Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Samweli

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Samweli

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Pili cha Samweli

JE, KUTAMBUA enzi kuu ya Yehova humaanisha tumtii kikamilifu? Je, sikuzote mtu mtimilifu hufanya yaliyo sawa mbele za Mungu? Ni mtu wa aina gani ambaye Mungu wa kweli humwona kuwa ‘anakubalika kwa moyo wake’? (1 Samweli 13:14) Kitabu cha Pili cha Samweli hujibu maswali hayo kwa njia yenye kuridhisha.

Kitabu hicho kiliandikwa na Gadi na Nathani. Manabii hao walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mfalme Daudi wa Israeli la kale. * Walimaliza kukiandika yapata mwaka wa 1040 K.W.K., mwishoni mwa utawala wa Daudi wa miaka 40, nacho kinazungumza hasa kumhusu Daudi na uhusiano wake pamoja na Yehova. Masimulizi hayo yenye kusisimua yanaonyesha jinsi taifa lenye mizozo linavyopata ufanisi na muungano chini ya mfalme hodari. Habari hiyo yenye kuvutia imejaa hisia zenye kina za wanadamu.

DAUDI AWA “MKUU ZAIDI NA ZAIDI”

(2 Samweli 1:1–10:19)

Itikio la Daudi anapopata habari za kifo cha Sauli na Yonathani linaonyesha hisia zake kuwaelekea na kumwelekea Yehova. Huko Hebroni, Daudi anawekwa kuwa mfalme wa kabila la Yuda, naye Ish-boshethi, mwana wa Sauli, anawekwa kuwa mfalme wa yale makabila mengine ya Israeli. Daudi ‘anaendelea kuwa mkuu zaidi na zaidi,’ na miaka saba na nusu hivi baadaye, anafanywa kuwa mfalme wa taifa lote la Israeli.—2 Samweli 5:10.

Daudi anateka Yerusalemu kutoka kwa Wayebusi na kuufanya mji mkuu wa ufalme wake. Jaribio lake la kwanza la kulihamisha sanduku la agano hadi Yerusalemu linatokeza msiba. Lakini, jaribio la pili linafanikiwa, na Daudi anacheza dansi kwa furaha. Yehova anafanya agano pamoja na Daudi kwa ajili ya ufalme. Daudi anawatiisha adui zake, na Mungu anaendelea kuwa pamoja naye.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:18—Kwa nini Yoabu na ndugu zake wawili wanaitwa wana watatu wa Seruya, mama yao? Katika Maandiko ya Kiebrania, kwa kawaida watu walitambulishwa kupitia ukoo wa baba. Huenda mume wa Seruya alikufa mapema, au huenda ilionekana kuwa hafai kutiwa katika masimulizi ya Biblia. Yawezekana kwamba Seruya alitajwa kwa sababu alikuwa dada ya Daudi au dada yake wa kambo. (1 Mambo ya Nyakati 2:15, 16) Baba ya ndugu hao watatu anatajwa tu kuhusiana na mahali alipozikwa huko Bethlehemu.—2 Samweli 2:32.

3:29—Maneno “mwanamume anayeshika gurudumu linalozunguka la kusokota nyuzi” yanamaanisha nini? Kwa kawaida, wanawake ndio waliofuma nguo. Kwa hiyo, huenda maneno hayo yakarejelea wanaume ambao hawakufaa katika vita, na hivyo kulazimika kufanya kazi ambayo kwa kawaida ilifanywa na mwanamke.

5:1, 2—Baada ya Ish-boshethi kuuawa, ni muda gani uliopita kabla ya Daudi kutawazwa kuwa mfalme wa taifa lote la Israeli? Ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba Ish-boshethi alianza utawala wake wa miaka miwili punde tu baada ya Sauli kufa, yapata wakati uleule ambapo Daudi alianza kutawala huko Hebroni. Daudi alitawala Yuda akiwa Hebroni kwa miaka saba na nusu. Punde baada ya kutawazwa kuwa mfalme wa taifa lote la Israeli, alihamisha mji wake mkuu hadi Yerusalemu. Hivyo, Daudi alitawazwa kuwa mfalme wa taifa lote la Israeli miaka mitano hivi baada ya kifo cha Ish-boshethi.—2 Samweli 2:3, 4, 8-11; 5:4, 5.

8:2—Ni Wamoabu wangapi waliouawa baada ya kupigwa na Israeli? Huenda idadi hiyo ilikadiriwa kwa kupima wala si kwa kuhesabu. Inaonekana kwamba Daudi aliwaagiza Wamoabu walale chini, wakiwa wamejipanga katika mstari. Halafu, akaagiza mstari huo upimwe kwa kamba. Inaonekana vipimo viwili vya kamba, au theluthi mbili ya Wamoabu waliuawa, na kipimo kimoja cha kamba, au theluthi moja hawakuuawa.

Mambo Tunayojifunza:

2:1; 5:19, 23. Daudi alimuuliza Yehova kabla ya kuanza kuishi huko Hebroni na kabla ya kwenda kupigana na adui zake. Sisi pia tunapaswa kutafuta mwongozo wa Yehova kabla ya kufanya maamuzi yanayoathiri hali yetu ya kiroho.

3:26-30. Matokeo ya kulipiza kisasi huwa mabaya sana.—Waroma 12:17-19.

3:31-34; 4:9-12. Daudi anatuwekea mfano mzuri kwa kutolipiza kisasi na kutokuwa na chuki.

5:12. Hatupaswi kusahau kamwe kwamba Yehova ametufunza katika njia zake na ametuwezesha kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye.

6:1-7. Ingawa Daudi alikuwa na nia nzuri, jaribio lake la kuhamisha Sanduku katika gari la kukokotwa lilikuwa kinyume cha amri ya Mungu, naye hakufaulu. (Kutoka 25:13, 14; Hesabu 4:15, 19; 7:7-9) Pia, yaliyotokea wakati Uza alipolishika Sanduku, yanaonyesha kwamba matakwa ya Mungu hayabadiliki hata kama mtu ana nia nzuri.

6:8, 9Katika hali fulani ngumu, kwanza Daudi alikasirika, kisha akaogopa, na hata labda akamlaumu Yehova kwa msiba huo. Lazima tujihadhari tusimlaumu Yehova kwa matatizo yanayotokea tunapopuuza amri zake.

7:18, 22, 23, 26. Tunapaswa kuiga sifa za Daudi ambazo ni, unyenyekevu, kujitoa kikamili kwa Yehova, na tamaa ya kulitukuza jina la Mungu.

8:2. Unabii uliotolewa yapata miaka 400 mapema unatimizwa. (Hesabu 24:17) Neno la Yehova hutimizwa sikuzote.

9:1, 6, 7Daudi alitimiza ahadi yake. Tunapaswa pia kujitahidi kutimiza ahadi zetu.

YEHOVA ALETA MSIBA DHIDI YA MTIWA-MAFUTA WAKE

(2 Samweli 11:1–20:26)

Yehova anamwambia Daudi hivi: “Tazama, ninaleta msiba juu yako kutoka katika nyumba yako mwenyewe; nami nitawachukua wake zako chini ya macho yako mwenyewe na kumpa mwanamume mwenzako, naye atalala na wake zako chini ya macho ya jua hili.” (2 Samweli 12:11) Kwa nini Yehova anasema hivyo? Kwa sababu ya dhambi ya Daudi na Bath-sheba. Ingawa Daudi anasamehewa baada ya kutubu, haepuki matokeo ya dhambi yake.

Kwanza, mtoto ambaye Bath-sheba anazaa anakufa. Kisha, Tamari, binti ya Daudi, ambaye ni bikira, analalwa kinguvu na Amnoni, ndugu yake wa kambo. Absalomu, ndugu ya Tamari, analipiza kisasi kwa kumuua Amnoni. Absalomu anapanga njama dhidi ya babake na kujitangaza kuwa mfalme huko Hebroni. Daudi analazimika kukimbia Yerusalemu. Absalomu analala na masuria kumi wa babake wanaoachwa nyuma kutunza nyumba. Daudi anaurudia utawala wake baada ya Absalomu kuuawa. Uasi unaoanzishwa na Sheba, Mbenyamini, unasababisha kifo chake.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

14:7—Ni nini kinachofananishwa na “mng’ao wa makaa yangu”? Mng’ao wa makaa yanayowaka polepole hutumiwa kufananisha mzao aliye hai.

19:29—Kwa nini Daudi aliitikia maelezo ya Mefiboshethi kama alivyofanya? Baada ya kumsikiliza Mefiboshethi, bila shaka Daudi alitambua kwamba alikosea alipokubali maneno ya Siba kijuujuu tu. (2 Samweli 16:1-4; 19:24-28) Yaelekea jambo hilo lilimkasirisha Daudi, naye hakutaka kusikia habari zaidi kulihusu.

Mambo Tunayojifunza:

11:2-15. Masimulizi yanayotaja waziwazi kasoro za Daudi yanathibitisha kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake.

11:16-27. Tunapofanya dhambi nzito, hatupaswi kujaribu kuifunika kama Daudi. Badala yake, tunapaswa kuiungama kwa Yehova na kutafuta msaada wa wazee kutanikoni.—Methali 28:13; Yakobo 5:13-16.

12:1-14. Nathani aliwawekea mfano mzuri wazee waliowekwa rasmi kutanikoni. Wanapaswa kuwasaidia wale wanaofanya dhambi warekebishe mwenendo wao. Wazee wanapaswa kutimiza daraka hilo kwa ustadi.

12:15-23. Daudi alitenda inavyofaa alipokabili msiba kwa sababu alikuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali hiyo.

15:12; 16:15, 21, 23. Ilipoonekana kwamba Absalomu angechukua utawala, kiburi na kujitakia makuu kulimfanya Ahithofeli, mshauri mwenye akili, awe msaliti. Kuwa na akili bila unyenyekevu na ushikamanifu, kunaweza kuwa mtego.

19:24, 30. Mefiboshethi alithamini kikweli fadhili zenye upendo za Daudi. Alikubali kwa utayari uamuzi wa Daudi kuhusu Siba. Uthamini wetu kwa Yehova na kwa tengenezo lake unapaswa kutuchochea kujitiisha.

20:21, 22. Hekima ya mtu mmoja inaweza kuwaepusha wengi wasipatwe na msiba.—Mhubiri 9:14, 15.

ACHA TUANGUKE “MKONONI MWA YEHOVA”

(2 Samweli 21:1–24:25)

Kunakuwa na njaa kwa miaka mitatu kwa sababu ya hatia ya Sauli ya kumwaga damu kwa kuwaua Wagibeoni. (Yoshua 9:15) Ili kulipiza kisasi, Wagibeoni wanaomba wapewe wana saba wa Sauli ili wawaue. Daudi anawapa wana hao, mvua inanyesha, na ukame unaisha. Majitu wanne Wafilisti ‘wanaanguka kwa mkono wa Daudi na kwa mkono wa watumishi wake.’—2 Samweli 21:22.

Daudi anafanya dhambi nzito kwa kuagiza watu wahesabiwe isivyo halali. Anatubu na kuchagua kuanguka “mkononi mwa Yehova.” (2 Samweli 24:14) Kwa hiyo, watu 70,000 wanakufa kutokana na tauni. Daudi anafuata amri ya Yehova, na tauni inakomeshwa.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

21:8—Inawezaje kusemwa kwamba Mikali, binti ya Sauli, alikuwa na wana watano, ingawa andiko la 2 Samweli 6:23 linasema kwamba alikufa bila mtoto? Watu wengi wanakubali kwamba wana hao walikuwa wa Merabu, dada ya Mikali aliyeolewa na Adrieli. Yaelekea Merabu alikufa mapema, na Mikali, ambaye hakuwa na mtoto, akawalea wavulana hao.

21:9, 10—Rispa alikesha kwa muda mrefu kadiri gani ili kulinda miili ya wanawe wawili na wajukuu watano wa Sauli waliouawa na Wagibeoni? Watu hao saba walitundikwa “katika siku za kwanza za mavuno,” yaani, Machi au Aprili. Miili yao iliachwa hadharani mlimani. Rispa aliilinda miili hiyo mchana na usiku hadi Yehova alipoonyesha kwamba hasira yake imetulia kwa kuleta mvua. Halikuwa jambo la kawaida kupata mvua kubwa kabla ya majira ya mavuno kumalizika mwezi wa Oktoba. Hivyo, huenda Rispa alikesha kwa muda wa miezi mitano au sita. Baadaye, Daudi aliagiza mifupa ya wanaume hao izikwe.

24:1—Kwa nini tendo la Daudi la kuwahesabu watu lilikuwa dhambi nzito? Sheria haikukataza kuwahesabu watu. (Hesabu 1:1-3; 26:1-4) Biblia haisemi kwa nini Daudi aliwahesabu watu. Hata hivyo, andiko la 1 Mambo ya Nyakati 21:1 linaonyesha kwamba Shetani alimchochea afanye hivyo. Vyovyote vile, Yoabu, mkuu wake wa majeshi, alijua kwamba uamuzi wa Daudi wa kuwahesabu watu ulikuwa mbaya, naye akajaribu kumshauri asifanye hivyo.

Mambo Tunayojifunza:

22:2-51. Wimbo wa Daudi unaonyesha kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli, tunayepaswa kumtegemea kabisa!

23:15-17. Daudi aliheshimu sana sheria ya Mungu kuhusu uhai na damu hivi kwamba wakati huu aliepuka kufanya chochote kile ambacho kingevunja sheria hiyo. Tunapaswa kusitawisha mtazamo kama huo kuelekea amri zote za Mungu.

24:10. Dhamiri ya Daudi ilimchochea kutubu. Je, tuna dhamiri kama hiyo inayotuchochea kutubu?

24:14. Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova ana rehema nyingi kuliko wanadamu. Je, sisi tuna uhakika huo?

24:17. Daudi alijuta kwamba dhambi yake ilifanya taifa zima liteseke. Mkosaji mwenye kutubu anapaswa kujutia aibu ambayo kutaniko limepata kwa sababu ya tendo lake.

Tunaweza Kuwa Watu ‘Wanaokubalika kwa Moyo wa Mungu’

Mfalme wa pili wa Israeli alikuwa mtu ‘anayekubalika kwa moyo wa Yehova.’ (1 Samweli 13:14) Daudi hakutilia shaka viwango vya uadilifu vya Yehova, naye alimtegemea Mungu katika maisha yake. Kila alipokosea, Daudi alikubali dhambi yake, akakubali nidhamu, na kurekebisha mwenendo wake. Daudi alidumisha utimilifu. Je, halingekuwa jambo la hekima kumwiga, hasa tunapokosea?

Maisha ya Daudi yanaonyesha waziwazi kwamba kutambua enzi kuu ya Yehova humaanisha kukubali viwango Vyake vya mema na mabaya, na kujitahidi kuvifuata huku tukidumisha utimilifu. Hilo linawezekana. Tunathamini kama nini mambo tunayojifunza katika Kitabu cha Pili cha Samweli! Ujumbe wake ambao uliongozwa na roho ya Mungu ni hai na una nguvu.—Waebrania 4:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ingawa Samweli hakushiriki kukiandika, kitabu hicho kimepewa jina lake kwa sababu mwanzoni, vitabu hivi viwili vya Samweli vilikuwa kunjo moja katika maandiko yaliyokubalika ya Kiebrania. Samweli aliandika sehemu kubwa ya Kitabu cha Kwanza cha Samweli.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Daudi aliendelea kuwa mnyenyekevu kwa kukumbuka yule aliyemweka imara akiwa mfalme

[Picha katika ukurasa wa 18]

“Tazama, ninaleta msiba juu yako kutoka katika nyumba yako mwenyewe”

Bath-sheba

Tamari

Amnoni