuo hayakujibu maswali yote. Yehova anakusudia nini kwa ajili ya wale waliokuwa wameoana kabla ya kufa? (Luka 20:34, 35) Je, ufufuo utatukia mahali ambapo watu walifia? Je, watafufuliwa karibu na mahali ambapo watu wa familia zao wanaishi? Kuna maswali mengi ambayo hayajajibiwa kuhusu mambo yanayohusiana na ufufuo. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka maneno haya ya Yeremia: “Yehova ni mwema kwa yule anayemtumaini, kwa nafsi inayoendelea kumtafuta. Ni jambo jema kwa mtu kuungojea, ndiyo, kimyakimya, wokovu wa Yehova.” (Maombolezo 3:25, 26) Katika wakati wa Yehova unaofaa, maswali yetu yote yatajibiwa kwa njia yenye kuridhisha kabisa. Kwa nini tuna uhakika kuhusu jambo hilo?

21 Tafakari maneno ya mtunga-zaburi yaliyoongozwa na roho ya Mungu alipoimba hivi kumhusu Yehova: “Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zaburi 145:16) Umri unapozidi kusonga, mapendezi yetu hubadilika. Hatutamani tena mambo tuliyoyapenda tulipokuwa watoto. Maoni yetu kuhusu maisha huathiriwa na matumaini yetu na pia mambo yanayotupata. Hata hivyo, katika ulimwengu mpya, bila shaka Yehova atatosheleza tamaa zetu zote zinazofaa.

22. Kwa nini tuna sababu nzuri ya kumsifu Yehova?

22 Jambo la maana sasa ni kwamba kila mmoja wetu awe mwaminifu. “Kinachoangaliwa katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu.” (1 Wakorintho 4:2) Sisi ni wasimamizi-nyumba wa habari njema tukufu za Ufalme wa Mungu. Bidii yetu ya kuwahubiria habari njema wote tunaokutana nao hutusaidia kudumu katika barabara inayoelekea kwenye uzima wa milele. Usisahau kamwe kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11) Ili kukabiliana na wasiwasi wowote usio wa lazima unaosababishwa na kuhangaikia mambo yanayoweza kutokea maishani, dumisha imani yenye nguvu katika tumaini tukufu la ufufuo. Hata kama inaonekana kwamba utakufa kabla ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo kuanza, unaweza kufarijiwa na uhakika wa kwamba kitulizo kitakuja. Katika wakati wa Yehova unaofaa, utaweza kurudia maneno haya ya Ayubu, ambayo alimwambia Muumba: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.” Na tumsifu Yehova, ambaye hutamani kuwafufua wale wote walio katika kumbukumbu yake!—Ayubu 14:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ona gazeti la Amkeni! la Julai 8, 1988, ukurasa wa 10, (la Kiingereza au Kifaransa) lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 3 Kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 662, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Watu watahukumiwa kwa msingi gani wakati wa kile kipindi cha Miaka Elfu?

• Kwa nini wengine watapata “ufufuo wa uzima” na wengine “ufufuo wa hukumu”?

• Tumaini la ufufuo linaweza kutufariji jinsi gani sasa?

• Andiko la Zaburi 145:16 linaweza kutusaidiaje kuhusiana na maswali ambayo hayajajibiwa kuhusu ufufuo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Imani katika ufufuo inaweza kutusaidiaje sasa?