Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumjua Mungu Huimarisha Familia

Kumjua Mungu Huimarisha Familia

“Msaada Wangu Unatoka Kwa Yehova”

Kumjua Mungu Huimarisha Familia

“UKUTA wa Berlin.” Hivyo ndivyo wenzi fulani wa ndoa huko Argentina walivyouita ukuta halisi ambao walijenga ili kugawanya nyumba yao mara mbili! Walikuwa wamekosana kabisa na walichukiana sana.

Kwa kuhuzunisha, wengine pia wanakabili hali kama hiyo. Kuna ugomvi, ukosefu wa uaminifu, na uhasama katika familia nyingi. Jambo hilo linasikitisha kwa sababu Mungu ndiye aliyeanzisha mpango wa familia. (Mwanzo 1:27, 28; 2:23, 24) Mpango huo ni zawadi kutoka kwa Mungu ambayo huwawezesha watu kuonyeshana upendo katika familia. (Ruthu 1:9) Watu wa familia wanapotimiza wajibu wao waliopewa na Mungu, wao humheshimu Yehova na kuwafurahisha wengine katika familia. *

Kwa kuwa Mungu ndiye aliyeanzisha familia, tunapaswa kuacha maoni yake yatusaidie kuelewa jinsi familia zinavyopaswa kuwa. Neno lake lina mashauri mengi yanayoweza kusaidia familia zifanikiwe, hasa zinapokabili magumu. Biblia inasema hivi kuhusu daraka la waume: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” Mume anapotimiza takwa hilo, mke hufurahia “kumheshimu sana.”—Waefeso 5:25-29, 33.

Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu uhusiano ulio kati ya wazazi na watoto wao: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Jambo hilo hufanya familia iwe na uchangamfu, na inakuwa rahisi kwa watoto kuwatii wazazi wao.—Waefeso 6:1.

Mambo yaliyotajwa hapo juu yanaonyesha ubora wa mashauri ya Biblia kuhusu maisha ya familia. Wengi hupata furaha katika familia wanapotii kanuni za Mungu. Kwa mfano, fikiria wale wenzi wa ndoa huko Argentina ambao wametajwa mwanzoni mwa makala hii. Baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kwa miezi mitatu, wote wawili walianza kutii mashauri ya Biblia yenye hekima kuhusu ndoa. Walijitahidi sana kuboresha mawasiliano yao, kuhangaikiana, na kusameheana. (Methali 15:22; 1 Petro 3:7; 4:8) Walijifunza kuzuia hasira, na walimwomba Mungu awasaidie mambo yalipoharibika. (Wakolosai 3:19) Muda si muda, “Ukuta wa Berlin” uliporomoka!

Mungu Anaweza Kuimarisha Familia

Kujua na kufuata viwango vya Mungu kunaweza kuimarisha familia kukabiliana na magumu. Hilo ni muhimu kwa kuwa ilitabiriwa kwamba familia zingekabili mashambulizi makali katika siku zetu. Paulo alitabiri kuzorota kwa maadili na upotovu wa wanadamu uliopo sasa. Alisema kwamba katika “siku za mwisho” kungekuwa na ukosefu wa ushikamanifu, ukosefu wa “upendo wa asili,” na hali ya kutotii wazazi, hata miongoni mwa wale ‘walio na namna ya ujitoaji-kimungu.’—2 Timotheo 3:1-5.

Kujitahidi kumpendeza Mungu kunaweza kuwasaidia watu wakabiliane na hali hizo mbaya zinazoikumba familia. Familia nyingi zimegundua kwamba zinahitaji msaada wa kiroho ili kukabiliana na magumu yao mengi. Ikiwa watu katika familia wanataka kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Mungu, wanapaswa kutumia kanuni za Biblia na kutambua kwamba “Yehova mwenyewe asipoijenga nyumba, ni bure kwamba wajenzi wake wameifanyia kazi ngumu.” (Zaburi 127:1) Ni lazima Mungu atangulizwe ili familia iwe na furaha.—Waefeso 3:14, 15.

Huko Hawaii, mwanamume mmoja anayeitwa Dennis alitambua kwamba jambo hilo ni kweli. Ingawa alidai kuwa Mkristo, alizoea kutumia matusi na kupigana. Baada ya kutumika jeshini, akawa mwenye jeuri na mwenye chuki hata zaidi. Anasema hivi: “Nilipigana mara nyingi. Sikujali yaliyonipata, na sikuogopa kufa. Niliendelea kutumia matusi na kupigana. Mke wangu ambaye ni Shahidi wa Yehova alinitia moyo nijifunze Biblia.”

Dennis alipinga jitihada za mke wake. Hata hivyo, maoni yake yalibadilika alipoona matendo ya Kikristo ya mke wake. Baada ya muda, Dennis alihudhuria mkutano wa Kikristo pamoja na mke wake na watoto wake. Kisha, akaanza kujifunza Biblia, naye akafanya maendeleo. Ingawa alikuwa amevuta sigara kwa miaka 28, aliacha zoea hilo na kuacha kushirikiana na marafiki waliofanya mambo aliyokuwa akijaribu kuyaepuka. Akiwa mwenye shukrani kwa Yehova, Dennis alisema: “Maisha ya familia yetu yaliboreka. Tulienda mikutanoni na katika huduma tukiwa familia. Watoto wangu wawili waliacha kuniogopa, kwa kuwa nilijifunza kuzuia hasira na kuacha kutumia matusi. Tuliongea pamoja na kufurahia mazungumzo ya Biblia. Kama singalijifunza Biblia, singalikuwa hai leo, kwa sababu nilikuwa na zoea la kukasirika upesi.”

Familia zinaweza kupata furaha zinapojitahidi kufanya mapenzi ya Yehova. Mambo ya hakika yameonyesha kwamba hali huwa afadhali hata kama ni mtu mmoja tu katika familia anayefuata kanuni za Biblia. Kujenga familia ya Kikristo ni kazi ngumu inayohitaji ustadi na wakati. Lakini watu katika familia hizo wana uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zao na atawasaidia kufanikiwa. Wanaweza kusema hivi kama mtunga-zaburi: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”—Zaburi 121:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona Kalenda ya Mwaka wa 2005 ya Mashahidi wa Yehova, Mei/Juni.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Kila familia mbinguni na duniani hupata jina kutokana” na Mungu.—WAEFESO 3:15

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

YEHOVA ANATHAMINI MPANGO WA FAMILIA

“Mungu akawabariki na Mungu akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.’”—Mwanzo 1:28.

“Mwenye furaha ni kila mtu anayemwogopa Yehova . . . Mke wako atakuwa kama mzabibu unaozaa matunda katika sehemu za ndani kabisa za nyumba yako.”—Zaburi 128:1, 3.