Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumeokolewa, Si Kupitia Matendo Tu, Bali Kupitia Fadhili Zisizostahiliwa

Tumeokolewa, Si Kupitia Matendo Tu, Bali Kupitia Fadhili Zisizostahiliwa

Tumeokolewa, Si Kupitia Matendo Tu, Bali Kupitia Fadhili Zisizostahiliwa

“Ninyi mmeokolewa kupitia imani . . . Si kutokana na matendo, ili mtu yeyote asiwe na sababu ya kujisifu.”—WAEFESO 2:8, 9.

1. Kuna tofauti gani kati ya Wakristo na watu kwa ujumla kuhusu mambo waliyotimiza, na kwa nini?

LEO watu hujivunia sana mambo ambayo wametimiza, na mara nyingi wao ni wepesi kujisifia mambo hayo. Wakristo ni tofauti. Wao huepuka kukazia kupita kiasi mafanikio yao, hata yale yanayohusiana na ibada ya kweli. Ingawa wanafurahia mambo ambayo watu wa Yehova wanatimiza kwa ujumla, hawakazii yale ambayo wao wenyewe wametimiza. Wanatambua kwamba katika utumishi wa Yehova, nia inayofaa ni muhimu kuliko mambo ambayo mtu ametimiza. Yeyote ambaye hatimaye atapewa zawadi ya uzima wa milele ataipata kupitia imani na fadhili zisizostahiliwa za Mungu, bali si kupitia mambo aliyotimiza.—Luka 17:10; Yohana 3:16.

2, 3. Paulo alijisifia nini, na kwa nini?

2 Mtume Paulo alitambua jambo hilo. Baada ya kusali mara tatu apate kitulizo kutokana na “mwiba katika mwili,” Yehova alimjibu hivi: “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha wewe; kwa maana nguvu zangu zinakamilishwa katika udhaifu.” Paulo alikubali uamuzi wa Yehova kwa unyenyekevu na kusema hivi: “Kwa furaha zaidi, basi, ni afadhali nijisifu kwa habari ya udhaifu wangu, ili nguvu za Kristo zibaki juu yangu kama hema.” Tunapaswa kuiga mtazamo wa unyenyekevu wa Paulo.—2 Wakorintho 12:7-9.

3 Hata ingawa Paulo alitimiza kazi za Kikristo kwa njia nzuri, alitambua kwamba mafanikio yake hayakutokana na uwezo wake mwenyewe. Alisema hivi huku akidhihirisha sifa ya kiasi: “Mimi, niliye mtu mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote, nilipewa fadhili hizi zisizostahiliwa, ili niwatangazie mataifa habari njema juu ya utajiri usiopimika wa Kristo.” (Waefeso 3:8) Hapa Paulo hajisifu wala hajioni kuwa mwadilifu kuliko wengine. “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.” (Yakobo 4:6; 1 Petro 5:5) Je, tunaiga mfano wa Paulo, na kwa unyenyekevu kujiona kuwa wadogo kuliko ndugu yetu aliye mdogo zaidi?

‘Kuwaona Wengine Kuwa Bora’

4. Kwa nini nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu kwetu kuwaona wengine kuwa bora kuliko sisi?

4 Mtume Paulo aliwashauri Wakristo hivi: ‘Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa bora kuliko ninyi.’ (Wafilipi 2:3) Huenda ikawa vigumu kufuata shauri hilo, hasa kama tuna daraka fulani. Labda inakuwa vigumu kwa sababu tumeathiriwa kwa kadiri fulani na roho ya kushindana ambayo imeenea sana ulimwenguni leo. Yaelekea tulipokuwa watoto tulifundishwa kushindana na ndugu na dada zetu nyumbani au na wanafunzi wenzetu darasani. Labda tulihimizwa sikuzote tujikakamue kuwa wanafunzi bora michezoni au shuleni. Bila shaka, ni vizuri kujitahidi kadiri tuwezavyo kutimiza jambo lolote linalofaa. Lakini, Wakristo hufanya hivyo si kwa sababu ya kujionyesha, bali ili wanufaike kikamili kutokana na jambo hilo na labda kuwanufaisha wengine pia. Hata hivyo, inaweza kuwa hatari ikiwa sikuzote tutataka kusifiwa kuwa namba moja. Jinsi gani?

5. Roho ya kushindana inaweza kutokeza nini isipodhibitiwa?

5 Isipodhibitiwa, roho ya kushindana au kujisifu inaweza kufanya mtu awe mwenye kiburi na kukosa heshima. Huenda akaonea wivu uwezo na mapendeleo ya wengine. Methali 28:22 inasema: “Mtu mwenye jicho la wivu hukimbilia vitu vyenye thamani, lakini hajui kwamba atakuwa na uhitaji.” Huenda hata kwa kimbelembele akataka kupata madaraka ambayo hastahili. Ili kutetea matendo yake, huenda akaanza kunung’unika na kuwachambua wengine, mambo ambayo Wakristo wanapaswa kuyaepuka. (Yakobo 3:14-16) Vyovyote vile, mtu huyo anakabili hatari ya kusitawisha mtazamo wa kujitanguliza.

6. Biblia hutoa onyo gani kuhusu roho ya kushindana?

6 Kwa hiyo, Biblia inawahimiza Wakristo hivi: “Na tusiwe wenye kujisifu, wenye kuchochea mashindano juu ya mtu na mwenzake, tukioneana wivu.” (Wagalatia 5:26) Mtume Yohana alitaja Mkristo mwenzake ambaye yaonekana alikuwa na roho hiyo. Alisema: “Niliandikia kutaniko jambo fulani, lakini Diotrefe, anayependa kuwa na mahali pa kwanza katikati yao, hapokei kwa heshima jambo lolote kutoka kwetu. Hiyo ndiyo sababu, nikija, nitakumbusha matendo yake ambayo anaendelea kufanya, akipiga porojo juu yetu kwa maneno maovu.” Hiyo ni hali mbaya kama nini kumpata Mkristo!—3 Yohana 9, 10.

7. Inafaa Mkristo aepuke nini kuhusiana na ushindani ambao anapata kazini?

7 Bila shaka, ni jambo lisilopatana na akili kufikiri kwamba Mkristo anaweza kuepuka kabisa mambo yote yanayotokeza mashindano. Kwa mfano, huenda kazi yake ikakabiliwa na ushindani wa kiuchumi kutoka kwa wengine au kwa makampuni yanayotengeneza bidhaa zilezile au kutoa huduma zilezile. Lakini, hata katika hali hizo, inafaa Mkristo afanye biashara yake kwa heshima, upendo, na kuwafikiria wengine. Atakataa mazoea yasiyo halali au yasiyo ya Kikristo na kuepuka kuwa mtu anayejulikana hasa kuwa mshindani. Hataona kwamba jambo lililo muhimu zaidi maishani ni kuwa namba moja. Ikiwa Mkristo anahitaji kuepuka roho ya kushindana katika mambo ya ulimwengu, basi ni muhimu hata zaidi aepuke roho hiyo katika mambo ya ibada!

“Si kwa Kujilinganisha na Mtu Yule Mwingine”

8, 9. (a) Kwa nini wazee Wakristo hawapaswi kushindana? (b) Kwa nini andiko la 1 Petro 4:10 linawahusu watumishi wote wa Mungu?

8 Mtazamo ambao Wakristo wanapaswa kuwa nao katika ibada unaonyeshwa katika maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.” (Wagalatia 6:4) Wazee kutanikoni wanajua kwamba hawashindani, hivyo wao hushirikiana na kufanya kazi kwa umoja wakiwa baraza. Wao hufurahia yale ambayo kila mmoja wao anaweza kufanya ili kuboresha hali ya kutaniko kwa ujumla. Hivyo, wao huepuka mashindano ambayo huleta mvurugo nao huweka mfano mzuri wa umoja kwa wengine kutanikoni.

9 Huenda wazee fulani wakawa na ufahamu zaidi au wakafanya mambo kwa ustadi kuliko wengine kwa sababu ya umri, uzoefu, au uwezo wa kiasili. Kwa sababu hiyo, wazee wana majukumu tofauti-tofauti katika tengenezo la Yehova. Badala ya kujilinganisha na wengine, wao hukumbuka shauri hili: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.” (1 Petro 4:10) Kwa kweli, andiko hili linawahusu watumishi wote wa Yehova kwa kuwa kwa kadiri fulani wote wamepata zawadi ya ujuzi sahihi, na wote wanafurahia pendeleo la kushiriki katika huduma ya Kikristo.

10. Yehova atakubali utumishi wetu ikiwa tutafanya nini?

10 Yehova hupendezwa tu na utumishi wetu mtakatifu ikiwa tunamtumikia kwa sababu ya upendo na kujitolea, bali si kwa sababu ya kujikweza juu ya wengine. Kwa hiyo, ni muhimu kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu utendaji wetu unaounga mkono ibada ya kweli. Ingawa hakuna yeyote anayeweza kujua nia ya mwingine, Yehova ‘anaipima mioyo.’ (Methali 24:12; 1 Samweli 16:7) Hivyo, tunapaswa kujiuliza hivi mara kwa mara: ‘Mimi humtumikia Yehova nikiwa na nia gani?’—Zaburi 24:3, 4; Mathayo 5:8.

Maoni Yafaayo Kuhusu Matendo Yetu ya Imani

11. Ni maswali gani kuhusu utendaji wetu katika huduma yanayofaa kufikiriwa?

11 Ikiwa nia yetu ndiyo muhimu zaidi ili kupata kibali cha Yehova, basi tunapaswa kuhangaikia kwa kadiri gani matendo yetu ya imani? Mradi tu tunafanya huduma yetu kwa nia ifaayo, je, ni lazima tuweke rekodi ya yale tunayofanya au kiwango tunachotimiza katika huduma? Hayo ni maswali yafaayo kwa kuwa hatutaki kuona namba kuwa muhimu kuliko yale tunayotimiza katika utumishi wetu kwa Yehova wala hatutaki kutoa ripoti nzuri kuwe hangaiko letu kuu tunaposhiriki katika utendaji wa Kikristo.

12, 13. (a) Sisi huweka rekodi ya utumishi wa shambani kwa sababu zipi? (b) Tuna sababu zipi za kufurahi tunapotazama ripoti ya ulimwenguni pote ya kazi yetu ya kuhubiri?

12 Ona yale ambayo kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova kinasema: “Wafuasi wa mapema wa Yesu Kristo walitaka sana kujua ripoti za maendeleo ya kazi ya kuhubiri. (Marko 6:30) Kitabu cha Biblia cha Matendo kinatuambia kwamba kulikuwa na watu 120 hivi roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi siku ya Pentekoste. Muda si muda idadi ya wanafunzi iliongezeka hadi 3,000 kisha 5,000. . . . (Mdo. 1:15; 2:5-11, 41, 47; 4:4; 6:7) Habari hizo za maongezeko ziliwatia moyo kama nini wanafunzi!” Kwa sababu hiyohiyo, leo Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuweka rekodi sahihi kuhusu kazi inayofanywa ulimwenguni pote ili kutimiza maneno haya ya Yesu: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Ripoti hizo huonyesha waziwazi kazi inayotimizwa ulimwenguni. Pia zinaonyesha mahali msaada unapohitajiwa, na vilevile idadi na aina ya vichapo vinavyohitajiwa ili kuendeleza kazi ya kuhubiri.

13 Hivyo, kuripoti kazi yetu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme hutuwezesha kuitimiza vizuri zaidi. Isitoshe, je, hatutiwi moyo tunaposikia kuhusu kazi ambayo ndugu zetu wanafanya katika sehemu nyingine ulimwenguni? Habari kuhusu ukuzi duniani pote hutufurahisha sana, hutuchochea tujitahidi zaidi, na kutuhakikishia kwamba Yehova anabariki kazi yetu. Ni jambo lenye kufurahisha kama nini kujua kwamba ripoti yetu imetiwa ndani ya ripoti hiyo ya ulimwenguni pote! Ripoti yetu ni ndogo ikilinganishwa na ile ya ulimwenguni pote, lakini Yehova haipuuzi. (Marko 12:42, 43) Kumbuka kwamba ripoti ya ulimwenguni pote haiwezi kuwa kamili bila ripoti yako.

14. Mbali na kuhubiri na kufundisha, ni mambo gani mengine yanayohusika katika ibada yetu kwa Yehova?

14 Bila shaka, kuna mambo mengi ambayo kila Shahidi hufanya ili kutimiza daraka lake akiwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu lakini hayaonyeshwi kwenye ripoti yake. Kwa mfano, ripoti hiyo haitii ndani funzo la kibinafsi la Biblia la ukawaida, kuhudhuria na kushiriki kwenye mikutano ya Kikristo, majukumu mbalimbali kutanikoni, kusaidia waamini wenzake, michango ya kusaidia kazi ya Ufalme ulimwenguni pote, na kadhalika. Hivyo, ingawa ripoti ya utumishi wa shambani ni muhimu na hutusaidia kuendelea kuhubiri kwa bidii bila kulegea, tunapaswa kuwa na maoni yanayofaa kuihusu. Haipaswi kuonwa kama leseni ya kiroho au pasipoti ya kupata uzima wa milele.

“Walio na Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”

15. Ingawa matendo peke yake hayawezi kutuokoa, kwa nini hayo ni muhimu?

15 Ni wazi kwamba hata ingawa matendo peke yake hayawezi kutuokoa, hayo ni muhimu. Hiyo ndiyo sababu Wakristo wanaitwa “watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema” na wanatiwa moyo ‘wafikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.’ (Tito 2:14; Waebrania 10:24) Yakobo, mwandikaji mwingine wa Biblia, anasema waziwazi hivi: “Kama vile ambavyo mwili bila roho umekufa, vivyo hivyo pia imani bila matendo imekufa.”—Yakobo 2:26.

16. Ni nini kilicho muhimu hata zaidi kuliko matendo, lakini tunapaswa kujihadhari na nini?

16 Ingawa matendo mema ni muhimu, nia yetu ya kuyatenda ni muhimu hata zaidi. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kuchunguza nia yetu mara kwa mara. Hata hivyo, kwa kuwa hakuna mwanadamu anayeweza kujua kikweli nia ya wengine, lazima tujihadhari tusiwahukumu wengine. Tunaulizwa hivi: “Wewe ni nani ili umhukumu mtumishi wa nyumbani wa mwingine?” Jibu ni wazi: “Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au kuanguka.” (Waroma 14:4) Yehova, Bwana wa wote, na Mwamuzi aliyemweka rasmi Kristo Yesu, watatuhukumu si kwa kutegemea matendo yetu tu bali pia kwa kutegemea nia yetu, nafasi zetu, upendo wetu, na kujitolea kwetu. Yehova na Kristo Yesu tu ndio wanaoweza kuhukumu kwa haki kama tumefanya yale ambayo Wakristo wanahimizwa kufanya kulingana na maneno haya ya mtume Paulo: “Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, ukilitumia sawasawa neno la kweli.”—2 Timotheo 2:15; 2 Petro 1:10; 3:14.

17. Tunapojitahidi kufanya kabisa yote tuwezayo, kwa nini tukumbuke andiko la Yakobo 3:17?

17 Yehova hatazamii tutimize mengi kuliko uwezo wetu. Andiko la Yakobo 3:17 linasema kwamba, kati ya mambo mengine, ‘hekima inayotoka juu ni yenye usawaziko.’ Tukimwiga Yehova kwa njia hiyo tutakuwa tumetenda kwa hekima na kutimiza jambo la maana. Hivyo, tunapaswa kuwa na usawaziko kuhusu mambo tunayotazamia kutimiza au yale tunayowatazamia ndugu zetu watimize.

18. Tunaweza kutazamia nini tunapokuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu matendo yetu na fadhili zisizostahiliwa za Yehova?

18 Mradi tu tunadumisha maoni yenye usawaziko kuhusu matendo yetu ya imani na kuhusu fadhili zisizostahiliwa za Yehova, tutaendelea kuwa na shangwe inayowatambulisha watumishi wa kweli wa Yehova. (Isaya 65:13, 14) Tunaweza kufurahi kwamba Yehova anamwaga baraka juu ya watu wake kwa ujumla, licha ya yale ambayo kila mmoja wetu anaweza kutimiza. Tunapodumu katika “sala na dua pamoja na kutoa shukrani,” tutamwomba Mungu atusaidie kufanya kabisa yote tunayoweza. Kisha, pasipo shaka, “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:4-7) Naam, tunaweza kupata faraja na kutiwa moyo kwa kujua kwamba tunaweza kuokolewa, si kupitia matendo tu, bali kupitia fadhili zisizostahiliwa za Yehova!

Je, Unaweza Kueleza Ni kwa Nini Wakristo

• huepuka kujisifia mambo waliyotimiza?

• huepuka kuonyesha roho ya kushindana?

• huripoti utendaji wao wa Kikristo katika huduma ya shambani?

• huepuka kuwahukumu Wakristo wenzao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

“Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha wewe”

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Wazee hufurahia yale ambayo kila mmoja wao anaweza kufanya ili kuboresha hali ya kutaniko

[Picha katika ukurasa wa 18, 19]

Ripoti ya ulimwenguni pote haiwezi kuwa kamili bila ripoti yako