Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Wengi Hawatumii Akili Zao?

Kwa Nini Watu Wengi Hawatumii Akili Zao?

Kwa Nini Watu Wengi Hawatumii Akili Zao?

“SHIDA yake ni nini? Hapaswi kufanya hivyo,” anasema mtu fulani. Mwingine anatikisa kichwa na kwenda zake huku akisema, “Kama angetumia akili yake kidogo tu hangefanya hivyo.” Je, umewahi kusikia watu wakisema hivyo? Ni nini maana ya kutumia akili?

Neno “akili” hufafanuliwa kuwa “uwezo wa kufikiri na kuamua kwa busara,” “uwezo wa kuelewa mambo,” “ufahamu,” “hekima,” au “busara.” Kuwa na akili humaanisha kwamba mtu ana uwezo wa kuamua mambo kwa kutumia akili. Ni wazi kwamba kutumia akili kunatia ndani kutumia uwezo wetu wa kufikiri. Hata hivyo, watu wengi huacha wengine wafikiri kwa niaba yao. Badala ya kujiamulia mambo wenyewe, wao hufuata maoni ya vyombo vya habari, ya marika wao, au yale yanayopendwa na wengi.

Inaonekana katika ulimwengu wa leo watu wengi hawatumii akili zao. Tunawezaje kupata uwezo wa kutumia akili? Kuna manufaa gani ya kutumia akili?

Tunapataje Uwezo wa Kutumia Akili?

Inawezekana kuwa na uwezo wa kutumia akili zetu, ingawa kusitawisha uwezo huo huchukua muda na huhitaji tufikirie mambo kwa makini na kujitahidi daima. Hebu tuchunguze mambo matatu ambayo yanaweza kutusaidia kupata uwezo wa kutumia akili.

Jifunze Biblia, na ufuate mashauri yake. Biblia, ambayo iliandikwa katika lugha bora na kwa hoja zilizo wazi, hutusaidia sana kupata hekima na busara. (Waefeso 1:8) Kwa mfano, mtume Paulo anawashauri Wakristo wenzake hivi: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.” (Wafilipi 4:8) Tukiendelea kufuata shauri hilo, tutafanya maamuzi mazuri na yenye busara.

Jifunze kutokana na uzoefu. Akilinganisha kutumia akili na uzoefu maishani, mtungaji mmoja wa mashairi Mswisi alisema hivi: “Kutumia akili . . . huhusisha uzoefu na uwezo wa kuona kimbele.” Kwa kweli, “mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” (Methali 14:15) Uwezo wa kutumia akili unaweza kusitawishwa kupitia kutazama, kupata mazoezi, na uzoefu. Tunaweza kujifunza kufanya mambo vizuri zaidi kadiri wakati unavyopita. Hata hivyo, tunahitaji kuwa wanyenyekevu na wapole ili kujifunza kutokana na makosa yetu. Mtazamo wa kujidai, kujivuna, na kuwa wenye vichwa vigumu huonyesha kwamba watu katika siku hizi za mwisho hawatumii akili zao vizuri.—2 Timotheo 3:1-5.

Chagua marafiki kwa hekima. Marafiki wetu wanaweza kutusaidia au kutuzuia tusitende kwa hekima au kwa akili. Andiko la Methali 13:20 linasema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” Hatupaswi kukubali njia ya kufikiri au mawazo ya wale wasiomtii Mungu na ambao hulipuuza Neno lake. Andiko la Methali 17:12 linasema hivi: “Afadhali mtu akutane na dubu aliyepoteza watoto wake kuliko kukutana na mjinga katika upumbavu wake.”

Faida za Kutumia Akili

Ni muhimu kusitawisha uwezo wa kutumia akili. Hilo hufanya maisha yawe yenye kupendeza na hata huokoa wakati. Uwezo wa kutumia akili huenda hata ukapunguza mfadhaiko ambao mara nyingi hutokana na kufanya mambo bila kufikiri. Wale wanaokosa uwezo wa kuamua mambo ifaavyo hufanya maisha yawe magumu zaidi kwao wenyewe. Biblia inasema hivi: “Kazi ngumu ya wajinga huwachosha.” (Mhubiri 10:15) Watu hao wanaweza kufanya kazi mfululizo na kujichosha bila kutimiza jambo lolote lenye faida.

Biblia ina mashauri mengi yenye manufaa kuhusu usafi, mawasiliano, kufanya kazi kwa bidii, kupambana na umaskini, na mambo mengine mengi maishani. Mamilioni ya watu wanaweza kukubali kwamba kufanikiwa au kutofanikiwa maishani kumetegemea jinsi ambavyo wamefuata kanuni za Biblia ambazo zimewasaidia kuonyesha hekima.

Kutumia akili hutuwezesha kutimiza mengi kuliko kufuata tu maagizo au sheria nyingi zilizowekwa. Hutusaidia kutimiza majukumu yetu. Hata hivyo, zaidi ya kutumia akili tunahitaji pia kupata ujuzi. Andiko la Methali 1:5 linasema hivi: “Mtu mwenye hekima atasikiliza na kupata mafundisho zaidi.” Tunapaswa pia kujifunza kuchanganua habari tunazopata na kufikia mikataa inayofaa kutokana na habari hizo. Hilo hutusaidia ‘kutembea katika hekima.’—Methali 28:26.

Sifa ya kiasi huambatana na uwezo wa kutumia akili. Ingawa huenda tukataka kutimiza mambo mengi, tunahitaji kuwa na usawaziko na kutofanya mambo yanayozidi uwezo wetu. Ni kweli kwamba mtume Paulo anatuambia ‘tuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Wakorintho 15:58) Hata hivyo, shauri hilo linapaswa kusawazishwa na kanuni inayopatikana kwenye Mhubiri 9:4: “Mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa.” Kutunza ifaavyo afya yetu tunapoendelea kumtumikia Yehova kunaweza kutusaidia kuishi muda mrefu na hivyo kuendelea kuwa watendaji. Kutumia akili kunaweza kutusaidia kuwa na usawaziko ambao hutuwezesha kutimiza mambo ya lazima bila kupoteza shangwe yetu. Naam, kutumia akili huleta faida nyingi.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Mashauri mengi mazuri yanapatikana katika Biblia

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunaweza kupata uwezo wa kutumia akili kwa kutazama, kupata mazoezi, na uzoefu