Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Endelea Kujizuia Chini ya Uovu’

‘Endelea Kujizuia Chini ya Uovu’

‘Endelea Kujizuia Chini ya Uovu’

“Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, . . . akiendelea kujizuia chini ya uovu.”—2 TIMOTHEO 2:24.

1. Tunapokuwa katika utendaji wa Kikristo, kwa nini mara kwa mara sisi hukutana na watu wanaosema kwa ukali?

WEWE hutendaje unapokabiliana na watu ambao hawapendezwi nawe au kile unachowakilisha? Akieleza kuhusu siku za mwisho, mtume Paulo alitabiri kwamba watu wangekuwa wenye ‘kukufuru, wachongezi, wasiojizuia, na wakali.’ (2 Timotheo 3:1-5, 12) Huenda ukakutana na watu kama hao katika huduma yako au katika utendaji mbalimbali.

2. Ni maandiko gani yanayoweza kutusaidia kushughulika kwa hekima na watu wanaosema nasi kwa ukali?

2 Si watu wote wanaotumia maneno makali ambao hawapendezwi na mambo yaliyo sawa. Huenda magumu au kukata tamaa kukawafanya watu waseme kwa ukali. (Mhubiri 7:7) Wengi hutenda hivyo kwa sababu wanaishi na kufanya kazi mahali ambapo watu wamezoea kusema kwa ukali. Hata hivyo, hilo halifanyi usemi huo ukubalike kwetu tukiwa Wakristo, bali hilo hutusaidia kuelewa kwa nini watu wengine huutumia. Tufanyeje watu wakisema nasi kwa ukali? Andiko la Methali 19:11 linasema hivi: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.” Nalo andiko la Waroma 12:17, 18 linatushauri hivi: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”

3. Amani inahusikaje katika ujumbe tunaohubiri?

3 Ikiwa kwa kweli sisi ni wenye amani, hilo litaonekana wazi katika mtazamo wetu. Litaonekana katika yale tunayosema na kufanya, na pengine pia katika uso na sauti yetu. (Methali 17:27) Alipowatuma mitume wake waende kuhubiri, Yesu aliwashauri hivi: “Mnapoingia ndani ya nyumba, wapeni salamu watu wa nyumba hiyo; na ikiwa nyumba hiyo inastahili, acheni amani mnayoitakia ikae juu yake; lakini ikiwa haistahili, acheni amani yenu irudi kwenu.” (Mathayo 10:12, 13) Ujumbe tunaohubiri ni habari njema. Biblia inauita “habari njema ya amani,” “habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu,” na “hii habari njema ya ufalme.” (Waefeso 6:15; Matendo 20:24; Mathayo 24:14) Kusudi letu si kuchambua-chambua imani ya watu wengine wala kubishana nao kuhusu maoni yao, bali ni kuwaeleza habari njema kutoka katika Neno la Mungu.

4. Unaweza kusema nini unapoambiwa, “Mimi sipendezwi” hata kabla hujasema kusudi la ziara yako?

4 Hata bila kusikiliza, huenda mwenye nyumba akasema hivi: “Mimi sipendezwi.” Katika visa vingi, unaweza kusema hivi: “Nilitaka tu kukusomea andiko moja fupi katika Biblia.” Huenda asikatae wazo hilo. Katika visa vingine, huenda ikafaa kusema: “Nilitaka kukueleza kuhusu wakati ambapo hakutakuwa na ukosefu wa haki na watu wote watajifunza kupendana.” Ikiwa mwenye nyumba haonyeshi mara moja tamaa ya kutaka kujua mengi zaidi, unaweza kuongeza hivi: “Inaonekana nimekuja wakati usiofaa.” Hata kama mwenye nyumba haitikii kwa amani, je, tukate kauli kwamba ‘hastahili’? Hata mtu aitikieje, kumbuka shauri la Biblia la kuwa ‘mpole kwa wote, mwenye kujizuia chini ya uovu.’—2 Timotheo 2:24.

Mwenye Dharau Lakini Asiye na Ujuzi

5, 6. Sauli aliwatendeaje wafuasi wa Yesu, na kwa nini alitenda hivyo?

5 Katika karne ya kwanza, mwanamume aliyeitwa Sauli alijulikana sana kwa usemi wake wenye dharau na hata kwa mwenendo wake wenye jeuri. Biblia inasema kwamba alikuwa ‘akiwatisha wanafunzi wa Bwana na alitaka kuwaua.’ (Matendo 9:1, 2) Baadaye, alikiri kwamba alikuwa “mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau.” (1 Timotheo 1:13) Ingawa huenda baadhi ya watu wake wa ukoo walikuwa Wakristo tayari, alisema hivi kuhusu mtazamo wake kuwaelekea wafuasi wa Kristo: “Kwa kuwa nilikuwa nimejawa na wazimu kupita kiasi juu yao, nilifikia hatua ya kuwatesa hata katika majiji ya nje.” (Matendo 23:16; 26:11; Waroma 16:7, 11) Hakuna uthibitisho kwamba wanafunzi walijaribu kujadiliana na Sauli hadharani alipokuwa akitenda hivyo.

6 Kwa nini Sauli alitenda hivyo? Miaka mingi baadaye, aliandika hivi: “Nilikosa ujuzi nami nilitenda kwa ukosefu wa imani.” (1 Timotheo 1:13) Alikuwa Farisayo, ambaye alielimishwa “kwa usahihi kabisa Sheria ya mababu.” (Matendo 22:3) Ingawa yaonekana Gamalieli, mwalimu wa Sauli, hakuwa mbaguzi, kuhani mkuu Kayafa, ambaye Sauli alishirikiana naye alikuwa na msimamo mkali. Kayafa ndiye aliyeongoza njama ya kumuua Yesu Kristo. (Mathayo 26:3, 4, 63-66; Matendo 5:34-39) Baadaye, Kayafa alihakikisha kwamba mitume wa Yesu walipigwa viboko, naye akawaagiza kwa ukali waache kusema kuhusu jina la Yesu. Kayafa ndiye aliyeongoza kile kikao cha Sanhedrini kilichojaa vurugu wakati Stefano alipopelekwa kupigwa mawe. (Matendo 5:27, 28, 40; 7:1-60) Sauli alitazama Stefano akipigwa mawe, naye Kayafa akamwagiza Sauli aendelee kuwakandamiza wafuasi wa Yesu kwa kuwakamata huko Damasko. (Matendo 8:1; 9:1, 2) Chini ya ushawishi huo wa Kayafa, Sauli alifikiri kuwa mwenendo wake ulionyesha kwamba ana bidii kwa Mungu, lakini ni wazi kwamba hakuwa na imani ya kweli. (Matendo 22:3-5) Kwa sababu hiyo, Sauli alikosa kutambua kwamba Yesu ndiye Masihi wa kweli. Lakini Sauli alitambua mwenendo wake hatari wakati Yesu aliyefufuliwa alipozungumza naye kimuujiza kwenye barabara inayoelekea Damasko.—Matendo 9:3-6.

7. Matokeo yalikuwa nini Sauli alipokutana na Yesu kwenye barabara iliyoelekea Damasko?

7 Punde tu baada ya tukio hilo, mwanafunzi Anania alitumwa akamhubirie Sauli. Je, ungekuwa tayari kwenda kumhubiria? Anania aliogopa, lakini alizungumza naye kwa upole. Mtazamo wa Sauli ulikuwa umebadilika kwa sababu ya kukutana na Yesu kimuujiza kwenye barabara iliyoelekea Damasko. (Matendo 9:10-22) Baadaye, aliitwa mtume Paulo, mmishonari Mkristo mwenye bidii.

Mpole Lakini Jasiri

8. Yesu alionyeshaje mtazamo kama wa Baba yake kuelekea watu waliotenda mabaya?

8 Yesu alikuwa mhubiri wa Ufalme mwenye bidii ambaye alikuwa mpole lakini jasiri katika kushughulika na watu. (Mathayo 11:29) Alionyesha mtazamo wa Baba yake wa mbinguni, ambaye huwahimiza waovu waache njia zao mbaya. (Isaya 55:6, 7) Wakati watenda-dhambi walipoonyesha nia ya kubadilika, Yesu alitambua jambo hilo, naye akawatia moyo. (Luka 7:37-50; 19:2-10) Badala ya kuwahukumu watu kwa kutegemea sura ya nje, Yesu aliiga fadhili, subira, na ustahimilivu wa Baba yake kwa kutumaini kwamba watu hao wangetubu. (Waroma 2:4) Ni mapenzi ya Yehova kwamba watu wa namna zote watubu na kuokolewa.—1 Timotheo 2:3, 4.

9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi andiko la Isaya 42:1-4 lilivyotimizwa kuhusiana na Yesu?

9 Akionyesha maoni ya Yehova kumhusu Yesu Kristo, Mathayo, mwandikaji wa Injili, anataja maneno haya ya unabii: “Tazama! Mtumishi wangu ambaye nilimchagua, mpendwa wangu, ambaye nafsi yangu ilimkubali! Nitatia roho yangu juu yake, na yaliyo haki atayafanya kuwa wazi kwa mataifa. Hatagombeza, wala hatapaaza sauti kubwa, wala yeyote hatasikia sauti yake katika njia pana. Hakuna tete lililovunjika ambalo ataliponda, na hakuna utambi wa kitani unaotoa moshi atakaouzima, mpaka atakapoileta haki kwa mafanikio. Kwa kweli, mataifa yatalitumainia jina lake.” (Mathayo 12:17-21; Isaya 42:1-4) Kupatana na maneno hayo ya unabii, Yesu hakujihusisha na mabishano yenye kelele. Hata alipokuwa chini ya mkazo, alifundisha kweli kwa njia iliyowavutia watu wenye mioyo minyoofu.—Yohana 7:32, 40, 45, 46.

10, 11. (a) Ingawa Mafarisayo walikuwa kati ya wapinzani wa Yesu waliosema waziwazi zaidi, kwa nini aliwahubiria baadhi yao? (b) Ni majibu ya aina gani ambayo mara kwa mara Yesu aliwatolea wapinzani wake, lakini hakufanya nini?

10 Wakati wa huduma yake, Yesu alizungumza na Mafarisayo wengi. Ingawa baadhi yao walijaribu kumnasa kwa maneno, Yesu hakukata kauli kwamba wote walikuwa na nia mbaya. Yaelekea Simoni, aliyekuwa Farisayo mwenye kuchambua-chambua, alitaka kumwona Yesu kwa ukaribu zaidi, hivyo akamwalika kwa ajili ya mlo. Yesu alikubali mwaliko huo, naye akawahubiria wale waliokuwapo. (Luka 7:36-50) Pindi moja, Farisayo mmoja mashuhuri aliyeitwa Nikodemo alienda kumwona Yesu kwa siri usiku. Yesu hakumlaumu kwa kungoja kuwe na giza ili kuja kumwona. Badala yake, alimhubiria Nikodemo kuhusu upendo ambao Mungu alionyesha kwa kumtuma Mwana wake ili kufungua njia kwa ajili ya wokovu wa wale wanaoamini. Kwa fadhili, Yesu pia alitaja umuhimu wa kuonyesha utii kwa mpango wa Mungu. (Yohana 3:1-21) Baadaye, Nikodemo alimtetea Yesu wakati habari nzuri kumhusu ilipopuuzwa na Mafarisayo wengine.—Yohana 7:46-51.

11 Yesu alikuwa na uwezo wa kutambua unafiki wa wale waliokuwa wakijaribu kumnasa kwa maneno. Hakuruhusu wapinzani wamhusishe katika mabishano yasiyo na maana. Hata hivyo, ilipofaa, alitoa jibu fupi na lenye nguvu kwa kutaja kanuni fulani, kwa kutumia mfano, au kwa kunukuu andiko. (Mathayo 12:38-42; 15:1-9; 16:1-4) Nyakati nyingine, Yesu alinyamaza ilipokuwa wazi kwamba hakuna matokeo mazuri ambayo yangepatikana kwa kujibu.—Marko 15:2-5; Luka 22:67-70.

12. Hata alipopigiwa kelele, Yesu aliwezaje kuwasaidia watu?

12 Mara kwa mara, Yesu alipigiwa kelele na watu waliokuwa na roho wachafu. Hilo lilipotukia, alijizuia na hata alitumia nguvu zake alizopewa na Mungu ili kuwaletea kitulizo. (Marko 1:23-28; 5:2-8, 15) Ikiwa watu fulani wanakuwa na hasira na kutupigia kelele tunapohubiri, sisi pia tunahitaji kujizuia, na kujitahidi kushughulikia hali hiyo kwa fadhili na busara.—Wakolosai 4:6.

Katika Familia

13. Kwa nini nyakati nyingine watu humpinga mtu wa familia anayeanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova?

13 Mara nyingi uhitaji wa kujizuia wa wafuasi wa Yesu unakuwa wazi zaidi katika familia. Mtu ambaye moyo wake umeguswa sana na kweli ya Biblia hutamani familia yake iitikie kwa njia hiyohiyo. Lakini kama Yesu alivyosema, huenda watu wa familia wakatupinga vikali. (Mathayo 10:32-37; Yohana 15:20, 21) Kuna sababu mbalimbali zinazoweza kutokeza hali hiyo. Kwa mfano, ingawa mafundisho ya Biblia yanaweza kutusaidia kuwa wanyoofu, wenye kutegemeka, na wenye heshima, Maandiko pia yanafundisha kwamba katika hali yoyote ile wajibu wetu mkubwa zaidi ni kwa Muumba wetu. (Mhubiri 12:1, 13; Matendo 5:29) Huenda mtu fulani katika familia akakasirika kwa kuhisi kwamba mamlaka yake katika familia yanapungua kwa kadiri fulani kwa sababu ya ushikamanifu wetu kwa Yehova. Tunaposhughulika na hali kama hiyo, ni muhimu kufuata mfano wa Yesu wa kujizuia.—1 Petro 2:21-23; 3:1, 2.

14-16. Ni nini kilichowabadili baadhi ya watu ambao mwanzoni waliwapinga watu wa familia zao?

14 Wengi wa wale wanaomtumikia Yehova sasa walikuwa na mwenzi wa ndoa au mtu mwingine wa familia aliyepinga mabadiliko waliyokuwa wakifanya walipoanza kujifunza Biblia. Huenda wapinzani hao walisikia habari zisizofaa kuhusu Mashahidi wa Yehova, na pengine waliogopa kwamba kungekuwa na uvutano mbaya katika familia. Ni nini kilichowafanya wabadili mtazamo wao? Katika visa vingi, mfano mzuri wa mwamini ulikuwa na uvutano mzuri. Nyakati nyingine upinzani katika familia ulipungua kwa sababu mwamini alisimama imara kwa kufuata mashauri ya Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri, huku pia akitimiza madaraka ya familia na kujizuia licha ya kutukanwa.—1 Petro 2:12.

15 Huenda pia mpinzani akawa amekataa kusikiliza maelezo yoyote kutoka katika Biblia kwa sababu ya chuki isiyo na msingi au kiburi. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kuhusu mtu mmoja huko Marekani aliyesema kwamba aliipenda sana nchi yake. Siku moja, mtu huyo alichukua mavazi yake yote na kuondoka wakati mke wake alipokuwa kwenye kusanyiko la wilaya. Wakati mwingine, alitoka nyumbani akiwa na bunduki na kutishia kujiua. Kila mara alipofanya mambo yasiyofaa, mtu huyo aliilaumu dini ya mke wake. Lakini mke wake aliendelea kujitahidi kufuata mashauri ya Biblia. Miaka 20 baada ya mke wake kubatizwa, mtu huyo pia akawa Shahidi wa Yehova. Huko Albania, mwanamke mmoja alikasirika kwa sababu binti yake alijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na baadaye akabatizwa. Mama huyo aliharibu Biblia ya binti yake mara 12. Kisha siku moja alifungua Biblia mpya ambayo binti yake aliacha kwenye meza. Bila kutarajia, Biblia ikafunguka kwenye andiko la Mathayo 10:36, na mama huyo akatambua kwamba yaliyosemwa hapo yalimhusu. Hata hivyo, kwa sababu mama huyo alihangaikia sana hali ya binti yake, alimsindikiza hadi kwenye mashua ili asafiri pamoja na Mashahidi wengine kwenda kwenye kusanyiko la wilaya nchini Italia. Mama huyo alipoona upendo, kukumbatiana, na tabasamu za wale waliokuwa wakisafiri na kusikia vicheko vyao vya furaha, hisia zake zilianza kubadilika. Punde baada ya tukio hilo, alikubali kujifunza Biblia. Leo yeye hujitahidi kuwasaidia wengine ambao mwanzoni huonyesha upinzani.

16 Katika kisa fulani, wakati mwanamke mmoja alipokuwa akielekea kwenye Jumba la Ufalme, mume wake alimkabili huku akiwa amebeba kisu na kumshutumu vikali. Mke wake alimjibu kwa upole: “Ingia katika Jumba la Ufalme, na ujionee mwenyewe.” Alikubali, na baada ya muda akawa mzee Mkristo.

17. Ni mashauri gani ya Biblia yanayoweza kusaidia wakati hali ya kutoelewana inapotokea katika familia ya Kikristo?

17 Hata ikiwa kila mtu katika familia yako ni Mkristo, nyakati nyingine huenda kukawa na hali ya kutoelewana, na kwa sababu ya kutokamilika kwa wanadamu, watu wa familia wanaweza kutumia maneno makali. Shauri hili lilifaa kwa Wakristo wa Efeso la kale: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Waefeso 4:31) Yaelekea Wakristo wa Efeso waliathiriwa na mazingira yao, hali yao ya kutokamilika, na hata wengine waliathiriwa na maisha yao ya zamani. Ni nini kingewasaidia kubadilika? Walihitaji ‘kufanywa upya katika nguvu zilizoendesha akili zao.’ (Waefeso 4:23) Matunda ya roho ya Mungu yangeonekana wazi zaidi katika maisha yao kama wangeendelea kujifunza Neno la Mungu, kutafakari kuhusu jinsi linavyopaswa kuongoza maisha yao, kushirikiana na Wakristo wenzao, na kusali kwa bidii. Wangejifunza kuwa ‘wenye fadhili kwa mtu na mwenzake, wenye huruma nyororo, wakisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe kwa hiari.’ (Waefeso 4:32) Haidhuru yale ambayo huenda wengine wakafanya, tunahitaji kujizuia, kuwa wenye fadhili, wenye huruma, na wenye kusamehe. Kwa kweli, hatupaswi ‘kumlipa yeyote uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17, 18) Ni vizuri sikuzote kuonyesha upendo wa kweli kwa kumwiga Mungu.—1 Yohana 4:8.

Shauri kwa Wakristo Wote

18. Kwa nini shauri linalopatikana kwenye 2 Timotheo 2:24 lilifaa kwa mzee katika Efeso la kale, na linawezaje kuwafaidi Wakristo wote?

18 Shauri juu ya kuendelea “kujizuia chini ya uovu” linawahusu Wakristo wote. (2 Timotheo 2:24) Lakini shauri hilo lilitolewa kwanza kwa Timotheo, ambaye alilihitaji alipotumika akiwa mzee huko Efeso. Baadhi ya watu katika kutaniko hilo walitoa maoni yao waziwazi na kufundisha uwongo. Walikosa kuthamini umuhimu wa imani, upendo, na dhamiri njema kwa sababu hawakutambua vizuri kusudi la Sheria ya Musa. Kiburi kilitokeza mizozo walipojiingiza katika mabishano juu ya maneno, huku wakikosa kuelewa umuhimu wa mafundisho ya Kristo na ujitoaji-kimungu. Ili kushughulikia hali hiyo, Timotheo alipaswa kuitetea kweli ya Biblia kwa uthabiti. Hata hivyo, alihitaji kushughulika na ndugu zake kwa upole. Kama vile wazee wa siku hizi, alijua kwamba kundi halikuwa lake na kwa hiyo alipaswa kushughulika na wengine katika njia ambayo ingeendeleza upendo na umoja wa Kikristo.—Waefeso 4:1-3; 1 Timotheo 1:3-11; 5:1, 2; 6:3-5.

19. Kwa nini ni muhimu kwetu sote ‘kutafuta upole’?

19 Mungu anawahimiza watu wake ‘watafute upole.’ (Sefania 2:3) Neno la Kiebrania “upole” linamaanisha mwelekeo unaomwezesha mtu kuvumilia ubaya kwa subira, bila kuudhika wala kulipiza kisasi. Na tumwombe Yehova msaada kwa bidii ili tuweze kuonyesha sifa ya kujizuia na hivyo kumwakilisha ifaavyo, hata chini ya hali ngumu.

Ulijifunza Nini?

• Unapoambiwa maneno yenye dharau, ni maandiko gani yanayoweza kukusaidia?

• Kwa nini Sauli alitenda kwa dharau?

• Mfano wa Yesu unatusaidiaje kushughulika ifaavyo na watu wa aina zote?

• Tunaweza kupata faida gani kwa kujizuia tunaposema na watu wa familia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ingawa Sauli alikuwa na sifa mbaya, Anania alimtendea kwa fadhili

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mkristo anaweza kutuliza upinzani katika familia kwa kutimiza madaraka yake kwa uaminifu

[Picha katika ukurasa wa 30]

Wakristo huendeleza upendo na umoja