Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kazi Ni Baraka au Ni Laana?

Je, Kazi Ni Baraka au Ni Laana?

Je, Kazi Ni Baraka au Ni Laana?

‘Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kuona mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.’—Mhubiri 2:24.

“MIMI huhisi nimeishiwa na nguvu kabisa baada ya kazi.” Katika uchunguzi mmoja uliofanywa majuzi, theluthi moja ya wafanyakazi walisema hivyo ndivyo wanavyohisi mara nyingi. Jambo hilo halishangazi kwa kuwa watu hukabili mkazo kazini. Mbali na kufanya kazi muda mrefu, wao pia hufanyia kazi nyingine nyingi nyumbani, na mara nyingi wakubwa wao hata hawawapongezi.

Tangu bidhaa zilipoanza kuzalishwa kwa wingi, wafanyakazi wengi huhisi kwamba kazi yao si muhimu. Mara nyingi msukumo wao na uwezo wao wa kubuni mambo hukandamizwa. Hilo huathiri mtazamo wa watu kuhusu kazi. Wao huacha kuvutiwa na kazi yao. Tamaa ya kutaka kufanya kazi bora au kuifanya kwa ustadi hukandamizwa kwa urahisi. Mambo hayo yanaweza kumfanya mtu asipendezwe na kazi yake, na hata labda kuichukia.

Kuchunguza Mtazamo Wetu

Ni kweli kwamba hatuwezi kubadili hali zetu nyakati zote. Lakini je, hukubali kwamba tunaweza kubadili mtazamo wetu? Ikiwa unahisi kwamba umeathiriwa kwa kadiri fulani na maoni mabaya kuhusu kazi, itafaa uchunguze maoni na kanuni za Mungu kuhusu habari hii. (Mhubiri 5:18) Wengi wamegundua kwamba kuchunguza mambo hayo kumewasaidia kupata furaha na uradhi kwa kadiri fulani kutokana na kazi yao.

Mungu ndiye Mfanyakazi Mkuu Zaidi. Mungu ni mfanyakazi. Huenda hatujawahi kumfikiria kuwa mfanyakazi, lakini hivyo ndivyo anavyojitambulisha kwanza katika Biblia. Simulizi la Mwanzo linaanza kwa kutaja jinsi Yehova alivyoumba mbingu na dunia. (Mwanzo 1:1) Fikiria kazi mbalimbali ambazo Mungu alifanya alipoanza kuumba. Alikuwa mbuni, msimamizi, injinia, msanii, mtaalamu wa kuteua vifaa vya kazi, mjenzi, mwanakemia, mwanabiolojia, mratibu, mtaalamu wa wanyama na lugha, na kadhalika.—Methali 8:12, 22-31.

Kazi ya Mungu ilikuwaje? Biblia inasema ilikuwa “nzuri,” ‘njema sana.’ (Mwanzo 1:4, 31) Kwa kweli, uumbaji ‘unatangaza utukufu wa Mungu,’ nasi pia tunapaswa kumsifu!—Zaburi 19:1; 148:1.

Hata hivyo, Mungu hakumaliza kazi yake kwa kuumba mbingu halisi, dunia, na watu wawili wa kwanza. Mwana wa Yehova, Yesu Kristo, alisema: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa.” (Yohana 5:17) Naam, Yehova anaendelea kufanya kazi kwa kutosheleza mahitaji ya viumbe wake, kuwapa chakula, na kuwaokoa waabudu wake waaminifu. (Nehemia 9:6; Zaburi 36:6; 145:15, 16) Hata anawatumia wanadamu, ambao ni ‘wafanyakazi wenzake,’ kusaidia katika kazi mbalimbali.—1 Wakorintho 3:9.

Kazi inaweza kuwa baraka. Lakini, je, Biblia haisemi kwamba kazi ni laana? Huenda mtu akafikiri kwamba andiko la Mwanzo 3:17-19 linamaanisha kuwa Adamu na Hawa walipoasi, Mungu aliwaadhibu kwa kuwapa kazi yenye kulemea. Alipokuwa akiwahukumu watu hao wa kwanza, Mungu alimwambia Adamu hivi: “Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo.” Je, kwa maneno hayo Mungu aliilaani kazi kwa ujumla?

La. Badala yake, Paradiso ya Edeni haingepanuliwa wakati huo kwa sababu Adamu na Hawa walikosa uaminifu. Mungu aliulaani udongo. Mwanadamu angehitaji kutoa jasho ili apate riziki kutokana na udongo.—Waroma 8:20, 21.

Biblia inaonyesha kwamba kazi si laana, bali ni baraka na tunapaswa kuipenda sana. Kama ilivyotajwa juu, Mungu ni mfanyakazi mwenye bidii. Kwa kuwa amewaumba wanadamu kwa mfano wake, Yehova amewapa uwezo na mamlaka ya kusimamia uumbaji wake uliopo duniani. (Mwanzo 1:26, 28; 2:15) Mungu aliwapa wanadamu kazi hiyo kabla hajasema maneno yaliyo katika Mwanzo 3:19. Ikiwa kazi ingekuwa laana au jambo ovu, Yehova hangewahimiza wanadamu waifanye. Noa na familia yake walikuwa na kazi nyingi ya kufanya kabla na baada ya Gharika. Baada ya Yesu kuja duniani, wanafunzi wake walihimizwa pia wafanye kazi.—1 Wathesalonike 4:11.

Hata hivyo, sote tunajua kwamba kazi inaweza kuwa yenye kulemea sana siku hizi. Mfadhaiko, hatari, uchovu, kukata tamaa, mashindano, udanganyifu, na ukosefu wa haki ni baadhi ya “miiba na mibaruti” inayosababishwa na kazi. Lakini kazi yenyewe si laana. Kwenye Mhubiri 3:13, Biblia inasema kwamba kazi na matunda yake ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Ona sanduku lenye kichwa “Kukabiliana na Mfadhaiko Unaosababishwa na Kazi.”

Unaweza kumtukuza Mungu kwa kazi yako. Sikuzote watu wamesifu kazi bora. Ubora wa kazi ni mojawapo ya mambo muhimu ambayo mtu anahitaji kuzingatia ili awe na maoni kama ya Biblia kuhusu kazi. Kazi ya Mungu ni bora kabisa. Ametupa vipawa na ustadi, naye anataka tuvitumie vizuri. Kwa mfano, wakati wa ujenzi wa ile maskani katika Israeli ya kale, Yehova aliwajaza hekima, uelewaji, na ujuzi watu kama Bezaleli na Oholiabu ili wafanye kazi za ufundi na kutimiza majukumu mbalimbali. (Kutoka 31:1-11) Hilo linaonyesha kwamba Mungu alipendezwa sana na kusudi la kazi hiyo, ufundi waliotumia, ubuni, na mambo mengine yaliyohusiana na kazi yao.

Jambo hilo linaweza kubadili sana maoni yetu kuhusu vipawa tulivyo navyo na mazoea yetu ya kazi. Linatusaidia kuona mambo hayo kuwa zawadi kutoka kwa Mungu, ambazo hazipaswi kupuuzwa. Hivyo, Wakristo wanashauriwa kufanya kazi yao kana kwamba Mungu mwenyewe anaikagua: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kama kwa wanadamu.” (Wakolosai 3:23) Watumishi wa Mungu wanaamuriwa wafanye kazi njema, na hilo hufanya ujumbe wao uwavutie wafanyakazi wenzao na watu wengine.—Ona sanduku lenye kichwa “Kutumia Kanuni za Biblia Kazini.”

Hivyo, tunapaswa kujichunguza tuone ikiwa sisi hufanya kazi bora na kwa bidii. Je, Mungu anapendezwa na jinsi tunavyofanya kazi? Je, tunaridhika na jinsi tunavyofanya kazi zetu? Ikiwa sivyo, basi tunahitaji kufanya maendeleo.—Methali 10:4; 22:29.

Uwe na usawaziko kati ya kazi na mambo ya kiroho. Ingawa ni vizuri kufanya kazi kwa bidii, kuna jambo jingine muhimu linalohitajiwa ili kupata uradhi kazini na maishani. Tunahitaji kuzingatia mambo ya kiroho. Mfalme Sulemani, aliyefanya kazi kwa bidii na kufurahia utajiri na starehe maishani, alikata kauli hii: “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13.

Ni wazi kwamba tunapaswa kuzingatia mapenzi ya Mungu tunapofanya jambo lolote lile. Je, tunafanya mambo kupatana na mapenzi yake au kinyume chake? Je, tunajitahidi kumpendeza Mungu, au tunajitahidi tu kujipendeza? Tusipofanya mapenzi ya Mungu, hatimaye tutaumia kwa kukata tamaa, kuhisi upweke, na kujiona kuwa bure kabisa.

Steven Berglas alisema kwamba wakubwa wa kazi waliochoka kupindukia ‘hutafuta jambo linalowapendeza sana na kulifanya kuwa sehemu ya maisha yao.’ Hakuna jambo bora kuliko kumtumikia Yule aliyetupa ustadi na vipawa vya kufanya kazi inayofaa. Hatuwezi kukosa uradhi tunapofanya kazi inayompendeza Muumba wetu. Yesu aliona kazi aliyopewa na Yehova kuwa yenye kujenga, yenye kuridhisha, na yenye kuburudisha kama chakula. (Yohana 4:34; 5:36) Kumbuka kwamba Mungu, aliye Mfanyakazi Mkuu Zaidi, anatualika tuwe “wafanyakazi [wenzake].”—1 Wakorintho 3:9.

Kumwabudu Mungu na kukua kiroho hutuwezesha kupata uradhi kutokana na kazi na majukumu yetu. Kwa kuwa mara nyingi watu hukabili mkazo, mizozano, na hudaiwa mengi kazini, imani yetu yenye nguvu na hali yetu ya kiroho inaweza kutuimarisha tunapoendelea kujitahidi kuwa wafanyakazi na wasimamizi bora. Kwa upande mwingine, mambo tunayokabili maishani katika ulimwengu huu usiomwogopa Mungu yanaweza kutusaidia kuona mahali tunapohitaji kuimarisha imani yetu.—1 Wakorintho 16:13, 14.

Wakati Ambapo Kazi Itakuwa Baraka

Wale wanaojitahidi sasa kumtumikia Mungu kwa bidii wanaweza kutazamia wakati ambapo atarudisha Paradiso na kutakuwa na kazi nyingi nzuri dunia pote. Isaya, nabii wa Yehova, alitabiri hivi kuhusu maisha ya wakati huo: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. . . . Wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.”—Isaya 65:21-23.

Kazi itakuwa baraka iliyoje wakati huo! Kwa kujifunza kuhusu mapenzi ya Mungu na kuishi kupatana nayo, na uwe miongoni mwa wale waliobarikiwa na Yehova na sikuzote ‘kuona mema kwa ajili ya kazi yako yote iliyo ngumu.’—Mhubiri 3:13.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Mungu ndiye Mfanyakazi Mkuu Zaidi: Mwanzo 1:1, 4, 31; Yohana 5:17

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Kazi inaweza kuwa baraka: Mwanzo 1:28; 2:15; 1 Wathesalonike 4:11

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Unaweza kumtukuza Mungu kwa kazi yako: Kutoka 31:1-11; Wakolosai 3:23

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Uwe na usawaziko kati ya kazi na mambo ya kiroho: Mhubiri 12:13; 1 Wakorintho 3:9

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

KUKABILIANA NA MFADHAIKO UNAOSABABISHWA NA KAZI

Wataalamu wa tiba wanasema kwamba mfadhaiko unaosababishwa na kazi ni moja kati ya hatari zinazotokea kazini. Mfadhaiko huo unaweza kusababisha vidonda vya tumbo, mshuko wa moyo, na hata unaweza kumfanya mtu ajiue. Wajapani huelezea mfadhaiko huo kwa kutumia neno karoshi, linalomaanisha “kifo kinachosababishwa na kufanya kazi kupita kiasi.”

Mambo mbalimbali yanayohusiana na kazi yanaweza kuchangia mfadhaiko. Mambo hayo yanatia ndani mabadiliko ya saa au hali za kazi, kutoelewana na wasimamizi, mabadiliko ya madaraka au ya kazi, kustaafu, na kufutwa kazi. Wanapokabili mfadhaiko huo, wengine hujaribu kubadili kazi au mazingira kazini. Baadhi yao hawakubali kwamba wana mfadhaiko na hatimaye unaathiri sehemu nyingine za maisha yao, hasa familia. Watu wengine hata huumia kihisia, na hatimaye hushuka moyo na kukata tamaa.

Wakristo wametayarishwa vizuri ili kukabiliana na mfadhaiko unaosababishwa na kazi. Biblia ina kanuni nyingi za msingi zinazoweza kututegemeza katika nyakati ngumu na kutuimarisha kiroho na kihisia. Kwa mfano, Yesu alisema: “Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.” Hapa tunahimizwa kushughulikia matatizo ya leo, si ya kesho. Tukifanya hivyo, tunaepuka kuhangaikia matatizo yetu kupita kiasi, jambo ambalo huzidisha mfadhaiko.—Mathayo 6:25-34.

Ni muhimu Wakristo wategemee nguvu za Mungu, bali si zao wenyewe. Tunapohisi kwamba tumelemewa kabisa, Mungu anaweza kutupa amani na shangwe mioyoni mwetu, na kutupa hekima ya kushughulikia matatizo yoyote yale. Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake.”—Waefeso 6:10; Wafilipi 4:7.

Mwishowe, hata hali ngumu zinaweza kuleta matokeo mazuri. Majaribu yanaweza kutufanya tumtafute Yehova na kumtegemea. Pia, yanaweza kutuchochea tuendelee kusitawisha utu wa Kikristo na uwezo wa kuvumilia hali ngumu. Paulo anatushauri hivi: “Na tufurahi tukiwa katika dhiki, kwa kuwa tunajua kwamba dhiki hutokeza uvumilivu; nao uvumilivu, hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini.”—Waroma 5:3, 4.

Kwa hiyo, hata mfadhaiko unaweza kutuchochea kukua kiroho badala ya kutuhuzunisha au kutufanya tukate tamaa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

KUTUMIA KANUNI ZA BIBLIA KAZINI

Mtazamo na tabia ya Mkristo anapokuwa kazini zinaweza kufanya ujumbe wa Biblia uwavutie wafanyakazi wenzake na watu wengine. Katika barua yake kwa Tito, mtume Paulo anawashauri wafanyakazi “wajitiishe kwa [wasimamizi] wao katika mambo yote, na kuwapendeza kikamili, wasiwe wakiwajibu kwa ujeuri, wasiwe wakiiba, bali wawe wakionyesha uaminifu mwema kwa ukamili, ili walipambe fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote.”—Tito 2:9, 10.

Kwa mfano, hebu ona yale ambayo mfanyabiashara mmoja aliandika katika barua yake kwa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova: “Ninaandika ili kuomba ruhusa ya kuwapa kazi Mashahidi wa Yehova. Ninataka kufanya hivyo kwa sababu wao ni wanyoofu na waaminifu, na hawawezi kudanganya. Ninawaamini Mashahidi wa Yehova tu. Tafadhali nisaidieni.”

Kyle ni Mkristo anayefanya kazi ya kuwapokea wageni kwenye shule ya kibinafsi. Kwa sababu ya kutoelewana, mfanyakazi mwenzake alimtukana mbele ya wanafunzi fulani. Kyle anasema hivi: “Ilinibidi niwe mwangalifu nisije nikaliletea suto jina la Yehova.” Kwa muda wa siku tano zilizofuata, Kyle alifikiria jinsi ambavyo angetumia kanuni za Biblia. Kanuni moja inapatikana kwenye Waroma 12:18, nayo inasema: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.” Alimtumia mfanyakazi mwenzake barua-pepe na kumwomba msamaha kwa kutoelewana naye. Kyle alimwomba abaki baada ya kazi ili watatue jambo hilo. Walipofanya hivyo, mfanyakazi huyo alipunguza hasira yake na kukubali kwamba Kyle alitumia hekima. Alimwambia Kyle hivi: “Nafikiri umefanya hivyo kwa sababu ya dini yako.” Kisha akamkumbatia kwa uchangamfu halafu wakaagana. Kyle alikata kauli gani? “Tunapotumia kanuni za Biblia tunafanya yaliyo sawa.”

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Watu wengi huhisi kwamba kazi yao si muhimu

[Hisani]

Japan Information Center, Consulate General of Japan in NY

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

Globe: NASA photo