Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Baada ya kusikia kwamba Petro aliyekuwa mfungwa alikuwa mlangoni, kwa nini wanafunzi walisema: “Ni malaika wake”?—Matendo 12:15.

Huenda wanafunzi walifikiri kimakosa kwamba malaika aliyemwakilisha Petro alikuwa amesimama langoni. Fikiria muktadha wa andiko hilo.

Petro alikuwa ametiwa gerezani na Herode, ambaye alimuua Yakobo. Hivyo, wanafunzi walikuwa na sababu nzuri ya kuamini kwamba Petro alikuwa pia amekwisha uawa. Akiwa amefungwa minyororo, Petro alilindwa na vikundi vya askari wanne waliofanya kazi kwa zamu nne. Kisha usiku mmoja, malaika akamweka huru kimuujiza na kumtoa nje ya gereza. Petro alipotambua yale yaliyokuwa yakitukia, alisema hivi: “Sasa ninajua hakika kwamba Yehova alimtuma malaika wake na kunikomboa kutoka mkononi mwa Herode.”—Matendo 12:1-11.

Mara moja Petro alienda nyumbani kwa Maria mama ya Yohana Marko, ambako wanafunzi wengi walikuwa wamekusanyika. Alipopiga hodi kwenye mlango, kijakazi anayeitwa Roda akaenda kumfungulia. Alipoitambua sauti ya Petro, akakimbia kwenda kuwaeleza wengine bila hata kumfungulia. Kwanza, wanafunzi hawakuamini kwamba Petro alikuwa amesimama langoni. Badala yake, walifikiri kimakosa kwamba: “Ni malaika wake.”—Matendo 12:12-15.

Je, wanafunzi waliamini kwamba Petro alikuwa amekwisha uawa na kwamba roho yake isiyo na mwili ilikuwa imesimama langoni? Hilo halingewezekana, kwa kuwa wafuasi wa Yesu walijua ukweli wa Maandiko kuhusu wafu, kwamba “hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5, 10) Hivyo basi, wanafunzi walimaanisha nini waliposema: “Ni malaika wake”?

Wanafunzi wa Yesu walijua kwamba katika historia yote, malaika waliwasaidia watu wa Mungu. Kwa mfano, Yakobo alizungumza kuhusu ‘malaika ambaye alikuwa akimponya katika misiba yote.’ (Mwanzo 48:16) Na kuhusu mtoto fulani aliyekuwa kati yao, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Angalieni msimdharau mmoja wa hawa wadogo; kwa maana ninawaambia ninyi kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huuona uso wa Baba yangu aliye mbinguni.”—Mathayo 18:10.

Inapendeza kuona kwamba Biblia ya Young’s Literal Translation of the Holy Bible inatafsiri neno agʹge·los (“malaika”) kuwa “mjumbe.” Yaelekea Wayahudi fulani waliamini kwamba kila mtumishi wa Mungu alikuwa na malaika wake, yaani “malaika mlinzi.” Bila shaka, maoni hayo hayafundishwi moja kwa moja katika Neno la Mungu. Hata hivyo, inawezekana kwamba wanafunzi waliposema, “Ni malaika wake,” walikuwa wakifikiri kwamba malaika fulani aliyemwakilisha Petro alikuwa amesimama langoni.