Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufurahia “Uzima wa Sasa” Kikamili

Kufurahia “Uzima wa Sasa” Kikamili

Simulizi la Maisha

Kufurahia “Uzima wa Sasa” Kikamili

LIMESIMULIWA NA TED BUCKINGHAM

Baada ya kuwa katika huduma ya wakati wote kwa miaka sita na katika ndoa kwa miezi sita, nilipatwa ghafula na ugonjwa wa polio. Ilikuwa mwaka wa 1950, nami nilikuwa tu na umri wa miaka 24. Miezi tisa niliyokaa katika hospitali ilinipa wakati mwingi wa kutafakari juu ya maisha yangu. Kwa kuwa sasa nilikuwa mlemavu, maisha yangu na ya mke wangu Joyce yangekuwaje wakati ujao?

MNAMO mwaka wa 1938, baba yangu ambaye hakupenda mambo ya dini, alipata nakala ya kitabu Government. * Huenda misukosuko ya kisiasa na kutazamia vita kulimchochea kuchukua kitabu hicho. Kama nijuavyo, hakuwahi kukisoma, lakini mama yangu ambaye alipenda sana dini alikisoma. Mama alikubali ujumbe wa kitabu hicho mara moja. Aliachana na Kanisa la Anglikana, na licha ya upinzani wa baba yangu, Mama akawa Shahidi wa Yehova naye akabaki mwaminifu hadi alipokufa mwaka wa 1990.

Mama alinipeleka kwenye mkutano wangu wa kwanza wa Kikristo kwenye Jumba la Ufalme huko Epsom, kusini ya London. Kutaniko la huko lilikutana katika jengo la zamani lililokuwa duka, nasi tulisikiliza hotuba iliyorekodiwa ya J. F. Rutherford, aliyesimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova wakati huo. Niliguswa moyo sana na hotuba hiyo.

Hali ilizidi kuwa yenye hatari wakati jiji la London liliposhambuliwa kwa mabomu. Hivyo, mwaka wa 1940 baba yangu akaamua kuhamishia familia yake mahali salama, yaani, Maidenhead, mji mdogo ulio umbali wa kilometa 45 magharibi ya London. Kuhama kwetu kulikuwa muhimu, kwa kuwa tulitiwa moyo sana na washiriki 30 wa kutaniko la eneo hilo. Fred Smith, Mkristo mkomavu aliyebatizwa mwaka wa 1917, alipendezwa nami naye akanizoeza kuwa mhubiri mwenye ustadi. Bado namshukuru sana kwa mfano mzuri na msaada wake wenye upendo.

Naanza Utumishi wa Wakati Wote

Mnamo Machi 1941, nikiwa na umri wa miaka 15, nilibatizwa kwenye Mto Thames huku kukiwa na baridi. Kufikia wakati huo, ndugu yangu mkubwa, Jim, alikuwa mweneza-injili wa wakati wote. Leo, yeye na mke wake, Madge, wanaishi huko Birmingham, baada ya kumtumikia Yehova karibu maisha yao yote katika kazi ya mzunguko na ya wilaya kotekote Uingereza. Dada yangu mdogo, Robina, na mume wake Frank, bado ni watumishi waaminifu wa Yehova.

Nilifanya kazi ya hesabu katika kampuni ya mtengenezaji mmoja wa nguo. Siku moja mkurugenzi mkuu aliniita ofisini mwake ili kunipa kazi ya kununua bidhaa za kampuni. Ilionekana kwamba kazi hiyo ingenifaidi sana baadaye. Hata hivyo, kwa muda fulani, nilikuwa nikifikiria kufuata mfano mzuri wa ndugu yangu. Basi, kwa upole, nikakataa kazi hiyo na kumweleza kwa nini niliikataa. Nilishangaa aliponipongeza kwa uchangamfu kwa kuwa nilitaka kufuatia utendaji muhimu wa Kikristo. Hivyo, baada ya kusanyiko moja la wilaya huko Northampton mwaka wa 1944, nikawa mhubiri wa wakati wote.

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa kwenye jiji la Exeter, katika jimbo la Devon. Jiji hilo lilianza kusitawi polepole baada ya kupigwa kwa mabomu wakati wa vita. Niliishi pamoja na mapainia wengine wawili. Mapainia hao, Frank na Ruth Middleton, walinionyesha fadhili nyingi sana. Nilikuwa na umri wa miaka 18 tu nami sikujua sana kufua nguo na kupika, lakini hali iliboreka nilipojifunza kazi hizo.

Nilihubiri pamoja na Victor Gurd kutoka Ireland, aliyekuwa na umri wa miaka 50. Victor alikuwa mhubiri tangu miaka ya 1920. Alinifundisha kupanga wakati wangu ifaavyo, kupenda sana kuisoma Biblia, na kutambua thamani ya tafsiri mbalimbali za Biblia. Katika miaka hiyo ya mapema, mfano mzuri wa Victor wa kusimama imara ndilo jambo nililohitaji hasa.

Kutounga Mkono Vita Kwatokeza Magumu

Vita vilikuwa vinakaribia kwisha, lakini bado wenye mamlaka walikuwa wakiwatafuta wanaume vijana kwa ajili ya utumishi wa jeshi. Nilikuwa nimefikishwa mbele ya mahakama moja mwaka wa 1943 huko Maidenhead, ambako niliomba waziwazi kutofanya kazi ya jeshi kwa sababu nilikuwa mhubiri wa Injili. Ingawa rufani yangu ilikataliwa, niliamua kwenda katika mgawo wangu huko Exeter. Hivyo, siku moja nikiwa huko niliagizwa nifike mbele ya mahakama ya eneo hilo. Nilihukumiwa miezi sita ya kazi ngumu gerezani. Hakimu alisikitika kwamba hakuruhusiwa atoe hukumu ya muda mrefu. Baada ya kufungwa kwa miezi sita, nilirudishwa tena gerezani kwa miezi minne zaidi.

Kwa kuwa mimi tu ndiye niliyekuwa Shahidi gerezani, walinzi wa gereza walikuwa wakiniita Yehova. Haikuwa rahisi kuitikia nilipoitwa kwa jina hilo, lakini ilinibidi nifanye hivyo. Hata hivyo, lilikuwa pendeleo kusikia jina la Mungu likitajwa kila siku! Hilo liliwafanya wafungwa wengine wajue kwamba nilikuwa gerezani kwa sababu niliheshimu dhamiri yangu nikiwa Shahidi wa Yehova. Baadaye, Norman Castro aliletwa kwenye gereza hilo, nasi tukaanza kuitwa Musa na Haruni.

Nilihamishwa kutoka Exeter hadi Bristol, na mwishowe nikapelekwa kwenye gereza la Winchester. Sikuzote hali hazikuwa zenye kupendeza, lakini kuwa wacheshi kulitusaidia. Mimi na Norman tulifurahia kuadhimisha Ukumbusho pamoja tulipokuwa huko Winchester. Francis Cooke aliyetutembelea gerezani, alitutolea hotuba nzuri.

Mabadiliko Baada ya Vita

Kwenye kusanyiko la wilaya huko Bristol mwaka wa 1946, ambako kitabu cha kujifunzia Biblia “Let God Be True” kilitolewa, nilikutana na msichana mrembo, Joyce Moore, aliyekuwa pia painia huko Devon. Urafiki wetu ulikua, nasi tukafunga ndoa miaka minne baadaye huko Tiverton, ambako niliishi tangu mwaka wa 1947. Tulikodi chumba kimoja kwa dola 1.10 za Marekani kila juma. Tulifurahia sana maisha hayo!

Katika mwaka wetu wa kwanza wa ndoa, tulihamia kusini huko Brixham, mji maridadi wa bandarini ambako ufundi wa kuvua samaki kwa kukokota wavu ulianzishwa. Hata hivyo, tulikuwa hatujakaa sana huko nilipopatwa na ugonjwa wa polio tukiwa safarini kwenda London kwenye kusanyiko la wilaya. Nilipoteza fahamu. Hatimaye, niliondoka hospitalini baada ya miezi tisa, kama nilivyosema mwanzoni. Tangu wakati huo, mkono wangu wa kuume na miguu yote miwili iliathiriwa vibaya, na ilinibidi nitembee kwa kutumia mkongojo. Sikuzote mke wangu mpendwa alikuwa rafiki yangu mwenye furaha na mwenye kutia moyo, hasa kwa sababu alijitahidi kuendelea katika huduma ya wakati wote. Lakini tungefanya nini sasa? Muda si muda nilijifunza kwamba mkono wa Yehova si mfupi kamwe.

Mwaka uliofuata tulihudhuria kusanyiko huko Wimbledon, London. Wakati huo, nilikuwa nikitembea bila mkongojo. Tukiwa huko tulikutana na Pryce Hughes ambaye alisimamia kazi nchini Uingereza. Mara moja aliniambia: “Tunakuhitaji katika kazi ya mzunguko!” Jambo hilo lilinitia moyo sana! Lakini je, nilikuwa na afya nzuri vya kutosha? Mimi na Joyce tulikuwa na mashaka kuhusu kazi hiyo, lakini baada ya juma moja la mazoezi na kumtegemea Yehova kabisa, tulianza safari ya kurudi kusini-magharibi mwa Uingereza ambako nilitumwa kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 25 tu, lakini bado ninakumbuka kwa shukrani fadhili na subira ya Mashahidi ambao walinisaidia sana.

Mimi na Joyce tuliona kwamba kati ya utendaji mbalimbali wa kiroho, kutembelea makutaniko kulitusaidia kuwa karibu zaidi na ndugu na dada zetu Wakristo. Hatukuwa na gari, hivyo tulisafiri ama kwa gari-moshi ama kwa basi. Ingawa bado nilikabiliana na vizuizi vilivyosababishwa na ugonjwa wangu, tulifurahia mapendeleo yetu hadi mwaka wa 1957. Yalikuwa maisha yenye kuridhisha, lakini mwaka huohuo tulikabili jambo lingine gumu.

Twaenda Katika Utumishi wa Umishonari

Tulisisimuka sana tulipopokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 30 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Nilikuwa nikipata nafuu kutokana na ugonjwa wa kupooza. Hivyo, mimi na Joyce tulikubali kwa furaha mwaliko huo. Kutokana na yale tuliyoyaona maishani tulijua kwamba sikuzote Yehova hututia nguvu tukijitahidi kufanya mapenzi yake. Miezi mitano ya mafundisho mengi kwenye shule hiyo, iliyofanywa katika majengo maridadi huko South Lansing, New York, Marekani, ilipita haraka. Wanafunzi wengi walikuwa wamefunga ndoa na walikuwa waangalizi wanaosafiri. Wanafunzi walipoulizwa ikiwa kuna yeyote angependa kutumika kama mmishonari katika nchi ya kigeni, tulikuwa kati ya wale waliokubali. Tulitumwa wapi? Huko Uganda, Afrika Mashariki!

Kwa kuwa wakati huo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku nchini Uganda, nilishauriwa nikae katika nchi hiyo na kutafuta kazi ya kimwili. Baada ya safari ndefu kwa gari-moshi na kwa mashua, tulifika Kampala, Uganda. Maofisa wa uhamiaji hawakufurahi kutuona, nao wakaturuhusu tukae kwa miezi michache tu. Baadaye, tuliamuriwa kuondoka. Kwa kufuata maagizo kutoka makao makuu, tulisafiri hadi Northern Rhodesia (ambayo sasa ni Zambia). Tukiwa huko tulifurahi sana kuonana tena na wanne kati ya wanafunzi wenzetu wa Shule ya Gileadi, yaani Frank na Carrie Lewis, na Hayes na Harriet Hoskins. Muda mfupi baadaye tulipewa mgawo mpya huko Southern Rhodesia (ambayo sasa ni Zimbabwe).

Tulisafiri kwa gari-moshi nasi tuliona kwa mara ya kwanza Maporomoko ya Victoria kabla ya kufika Bulawayo. Tulikaa kwa kipindi fulani pamoja na familia ya akina McLuckie ambao walikuwa kati ya Mashahidi wa kwanza kuishi huko. Lilikuwa pendeleo kujuana nao vizuri kwa muda wa miaka 16 iliyofuata.

Kuzoea Mabadiliko

Baada ya kuzoezwa kwa majuma mawili ili kulifahamu vizuri eneo la Afrika, niliwekwa rasmi kutumika nikiwa mwangalizi wa wilaya. Tulipohubiri mashambani barani Afrika ilitubidi kubeba maji, chakula, malazi, nguo, kifaa na kitambaa kikubwa cha kuonyeshea sinema, jenereta, na vitu vingine vya lazima. Vitu hivyo vyote vilipakiwa katika lori lenye nguvu ambalo lingeweza kupita kwenye barabara mbovu.

Nilifanya kazi pamoja na waangalizi wa mizunguko Waafrika huku Joyce akiwasaidia kwa furaha wake na watoto wao ambao waliandamana nao. Inachosha kutembea katika maeneo tambarare ya Afrika, hasa wakati wa joto la mchana. Lakini punde si punde, niliona kwamba katika hali hiyo ya hewa, ilikuwa rahisi kwangu kuvumilia udhaifu wangu wa kimwili, nami nilifurahia sana jambo hilo.

Kwa ujumla watu walikuwa maskini. Wengi walishikilia mila na ushirikina na kuoa zaidi ya mke mmoja, lakini waliiheshimu sana Biblia. Katika maeneo fulani, mikutano ya kutaniko ilifanywa chini ya miti mikubwa yenye kivuli, na wakati wa jioni tulitumia taa za mafuta zilizoning’inizwa. Tulipojifunza Neno la Mungu chini ya anga yenye nyota, sikuzote tulistaajabishwa na sehemu hiyo ya uumbaji mtukufu wa Mungu.

Kuonyesha sinema za Watch Tower Society katika maeneo ya Kiafrika ni jambo lingine ambalo hatutalisahau. Tulipoonyesha sinema hizo, tulitazamia hudhurio la watu 1,000 au zaidi, ingawa kwa kawaida kutaniko lilikuwa na Mashahidi 30 hivi!

Bila shaka, katika nchi za joto, inawezekana mtu kuwa mgonjwa mara kwa mara, lakini sikuzote ni muhimu kuwa na mtazamo mzuri. Mimi na Joyce tulikabiliana na hali hiyo vizuri. Nilipatwa mara kwa mara na malaria, naye Joyce alipatwa na ugonjwa unaosababishwa na amiba.

Baadaye, tuliitwa kwenye ofisi ya tawi huko Salisbury (ambayo sasa ni Harare), ambako tulikuwa na pendeleo la kufanya kazi pamoja na watumishi wengine waaminifu wa Yehova, wakiwemo Lester Davey na George na Ruby Bradley. Serikali iliniweka rasmi kuwa ofisa wa ndoa. Hilo liliniwezesha kuhalalisha ndoa za ndugu Waafrika, na hivyo kuimarisha kifungo cha ndoa ya Kikristo katika makutaniko. Miaka michache baadaye, nilipewa pendeleo lingine, yaani, kutembelea makutaniko yasiyo ya Kibantu nchini. Kwa zaidi ya miaka kumi, mimi na Joyce tulifurahia kujuana na ndugu zetu katika kazi yetu ya kusafiri, nasi tulipendezwa na maendeleo yao ya kiroho. Wakati huo tuliwatembelea pia ndugu zetu huko Botswana na Msumbiji.

Twahama Tena

Baada ya miaka mingi yenye furaha huko kusini mwa Afrika, tulipokea mgawo mpya wa kwenda Sierra Leone, Afrika Magharibi, mwaka wa 1975. Baada ya muda mfupi, tulikuwa kwenye ofisi ya tawi tukifurahia mgawo wetu mpya. Lakini muda si muda nilishambuliwa vikali na malaria, nikawa dhaifu, na hatimaye nikalazimika kwenda kupata matibabu London. Nikiwa huko nikashauriwa nisirudi Afrika. Tulihuzunishwa na jambo hilo, lakini mimi na Joyce tulikaribishwa kwa uchangamfu katika familia ya Betheli ya London. Ndugu wengi Waafrika katika makutaniko mengi ya London walitufanya tujihisi tuko nyumbani kabisa. Afya yangu ilipoanza kuwa nzuri, tulizoea hali nyingine ya maisha, na niliombwa kusimamia Idara ya Ununuzi. Kwa sababu ya mpanuko ambao tumeona katika miaka ambayo imepita, kazi hiyo imekuwa yenye kufurahisha sana.

Mapema katika miaka ya 1990, mke wangu mpendwa Joyce alipatwa na ugonjwa fulani wa mfumo wa neva, naye akafa mwaka wa 1994. Alikuwa mke mwenye upendo, mshikamanifu, na mwaminifu, ambaye sikuzote alikuwa tayari kufanya mabadiliko katika hali mbalimbali tulizokabili pamoja. Ili kukabiliana na hali kama hiyo, nimeelewa kwamba ni muhimu kuona mambo kwa njia ya kiroho na kuendelea kutazama mbele. Kusali kwa Yehova ili anisaidie kuwa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho, kutia ndani kuhubiri, hunisaidia sana nisifikirie hali hiyo.—Methali 3:5, 6.

Kutumikia Betheli ni pendeleo na njia bora ya maisha. Hapa ninafanya kazi na vijana wengi na kuna mambo mengi ya kufurahia. Jambo moja lenye kufurahisha ni hesabu ya wageni tunaopokea hapa London. Nyakati nyingine ninaona marafiki wapendwa kutoka maeneo ya Afrika ambako nilitumikia, na hilo hunikumbusha mambo mengi yenye kufurahisha. Yote hayo hunisaidia kuendelea kufurahia kikamili “uzima wa sasa” na kufikiria uzima “utakaokuja” nikiwa na uhakika na tumaini.—1 Timotheo 4:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kilichochapishwa mwaka wa 1928 na Mashahidi wa Yehova, lakini hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na mama yangu mwaka wa 1946

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mimi na Joyce siku ya arusi yetu mwaka wa 1950

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwenye kusanyiko la wilaya huko Bristol mwaka wa 1953

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kutumikia kikundi cha mbali (juu) na kutaniko (kushoto) huko Southern Rhodesia, ambayo sasa ni Zimbabwe