Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhubiri Mahali Ambapo Ukristo Ulisitawi Zamani

Kuhubiri Mahali Ambapo Ukristo Ulisitawi Zamani

Kuhubiri Mahali Ambapo Ukristo Ulisitawi Zamani

MATUKIO makubwa ya kidini na ya kitamaduni ambayo yamekuwa na uvutano juu ya historia ya ulimwengu yametokea huko Italia, peninsula inayoingia kwenye Bahari ya Mediterania. Nchi hiyo inawavutia watalii wengi sana kwa sababu ya umaridadi wa maeneo yake mbalimbali, sanaa zake maarufu, na vyakula vyake vitamu. Pia elimu ya Biblia imesitawi sana katika nchi hiyo.

Huenda Ukristo wa kweli ulifika kwanza Roma—mji mkuu wa serikali kuu ya ulimwengu ya wakati huo—wakati Wayahudi na watu waliogeuza imani na kuwa Wakristo kwenye Pentekoste 33 W.K. waliporudi katika nchi zao kutoka Yerusalemu. Yapata mwaka wa 59 W.K., mtume Paulo alitembelea Italia kwa mara ya kwanza. ‘Aliwakuta akina ndugu’ katika eneo la Puteoli lililo karibu na bahari.—Matendo 2:5-11; 28:11-16.

Kama ilivyotabiriwa na Yesu na mitume wake, kabla ya mwisho wa karne ya kwanza W.K., vikundi vya watu walioasi imani vilijiondoa hatua kwa hatua katika Ukristo wa kweli. Hata hivyo, kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo, wanafunzi wa kweli wa Yesu wameongoza kazi ya kuhubiri habari njema ulimwenguni pote, kutia ndani nchi ya Italia.—Mathayo 13:36-43; Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:3-8; 2 Petro 2:1-3.

Mwanzo Wenye Kuvunja Moyo

Mwaka wa 1891, Charles Taze Russell, ambaye alikuwa akiongoza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ya Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo), alitembelea majiji fulani ya Italia kwa mara ya kwanza. Baada ya kuhubiri huko alikiri kwamba hakutarajia kupata matokeo makubwa aliposema: “Hatukuona chochote kilichotutia moyo ili kutumaini mavuno yoyote huko Italia.” Mapema mwaka wa 1910, Ndugu Russell alirudi tena Italia naye akatoa hotuba inayotegemea Biblia katika ukumbi wa michezo katikati ya mji wa Roma. Matokeo yakawaje? Aliripoti hivi: “Kwa ujumla, mkutano huo haukufanikiwa sana.”

Sababu moja iliyofanya kusiwe na maendeleo makubwa mwanzoni katika kazi ya kuhubiri huko Italia ni kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiteswa na utawala wa kimabavu wa Wafashisti. Katika kipindi hicho, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova wasiozidi 150 nchini, wengi wao walikuwa wamefundishwa kweli za Biblia na watu wa ukoo au marafiki walioishi nchi nyingine.

Maendeleo Makubwa

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, wamishonari wengi walitumwa Italia. Lakini kama inavyoonyeshwa na barua zilizopatikana katika hifadhi za vitu vya kale vya serikali, wakuu wa Vatikani waliomba serikali iwafukuze wamishonari hao. Wamishonari wengi walilazimika kuhama nchini.

Licha ya vizuizi hivyo, umati huko Italia ulianza kumiminika kwenye “mlima” wa ibada ya Yehova. (Isaya 2:2-4) Ongezeko la Mashahidi limekuwa kubwa sana. Katika mwaka wa 2004 kulikuwa na kilele cha wahubiri wa habari njema 233,527, yaani, mhubiri 1 kwa wakaaji 248, na watu 433,242 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Mwaka huo, kulikuwa na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova 3,049 ambayo yalikusanyika katika Majumba ya Ufalme maridadi. Hivi karibuni, kumekuwa na ongezeko kubwa hasa katika vikundi mbalimbali vya wageni.

Kuhubiri Katika Lugha Mbalimbali

Wahamiaji wengi kutoka Afrika, Asia, na Ulaya Mashariki huenda Italia kutafuta kazi au maisha bora, na wengine hufanya hivyo ili kuepuka hali zenye kuhuzunisha. Watu hao wengi wanaweza kusaidiwaje kiroho?

Mashahidi wengi huko Italia wanajitahidi kujifunza lugha ngumu za kigeni, kama vile Kialbania, Kiamhara, Kiarabu, Kibengali, Kichina, Kipunjabi, Kisinhala, na Kitagalogi. Tangu mwaka wa 2001, mipango ya kufundisha lugha ilifanywa ili kuwasaidia Mashahidi hao wajue kuhubiri katika lugha za kigeni. Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, Mashahidi 3,711 walihudhuria shule 79 zilizoendeshwa katika lugha 17. Kwa njia hiyo makutaniko 146 na vikundi 274 vimeanzishwa katika lugha 25. Hivyo, watu wengi wanyoofu wamesikia habari njema nao wameanza kujifunza Biblia. Mara nyingi matokeo yamekuwa ya kustaajabisha.

Mhudumu mmoja Shahidi wa Yehova alizungumza na George kuhusu Biblia. George anatoka India naye anazungumza Kimalayalamu. Licha ya kuwa na matatizo makubwa kuhusiana na kazi, George alikubali kwa furaha funzo la Biblia. Siku chache baadaye, Gil, rafiki ya George, ambaye ni Mhindi anayezungumza Kipunjabi, alienda kwenye Jumba la Ufalme, na huko akaanza kufundishwa Biblia. Gil alimjulisha David, ambaye ni Mhindi anayezungumza Kitelugu, kwa Mashahidi. Punde si punde, David alianza kujifunza Biblia. Wahindi wengine wawili, Sonny na Shubash, walikuwa wakiishi katika nyumba hiyohiyo pamoja na David. Wote wawili wakajiunga katika funzo hilo la Biblia.

Majuma kadhaa baadaye, Mashahidi walipokea simu kutoka kwa Dalip, anayezungumza Kimarathi. Alisema hivi: “Mimi ni rafiki ya George. Je, mnaweza kunifundisha Biblia?” Baadaye, Sumit ambaye anazungumza Kitamili akataka pia kujifunza Biblia. Mwishowe, rafiki mwingine wa George akapiga simu ili kuomba funzo la Biblia. Halafu, George akamleta kijana mwingine anayeitwa Max, kwenye Jumba la Ufalme. Yeye pia akaomba afundishwe Biblia. Hadi sasa, mafunzo ya Biblia sita yanaongozwa na mipango inafanywa kwa ajili ya mengine manne zaidi. Mafunzo hayo yanaongozwa kwa Kiingereza, ingawa vichapo vya Kihindi, Kimalayalamu, Kimarathi, Kipunjabi, Kitamili, Kitelugu, na Kiurdu vinatumiwa pia.

Viziwi “Wanasikia” Habari Njema

Kuna zaidi ya viziwi 90,000 huko Italia. Katikati ya miaka ya 1970, Mashahidi walianza kufikiria kuwafundisha viziwi kweli za Biblia. Mwanzoni, baadhi ya Mashahidi ambao ni viziwi waliwafundisha Lugha ya Ishara ya Italia wahudumu wenzao waliokubali kusaidia watu walio na tatizo la kusikia. Halafu, viziwi wengi zaidi walianza kuonyesha kupendezwa na Biblia. Leo, zaidi ya watu 1,400 wanaotumia Lugha ya Ishara ya Italia wanahudhuria mikutano ya Kikristo. Makutaniko 15 na vikundi 52 vinafanya mikutano katika lugha hiyo ya ishara.

Mwanzoni, kuhubiria viziwi kulitegemea hasa mipango ya kila Shahidi. Lakini mwaka wa 1978, ofisi ya tawi ya Italia ya Mashahidi wa Yehova ilianza kupanga makusanyiko ya wilaya kwa ajili ya viziwi. Mnamo Mei mwaka huohuo, ilitangazwa kwamba kwenye kusanyiko la kimataifa lijalo huko Milan, kungekuwa na programu kwa ajili ya viziwi. Kusanyiko la kwanza la mzunguko kwa ajili ya viziwi lilifanywa kwenye Jumba la Kusanyiko huko Milan, mnamo Februari 1979.

Tangu wakati huo, ofisi ya tawi imetoa uangalifu mkubwa juu ya kuwalisha kiroho viziwi kwa kuwatia moyo wahubiri wengi waboreshe ustadi wao wa lugha ya ishara. Kuanzia mwaka wa 1995, mapainia wa pekee (waeneza-injili wa wakati wote) wametumwa katika vikundi kadhaa ili kuwazoeza Mashahidi ambao ni viziwi katika kuhubiri na kupanga mikutano ya Kikristo. Majumba matatu ya Kusanyiko yana video za kisasa ili kuwasaidia wahudhuriaji kutazama programu inapoendelea. Na kanda za video za vichapo vya Kikristo zinapatikana ili kuwalisha kiroho viziwi.

Watu wametambua kwamba Mashahidi wanahangaikia sana hali ya kiroho ya viziwi. Gazeti P@role & Segni linalotolewa na Shirika la Viziwi la Italia, lilinukuu barua moja iliyotumwa na askofu mmoja Mkatoliki ambayo ilisema hivi: “Kuwa kiziwi ni jambo lisilopendeza katika maana ya kwamba mtu ambaye ni kiziwi anahitaji uangalifu kila mara. Kwa mfano, anaweza kufika kanisani peke yake bila tatizo lolote, lakini anahitaji msaada wa mkalimani ili kufuata kila jambo linalosomwa, kusemwa, au kuimbwa wakati wa ibada.” Gazeti hilo linaongezea kusema kwamba, askofu huyo “anaeleza kuwa, kwa kusikitisha, kanisa halijajitayarisha kushughulikia tatizo hilo na kwamba watu wengi ambao ni viziwi wanashughulikiwa vizuri katika Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova kuliko katika makanisa.”

Habari Njema Inahubiriwa kwa Wafungwa

Je, inawezekana mtu kuwa huru na bado ni mfungwa? Naam, kwa sababu Neno la Mungu lina nguvu ya ‘kuwaweka huru’ wale wanaolikubali na kulifuata maishani mwao. Ujumbe ambao Yesu aliwatangazia “mateka” uliwaweka huru kutokana na dhambi na dini ya uwongo. (Yohana 8:32; Luka 4:16-19) Huko Italia, matokeo bora yanapatikana kwa kuhubiri katika magereza. Karibu wahudumu 400 ambao ni Mashahidi wa Yehova wameruhusiwa na serikali kuwatembelea wafungwa ili kuwapa msaada wa kiroho. Mashahidi wa Yehova ni tengenezo la kwanza lisilo la Kikatoliki ambalo limeomba na kupata kibali hicho.

Ujumbe wa Biblia unaweza kuenezwa kwa njia zisizotarajiwa. Wafungwa wanazungumza na wafungwa wenzao kuhusu kazi ya elimu ya Biblia ya Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu hiyo, baadhi ya wafungwa hao, waliomba watembelewe na mhudumu Shahidi. Au watu wa familia ambao wameanza kujifunza Biblia wanawatia moyo wafungwa kuomba watembelewe na Mashahidi. Baadhi ya wafungwa wanaotumikia vifungo vya maisha kwa sababu ya mauaji au uhalifu mwingine mkubwa wametubu na kubadilika kabisa. Hilo linawatayarisha kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu na kubatizwa.

Katika magereza mengi, mipango imefanywa ili kutoa hotuba za watu wote zinazotegemea Biblia, kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu, na kuonyesha kanda za video za programu za Biblia zinazotolewa na Mashahidi wa Yehova. Wafungwa wengi wanahudhuria mikutano hiyo.

Ili kuwasaidia vizuri wafungwa, ulimwenguni pote Mashahidi wamegawanya magazeti ambayo yanazungumzia habari ambazo zitawasaidia wafungwa. Kwa mfano, gazeti la Amkeni! la Mei 8, 2001, lilizungumzia habari “Je, Wafungwa Wanaweza Kurekebishwa?” Halafu toleo la Aprili 8, 2003 lilikuwa na habari “Ufanye Nini Kijana Wako Akitumia Dawa za Kulevya?” Maelfu ya nakala zimetolewa kwa wafungwa. Kwa sababu hiyo, mamia ya mafunzo ya Biblia yanaongozwa. Baadhi ya walinzi wa magereza pia wameonyesha kupendezwa na ujumbe wa Biblia.

Baada ya kupokea kibali cha pekee kutoka kwa wakuu, mfungwa mmoja anayeitwa Costantino alibatizwa kwenye Jumba la Ufalme huko San Remo, na Mashahidi 138 wa mahali hapo walikuwepo. “Nilihisi upendo mwingi sana,” alisema Costantino, ambaye baada ya ubatizo wake alionekana amejawa na hisia. Gazeti moja liliripoti maneno yafuatayo ya mlinzi wa gereza: “Tulitoa kibali hiki . . . kwa furaha kubwa. Jambo lolote linalomsaidia mfungwa afanye marekebisho ya kibinafsi, ya kiroho na katika mahusiano yake na wengine, linapaswa kuzingatiwa.” Mke wa Costantino na binti yake walivutiwa na jinsi ujuzi sahihi wa Biblia ulivyobadili maisha ya Costantino: “Tunajivunia kuwa na Costantino kwa sababu ya mabadiliko ambayo amefanya. Amekuwa mtulivu, na anatuhangaikia zaidi. Tumeanza kumtumaini tena na kumheshimu.” Wao pia wameanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo.

Sergio, alikuwa amehukumiwa kifungo hadi mwaka 2024 kwa sababu ya wizi, kushambulia watu kwa silaha, biashara ya dawa za kulevya, na mauaji. Baada ya kuchunguza Maandiko kwa miaka mitatu na kufanya mabadiliko makubwa maishani mwake, Sergio aliamua kubatizwa. Yeye ni mfungwa wa 15 katika gereza la Porto Azzurro, kwenye kisiwa cha Elba, kubatizwa ili kuwa Shahidi wa Yehova. Alibatizwa ndani ya kidimbwi chenye kubebeka kilichowekwa kwenye uwanja wa michezo wa gereza, huku baadhi ya wafungwa wenzake wakiwepo.

Leonardo, ambaye anatumikia kifungo cha miaka 20, alipewa kibali cha pekee ili abatizwe kwenye Jumba la Ufalme huko Parma. Alipohojiwa na gazeti la mahali hapo, Leonardo alisema kwamba alitaka “kuonyesha wazi kwamba aliamua kuwa Shahidi wa Yehova, si kwa sababu ya kuepuka kufungwa gerezani, bali ili kutosheleza uhitaji mkubwa wa kiroho ambao alikuwa nao.” Leonardo alisema: “Nimefanya makosa mengi maishani mwangu, lakini hayo ni mambo ya zamani. Nimebadilika, ingawa si kwa ghafula. Nitahitaji kuendelea kuwa mnyoofu.”

Salvatore, ambaye alihukumiwa kwa sababu ya mauaji, yuko chini ya ulinzi mkali katika gereza la Spoleto. Ubatizo wake ambao ulifanyika gerezani, uliwashangaza wengi. Mlinzi wa gereza hilo alisema hivi: “Umuhimu wa kuchagua njia inayomwezesha mtu kurekebisha tabia yake kuwaelekea wengine unapaswa kuungwa mkono ili kuwafaidi wafungwa wengine na jamii kwa ujumla.” Kwa sababu ya mabadiliko ambayo Salvatore amefanya, sasa mke wake na binti yake mmoja wanahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Mfungwa fulani ambaye Salvatore alimhubiria alibatizwa na kuwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu.

Kulikuwa na ongezeko la Wakristo wa mapema huko Italia. (Matendo 2:10; Waroma 1:7) Katika wakati huu wa mavuno, ukuzi wa kiroho na mpanuko unaendelea katika maeneo yaleyale ambako Paulo na Wakristo wenzake walijitahidi sana kuhubiri habari njema.—Matendo 23:11; 28:14-16.

[Ramani katika ukurasa wa 13]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

ITALIA

Roma

[Picha katika ukurasa wa 15]

Jumba la Kusanyiko la Bitonto na kutaniko moja la Lugha ya Ishara ya Italia huko Roma

[Picha katika ukurasa wa 16]

Wafungwa ‘wanawekwa huru’ na kweli ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 17]

Ukuzi wa kiroho unaendelea mahali ambapo Ukristo ulisitawi zamani