Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mume na Mke Wasipoelewana

Mume na Mke Wasipoelewana

Mume na Mke Wasipoelewana

INGAWA ugomvi hutokea mara kwa mara katika ndoa, hakuna mume au mke mwenye akili timamu ambaye huufurahia. Kwa kawaida, mwenzi mmoja husema jambo linalomwudhi mwenzake. Ndipo wao huinua sauti, hupandwa na hasira, na kuanza kubishana vikali, huku wakitumia maneno ya dhihaka. Kisha wote wawili hunyamaziana kabisa. Baada ya muda, hasira hutulia nao huombana msamaha. Amani hupatikana tena, angalau hadi hali ya kutoelewana itakapotokea tena.

Kugombana kati ya mume na mke ni jambo ambalo huzungumziwa na kufanyiwa mzaha mara nyingi katika vipindi vya televisheni, lakini ukweli ni kwamba hilo si jambo la kuchekesha. Methali moja ya Biblia inasema: “Maneno ya ovyo hujeruhi kama upanga.” (Methali 12:18, Biblia Habari Njema) Naam, maneno makali huendelea kuumiza hisia muda mrefu baada ya mabishano kwisha. Mabishano yanaweza hata kusababisha jeuri.—Kutoka 21:18.

Bila shaka, nyakati nyingine matatizo hutokea katika ndoa kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu. (Mwanzo 3:16; 1 Wakorintho 7:28) Hata hivyo, mabishano makali yanayotokea mara nyingi hayapaswi kupuuzwa na kuonwa kuwa jambo la kawaida tu. Watafiti wamesema kwamba mabishano yanapotokea mara nyingi, inaelekea sana kwamba wenzi wa ndoa watatalikiana. Hivyo, ni muhimu wewe na mwenzi wako mjifunze kushughulikia kwa njia ya amani hali ya kutoelewana.

Kuchanganua Hali

Ikiwa ninyi hubishana sana katika ndoa yenu, jaribu kuona mabishano yenu huwa yanachukua mwelekeo gani. Kwa kawaida, ni nini hutokea wakati wewe na mwenzi wako mnapokosa kukubaliana juu ya jambo fulani? Je, ninyi hushindwa kujidhibiti katika mazungumzo yenu, kisha huanza kurushiana matukano na mashtaka? Ikiwa ndivyo, mnaweza kufanya nini?

Kwanza, chunguza kwa unyoofu jinsi wewe binafsi unavyochangia tatizo hilo. Je, wewe hukasirika haraka? Je, wewe ni mbishi? Mwenzi wako anaweza kusema nini juu yako kuhusiana na jambo hilo? Ni muhimu kufikiria swali hilo la mwisho, kwa kuwa huenda wewe na mwenzi wako mkawa na maoni tofauti kuhusu kile ambacho hufanya mtu awe mbishi.

Kwa mfano, tuseme mwenzi wako hapendi kuongea sana, lakini wewe huzungumza waziwazi na kwa hisia nyingi. Huenda ukasema: “Nilipokuwa nikikua, hivyo ndivyo kila mtu katika familia yetu alivyozungumza. Hayo si mabishano!” Na labda huyaoni kuwa mabishano. Hata hivyo, huenda mwenzi wako akayaona mambo ambayo wewe unafikiri kwamba ni mazungumzo ya wazi kuwa mabishano makali yenye kuumiza. Kutambua tu kwamba wewe na mwenzi wako huwasiliana kwa njia tofauti kunaweza kuwasaidia mwepuke kutoelewana.

Pia, kumbuka kwamba watu hawainui sauti kila mara wanapobishana. Paulo aliwaandikia Wakristo hivi: “Kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) “Kupiga kelele” ni kuinua sauti, nayo “matukano” hurejelea kiini cha yale yanayosemwa. Kulingana na maoni hayo, hata maneno yaliyonong’onwa yanaweza kuwa yenye ubishi ikiwa yanaudhi au ni yenye dharau.

Kwa kufikiria mambo hayo yaliyotajwa, chunguza tena jinsi unavyoshughulikia hali ya kutoelewana kati yako na mwenzi wako. Je, wewe ni mbishi? Kama vile tumekwisha ona, jibu la swali hilo linategemea hasa maoni ya mwenzi wako. Badala ya kumpuuza mwenzi wako kuwa mtu mwenye hisia nyepesi, jaribu kujiona kama vile yeye anavyokuona, na ufanye marekebisho yanayohitajiwa. Paulo aliandika: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.

“Kazieni Uangalifu Jinsi Mnavyosikiliza”

Maneno haya ya Yesu yanaonyesha njia nyingine ya kushughulikia hali ya kutoelewana: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.” (Luka 8:18) Ni kweli kwamba Yesu hakuwa akizungumza kuhusu mawasiliano katika ndoa. Hata hivyo, kanuni hiyo inaweza kutumiwa pia katika hali hii. Wewe humsikiliza mwenzi wako vizuri kadiri gani? Je, wewe humsikiliza hata kidogo? Au wewe humkatiza ghafula kwa kutatua matatizo kijuujuu bila kuyaelewa vizuri? Biblia inasema: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” (Methali 18:13) Hivyo, hali ya kutoelewana ikitokea, wewe na mwenzi wako mnahitaji kuzungumzia jambo hilo na kila mmoja amsikilize mwenzake kwa makini.

Badala ya kupuuza maoni ya mwenzi wako, jitahidi kuonyesha “hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8) Katika Kigiriki cha awali, neno hisia-mwenzi linamaanisha kuteseka pamoja na mtu mwingine. Ikiwa mwenzi wako amehuzunishwa na jambo fulani, unapaswa kuhuzunika pia. Jitahidi kuona jambo hilo jinsi anavyoliona.

Yaonekana, Isaka aliyemwogopa Mungu alifanya hivyo. Biblia inatuambia kwamba mke wake, Rebeka, alifadhaishwa sana na jambo fulani la kifamilia lililohusisha mwana wake Yakobo. Alimwambia Isaka hivi: “Nimekuja kuyachukia sana haya maisha yangu kwa sababu ya binti za Hethi. Yakobo akichukua mke kutoka kwa binti za Hethi kama hawa kutoka kwa binti za hii nchi, basi maisha yana faida gani kwangu?”—Mwanzo 27:46.

Ni kweli kwamba Rebeka alitia chumvi kwa sababu ya hangaiko. Je, kwa kweli yeye aliyachukia maisha yake? Je, angechagua kufa kama mwana wake angeoa mmoja wa binti za Hethi? Labda hangefanya hivyo. Lakini Isaka hakupuuza hisia za Rebeka. Badala yake Isaka alitambua kwamba hangaiko la Rebeka lilifaa, hivyo akachukua hatua. (Mwanzo 28:1) Fanya vivyo hivyo mwenzi wako akihangaika kuhusu jambo fulani wakati ujao. Badala ya kulipuuza hangaiko lake, msikilize, heshimu maoni yake, na uitikie kwa huruma.

Kusikiliza na Ufahamu

Methali moja ya Biblia inasema: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.” (Methali 19:11) Mabishano yanapokuwa makali, ni rahisi kuitikia maneno yote makali ya mwenzi wako bila kufikiri. Lakini, kwa kawaida jambo hilo huchochea moto. Kwa hiyo, unapomsikiliza mwenzi wako, jitahidi kusikia si maneno yake tu bali pia kuelewa hisia zake. Ufahamu huo utakusaidia kupuuza mambo yenye kuudhi anayosema na kuzingatia kiini cha tatizo.

Kwa mfano, tuseme mke wako anakwambia hivi: “Wewe hutumii wakati pamoja nami kamwe!” Unaweza kuudhika na kulipinga dai lake kwa kutaja mambo ya hakika. “Nilikaa nawe siku nzima mwezi uliopita!” huenda ukamjibu. Lakini ukimsikiliza kwa makini, huenda ukagundua kwamba kile ambacho mke wako anataka si ukae naye kwa muda mrefu zaidi. Badala yake, huenda anataka uhakikisho na anakuambia kwamba anahisi amepuuzwa na hapendwi.

Tuseme kwamba wewe ni mke na mume wako anaonyesha hangaiko kuhusu kitu fulani ulichonunua hivi karibuni. Kisha anauliza hivi bila kuamini: “Unawezaje kutumia pesa nyingi hivyo?” Huenda ukataka kujitetea mara moja kwa kumweleza kinaganaga hali ya kifedha ya familia au kwa kulinganisha kitu hicho na kingine alichonunua. Hata hivyo, ufahamu utakusaidia kuona kwamba huenda mume wako hazungumzi kuhusu kiasi cha pesa ulizotumia. Badala yake, huenda amefadhaika kwa sababu hakuhusishwa ulipoamua kununua kitu hicho.

Bila shaka, wenzi mbalimbali wa ndoa wana njia tofauti-tofauti za kuamua ni wakati mwingi kadiri gani watakaotumia pamoja na ni vitu gani watakavyonunua. Jambo tunalopaswa kujifunza ni kwamba hali ya kutoelewana inapotokea, ufahamu utapunguza hasira yako na kukuwezesha kutambua masuala halisi yanayohusika. Badala ya kutenda bila kufikiri, fuata himizo la Yakobo, mwandikaji wa Biblia, na uwe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.”—Yakobo 1:19.

Unapozungumza na mwenzi wako, kumbuka kwamba jinsi unavyoongea naye ni muhimu. Biblia inasema kwamba “ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Hali ya kutoelewana inapotokea kati yako na mwenzi wako, je, maneno yako huumiza au huponya? Je, huzuia au husaidia kuleta maelewano? Kama vile ambavyo tumekwisha ona, kujibu bila kufikiri au kujibu kwa hasira huchochea ugomvi tu.—Methali 29:22.

Ikiwa kutoelewana hutokeza hali ya kurushiana maneno makali, jitahidi sana usikengeuke. Zingatia kile kilichosababisha ugomvi bali si mwenzi wako. Hangaikia zaidi kile unachopaswa kufanya wala si nani aliye na kosa. Uwe mwangalifu maneno yako yasichochee ugomvi zaidi. Biblia inasema: “Neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Methali 15:1) Naam, mambo unayosema na jinsi unavyoyasema yanaweza kufanya mwenzi wako akusikilize au asikusikilize.

Azimia Kusuluhisha Bali Si Kushinda

Tunaposhughulikia tatizo la kutoelewana, lengo letu ni kulisuluhisha bali si kupata ushindi. Unawezaje kupata suluhisho? Njia iliyo hakika zaidi ni kutafuta na kutumia shauri la Biblia, na waume hasa wanapaswa kuchukua hatua ya kwanza kufanya hivyo. Badala ya kuwa mwepesi kutoa kauli zenye nguvu kuhusu masuala au matatizo mnayokabili, kwa nini usitafute maoni ya Yehova kuyahusu? Sali kwake, na utafute amani ya Mungu itakayoilinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili. (Waefeso 6:18; Wafilipi 4:6, 7) Jitahidi kabisa kutafuta si faida zako za kibinafsi tu bali pia za mwenzi wako.—Wafilipi 2:4.

Kwa kawaida, kile ambacho hufanya hali iwe mbaya zaidi ni kuacha uchungu na hisia zisizodhibitiwa zitawale mawazo na matendo yako. Kwa upande mwingine, kukubali kurekebishwa na shauri la Neno la Mungu huleta amani, mapatano, na baraka za Yehova. (2 Wakorintho 13:11) Kwa hiyo, ongozwa na “hekima inayotoka juu,” onyesha sifa za Kikristo, na upate faida kama “wale wanaofanya amani.”—Yakobo 3:17, 18.

Kwa kweli, wote wanapaswa kujifunza kushughulikia hali ya kutoelewana kwa njia ya amani, hata kama kwa kufanya hivyo mtu atajinyima mambo fulani anayopenda. (1 Wakorintho 6:7) Naam, fuata shauri la Paulo la kuondolea mbali “ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu. . . . Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya.”—Wakolosai 3:8-10.

Nyakati nyingine utasema mambo ambayo utajutia baadaye. (Yakobo 3:8) Hali hiyo inapotokea, mwombe mwenzi wako msamaha. Endelea kujitahidi. Baada ya muda, yaelekea wewe na mwenzi wako mtaona mabadiliko makubwa kuhusiana na jinsi mnavyoshughulikia hali ya kutoelewana.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

Njia Tatu za Kutuliza Mabishano

Msikilize mwenzi wako. Methali 10:19

Heshimu maoni yake. Wafilipi 2:4

Itikia kwa upendo. 1 Wakorintho 13:4-7

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

Unachoweza Kufanya Sasa

Mwulize mwenzi wako maswali yafuatayo, na usikilize majibu yake bila kumkatiza. Kisha mwenzi wako anaweza kukuuliza maswali hayohayo pia.

• Je, mimi ni mbishi?

• Je, mimi husikiliza kwa makini unaposema, au hujibu bila kufikiri hata kabla hujamaliza kuzungumza?

• Je, mimi huzungumza bila kujali au kwa hasira?

• Sisi wawili tunaweza kufanya nini ili kuboresha njia yetu ya kuwasiliana, hasa tusipokubaliana juu ya jambo fulani?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, wewe husikiliza?

[Picha katika ukurasa wa 22]

“Nahisi nimepuuzwa na kutopendwa”

[Picha katika ukurasa wa 22]

“Hutumii wakati pamoja nami!”

[Picha katika ukurasa wa 22]

“Nilikaa nawe siku nzima mwezi uliopita!”