Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ulimwengu Unaelekea Wapi?

Ulimwengu Unaelekea Wapi?

Ulimwengu Unaelekea Wapi?

ULIMWENGU WENYE UMOJA. Maneno hayo yanavutia sana. Bila shaka, kila mtu angependa ulimwengu uwe na umoja. Naam, watu wamezungumzia sana umoja. Viongozi wa ulimwengu wameuzungumzia mara nyingi katika mikutano yao. Mnamo Agosti 2000, zaidi ya viongozi wa dini 1,000 walihudhuria Mkutano wa Milenia Kuhusu Amani ya Ulimwengu kwenye jengo la shirika la Umoja wa Mataifa huko New York. Walizungumzia masuluhisho ya mizozo ya ulimwengu. Lakini hata mkutano wenyewe ulikuwa na mizozo kama tu ilivyo ulimwenguni. Mtaalamu mmoja wa sheria za Kiislamu kutoka Jerusalem alikataa kuuhudhuria eti kwa sababu rabi Myahudi alikuwepo. Wengine waliudhika kwa sababu Dalai Lama hakukaribishwa kuhudhuria siku mbili za kwanza eti kwa sababu hilo lingekasirisha China.

Mnamo Oktoba 2003, mkutano wa Ushirikiano wa Kiuchumi wa Mataifa ya Asia na Pasifiki ulifanywa huko Thailand. Mataifa 21 yaliyohudhuria mkutano huo yalizungumzia masuala ya usalama ulimwenguni. Yaliazimia kuvunja makundi ya magaidi na kukubaliana kuhusu njia za kufanya ulimwengu uwe salama zaidi. Lakini mkutano huo ulipokuwa ukiendelea, baadhi ya wawakilishi waliteta kuhusu maelezo ya waziri mkuu mmoja ambayo yalitajwa kuwa mashtaka yaliyojaa chuki kuwaelekea Wayahudi.

Kwa Nini Hakuna Umoja?

Ijapokuwa jitihada za kuleta umoja ulimwenguni zimezungumziwa sana, hatujaona mabadiliko makubwa. Licha ya jitihada za watu wengi wenye nia nzuri, kwa nini wanadamu wameshindwa kuleta umoja ulimwenguni hata katika karne ya 21?

Swali hilo lilijibiwa kwa sehemu na mmoja kati ya mawaziri wakuu waliohudhuria ule mkutano wa ushirikiano wa kiuchumi. Alisema hivi, “Kuna jambo hili linaloitwa utaifa.” Naam, wanadamu wamelewa utaifa. Kila taifa na kabila linachochewa na tamaa ya kujitawala. Hali ya mataifa kutaka kujitawala na roho ya mashindano na pupa hufanya mambo yawe mabaya zaidi. Mara nyingi, masilahi ya taifa yasipopatana na masilahi ya watu ulimwenguni pote, masilahi ya taifa ndiyo hutangulizwa.

Maneno ya mtunga-zaburi, “tauni inayosababisha shida,” yanaufafanua vizuri utaifa. (Zaburi 91:3) Utaifa umekuwa kama tauni inayowakumba wanadamu, na umesababisha mateso makubwa sana. Utaifa umekuwepo kwa karne nyingi, nao umetokeza chuki kuelekea watu wengine. Leo, utaifa unaendelea kusababisha migawanyiko, na viongozi hawajafaulu kuukomesha.

Viongozi wengi wanatambua kwamba utaifa na ubinafsi ndivyo visababishi vya matatizo ya ulimwengu. Kwa mfano, U Thant, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, alisema: “Matatizo mengi tunayokabili leo yamesababishwa na maoni yenye kasoro . . . Mojawapo ya maoni hayo ni kushikilia sana utaifa, yaani, ‘vyovyote vile, taifa langu ndilo bora.’” Hata hivyo, leo mataifa yenye ubinafsi mwingi yanazidi kung’ang’ania utawala. Mataifa yenye nguvu hayataki kupunguza mamlaka yake hata kidogo. Kwa mfano, gazeti International Herald Tribune lilisema hivi kuhusu Jumuiya ya Ulaya: “Bado mashindano na kutoaminiana ndicho kiini cha siasa za Ulaya. Mataifa mengi ya Jumuiya ya Ulaya yangali yanaona kwamba haifai kwa taifa lingine katika jumuiya hiyo kuwa na mamlaka zaidi na kuongoza mambo.”

Neno la Mungu, Biblia, linafafanua kwa usahihi matokeo ya utawala wote wa wanadamu, kwa kusema: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Kwa kuugawanya ulimwengu katika mataifa mbalimbali, wanadamu wameona kanuni hii ya Biblia ikitimia wakiwa vikundi au mtu mmoja-mmoja: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.”—Methali 18:1.

Muumba wetu, ambaye anajua tunachohitaji, hakukusudia kamwe wanadamu waanzishe serikali zao na kujitawala. Kwa kuanzisha serikali zao, wanadamu wamepuuza kusudi la Mungu nao hawatambui kwamba vitu vyote ni vyake. Zaburi 95:3-5 inasema: “Yehova ni Mungu mkuu na Mfalme mkuu juu ya miungu mingine yote, yeye ambaye mkononi mwake mna vina vya ndani sana vya dunia na ambaye vilele vya milima ni vyake; ambaye bahari, aliyoiumba yeye mwenyewe, ni yake na ambaye mikono yake mwenyewe iliifanyiza nchi kavu.” Mungu ndiye ana haki ya kutawala, na watu wote wanapaswa kujitiisha kwake. Mataifa yanapinga mapenzi ya Mungu kwa kuendelea kutetea serikali zao.—Zaburi 2:2.

Ni Nini Kinachohitajiwa?

Ulimwengu utakuwa na umoja tu wakati kutakapokuwa na serikali moja inayowajali watu wote. Watu wengi wanaofikiria mambo kwa makini wanatambua uhitaji huo. Hata hivyo, mara nyingi wanatafuta suluhisho mahali pasipofaa. Kwa mfano, watu wengi, kutia ndani viongozi wa dini, wamewahimiza watu watumaini Umoja wa Mataifa ulete umoja ulimwenguni. Lakini, hata yawe na malengo mazuri jinsi gani, mashirika ya wanadamu hayajaweza kamwe kusuluhisha matatizo ya wanadamu ulimwenguni pote. Badala yake, mengi ya mashirika hayo yamegawanyika sawa na vile mataifa yalivyogawanyika.

Biblia inaonya juu ya kuyatumainia mashirika ya wanadamu ili kupata suluhisho inaposema hivi: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.” (Zaburi 146:3) Je, hiyo inamaanisha kwamba haiwezekani kuwa na ulimwengu wenye umoja? La hasha, kwa kuwa kuna njia nyingine ya kupata suluhisho.

Watu wengi hawajui kwamba tayari Mungu amesimamisha serikali ambayo inaweza kuunganisha ulimwengu. Biblia inasema hivi kumhusu Yehova Mungu: “Mimi, naam, mimi nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu. Niombe, ili nikupe mataifa yawe urithi wako na miisho ya dunia iwe miliki yako mwenyewe.” (Zaburi 2:6, 8) Ona kwamba andiko hilo linasema Yehova Mungu ‘amemweka mfalme wake,’ na katika mstari wa 7 anamwita “mwanangu.” Huyo si mwingine ila Yesu Kristo, Mwana wa roho wa Mungu aliye mkuu zaidi, naye amepewa mamlaka juu ya mataifa yote.

Jinsi Ulimwengu Utakavyokuwa na Umoja

Watu wengi hawatambui serikali hiyo ya mbinguni ambayo Mungu amesimamisha. Mataifa yanaendelea kushikilia kwa nguvu kile yanachofikiri kuwa haki yao ya kutawala. Hata hivyo, Mungu hataendelea kuwavumilia wale wanaokataa kutambua haki yake ya kutawala na serikali ambayo amesimamisha. Zaburi 2:9 inasema hivi kuhusu wale wanaokataa utawala huo: “[Wewe Mwana, Yesu Kristo] utawavunja kwa fimbo ya chuma ya enzi, utawavunja vipande-vipande, kama chombo cha mfinyanzi.” Yawe yanatambua jambo hilo au la, mataifa sasa yako katika mwendo ambao utaishia katika pambano pamoja na Mungu. Kitabu cha mwisho cha Biblia kinasema juu ya “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wakikusanyika pamoja “kwa vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufunuo 16:14) Mataifa yatakomeshwa kabisa pamoja na migawanyiko yao. Kisha serikali ya Mungu itatawala bila kipingamizi chochote.

Akiwa Mtawala wa Ulimwengu Wote, Yehova Mungu kupitia Mwana wake atatumia nguvu kwa hekima kuleta mabadiliko yanayohitajiwa ili kutokeza ulimwengu wenye umoja. Serikali ya Mungu italeta umoja wa kweli na baraka kwa watu wote wanaopenda uadilifu. Tafadhali tenga dakika chache usome katika Biblia yako Zaburi ya 72. Zaburi hiyo ina unabii unaoonyesha mambo ambayo utawala wa Mwana wa Mungu utawafanyia wanadamu. Watu watafurahia umoja ulimwenguni, na matatizo yote yanayowakabili kama vile uonevu, jeuri, umaskini, na mengineyo, yatakwisha.

Katika ulimwengu wa leo uliogawanyika, watu wengi huona kwamba tumaini hilo ni ndoto. Lakini ni kosa kufikiri hivyo. Ahadi za Mungu hazijakosa kamwe kutimia, na kamwe hazitakosa kutimia. (Isaya 55:10, 11) Je, ungependa kuona ulimwengu wenye umoja? Unaweza kuuona. Kwa kweli, kuna watu ambao tayari wameanza kujitayarisha kwa ajili ya wakati huo. Ingawa wametoka katika mataifa yote, wao hawapigani, badala yake sasa wanajitiisha kwa umoja chini ya utawala wa Mungu. (Isaya 2:2-4) Hao ni akina nani? Ni Mashahidi wa Yehova. Tafadhali kubali mwaliko wa kuhudhuria mikutano yao. Yaelekea utafurahia kushirikiana na watu wanaoweza kukusaidia kujitiisha chini ya utawala wa Mungu na kufurahia umoja utakaodumu milele.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Watu wa mataifa yote wanajitayarisha kuishi katika ulimwengu wenye umoja

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

Saeed Khan/AFP/Getty Images

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

Woman grieving: Igor Dutina/AFP/Getty Images; protesters: Said Khatib/AFP/Getty Images; armored cars: Joseph Barrak/AFP/Getty Images