Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Usio na Umaskini Unakaribia

Ulimwengu Usio na Umaskini Unakaribia

Ulimwengu Usio na Umaskini Unakaribia

PICHA za Paradiso, kama ile iliyo kwenye jalada la gazeti hili, huwavutia watu wanaokabili umaskini. Wenzi wa kwanza wa ndoa, Adamu na Hawa, waliishi katika Paradiso halisi. Waliishi katika bustani ya Edeni. (Mwanzo 2:7-23) Ingawa Paradiso hiyo ilipotea, si ndoto kuamini kwamba kutakuwa na paradiso wakati ujao katika ulimwengu usio na umaskini. Imani hiyo inategemea kabisa ahadi zinazopatikana katika Biblia.

Hebu fikiria ahadi ambayo Yesu Kristo alitoa siku ya mwisho ya maisha yake duniani. Mmoja wa wale watenda-maovu waliokufa pamoja na Yesu aliamini kwamba Mungu anaweza kutatua matatizo ya wanadamu. Alisema hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba mtenda-maovu huyo aliamini kuwa Yesu atatawala akiwa Mfalme na kwamba wafu watafufuliwa. Yesu alimjibu hivi: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:42, 43.

Biblia inasema hivi kuhusu wale watakaoishi katika Paradiso: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.” (Isaya 65:21) Naam, “wataketi, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakutakuwa na mtu yeyote anayewatetemesha; kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hivyo.”—Mika 4:4.

Lakini, kwa nini kuna umaskini leo? Mungu huwasaidiaje maskini? Umaskini utakwisha wakati gani?

Kwa Nini Kuna Umaskini?

Paradiso ambamo Adamu na Hawa waliwekwa ilipotea kwa sababu ya uasi ulioanzishwa na malaika mwovu anayeitwa Shetani Ibilisi. Kwa kutumia nyoka kuwa msemaji wake, Shetani alimshawishi Hawa avunje sheria ya Mungu iliyokataza kula matunda ya mti fulani. Shetani alimdanganya Hawa kwamba atakuwa na maisha bora akikataa kuongozwa na Mungu. Hawa alipompa Adamu tunda lililokatazwa, Adamu pia alikula, hivyo akamuunga mkono mke wake na kumkataa Mungu.—Mwanzo 3:1-6; 1 Timotheo 2:14.

Kwa haki, wenzi hao walioasi walifukuzwa katika Paradiso, na tangu wakati huo iliwabidi wajikakamue ili waendelee kuishi. Yehova amemruhusu Shetani aendelee kuwatawala wanadamu wenye dhambi mpaka sasa, hivyo kuonyesha waziwazi matokeo ya kutomtii Mungu. Historia ya mwanadamu imeonyesha kwamba wanadamu hawawezi kuleta Paradiso duniani. (Yeremia 10:23) Badala yake, kutofuata mwongozo wa Mungu kumesababisha matatizo makubwa, kama vile umaskini.—Mhubiri 8:9.

Hata hivyo, maskini hawajatupwa kabisa katika ulimwengu huu wenye shida nyingi. Neno la Mungu, Biblia, lililoongozwa na roho yake, lina mashauri bora kwa ajili yao.

“Msihangaike Kamwe”

Yesu alipozungumza na umati mkubwa uliotia ndani maskini wengi, alisema: “Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao? . . . Kwa hiyo msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mathayo 6:26-33.

Maskini hahitaji kuiba. (Methali 6:30, 31) Mahitaji yake yatatoshelezwa akimtanguliza Mungu maishani mwake. Hebu ona kisa cha mtu anayeitwa Tukiso, ambaye anaishi katika nchi ya Lesotho, kusini mwa Afrika. Mwaka wa 1998, majeshi kutoka nchi nyingine yaliingia Lesotho ili kukomesha maasi dhidi ya serikali. Kwa sababu ya vita hivyo, maduka yaliporwa, watu wakapoteza kazi, na kukawa na ukosefu mkubwa wa chakula.

Tukiso aliishi katika eneo la mji mkuu lenye umaskini mkubwa sana. Majirani wake wengi walikuwa wamepora maduka ili wapate riziki. Tukiso aliporudi kwenye chumba chake, alipata kwamba mwanamke aliyekuwa akiishi naye anayeitwa Maseiso, alikuwa amepora vyakula vingi. Tukiso alimwambia hivi: “Peleka vitu hivi nje.” Kisha akamweleza kwamba sheria ya Mungu inakataza wizi. Maseiso alitii. Majirani waliwadhihaki na kuchukua vyakula hivyo vilivyoibwa.

Tukiso alifanya hivyo kwa sababu ya mambo aliyokuwa amefundishwa na Mashahidi wa Yehova kupitia funzo la Biblia. Je, alikufa njaa kwa sababu ya kutii sheria ya Mungu? La. Baadaye, wazee wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova aliloshirikiana nalo waliwasiliana naye na kumletea chakula. Mashahidi wa Yehova katika nchi jirani ya Afrika Kusini walikuwa wametuma zaidi ya tani mbili za chakula ili kuwasaidia ndugu na dada zao Wakristo nchini Lesotho. Maseiso alivutiwa na jinsi Tukiso alivyomtii Mungu na msaada wenye upendo kutoka kwa kutaniko hilo. Yeye pia alianza kujifunza Biblia. Baadaye, walifunga ndoa kisheria, nao wakastahili kubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Wangali wanamtumikia Mungu kwa uaminifu.

Yehova Mungu huwajali maskini. (Ona sanduku lenye kichwa “Mungu Huwaonaje Maskini?”) Kwa upendo, ameandaa mipango ya kuwasaidia watu walio kama Tukiso na Maseiso wajifunze mengi zaidi juu yake. Na katika Neno lake, ametoa mashauri yanayoweza kutumiwa maishani.

Mipango Yenye Manufaa

Sikuzote, Mashahidi wa Yehova wamejitahidi kuiga mfano wa Mungu wa kuwajali maskini. (Wagalatia 2:10) Wakristo wa kweli wanapoathiriwa na msiba katika nchi fulani, mara nyingi mipango hufanywa ili kuwasaidia. Jambo la maana zaidi ni kwamba Mashahidi huhangaikia mahitaji ya kiroho ya watu wote, kutia ndani maskini. (Mathayo 9:36-38) Katika miaka 60 iliyopita, maelfu ya wahudumu waliozoezwa wamejitolea kuwa wamishonari katika nchi nyingine. Kwa mfano, mume na mke wamishonari kutoka Ufini walijifunza Kisotho na hivyo wakawafundisha Tukiso na Maseiso wawe wanafunzi wa Yesu. (Mathayo 28:19, 20) Mara nyingi wamishonari hujinyima maisha ya starehe katika nchi zenye ufanisi na kuhamia nchi zenye umaskini.

Wakristo wa kweli hawapaswi kuiba ili kupata riziki. Badala yake, wanaamini kwamba Yehova Mungu anaweza kutosheleza mahitaji yao. (Waebrania 13:5, 6) Njia moja ambayo Yehova hutumia kutosheleza mahitaji ya watu wake ni undugu wa ulimwenguni pote wa waabudu wake ambao hutunzana.

Pia, Yehova huwasaidia maskini kwa kuwapa mashauri wanayoweza kutumia maishani. Kwa mfano, Biblia inaamuru hivi: “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (Waefeso 4:28) Watu wengi wasioajiriwa wameamua kuanzisha kazi zao na kufanya kazi ngumu, kama vile kupanda mboga katika bustani. Isitoshe, Biblia huwasaidia maskini kuweka akiba ya pesa kwa kuwafundisha kuepuka mazoea mabaya, kama vile ulevi.—Waefeso 5:18.

Umaskini Utaisha Wakati Gani?

Biblia inaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za utawala wa Shetani. (2 Timotheo 3:1) Karibuni, Yehova Mungu atamtuma Yesu Kristo kuwahukumu wanadamu. Ni nini kitakachotukia wakati huo? Yesu alijibu swali hilo katika mfano wake mmoja. Alisema: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi.”—Mathayo 25:31-33.

Kondoo wanaotajwa katika mfano huo ni watu wanaojitiisha chini ya utawala wa Yesu. Yesu aliwafananisha na kondoo kwa sababu wanamfuata akiwa Mchungaji wao. (Yohana 10:16) Watu hao wanaofananishwa na kondoo watapata uzima chini ya utawala mkamilifu wa Yesu. Watafurahia maisha katika ulimwengu mpya usio na umaskini. Watu wanaofananishwa na mbuzi, ambao wanakataa utawala wa Yesu, wataharibiwa milele.—Mathayo 25:46.

Ufalme wa Mungu utakomesha uovu. Hivyo, umaskini hautakuwapo tena. Badala yake, dunia itakaliwa na watu wanaopendana na kuhangaikiana. Undugu wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova unaonyesha kwamba ulimwengu huo mpya utakuwapo, kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yohana 13:35.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6, 7]

MUNGU HUWAONAJE MASKINI?

Biblia inamfafanua Muumba wa wanadamu kuwa “Yeye anayewapa wenye njaa mkate.” (Zaburi 146:7) Ina mistari zaidi ya mia moja inayoonyesha kwamba Mungu anawajali maskini.

Kwa mfano, Yehova alipowapa Waisraeli wa kale Sheria yake, aliwaamuru wakulima Waisraeli wasivune kabisa kingo za mashamba yao. Hawakupaswa kukusanya matunda yaliyosalia kwa kupitia tena mzeituni au mzabibu. Sheria hizo zilikuwa maandalizi yenye upendo kwa wageni, mayatima, wajane, na watu wengine walioteseka.—Mambo ya Walawi 19:9, 10; Kumbukumbu la Torati 24:19-21.

Zaidi ya hayo, Mungu aliwaamuru Waisraeli hivi: “Msimtese mjane yeyote wala mvulana asiye na baba. Mkimtesa hata kidogo, naye anililie hata kidogo, sitakosa kukisikia kilio chake; nayo hasira yangu itawaka kwelikweli, nami hakika nitawaua kwa upanga, na wake zenu watakuwa wajane, nao wana wenu watakuwa wavulana wasio na baba.” (Kutoka 22:22-24) Kwa kusikitisha, matajiri wengi Waisraeli walipuuza maneno hayo. Kwa sababu ya kosa hilo na makosa mengineyo, Yehova Mungu aliwaonya Waisraeli kupitia manabii wake. (Isaya 10:1, 2; Yeremia 5:28; Amosi 4:1-3) Hatimaye, Mungu aliwafanya Waashuru na baadaye Wababiloni watwae maeneo ya Waisraeli. Waisraeli wengi waliuawa, na waokokaji wakapelekwa katika mataifa mengine wakiwa mateka.

Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliwahangaikia maskini kwa upendo kama Baba yake. Yesu alisema hivi kuhusu kusudi la huduma yake: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema.” (Luka 4:18) Hiyo haimaanishi kwamba Yesu aliwahudumia maskini tu. Aliwasaidia matajiri pia. Lakini, alipofanya hivyo, mara nyingi alionyesha kwamba anawahangaikia maskini. Kwa mfano, alimshauri hivi mtawala mmoja tajiri: “Uza vitu vyote ulivyo navyo uwagawie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.”—Luka 14:1, 12-14; 18:18, 22; 19:1-10.

Yehova Mungu na Mwana wake huwajali sana maskini. (Marko 12:41-44; Yakobo 2:1-6) Yehova anaonyesha kwamba anawajali maskini kwa kuwakumbuka mamilioni ya maskini waliokufa. Wote hao watafufuliwa katika ulimwengu mpya usio na umaskini.—Matendo 24:15.

[Picha]

Undugu wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova unaonyesha kwamba kutakuwa na ulimwengu mpya

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tukiso na Maseiso wakiwa na mmishonari aliyejifunza Biblia pamoja na Tukiso

[Picha katika ukurasa wa 5]

Maseiso akiwa mlangoni pa nyumba yake pamoja na mmishonari aliyejifunza Biblia pamoja naye