Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usife Moyo Katika Kufanya Yaliyo Mema

Usife Moyo Katika Kufanya Yaliyo Mema

Usife Moyo Katika Kufanya Yaliyo Mema

“DUMISHENI mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa,” akashauri mtume Petro. (1 Petro 2:12) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “-zuri” linarejelea kitu ambacho ni “maridadi, chenye kuheshimika, na bora.” Siku hizi, huenda likaonekana kuwa jambo lisilowezekana kutarajia watu wajiendeshe kwa heshima. Hata hivyo, kwa ujumla, leo watu wa Yehova wanalifuata shauri hilo la Petro. Kwa kweli, wanajulikana ulimwenguni pote kwa mwenendo wao mzuri.

Hilo ni muhimu hasa tunapofikiria magumu na matatizo tunayokabili katika ‘nyakati hizi hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1) Tunapatwa na majaribu kila siku, na ni kawaida kwa Wakristo kukabili upinzani maishani. Isitoshe, ingawa majaribu fulani ni ya muda mfupi tu, mengine ni ya kudumu, na hata huzidi kuwa makali. Hata hivyo, mtume Paulo alishauri hivi: “Na tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.” (Wagalatia 6:9) Tunawezaje kuendelea kufanya yaliyo mema huku tukikabiliana na majaribu yenye kuvunja moyo na uadui usiokoma?

Msaada wa Kufanya Yaliyo Mema

Ni wazi kwamba kuwa ‘maridadi, mwenye kuheshimika, na bora’ huhusisha utu wa ndani, yaani, sifa ya moyoni. Hivyo, kudumisha mwenendo mzuri tunapokabili majaribu na magumu si jambo tunalotenda bila kufikiri, bali ni matokeo ya kufuata na kutumia kanuni za Biblia katika hali zote za maisha. Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia katika hali hizo? Fikiria mambo yafuatayo.

Sitawisha mtazamo wa akili wa Kristo. Unyenyekevu unahitajiwa ili kuvumilia jambo ambalo huenda likaonekana si la haki. Yaelekea mtu anayejifikiria sana hawezi kuvumilia kutendewa vibaya. Hata hivyo, Yesu, “alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo.” (Wafilipi 2:5, 8) Kwa kumwiga, ‘hatutachoka wala kuzimia’ katika utumishi wetu mtakatifu. (Waebrania 12:2, 3) Jizoeze kutii kwa unyenyekevu kwa kuwa tayari kushirikiana na wale wanaoongoza katika kutaniko lenu. (Waebrania 13:17) Jifunze kuwaona wengine kuwa “bora kuliko” wewe, kwa kutanguliza masilahi yao.—Wafilipi 2:3, 4.

Kumbuka kwamba Yehova anakupenda. Tunapaswa kuwa na uhakika kwamba Yehova “yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Anatujali sana naye anataka tupate uzima wa milele. (1 Timotheo 2:4; 1 Petro 5:7) Kukumbuka kwamba hakuna chochote kinachoweza kututenganisha na upendo wa Mungu kutatusaidia tusife moyo wakati wa majaribu.—Waroma 8:38, 39.

Mtegemee Yehova kabisa. Ni muhimu kumtegemea Yehova hasa inapoonekana kwamba majaribu hayatakoma au yanapohatarisha uhai wetu. Tunapaswa kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova hataruhusu jaribu lolote ambalo ‘linapita uwezo wetu wa kulihimili,’ na kwamba sikuzote “ataifanya njia ya kutokea.” (1 Wakorintho 10:13) Tunapomtegemea Yehova tunaweza hata kukabili kwa ujasiri tishio la kifo.—2 Wakorintho 1:8, 9.

Dumu katika sala. Ni muhimu kusali kutoka moyoni. (Waroma 12:12) Kusali kwa unyoofu ni mojawapo ya njia ambazo hutusaidia kumkaribia Yehova. (Yakobo 4:8) Kupitia mambo ambayo tumejionea, tunajifunza kwamba “hata tukiomba nini . . . , yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Yehova akiruhusu tatizo liendelee ili kujaribu utimilifu wetu, sisi humwomba msaada ili kulivumilia. (Luka 22:41-43) Sala hutufundisha kwamba kamwe hatuko peke yetu, na kwamba Yehova akiwa upande wetu, sikuzote tutaibuka washindi.—Waroma 8:31, 37.

Matendo Mazuri Yanaleta ‘Sifa na Heshima’

Mara kwa mara, Wakristo wote ‘huhuzunishwa na majaribu ya namna mbalimbali.’ Hata hivyo, hatupaswi ‘kufa moyo katika kufanya yaliyo mema.’ Unapokuwa chini ya mkazo, jipe moyo kwa kujua kwamba mwishowe uaminifu wako utakuwa “sababu ya sifa na utukufu na heshima.” (1 Petro 1:6, 7) Tumia kikamili maandalizi yote ya kiroho kutoka kwa Yehova ili kuimarisha imani yako. Unapohitaji msaada wa kibinafsi, waone wale wanaotumika wakiwa wazee, walimu, na washauri katika kutaniko la Kikristo. (Matendo 20:28) Hudhuria kwa ukawaida mikutano yote ya kutaniko ambayo ‘hutuchochea katika upendo na matendo mazuri.’ (Waebrania 10:24) Programu ya kusoma Biblia kila siku na funzo la kibinafsi vitakusaidia kuendelea kuwa chonjo na mwenye nguvu kiroho. Pia utakuwa mwenye nguvu kiroho unaposhiriki kwa ukawaida katika huduma ya Kikristo.—Zaburi 1:1-3; Mathayo 24:14.

Kadiri unavyoona upendo na utunzaji wa Yehova, ndivyo tamaa yako ya kuwa mwenye “bidii kwa ajili ya kazi njema” inavyoongezeka. (Tito 2:14) Kumbuka kwamba “yule ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Naam, azimia ‘kutokufa moyo katika kufanya yaliyo mema’!

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Tunapaswa kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova hataruhusu jaribu lolote ambalo ‘linapita uwezo wetu wa kulihimili,’ na kwamba sikuzote “ataifanya njia ya kutokea”

[Picha katika ukurasa wa 30]

Kuwa na utendaji mwingi wa kiroho kunaweza kututayarisha kukabiliana na majaribu