Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Enyi Vijana, Msifuni Yehova!

Enyi Vijana, Msifuni Yehova!

Enyi Vijana, Msifuni Yehova!

“Msifuni Yehova kutoka duniani, . . . enyi vijana, nanyi mabikira pia.”—Zaburi 148:7, 12.

1, 2. (a) Vijana wengi wanajua wana vizuizi vya aina gani? (b) Kwa nini vijana hawapaswi kuchukia vizuizi ambavyo wazazi wao huwawekea?

MARA nyingi vijana huwa wanajua vizuri mambo ambayo bado hawaruhusiwi kufanya. Wengi wao wanaweza kukuambia umri ambao wanapaswa kuwa nao kabla ya kuruhusiwa kuvuka barabara peke yao, kulala wakiwa wamechelewa, au kuendesha gari. Huenda nyakati nyingine kijana akaona kwamba anapoomba ruhusa ya kufanya jambo fulani, mara nyingi yeye hujibiwa kwa maneno yaleyale, “Ngojea hadi uwe na umri mkubwa zaidi.”

2 Enyi vijana, mnajua kwamba wazazi wenu huona ni jambo la hekima kuwawekea vizuizi hivyo, labda ili kuwalinda. Pia, mnajua kabisa kwamba Yehova hufurahi mnapowatii wazazi wenu. (Wakolosai 3:20) Je, nyakati nyingine ninyi huhisi kwamba bado hamjaanza kufurahia maisha? Je, mmekatazwa kufanya mambo yote muhimu hadi mtakapokuwa na umri mkubwa zaidi? Hiyo si kweli kabisa! Kuna kazi inayoendelea leo ambayo ni muhimu kuliko jambo lingine lolote ambalo huenda unangojea kufanya. Je, ninyi vijana mnaruhusiwa kufanya kazi hiyo? Ndiyo, mnaruhusiwa na pia mnaalikwa na Mungu Aliye Juu Zaidi kuifanya!

3. Yehova anawaalika vijana wafurahie pendeleo gani, na sasa tutazungumzia maswali gani?

3 Tunazungumzia kazi gani? Ona maneno ya andiko la msingi la makala hii: “Msifuni Yehova kutoka duniani, . . . enyi vijana, nanyi mabikira pia, enyi wazee pamoja na wavulana.” (Zaburi 148:7, 12) Andiko hilo linaonyesha una pendeleo kuu, yaani, unaweza kumsifu Yehova. Je, unafurahia kushiriki katika kazi hiyo ukiwa kijana? Wengi wanaifurahia. Ili kuelewa kwa nini inafaa uifurahie, acheni tuchunguze maswali matatu. Kwanza, kwa nini umsifu Yehova? Pili, unawezaje kumsifu kwa matokeo? Tatu, ni wakati gani unaofaa kuanza kumsifu?

Kwa Nini Umsifu Yehova?

4, 5. (a) Kulingana na Zaburi ya 148, tuko katika hali gani nzuri? (b) Vitu vilivyoumbwa ambavyo haviwezi kuongea wala kufikiri vinawezaje kumsifu Yehova?

4 Sababu kuu ya kumsifu Yehova ni kwamba yeye ndiye Muumba. Zaburi ya 148 inatusaidia kuzingatia ukweli huo. Hebu wazia jinsi ambavyo ungehisi kama ungekaribia watu wengi wanaoimba kwa umoja wimbo mzuri wenye kuchochea! Namna gani kama ungejua kwamba maneno ya wimbo huo ni ya kweli, nayo yanaeleza mambo unayojua ni muhimu, yenye kufurahisha, na yenye kutia moyo? Je, ungetamani kujifunza wimbo huo na kujiunga nao? Wengi wetu tungefanya hivyo. Zaburi ya 148 inaonyesha kwamba uko katika hali kama hiyo lakini nzuri zaidi. Zaburi hiyo inataja umati mkubwa ambao unamsifu Yehova kwa umoja. Lakini unapoisoma, unaweza ukaona jambo fulani lisilo la kawaida. Jambo gani?

5 Vitu vingi vinavyomsifu Yehova ambavyo vimetajwa katika Zaburi ya 148 haviwezi kuongea wala kufikiri. Kwa mfano, tunasoma kwamba jua, mwezi, nyota, theluji, upepo, milima, na vilima humsifu Yehova. Vitu hivyo visivyo na uhai vinawezaje kumsifu Yehova? (Mstari wa 38, na 9) Kwa njia ileile ambayo miti, viumbe wa baharini, na wanyama humsifu. (Mstari wa 79, na 10) Je, umewahi kutazama machweo yenye kuvutia, kutazama mwezi mpevu kwenye anga yenye nyota, kustaajabishwa na mandhari nzuri, au kucheka unapotazama wanyama wakicheza? Basi “umesikia” wimbo wa sifa wa vitu vilivyoumbwa. Vitu vyote ambavyo Yehova aliumba hutukumbusha kwamba yeye ndiye Muumba mweza-yote, na kwamba hakuna mwingine katika ulimwengu wote aliye na nguvu, hekima, au upendo mwingi kuliko yeye.—Waroma 1:20; Ufunuo 4:11.

6, 7. (a) Zaburi ya 148 inataja viumbe gani wenye akili kuwa wanamsifu Yehova? (b) Kwa nini tunaweza kuchochewa kumsifu Yehova? Toa mfano.

6 Zaburi ya 148 pia inasema kwamba viumbe wenye akili wanamsifu Yehova. Katika mstari wa 2, tunaona “jeshi” la mbinguni la malaika wa Yehova wakimsifu. Mstari wa 11 unawaalika wanadamu wenye nguvu na uwezo, kama vile wafalme na waamuzi, washiriki katika kumsifu Mungu. Ikiwa malaika wenye nguvu hufurahia kumsifu Yehova, ni mwanadamu gani ambaye kwa kweli anaweza kusema kwamba ni wa maana sana asiweze kumsifu? Kisha, mstari wa 12 na 13 unawaalika vijana wajiunge na wengine kumsifu Yehova. Je, unachochewa kufanya hivyo?

7 Fikiria mfano huu. Ikiwa rafiki yako angekuwa na kipawa cha pekee, labda katika michezo, sanaa, au muziki, je, ungewaeleza watu wa familia yenu na marafiki wengine kumhusu? Bila shaka. Kujifunza yote ambayo Yehova amefanya kunaweza pia kutuchochea kufanya vivyo hivyo. Kwa mfano, Zaburi 19:1, 2 inasema kwamba anga yenye nyota hufanya “maneno yabubujike.” Nasi tunapofikiria mambo ya ajabu ambayo Yehova amefanya, hatuwezi kuacha kuwaeleza wengine kumhusu Mungu wetu.

8, 9. Yehova anataka tumsifu kwa sababu gani?

8 Sababu nyingine kuu ya kumsifu Yehova ni kwamba yeye anataka tufanye hivyo. Kwa nini? Je, ni kwa sababu yeye anahitaji kusifiwa na wanadamu? La. Huenda wakati mwingine sisi wanadamu tukahitaji kusifiwa, lakini Yehova ni mkuu kuliko sisi. (Isaya 55:8) Yeye hana shaka kujihusu wala kuhusu sifa zake. (Isaya 45:5) Hata hivyo, yeye anataka tumsifu na anafurahi tunapofanya hivyo. Kwa nini? Fikiria sababu mbili. Kwanza, anajua kwamba tunahitaji kumsifu. Alituumba tukiwa na uhitaji wa kiroho, uhitaji wa kuabudu. (Mathayo 5:3) Yehova hufurahi anapoona tukitosheleza uhitaji huo, kama vile wazazi wako hufurahi kukuona ukila chakula wanachojua ni kizuri kwako.—Yohana 4:34.

9 Pili, Yehova anajua kwamba watu wengine wanahitaji kutusikia tukimsifu. Mtume Paulo alimwandikia kijana Timotheo maneno haya: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.” (1 Timotheo 4:16) Naam, unapomsifu Yehova Mungu kwa kuwafundisha wengine kumhusu, huenda wakamjua pia. Ujuzi huo unaweza kufanya wapate wokovu wa milele!—Yohana 17:3.

10. Kwa nini tunachochewa kumsifu Mungu?

10 Bado kuna sababu nyingine ya kumsifu Yehova. Kumbuka ule mfano wa rafiki yako mwenye kipawa cha pekee. Kama ungesikia wengine wakisema uwongo kumhusu na kuchongea jina lake, je, hungejitahidi hata zaidi kumsifu? Yehova amechongewa sana katika ulimwengu huu. (Yohana 8:44; Ufunuo 12:9) Hivyo, wale wanaompenda wanachochewa kusema kweli kumhusu. Je, wewe pia ungependa kudhihirisha upendo na shukrani zako kwa Yehova na kuonyesha kwamba unataka awe Mtawala wako badala ya kutawaliwa na Shetani, adui yake mkuu? Unaweza kufanya yote hayo kwa kumsifu Yehova. Basi, swali lingine ni, unawezaje kumsifu?

Jinsi Vijana Wengine Walivyomsifu Yehova

11. Ni mifano gani katika Biblia inayoonyesha kwamba vijana wanaweza kuwa na matokeo sana katika kumsifu Yehova?

11 Biblia inaonyesha kwamba vijana huwa na matokeo sana wanapomsifu Yehova. Kwa mfano, kuna msichana Mwisraeli aliyetekwa na Wasiria. Msichana huyo alimhubiria kwa ujasiri bimkubwa wake kumhusu Elisha, nabii wa Yehova. Kwa sababu ya maneno yake, muujiza ulitokea na ushahidi wenye nguvu ukatolewa. (2 Wafalme 5:1-17) Yesu pia alihubiri kwa ujasiri alipokuwa mtoto. Kati ya mambo yote yaliyotukia alipokuwa kijana ambayo yangeweza kuandikwa katika Biblia, Yehova alichagua jambo moja. Alichagua pindi ambapo, Yesu aliyekuwa na umri wa miaka 12, aliwauliza maswali walimu wa dini kwenye hekalu huko Yerusalemu na kuwastaajabisha kwa sababu ya uelewaji wake kuhusu njia za Yehova.—Luka 2:46-49.

12, 13. (a) Yesu alifanya nini hekaluni muda mfupi kabla ya kufa, na watu waliokuwepo walitendaje? (b) Yesu alihisije kuhusu sifa zilizotolewa na wavulana?

12 Alipokuwa mtu mzima, Yesu pia aliwachochea watoto wamsifu Yehova. Kwa mfano, siku chache kabla ya kufa, Yesu alienda hekaluni huko Yerusalemu. Biblia inasema kwamba alifanya “mambo ya kustaajabisha” huko. Aliwafukuza wale waliofanya mahali hapo patakatifu kuwa pango la wezi. Pia aliwaponya vipofu na vilema. Wote waliokuwepo, hasa viongozi wa dini, walipaswa kuchochewa kumsifu Yehova na Mwana wake, Masihi. Lakini inasikitisha kwamba siku hizo watu wengi hawakumsifu. Walijua kwamba Yesu alitumwa na Mungu, lakini waliwaogopa viongozi wa dini. Hata hivyo, kuna watu waliosema kwa ujasiri. Je, unawajua? Biblia inasema: ‘Wakuu wa makuhani na waandishi walipoyaona mambo ya kustaajabisha ambayo Yesu alifanya na wale wavulana waliokuwa wakipaaza sauti katika hekalu na kusema: “Mwokoe Mwana wa Daudi, tunaomba!” wakaghadhibika na kumwambia Yesu: “Je, unasikia mambo ambayo hawa wanasema?”’—Mathayo 21:15, 16; Yohana 12:42.

13 Makuhani hao walitumaini kwamba Yesu angewanyamazisha wavulana hao waliokuwa wakimsifu. Je, alifanya hivyo? La! Yesu aliwajibu hivi: “Ndiyo. Je, ninyi hamkusoma hili kamwe, ‘Kutoka katika kinywa cha watoto na wanaonyonya umetoa sifa’?” Ni wazi kwamba Yesu na Baba yake walipendezwa na sifa ambazo wavulana hao walitoa. Watoto hao walifanya jambo ambalo watu wote wazima waliokuwepo walipaswa kufanya. Katika akili zao changa, waliona mambo waziwazi kabisa. Walimwona mtu huyo akifanya mambo ya kustaajabisha, akizungumza kwa ujasiri na imani, na kuonyesha upendo mwingi kwa Mungu na kwa watu wake. Kama alivyosema, yeye alikuwa “Mwana [aliyeahidiwa] wa Daudi,” yaani, Masihi. Wavulana hao walibarikiwa kwa imani yao na kupata pendeleo la kutimiza unabii.—Zaburi 8:2.

14. Vijana husaidiwaje na vipawa vyao kumsifu Mungu?

14 Mifano hiyo inaweza kutufunza nini? Kwamba vijana wanaweza kumsifu Yehova kwa matokeo sana. Mara nyingi wao huwa na kipawa cha kuiona kweli waziwazi na kwa urahisi, nao huonyesha imani yao kwa bidii nyingi. Pia wana kipawa kinachotajwa kwenye Methali 20:29: “Uzuri wa vijana ni nguvu zao.” Naam, enyi vijana mna nguvu, nazo zinafaa sana katika kumsifu Yehova. Mnawezaje hasa kutumia vipawa hivyo?

Unawezaje Kumsifu Yehova?

15. Unahitaji kuwa na nia gani ili kumsifu Yehova kwa matokeo?

15 Kumsifu Yehova kwa njia yenye matokeo huanzia moyoni. Huwezi kumsifu Yehova kwa matokeo ikiwa unamsifu kwa sababu wengine wanataka ufanye hivyo. Kumbuka, hii ndiyo amri kuu kuliko zote: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Je, umemjua Yehova kibinafsi kupitia kujifunza Neno lake? Matokeo bora ya kujifunza Neno la Yehova ni kumpenda. Kwa kawaida, upendo huo huonyeshwa kwa kumsifu. Ikiwa nia yako ni wazi na ni yenye nguvu, basi uko tayari kumsifu Yehova kwa shauku.

16, 17. Mwenendo una umuhimu gani katika kumsifu Yehova? Toa mfano.

16 Hata kabla hujafikiria yale ambayo utasema, fikiria matendo yako. Kama sikuzote yule msichana Mwisraeli wa siku za Elisha hangekuwa mwenye adabu, mwenye heshima, au mnyoofu, je, unafikiri kwamba Wasiria waliomteka wangemsikiliza alipowaeleza kumhusu nabii wa Yehova? Yaelekea hawangemsikiliza. Vivyo hivyo, inaelekea watu watakusikiliza wakiona kwamba wewe ni mnyoofu, unawaheshimu, na una adabu. (Waroma 2:21) Fikiria mfano mmoja.

17 Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 11 huko Ureno alishinikizwa shuleni kusherehekea sikukuu ambazo zingechafua dhamiri yake inayoongozwa na Biblia. Alimweleza mwalimu wake kwa heshima kwa nini hangesherehekea sikukuu hizo, lakini mwalimu huyo akamdhihaki. Kwa muda fulani, mwalimu huyo alijaribu tena na tena kumwaibisha huku akidhihaki dini yake. Hata hivyo, msichana huyo aliendelea kumheshimu. Miaka kadhaa baadaye, dada huyo mchanga akawa painia wa kawaida, yaani, mhudumu wa wakati wote. Kwenye kusanyiko moja, alitazama watu wakibatizwa na kumtambua mmoja wao. Alikuwa yule mwalimu wake wa zamani! Baada ya kukumbatiana na kulia, mwanamke huyo alimwambia dada huyo kijana kwamba hakusahau kamwe mwenendo wake wenye heshima. Shahidi fulani alimtembelea, kisha mwalimu huyo akamweleza tabia ya mwanafunzi wake wa zamani. Hivyo, funzo la Biblia lilianzishwa, na mwanamke huyo akakubali kweli. Naam, mwenendo wako unaweza kuwa njia nzuri sana ya kumsifu Yehova!

18. Kijana anaweza kufanya nini ikiwa anasita kuanzisha mazungumzo kuhusu Biblia na kumhusu Yehova Mungu?

18 Je, nyakati nyingine wewe huona ni vigumu kuanzisha mazungumzo shuleni kuhusu imani yako? Si wewe tu unayehisi hivyo. Lakini unaweza kufanya iwe rahisi kwa wengine kukuuliza maswali kuhusu imani yako. Kwa mfano, ikiwa inaruhusiwa na inakubaliwa kisheria kufanya hivyo, kwa nini usibebe vichapo vinavyoifafanua Biblia na uvisome wakati wa chakula cha mchana au nyakati nyingine inaporuhusiwa kufanya hivyo shuleni? Huenda wanafunzi wenzako wakauliza kuhusu yale unayosoma. Kwa kuwajibu na kuwaeleza mambo unayoona kuwa yenye kupendeza kuhusu makala au kitabu unachosoma, huenda ukaanzisha mazungumzo mazuri. Kumbuka kuuliza maswali ili ujue imani ya mwanafunzi mwenzako. Msikilize kwa makini, na umweleze yale ambayo umejifunza katika Biblia. Kama visa vilivyotajwa kwenye ukurasa wa 29 vinavyoonyesha, vijana wengi wanamsifu Mungu shuleni. Hilo huwaletea furaha nyingi na huwasaidia wengi kumjua Yehova.

19. Vijana wanawezaje kuwa wenye matokeo zaidi wanapohubiri nyumba kwa nyumba?

19 Kuhubiri nyumba kwa nyumba ndiyo njia yenye matokeo zaidi ya kumsifu Yehova. Ikiwa bado hujaanza kuhubiri, kwa nini usiweke mradi wa kuanza? Ikiwa tayari wewe ni mhubiri, je, kuna miradi mingine unayoweza kujiwekea? Kwa mfano, badala ya kusema jambo lilelile kwenye kila nyumba, jitahidi kufanya maendeleo kwa kuomba madokezo kutoka kwa wazazi wako na Mashahidi wengine wenye uzoefu. Jifunze kutumia Biblia zaidi, kufanya ziara za kurudia zenye matokeo, na kuanzisha funzo la Biblia. (1 Timotheo 4:15) Kadiri unavyomsifu Yehova katika njia hizo, ndivyo utakavyokuwa mwenye matokeo zaidi na kufurahia huduma zaidi.

Ni Wakati Gani Unaofaa Kuanza Kumsifu Yehova?

20. Kwa nini vijana hawahitaji kuona kwamba wao ni wachanga sana wasiweze kumsifu Yehova?

20 Kati ya yale maswali matatu ambayo yamezungumziwa, jibu la swali hili la mwisho ndilo rahisi zaidi. Ona jibu la moja kwa moja la Biblia: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” (Mhubiri 12:1) Naam, sasa ndio wakati wa kuanza kumsifu Yehova. Ni rahisi sana kusema: “Mimi ni mchanga sana, siwezi kumsifu Yehova. Sina uzoefu. Nitangoja hadi nitakapokuwa na umri mkubwa zaidi.” Kuna wengine waliohisi hivyo. Kwa mfano, kijana Yeremia alimwambia Yehova hivi: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama, mimi hakika sijui jinsi ya kusema, kwa sababu mimi ni mvulana tu.” Yehova alimhakikishia kwamba hakuhitaji kuogopa. (Yeremia 1:6, 7) Vivyo hivyo, hatuhitaji kuogopa tunapomsifu Yehova. Hakuna madhara yanayoweza kutupata ambayo Yehova hawezi kuyaondoa kabisa.—Zaburi 118:6.

21, 22. Kwa nini vijana wanaomsifu Yehova wanalinganishwa na umande, na kwa nini ulinganishi huo unatia moyo?

21 Basi, tunawahimiza vijana hivi: Msisite kumsifu Yehova! Sasa, ukiwa ungali kijana ndio wakati bora zaidi wa kushiriki katika kazi muhimu zaidi inayofanywa duniani leo. Unapofanya hivyo, unakuwa sehemu ya familia nzuri, yaani, familia ya mbinguni na duniani ya wale wanaomsifu Yehova. Yehova anafurahi kwamba wewe ni sehemu ya familia yake. Ona maneno haya ambayo mtunga-zaburi aliongozwa na roho ya Yehova kusema kumhusu: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako. Katika fahari za utakatifu, kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko, una kundi lako la vijana kama matone ya umande.”—Zaburi 110:3.

22 Matone ya umande yanayomeremeta katika nuru ya asubuhi huvutia sana, sivyo? Yanang’aa na kuburudisha, nayo hayawezi kuhesabika. Hivyo ndivyo Yehova anavyowaona ninyi vijana ambao mnamsifu kwa uaminifu nyakati hizi za hatari. Ni wazi kwamba uamuzi wako wa kumsifu Yehova huufanya moyo wake ushangilie. (Methali 27:11) Basi, enyi vijana, msifuni Yehova!

Ungejibuje?

• Ni zipi baadhi ya sababu muhimu za kumsifu Yehova?

• Ni mifano gani ya Biblia inayoonyesha kwamba vijana wanaweza kuwa na matokeo sana katika kumsifu Yehova?

• Vijana wanawezaje kumsifu Yehova leo?

• Vijana wanapaswa kuanza kumsifu Yehova wakati gani, na kwa nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ikiwa rafiki yako angekuwa na kipawa cha pekee, je, hungewaeleza wengine jambo hilo?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Huenda wanafunzi wenzako wakataka kujua kuhusu imani yako

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ikiwa unataka kuboresha huduma yako, omba madokezo kutoka kwa Shahidi mwenye uzoefu