Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Daudi na Bath-sheba hawakuuawa kwa kufanya uzinzi, ingawa mtoto wao mchanga alikufa?

Sheria ya Musa ilisema: “Ikiwa mwanamume atapatikana akilala na mwanamke aliye na mume, wote wawili watauawa pamoja, yule mwanamume anayelala na mwanamke pamoja na huyo mwanamke. Kwa hiyo lazima utaondolea mbali lililo baya kutoka katika Israeli.” (Kumbukumbu la Torati 22:22) Kama Yehova Mungu angaliruhusu kesi ya hukumu kuhusiana na dhambi ya Daudi na Bath-sheba ishughulikiwe na waamuzi wa kibinadamu kupatana na Sheria, Daudi na Bath-sheba wangaliuawa. Kwa kuwa waamuzi hao hawangeweza kuisoma mioyo, hukumu yao ingetegemea mwenendo wa wakosaji kupatana na mambo yaliyothibitishwa. Mzinzi alipaswa kuuawa. Waamuzi wa Israeli hawakuruhusiwa kusamehe dhambi hiyo.

Kwa upande mwingine, Mungu wa kweli anaweza kuisoma mioyo na kusamehe dhambi akiona kuna sababu ya kufanya hivyo. Kwa kuwa kesi hiyo ilimhusu Daudi, ambaye Yehova alifanya agano la Ufalme pamoja naye, Yehova aliamua aishughulikie yeye mwenyewe. (2 Samweli 7:12-16) “Mwamuzi wa dunia yote” ana haki ya kuamua hivyo.—Mwanzo 18:25.

Yehova aliona nini alipouchunguza moyo wa Daudi? Maandishi ya utangulizi ya Zaburi ya 51 yanasema kwamba zaburi hii inaonyesha hisia za Daudi wakati “Nathani nabii alipoingia kwake baada ya Daudi kulala na Bath-sheba.” Zaburi 51:1-4 inasema: “Ee Mungu, unionyeshe kibali kulingana na fadhili zako zenye upendo. Ufutilie mbali makosa yangu kulingana na wingi wa rehema zako. Unioshe kabisa kutokana na kosa langu, na kunitakasa kutokana na dhambi yangu. Kwa maana mimi mwenyewe nayajua makosa yangu, na dhambi yangu iko mbele yangu daima. Dhidi yako wewe, wewe peke yako, nimetenda dhambi, nami nimefanya lililo baya machoni pako.” Bila shaka, Yehova aliona majuto ya Daudi kuwa uthibitisho wa toba ya kweli, hivyo akaamua kuna sababu ya kuwaonyesha rehema wakosaji hao. Isitoshe, Daudi mwenyewe alikuwa mwenye rehema, na Yehova huwaonyesha rehema wenye rehema. (1 Samweli 24:4-7; Mathayo 5:7; Yakobo 2:13) Kwa hiyo, Daudi alipoungama dhambi yake, Nathani alimwambia hivi: “Yehova naye ameacha dhambi yako ipite. Hutakufa.”—2 Samweli 12:13.

Daudi na Bath-sheba hawangeepuka madhara yote ya dhambi yao. Nathani alimwambia Daudi hivi: “Kwa kuwa bila shaka hukumheshimu Yehova kwa jambo hili, pia yule mwana, uliyemzaa, atakufa hakika.” Mtoto wao alishikwa na ugonjwa na kufa, ingawa Daudi alifunga na kuomboleza kwa siku saba.—2 Samweli 12:14-18.

Wengine hawaelewi ni kwa nini mtoto huyo alikufa, kwa kuwa andiko la Kumbukumbu la Torati 24:16 linasema: “Watoto wasiuawe kwa sababu ya akina baba.” Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba kama kesi hiyo ingalishughulikiwa na waamuzi wa kibinadamu, wazazi na pia mtoto aliyekuwa tumboni wangalikufa. Huenda pia kifo cha mtoto huyo kilimsaidia Daudi kuelewa vizuri zaidi jinsi Yehova alivyochukizwa na dhambi yake pamoja na Bath-sheba. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova alishughulikia kesi hiyo kwa njia ya haki, kwa kuwa “njia yake ni kamilifu.”—2 Samweli 22:31.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Daudi alitubu kikweli