Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuzijua Njia za Yehova

Kuzijua Njia za Yehova

Kuzijua Njia za Yehova

“Nijulishe . . . njia zako, nipate kukujua.”—Kutoka 33:13.

1, 2. (a) Kwa nini Musa alitenda kwa ukali alipomwona Mmisri akimtendea vibaya Mwebrania? (b) Musa alihitaji kujifunza nini ili astahili kumtumikia Yehova?

MUSA alikuwa amelelewa katika nyumba ya Farao na kufundishwa hekima iliyoheshimiwa sana na watawala wa Misri. Hata hivyo, Musa alijua kwamba hakuwa Mmisri. Wazazi wake walikuwa Waebrania. Akiwa na umri wa miaka 40, alitoka kwenda kuwaangalia ndugu zake, Waisraeli. Alipomwona Mmisri akimtendea vibaya Mwebrania mmoja, Musa hakutazama tu bila kufanya lolote. Alimpiga na kumuua Mmisri huyo. Musa alichagua kuwa upande wa watu wa Yehova, naye alifikiri kwamba Mungu alikuwa akimtumia ili kuwakomboa ndugu zake. (Matendo 7:21-25; Waebrania 11:24, 25) Kisa hicho kilipojulikana, mfalme wa Misri alimwona Musa kuwa mwasi, na Musa akalazimika kukimbia ili kuokoa uhai wake. (Kutoka 2:11-15) Ili Musa atumiwe na Mungu, alipaswa kuzijua vizuri njia za Yehova. Je, Musa angekubali kufundishwa?—Zaburi 25:9.

2 Katika miaka 40 iliyofuata, Musa alikuwa mkimbizi na mchungaji. Badala ya kuwa na uchungu mwingi kwa sababu yaelekea ndugu zake Waebrania hawakumheshimu, Musa alikubali kwenda uhamishoni kama Mungu alivyoruhusu. Ingawa miaka mingi ilipita bila yeye kutambuliwa na yeyote, Musa alikubali Yehova amsaidie kuboresha utu wake. Musa hakuwa anajisifu alipoandika maneno haya baadaye chini ya mwongozo wa roho takatifu ya Mungu: “Mtu huyu Musa alikuwa mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hesabu 12:3) Yehova alimtumia Musa kwa njia za pekee, naye atatubariki pia tukitafuta upole.—Sefania 2:3.

Musa Apewa Kazi

3, 4. (a) Yehova alimpa Musa kazi gani? (b) Musa alisaidiwaje?

3 Siku moja malaika aliyemwakilisha Yehova alizungumza na Musa karibu na Mlima Horebu kwenye Peninsula ya Sinai. Musa aliambiwa hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo. Nami ninashuka ili kuwakomboa kutoka katika mkono wa Wamisri na kuwatoa katika nchi hiyo mpaka kwenye nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Kutoka 3:2, 7, 8) Hivyo, Mungu alitaka Musa afanye kazi fulani, lakini alipaswa aifanye kulingana na vile Yehova alivyotaka.

4 Malaika wa Yehova aliendelea kusema: “Sasa njoo, nikutume kwa Farao, nawe uwatoe watu wangu wana wa Israeli kutoka Misri.” Musa alisita. Alihisi kwamba hastahili na kwamba ikiwa angetegemea uwezo wake mwenyewe, hangefanikiwa. Hata hivyo, Yehova alimhakikishia Musa hivi: “Nitakuwa pamoja nawe.” (Kutoka 3:10-12) Yehova alimpa Musa nguvu za kufanya miujiza mbalimbali ili kuthibitisha kwamba alikuwa kwa kweli ametumwa na Mungu. Haruni, ndugu ya Musa, angeandamana naye ili kuwa msemaji wake. Yehova angewafundisha yale ambayo wangesema na kufanya. (Kutoka 4:1-17) Je, Musa angetimiza kwa uaminifu kazi hiyo?

5. Kwa nini mtazamo wa Waisraeli ulikuwa tatizo kwa Musa?

5 Mwanzoni, wanaume wazee wa Israeli waliwaamini Musa na Haruni. (Kutoka 4:29-31) Hata hivyo, punde si punde, “maofisa wa wana wa Israeli” walimlaumu Musa na ndugu yake kwa kuwafanya ‘wanuke vibaya’ mbele ya Farao na watumishi wake. (Kutoka 5:19-21; 6:9) Waisraeli walipokuwa wakiondoka Misri, waliogopa walipoona magari ya Wamisri yakiwafuata. Huku Bahari Nyekundu ikiwa mbele yao na magari ya vita nyuma yao, walihisi wamenaswa, nao wakamlaumu Musa. Wewe ungefanyaje? Ingawa Waisraeli hawakuwa na mashua, Musa alifuata mwongozo wa Yehova na kuwahimiza watu wavunje kambi. Kisha Mungu akafanya maji ya Bahari Nyekundu yarudi nyuma, na Waisraeli wakapita katikati ya bahari juu ya nchi kavu.—Kutoka 14:1-22.

Suala Kuu Kuliko Ukombozi

6. Yehova alikazia nini alipomtuma Musa?

6 Yehova alikazia umuhimu wa jina lake alipomtuma Musa. Ilikuwa muhimu kuliheshimu jina hilo na Yule ambaye linawakilisha. Yehova alimwambia Musa hivi alipouliza kuhusu jina lake: “Nitakuwa kile nitakachokuwa.” Isitoshe, Musa alipaswa kuwaambia wana wa Israeli hivi: “Yehova Mungu wa mababu zenu, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu.” Kisha Yehova akaongeza hivi: “Hilo ndilo jina langu mpaka wakati usio na kipimo, na huo ndio ukumbusho wangu kwa kizazi baada ya kizazi.” (Kutoka 3:13-15) Watumishi wa Mungu ulimwenguni pote wanajua kwamba Yehova bado ndilo jina la Mungu.—Isaya 12:4, 5; 43:10-12.

7. Mungu alimhimiza Musa afanye nini licha ya kiburi cha Farao?

7 Walipoenda mbele ya Farao, Musa na Haruni walimtolea ujumbe kwa jina la Yehova. Lakini kwa kiburi Farao akasema hivi: “Yehova ni nani, hivi kwamba mimi niitii sauti yake na kuwaruhusu Israeli waende zao? Simjui Yehova hata kidogo na tena sitawaruhusu Israeli waende zao.” (Kutoka 5:1, 2) Farao alikuwa mwenye moyo mgumu na mdanganyifu. Hata hivyo, Yehova alimhimiza Musa amtolee Farao ujumbe tena na tena. (Kutoka 7:14-16, 20-23; 8:1, 2, 20) Musa aliona kwamba Farao alikuwa amekasirika. Je, kungekuwa na faida yoyote kumkabili tena? Waisraeli walitamani sana kukombolewa. Farao alikataa katakata. Wewe ungefanyaje?

8. Ni faida gani iliyotokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Farao, na matukio hayo yanapaswa kuwa na uvutano gani juu yetu?

8 Musa alitoa ujumbe mwingine, kwa kusema: “Hivi ndivyo Yehova Mungu wa Waebrania amesema: ‘Waruhusu watu wangu waende zao wapate kunitumikia.’” Pia Mungu alisema: “Kufikia sasa ningalikuwa nimenyoosha mkono wangu nipate kukupiga wewe na watu wako kwa tauni ili ufutiliwe mbali kutoka duniani. Lakini, kwa kweli, kwa sababu hii nimekuacha uendelee kuwako, ili kukuonyesha nguvu zangu na ili nifanye jina langu litangazwe katika dunia yote.” (Kutoka 9:13-16) Kwa kutekeleza hukumu juu ya Farao mwenye moyo mgumu, Yehova alikusudia kuonyesha nguvu zake kwa njia ambayo ingetoa onyo kwa wote wanaompinga. Onyo hilo pia lingemhusu Shetani Ibilisi, yule ambaye baadaye Yesu Kristo alimwita “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30; Waroma 9:17-24) Kama ilivyotabiriwa, jina la Yehova lilitangazwa duniani pote. Uvumilivu wake uliwawezesha Waisraeli wahifadhiwe hai pamoja na umati mkubwa uliojiunga nao kumwabudu. (Kutoka 9:20, 21; 12:37, 38) Tangu wakati huo, kutangazwa kwa jina la Yehova kumewafaidi mamilioni ya watu wengine ambao wamekubali ibada ya kweli.

Kushughulika na Watu Wagumu

9. Watu wa Musa walionyeshaje kwamba hawakumheshimu Yehova?

9 Waebrania walilijua jina la Mungu. Musa alilitumia alipozungumza nao, lakini sikuzote hawakuonyesha heshima inayofaa kuelekea Mwenye jina hilo. Mara tu baada ya Yehova kuwakomboa Waisraeli kimuujiza kutoka Misri, kulitukia nini walipokosa kupata kwa haraka maji safi ya kunywa? Walimnung’unikia Musa. Baadaye, walilalamika kuhusu chakula. Musa aliwaonya kwamba hawakuwa wakinung’unika tu juu yake na Haruni, bali juu ya Yehova. (Kutoka 15:22-24; 16:2-12) Kwenye Mlima Sinai, Yehova aliwapa Waisraeli Sheria, na wakati huohuo akafanya mambo yanayozidi nguvu za asili. Hata hivyo, kwa kutotii, watu hao walitengeneza ndama ya dhahabu ili kuiabudu, nao wakadai kwamba walikuwa wakifanya “sherehe kwa ajili ya Yehova.”—Kutoka 32:1-9.

10. Kwa nini ombi la Musa kwenye Kutoka 33:13 ni muhimu sana kwa waangalizi Wakristo leo?

10 Musa angeshughulikaje na watu ambao Yehova mwenyewe alisema kwamba wana shingo ngumu? Musa alimwomba Yehova hivi: “Tafadhali, ikiwa nimepata kibali machoni pako, nijulishe, tafadhali, njia zako, nipate kukujua, ili nipate kibali machoni pako.” (Kutoka 33:13) Waangalizi Wakristo wanaoshughulika na Mashahidi wa Yehova wa siku hizi wanalichunga kundi la watu wanyenyekevu zaidi kuliko taifa la Israeli. Hata hivyo, waangalizi hao pia husali hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe.” (Zaburi 25:4) Kuzijua njia za Yehova huwasaidia washughulikie hali mbalimbali kupatana na Neno la Mungu na kulingana na utu wake.

Yehova Anatarajia Nini kwa Watu Wake?

11. Yehova alitoa miongozo gani kwa Musa, na kwa nini tunapendezwa kuijua?

11 Kwenye Mlima Sinai, Yehova alieleza kwa mdomo yale aliyotarajia watu wake wafanye. Baadaye, Musa alipokea mabamba mawili yaliyokuwa yameandikwa zile Amri Kumi. Aliposhuka kutoka mlimani, aliwaona Waisraeli wakiabudu ndama ya kuyeyushwa, na kwa hasira akayatupa yale mabamba chini, na kuyavunja-vunja. Yehova aliandika tena zile Amri Kumi kwenye mabamba ya mawe ambayo Musa alichonga. (Kutoka 32:19; 34:1) Amri hizo hazikuwa zimebadilika tangu zitolewe mara ya kwanza. Musa alipaswa kuzifuata. Pia Mungu alimweleza Musa Yeye ni mtu wa aina gani, na kumwonyesha jinsi alivyopaswa kujiendesha akiwa mtumishi wake. Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, lakini yale ambayo Yehova alimwambia Musa yana kanuni nyingi za msingi ambazo hazibadiliki na ambazo bado zinawahusu wote wanaomwabudu Yehova. (Waroma 6:14; 13:8-10) Na tuchunguze baadhi ya kanuni hizo.

12. Kwa kuwa Yehova alitaka Waisraeli wajitoe kwake kikamili, walipaswa kufanya nini?

12 Jitoe kikamili kwa Yehova. Taifa lote la Israeli lilikuwepo Yehova aliposema kwamba anataka wajitoe kwake kikamili. (Kutoka 20:2-5) Waisraeli waliona mambo mengi yaliyothibitisha kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli. (Kumbukumbu la Torati 4:33-35) Licha ya yale ambayo mataifa mengine yalikuwa yakifanya, Yehova alionyesha wazi kwamba hangeruhusu watu wake washiriki katika ibada yoyote ya sanamu au kuwasiliana na pepo. Hawakupaswa kujitoa kwake kidesturi tu. Wote walipaswa kumpenda Yehova kwa moyo wao wote, kwa nafsi yao yote, na kwa nguvu zao zote. (Kumbukumbu la Torati 6:5, 6) Hilo lingetia ndani usemi wao, mwenendo wao, naam, kila sehemu ya maisha yao. (Mambo ya Walawi 20:27; 24:15, 16; 26:1) Yesu Kristo pia alionyesha wazi kwamba Yehova anataka tujitoe kwake kikamili.—Marko 12:28-30; Luka 4:8.

13. Kwa nini Waisraeli walipaswa kumtii Mungu kabisa, na ni nini kinachopaswa kutuchochea kumtii? (Mhubiri 12:13)

13 Kutii amri za Yehova kabisa. Waisraeli walihitaji kukumbushwa kwamba walipoingia katika uhusiano wa agano pamoja na Yehova waliweka nadhiri ya kumtii kabisa. Ni kweli kwamba walifurahia uhuru mwingi, lakini walipaswa kutii kabisa mambo hususa ambayo Yehova alikuwa ameamuru. Kwa kufanya hivyo, wangeonyesha kwamba wanampenda Mungu, na hilo lingewafaidi wao na watoto wao kwa sababu matakwa yote ya Yehova yalikuwa kwa faida yao.—Kutoka 19:5-8; Kumbukumbu la Torati 5:27-33; 11:22, 23.

14. Mungu alikaziaje kwa Waisraeli umuhimu wa kutanguliza mambo ya kiroho?

14 Tanguliza mambo ya kiroho. Taifa la Israeli halikupaswa kuruhusu mambo ya kimwili yachukue mahali pa mambo ya kiroho. Waisraeli hawakupaswa kufuatia tu vitu vya kimwili. Yehova alitenga wakati kila juma kwa ajili ya mambo ya kiroho, wakati ambao ungetumiwa tu kwa ajili ya ibada ya Mungu wa kweli. (Kutoka 35:1-3; Hesabu 15:32-36) Kila mwaka, wakati wa ziada ulipaswa kutengwa kwa ajili ya mikusanyiko mitakatifu. (Mambo ya Walawi 23:4-44) Mikusanyiko hiyo ilitoa nafasi ya kuzungumzia matendo yenye nguvu ya Yehova, kukumbushwa njia zake, na kumshukuru kwa ajili ya wema wake wote. Kadiri ambavyo watu hao wangeonyesha kwamba wamejitoa kwa Yehova, ndivyo wangezidi kumpenda na kumwogopa, nao wangesaidiwa kutembea katika njia zake. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Kanuni bora zilizomo katika maagizo hayo huwafaidi watumishi wa Yehova leo.—Waebrania 10:24, 25.

Kuthamini Sifa za Yehova

15. (a) Kwa nini ilikuwa muhimu kwa Musa kuthamini sifa za Yehova? (b) Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia kufikiria kwa uzito kila moja ya sifa za Yehova?

15 Kuthamini sifa za Yehova kungemsaidia Musa pia kushughulika na watu. Andiko la Kutoka 34:5-7 linasema kwamba Mungu alipita mbele ya uso wa Musa huku akisema: “Yehova, Yehova, Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli, anayehifadhi fadhili zenye upendo kwa ajili ya maelfu, anayesamehe kosa na ubaya na dhambi, lakini kwa vyovyote hatakosa kuadhibu, anayeleta adhabu kwa ajili ya kosa la akina baba juu ya wana na juu ya wajukuu, juu ya kizazi cha tatu na juu ya kizazi cha nne.” Tafakari juu ya maneno hayo. Jiulize: ‘Kila moja ya sifa hizo humaanisha nini? Yehova aliionyeshaje? Waangalizi Wakristo wanaweza kuionyeshaje? Sifa hiyo inapaswa kuwa na uvutano gani juu ya matendo ya kila mmoja wetu?’ Na tuchunguze mifano kadhaa.

16. Tunawezaje kuongeza uelewaji wetu kuhusu rehema za Mungu, na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo?

16 Yehova ni “Mungu mwenye rehema na neema.” Ikiwa una kitabu Insight on the Scriptures, unaweza kusoma maelezo yake chini ya kichwa “Mercy” katika Kiingereza (au Étude Perspicace des Écritures, chini ya kichwa “Miséricorde” katika Kifaransa). Au ufanye utafiti kuhusu habari hiyo kwa kutumia Watch Tower Publications Index (Index Des Publications De La Société Watch Tower) au programu ya kompyuta ya Watchtower Library (CD-ROM). * Tumia fahirisi ili kupata maandiko yanayozungumzia rehema. Utaona kwamba rehema za Yehova haziruhusu tu adhabu ipunguzwe nyakati fulani, bali pia zinatia ndani huruma nyororo. Huruma nyororo humchochea Mungu kuchukua hatua ili kuwaletea watu wake kitulizo. Ili kuthibitisha hilo, Mungu alitosheleza mahitaji ya kimwili na ya kiroho ya Waisraeli wakati wa safari yao kuelekea Nchi ya Ahadi. (Kumbukumbu la Torati 1:30-33; 8:4) Yehova alionyesha rehema kwa kutoa msamaha wakati makosa yalipofanywa. Aliwaonyesha watu wake wa kale rehema. Kwa hiyo, leo pia watumishi wake wanapaswa kuhurumiana.—Mathayo 9:13; 18:21-35.

17. Kuelewa neema za Yehova kunaweza kuendelezaje ibada ya kweli?

17 Rehema za Yehova huambatana na neema. Linganisha maana ya neno “neema” na maandiko yanayomtaja Yehova kuwa mwenye neema. Biblia inaonyesha kwamba neema za Yehova zinatia ndani kuwahangaikia kwa upendo watu wa hali ya chini miongoni mwa watu wake. (Kutoka 22:26, 27) Katika nchi yoyote ile, huenda wageni, na pia watu wengine, wakakabili hali mbaya. Alipowafundisha watu wake wasiwe na ubaguzi na waonyeshe wema kwa watu kama hao, Yehova aliwakumbusha kwamba walikuwa pia wageni katika nchi ya Misri. (Kumbukumbu la Torati 24:17-22) Namna gani sisi leo tukiwa watu wa Mungu? Kuwaonyesha wengine neema hutusaidia tuwe na umoja na kuwavuta wengine wamwabudu Yehova.—Matendo 10:34, 35; Ufunuo 7:9, 10.

18. Tunajifunza nini kutokana na yale ambayo Yehova aliwafundisha Waisraeli waepuke kuhusiana na watu wa mataifa mengine?

18 Hata hivyo, Waisraeli hawakupaswa kuacha kumpenda Yehova na viwango vyake vya maadili kwa sababu tu waliwahangaikia watu wa mataifa mengine. Kwa hiyo, walifundishwa kutoiga njia za mataifa yaliyowazunguka, kutofuata desturi zao za kidini, na kutoiga maisha yao yaliyopotoka. (Kutoka 34:11-16; Kumbukumbu la Torati 7:1-4) Mambo hayo pia yanatuhusu leo. Tunapaswa kuwa watu watakatifu kama Mungu wetu Yehova alivyo mtakatifu.—1 Petro 1:15, 16.

19. Kuelewa maoni ya Yehova kuhusu kutenda kosa kunawezaje kuwalinda watu wake?

19 Ili kuhakikisha kwamba Musa alielewa njia Zake, Yehova alionyesha wazi kwamba ingawa hakubaliani na dhambi, yeye si mwepesi wa hasira. Yeye huwapa watu wakati wa kujifunza matakwa yake na kuyatii. Mtu anapotubu, Yehova husamehe dhambi, lakini hakosi kutoa adhabu inayostahili kwa makosa mazito. Alimwonya Musa kwamba vizazi vijavyo vingeweza kupata matokeo mazuri au mabaya kutokana na yale ambayo Waisraeli walifanya. Kuthamini njia za Yehova kunaweza kuwalinda watu wake wasimlaumu kwa sababu ya hali ambazo wao wenyewe wamesababisha au kukata kauli kwamba anakawia kutenda.

20. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushughulika ifaavyo na waamini wenzetu na pia wale tunaokutana nao katika huduma yetu? (Zaburi 86:11)

20 Ikiwa unataka kuongeza ujuzi wako kuhusu Yehova na njia zake, endelea kufanya utafiti na kutafakari unaposoma Biblia. Chunguza kwa makini sehemu mbalimbali zenye kuvutia za utu wa Yehova. Fikiria katika sala jinsi unavyoweza kumwiga Mungu na kujitahidi kupatanisha maisha yako kabisa na kusudi lake. Hilo litakusaidia kuepuka mitego, kushughulika ifaavyo na waamini wenzako, na kuwasaidia wengine kumjua na kumpenda Mungu wetu mtukufu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Vyote vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ulijifunza Nini?

• Kwa nini sifa ya upole ilikuwa muhimu kwa Musa, na kwa nini ni muhimu kwetu?

• Ni jambo gani zuri lililotimizwa kwa kumkabili Farao kwa neno la Yehova tena na tena?

• Ni zipi baadhi ya kanuni za pekee ambazo Musa alifundishwa zinazotuhusu pia?

• Tunawezaje kuongeza uelewaji wetu kuhusu sifa za Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Musa alimtangazia Farao neno la Yehova kwa uaminifu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yehova alimfunulia Musa matakwa yake

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Tafakari juu ya sifa za Yehova