Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumsifu Yehova Shuleni

Kumsifu Yehova Shuleni

Kumsifu Yehova Shuleni

ULIMWENGUNI pote vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova wanatafuta nafasi za kumtukuza Mungu wakiwa shuleni, kupitia usemi na mwenendo. Ona baadhi ya mambo yanayoonyesha bidii yao.

Msichana mmoja ambaye ni Shahidi wa Yehova huko Ugiriki aliambiwa aandike ripoti kuhusu uchafuzi wa hewa. Baada ya kufanya utafiti kwenye Watch Tower Publications Index, alipata habari zinazofaa katika gazeti la Amkeni! Mwishoni mwa ripoti yake alitaja kwamba alipata habari zake katika gazeti hilo. Mwalimu alimweleza kuwa hiyo ni kati ya ripoti bora sana ambazo amewahi kusoma. Baadaye mwalimu huyo alitumia habari hizo kwenye semina naye akapata matokeo mazuri. Dada huyo mdogo aliamua kumpa mwalimu magazeti mengine ya Amkeni!, kutia ndani lile lenye mfululizo wenye kichwa, “Walimu Ni Muhimu Sana.” Baadaye, mwalimu alilisifu gazeti la Amkeni! darasani na baadhi ya wanafunzi wakaanza kuomba nakala za gazeti hilo. Dada huyo alilazimika kupeleka nakala za magazeti shuleni ili wanafunzi wasome makala nyingine.

Katika nchi ya Benin, barani Afrika, msichana mmoja Mkristo alikabili tatizo lisilo la kawaida. Kulingana na desturi, wazazi wa wanafunzi wengi katika shule yake waliamua kuwalipa walimu fulani kufundisha masomo magumu ili kuwaandaa watoto wao kwa ajili ya mitihani. Walimu hao waliamua kufundisha siku ya Jumamosi asubuhi. Shahidi huyo mdogo alikataa mpango huo na kusema hivi: “Jumamosi asubuhi ni wakati ambao kutaniko lote huhubiri pamoja. Hiyo ni pindi yenye furaha zaidi kwangu na siwezi kufanya jambo lingine lolote wakati huo.” Baba yake ambaye ni Shahidi na pia mzazi asiye na mwenzi, alikubaliana na wazo hilo na kujaribu kuwaomba wazazi na walimu wabadili ratiba hiyo. Wote walikataa. Msichana huyo aliamua kutoshiriki masomo hayo ya ziada na badala yake akajiunga na kutaniko katika mahubiri. Wanafunzi wenzake walimdhihaki na kumchochea aache kuhubiri na pia amwache Mungu. Wote walikuwa na hakika ataanguka mitihani hiyo. Kinyume chake, wanafunzi wote walioshiriki katika masomo ya ziada walianguka lakini dada yetu mdogo akafaulu. Dhihaka zikapungua. Sasa wanafunzi wenzake wanamwambia hivi, “Unapaswa kuendelea kumtumikia Mungu wako.”

Huko Jamhuri ya Cheki, msichana mwenye umri wa miaka 12 alitakiwa atayarishe habari fulani kuhusu kitabu chochote alichosoma. Mama yake alimtia moyo atumie kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Msichana huyo alianza kueleza habari yake kwa kuuliza swali hili: “Ni nani anayeweza kuwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi?” Kisha akaeleza juu ya Yesu, maisha yake hapa duniani, na mafundisho yake. Halafu akaizungumzia sura yenye kichwa, “Somo Juu ya Kusamehe.” Mwalimu wake akashangazwa na kusema, “Sijawahi kusikia ukitoa habari nzuri kama hii!” Mwalimu huyo alifurahi kupokea nakala ya kitabu hicho. Baadhi ya wanafunzi waliomba nakala pia. Siku iliyofuata msichana huyo alisisimuka alipowaachia wanafunzi vitabu 18.

Vijana kama hao wanafurahia sana kumsifu Yehova shuleni. Acheni sisi sote tuige bidii ya vijana hao.