Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Aliteswa kwa Sababu ya Imani Yake”

“Aliteswa kwa Sababu ya Imani Yake”

“Aliteswa kwa Sababu ya Imani Yake”

MJI wa Cernobbio ulio kaskazini mwa Italia umeanzisha makumbusho kwenye eneo la kupumzikia ili kuwakumbuka watu ambao haki zao za kibinadamu zilivunjwa. Moja ya mabamba yanayoonyeshwa ni la Narciso Riet, mzaliwa wa Ujerumani ambaye wazazi wake walikuwa Waitalia. Riet alipata kuwa Shahidi wa Yehova miaka ya 1930. Wakati wa utawala wa Hitler, Mashahidi wa Yehova waliteswa kwa sababu walimtukuza Mungu wa kweli Yehova na kukataa kumtukuza Hitler.

Riet alikimbilia Cernobbio baada ya askari walinzi kugundua kwamba alishiriki kuingiza nakala za Mnara wa Mlinzi kwenye kambi za mateso. Akiwa huko aliombwa atafsiri Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Kiitaliano na kuwasambazia waamini wenzake wa eneo la karibu. Kazi zake ziligunduliwa. Ofisa mmoja wa Hitler na askari waliokuwa chini yake waliivamia nyumba ya Riet, wakamkamata, na kuchukua vitu walivyofikiri ni uthibitisho wa kosa, yaani, Biblia mbili na barua chache! Riet alihamishiwa Ujerumani ambako alifungwa katika kambi ya mateso ya Dachau, na kuuawa muda mfupi kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kumalizika. Maneno kwenye bamba hilo la kumbukumbu yanasema, “Aliteswa kwa sababu ya imani yake.”

Imani ya Narciso Riet na mamia ya Mashahidi wengine ambao waliteswa na Wanazi, inawatia moyo Wakristo leo waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova, ambaye ndiye tu anayestahili ibada yao katika ulimwengu wote. (Ufunuo 4:11) Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu.” Mungu atayakumbuka matendo yao na kuwapa baraka kwa sababu ya ujasiri wao.—Mathayo 5:10; Waebrania 6:10.