Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ulimwengu Hauna Umoja?

Kwa Nini Ulimwengu Hauna Umoja?

Kwa Nini Ulimwengu Hauna Umoja?

“Hii ndiyo mara ya kwanza kwa jumuiya ya kimataifa kuungana tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu. . . . Hivyo, ulimwengu unaweza kutumia nafasi hii kutimiza ahadi ya muda mrefu ya kutokeza ulimwengu mpya.”

HIVYO ndivyo alivyosema rais mmoja wa Marekani mwishoni mwa karne ya 20. Wakati huo, matukio katika nchi mbalimbali yalionyesha kwamba muda si muda ulimwengu ungekuwa wenye umoja. Serikali za kimabavu zilianguka, moja baada ya nyingine. Ukuta wa Berlin uliporomoka, na huo ukawa mwanzo wa enzi mpya barani Ulaya. Muungano wa Sovieti, ambao watu wengi katika nchi za Magharibi waliuona kuwa kisababishi cha mizozo ya kimataifa, ulitoweka na watu wengi ulimwenguni wakashangaa. Vita Baridi vilikwisha, na ilitazamiwa kwamba silaha zingepunguzwa, kutia ndani zile za nyuklia. Ni kweli kwamba vita vilitokea katika Ghuba ya Uajemi, lakini vita hivyo vilionwa kuwa tatizo la muda mfupi tu, na watu wengi ulimwenguni waliendelea kujitahidi kutafuta amani.

Zaidi ya kutazamia mabadiliko ya kisiasa, watu walitarajia maendeleo katika sehemu nyingine za maisha. Hali ya maisha ilikuwa ikiboreka katika maeneo mengi ya ulimwengu. Maendeleo ya kitiba yaliwawezesha madaktari kufanya mambo ambayo hayangewezekana miaka kadhaa mapema. Uchumi ulisitawi haraka katika nchi nyingi hivi kwamba ilitarajiwa kungekuwa na ufanisi ulimwenguni pote. Ilionekana kwamba mambo yako shwari.

Leo, miaka kadhaa baadaye, tunajiuliza maswali haya: ‘Ni nini kilichotukia? Kwa nini ulimwengu hauna umoja kama ilivyokuwa imeahidiwa?’ Kinyume cha ilivyotarajiwa, inaonekana kwamba mambo yanakwenda kombo. Mara nyingi vyombo vya habari huripoti visa vya milipuko inayosababishwa na wapiganaji wa kujilipua kwa mabomu, mashambulizi ya kigaidi, ongezeko la silaha za maangamizi, na mambo mengine yenye kuhuzunisha. Matukio hayo yanazidi kugawanya ulimwengu. Hivi majuzi, mtaalamu mmoja mashuhuri wa uchumi alisema: “Tumenaswa katika ulimwengu uliojaa jeuri kwa sababu ya matendo ya watu ya kulipiza kisasi.”

Je, Ulimwengu Una Umoja au Umegawanyika?

Umoja wa Mataifa ulipoanzishwa, mojawapo ya malengo yake yalikuwa “kusitawisha uhusiano wa kirafiki kati ya mataifa kwa kuheshimu kanuni ya usawa baina ya watu na haki yao ya kujitawala.” Baada ya miaka 60 hivi, je, lengo hilo zuri limefikiwa? La hasha! Inaonekana mataifa yanafikiria “kujitawala” hasa badala ya kuwa na “uhusiano wa kirafiki.” Watu wa jamii na makabila mbalimbali ambao wanajitahidi juu chini kutambuliwa na kujitawala wamesababisha mgawanyiko mwingi ulimwenguni. Umoja wa Mataifa ulipoanzishwa ulikuwa na mataifa 51. Leo una mataifa 191.

Kama tulivyoona, mwishoni mwa karne ya 20, kulikuwa na matumaini makubwa ya kuwa na umoja ulimwenguni. Tangu wakati huo, matumaini hayo yamedidimia huku wanadamu wakishuhudia kugawanyika kwa ulimwengu hatua kwa hatua. Mgawanyiko na jeuri huko Yugoslavia, mapambano kati ya Chechnya na Urusi, vita vya Iraq, na mauaji makubwa yanayoendelea katika Mashariki ya Kati, yanaonyesha kwamba kuna utengano mkubwa.

Hakuna shaka kwamba jitihada nyingi za kuleta amani zimefanywa kwa nia njema. Hata hivyo, ni kana kwamba ulimwengu hauwezi kuwa na umoja. Basi, watu wengi wanajiuliza: ‘Kwa nini ni vigumu sana kuwa na umoja ulimwenguni? Ulimwengu unaelekea wapi?’

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

AP Photo/Lionel Cironneau

Arlo K. Abrahamson/AFP/ Getty Images