Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pande Mbili za Kazi

Pande Mbili za Kazi

Pande Mbili za Kazi

“Kufanya kazi—kufanya kazi! Inafurahisha sana kujua kwamba bado tuna kazi ya kufanya.”—Mwandishi Katherine Mansfield, (1888-1923).

JE, UNAKUBALIANA na maoni hayo kuhusu kazi? Unaionaje kazi? Je, wewe huona kazi kuwa jambo lisilofurahisha linalochukua muda mrefu? Au je, unapenda sana kazi yako hivi kwamba inatawala maisha yako?

Watu wengi hutumia wakati wao mwingi wakifanya kazi. Hali yetu ya maisha na makao yetu hutegemea kazi tunayofanya. Wengi huona kwamba kazi hutawala maisha yao, tangu ujanani hadi wanapostaafu. Wengine wetu hupata uradhi mwingi sana kutokana na jasho letu. Watu wengine hukadiria ubora wa kazi kwa kuangalia mapato au umaarufu unaotokana nayo, nao wengine huona kazi kuwa jambo linalowasaidia kupisha wakati au linalopoteza wakati wao.

Kuna wale wanaofanya kazi ili kupata riziki na kuna wale ambao kusudi lao kuu maishani ni kufanya kazi tu. Wengine hata hufa kwa sababu ya hali za kazi. Kwa mfano, ripoti moja ya hivi majuzi ya Umoja wa Mataifa ilisema kwamba kazi husababisha maumivu na kifo kwa kiwango kikubwa “kuliko vita au matumizi ya dawa za kulevya na ulevi vikijumlishwa pamoja.” Likizungumzia jambo hilo, gazeti The Guardian la London liliripoti hivi: “Kila mwaka, zaidi ya watu milioni mbili hufa kutokana na majeraha au magonjwa yanayosababishwa na kazi . . . Vumbi, kemikali, kelele na miale fulani husababisha kansa, ugonjwa wa moyo na kupooza.” Isitoshe, mambo mengine mawili ambayo hufanya kazi ichukize siku hizi ni kuwatumikisha watoto na kuwalazimisha watu kufanya kazi.

Kwa kuongezea, kuna ule “uchovu wa kupindukia” unaotajwa na mwanasaikolojia Steven Berglas. Anataja mfanyakazi mwenye bidii ambaye, ijapokuwa amefikia kilele cha kazi yake, anahisi “woga usioisha, wasiwasi, mfadhaiko, au kushuka moyo kwa sababu anaona kwamba amenaswa na kazi yake na hawezi kujinasua wala kupata furaha yoyote kutokana nayo.”

Tofauti Kati ya Kufanya Kazi kwa Bidii na Kufanya Kazi Kupindukia

Katika ulimwengu ambamo watu wengi hujikakamua kufanya kazi kwa muda mrefu, ni muhimu kujua tofauti kati ya kufanya kazi kwa bidii na kufanya kazi kupindukia. Watu wengi wanaofanya kazi kupindukia huhisi kwamba kazi inawafanya kuwa salama katika ulimwengu huu hatari na wenye kubadilika-badilika, hali wale wanaofanya kazi kwa bidii huona kazi kuwa jambo la lazima au linaloleta uradhi. Wale wanaofanya kazi kupindukia hawana nafasi ya kufanya mambo mengine maishani mwao, hali wale wanaofanya kazi kwa bidii hujua wakati wa kuondoka kazini, kuelekeza fikira kwa mambo mengine, au kusimamisha kazi ili kuhudhuria tukio fulani muhimu. Watu wanaofanya kazi kupindukia huhisi vizuri na husisimuka wanapofanya hivyo, hali watu wanaofanya kazi kwa bidii hawahisi hivyo wanapofanya kazi kupita kiasi.

Ni vigumu kutofautisha kati ya mambo hayo mawili kwa sababu siku hizi ulimwengu unawaunga mkono wale wanaofanya kazi kupindukia. Simu za mkononi na vifaa vingine huwawezesha watu kufanya kazi hata wanapokuwa nyumbani. Kwa kuwa kazi inaweza kufanyiwa mahali popote pale na wakati wowote ule, watu wengine hujiumiza kwa kufanya kazi kupindukia.

Watu wengine hutendaje wanapoathiriwa na maoni hayo yasiyofaa kuhusu kazi? Wataalamu wa elimu ya jamii wameona kwamba watu wanaofanya kazi kupindukia au wanaokabili mkazo mwingi sana wana mwelekeo wa kufanya mambo ya kiroho kazini na kuchanganya dini na kazi. Gazeti San Francisco Examiner liliripoti kwamba “sasa watu wengi wanachanganya dini na kazi.”

Ripoti moja ya majuzi ilisema hivi kuhusu Silicon Valley, kituo muhimu cha maendeleo ya teknolojia huko Marekani: “Wakubwa wanatambua kwamba magari yanazidi kupungua kazini kwa sababu watu wanaachishwa kazi, huku magari yakiongezeka kwenye mikutano ya kujifunza Biblia inayofanywa jioni.” Naam, watu wengi ulimwenguni wametambua kwamba Biblia inawasaidia sana kuwa na maoni mazuri kuhusu kazi, na hivyo kuwa na usawaziko zaidi maishani.

Biblia inaweza kutusaidiaje kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu kazi? Je, kuna kanuni za Kimaandiko zinazoweza kutusaidia kushughulikia vizuri matatizo yanayotokea kazini siku hizi? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.