Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Philo wa Aleksandria Aeleza Maandiko kwa Kukisia-Kisia

Philo wa Aleksandria Aeleza Maandiko kwa Kukisia-Kisia

Philo wa Aleksandria Aeleza Maandiko kwa Kukisia-Kisia

KATIKA mwaka wa 332 K.W.K., Aleksanda Mkuu alivamia Misri. Kabla ya kusonga mbele upande wa mashariki katika kampeni yake ya kumiliki ulimwengu, alianzisha jiji ambalo aliliita Aleksandria. Jiji hilo likawa kituo cha utamaduni wa Ugiriki. Yapata mwaka wa 20 K.W.K., shujaa mwingine alizaliwa huko. Yeye hakupigana kwa panga na mikuki, bali alitumia hoja za kifalsafa. Aliitwa Philo wa Aleksandria, au Philo Judaeus kwa sababu ya malezi yake ya Kiyahudi.

Kutawanyika kwa Wayahudi kulikotukia baada ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., kulifanya Wayahudi wengi waishi Misri. Maelfu waliishi huko Aleksandria. Hata hivyo, kulikuwa na matatizo kati ya Wayahudi na majirani wao Wagiriki. Wayahudi walikataa kuabudu miungu ya Wagiriki, nao Wagiriki wakayadharau Maandiko ya Kiebrania. Kwa sababu ya elimu yake ya Kigiriki na malezi yake ya Kiyahudi, Philo alijua mabishano hayo. Aliamini kwamba Dini ya Kiyahudi ndiyo ya kweli. Lakini tofauti na Wayahudi wengi, Philo alitafuta njia ya amani ili kuwaelekeza watu wasio Wayahudi kwa Mungu. Alitaka waikubali Dini ya Kiyahudi.

Maandishi ya Kale Yapata Maana Mpya

Kama ilivyokuwa kwa Wayahudi wengi walioishi huko Aleksandria, Kigiriki ndiyo iliyokuwa lugha ya kwanza ya Philo. Hivyo, uchunguzi wake ulitegemea tafsiri ya Septuajinti ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania. Alipokuwa akichunguza maandishi ya Septuajinti, alisadikishwa kwamba yalikuwa na mambo ya msingi ya falsafa na kwamba Musa alikuwa “mwanafalsafa stadi.”

Katika karne za mapema, wasomi Wagiriki hawakuamini hadithi za miungu ya kiume na ya kike, yaani, majitu na mashetani katika hekaya za kale. Walianza kufasiri tena hadithi hizo za kale za Wagiriki. Msomi James Drummond alisema hivi kuhusu njia waliyotumia: “Wanafalsafa walikuwa wakitafuta maana zisizoeleweka za hekaya, na kutokana na mambo ya kuchukiza na ya kipumbavu katika hekaya hizo walikata kauli kwamba waandikaji wake walinuia kuonyesha ukweli fulani wenye kuelimisha kupitia mifano yao yenye kuamsha hisia za kingono.” Philo alijaribu kutumia mbinu hiyo kufasiri Maandiko.

Kwa mfano, fikiria andiko la Mwanzo 3:22 katika tafsiri ya Bagster ya Septuajinti, ambalo linasema hivi: “Bwana Mungu aliwafanyia Adamu na mke wake mavazi ya ngozi na kuwavika.” Wagiriki walihisi kwamba Mungu Mweza-Yote alijishushia heshima kwa kufanya kazi kama hiyo. Hivyo Philo aliona maana ya mfano katika mstari huo naye akasema: “Mavazi ya ngozi ni usemi wa mfano wa neno ngozi, yaani, mwili wetu; kwa kuwa Mungu aliumba kwanza akili, naye akaiita Adamu; kisha akaumba nguvu zenye msukumo ambazo aliziita Uhai. Mwishowe, alifanya pia mwili ambao aliuita kwa usemi wa mfano, mavazi ya ngozi.” Hivyo Philo akajaribu kufanya tendo la Mungu la kuwavika mavazi Adamu na Hawa kuwa hoja ya kifalsafa iliyopaswa kuchunguzwa.

Pia fikiria andiko la Mwanzo 2:10-14, ambalo linaeleza kuhusu chanzo cha maji katika bustani ya Edeni. Andiko hilo linataja mito minne ambayo ilibubujika nje ya bustani. Philo alijaribu kutafuta maana ya maneno yanayofafanua bustani ya Edeni. Baada ya kueleza kuhusu nchi yenyewe, alisema hivi: “Huenda masimulizi hayo pia yana maana ya mfano; kwa kuwa mito hiyo minne inawakilisha sifa nne nzuri.” Alikisia kwamba Mto Pishoni unawakilisha busara, Mto Gihoni unamaanisha kuchukua mambo kwa uzito, Mto Tigri unafananisha uvumilivu, nao Mto Efrati unamaanisha haki. Hivyo, kulingana na Philo mito hiyo ni mifano tu (au, sitiari).

Philo alijaribu kupata maana ya mfano ili kuchanganua masimulizi ya uumbaji, habari kuhusu Kaini kumuua Abeli, Gharika ya siku za Noa, kuvurugwa kwa lugha huko Babeli, na kanuni nyingi za Sheria ya Musa. Kama inavyoonyeshwa na mfano uliotajwa katika fungu lililotangulia, mara nyingi Philo alikubaliana na maana halisi ya andiko la Biblia, kisha akaonyesha jinsi anavyolielewa kwa njia ya mfano kwa kutumia maneno haya: “Labda tunapaswa kufikiria mambo haya kuwa yanazungumzwa kwa njia ya mfano.” Kwa kusikitisha, katika maandishi ya Philo, mifano ndiyo inayokaziwa sana huku maana iliyo wazi ya Maandiko ikipotoshwa.

Mungu Ni Nani?

Philo alitetea hoja kuhusu kuwapo kwa Mungu kwa kutoa mfano wenye nguvu sana. Baada ya kueleza kuhusu nchi, mito, sayari, na nyota, alimalizia kwa kusema hivi: “Ulimwengu ni kati ya vitu vilivyotengenezwa kwa ustadi mkubwa sana, na ni kana kwamba ulitokezwa na mtu mwenye uzoefu na ujuzi kamili. Ni katika njia hiyo kwamba tumepata wazo la kuwapo kwa Mungu.” Hoja hiyo inapatana na akili.—Waroma 1:20.

Lakini Philo alipofafanua utu wa Mungu Mweza-Yote, alienda mbali sana na ukweli. Philo alidai kwamba Mungu “hana sifa hususa” na kwamba “hatuwezi kuelewa mambo” ya Mungu. Philo aliwavunja watu moyo wasijitahidi kumjua Mungu, akisema kwamba “kujaribu kuchunguza zaidi utu au sifa za Mungu ni upumbavu kabisa.” Kufikiri kwa namna hiyo hakutokani na Biblia, bali na mwanafalsafa mpagani Plato.

Philo alisema kwamba Mungu hawezi kueleweka kamwe, hivyo haiwezekani kumwita kwa jina. Aliongeza kusema hivi: “Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kudai kwamba hakuna jina hususa linalomfaa Mungu aliye hai.” Wazo hilo ni tofauti kabisa na ukweli!

Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu ana jina. Andiko la Zaburi 83:18 linasema hivi: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Andiko la Isaya 42:8 linamnukuu Mungu akisema: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” Kwa nini Philo, ambaye ni Myahudi anayejua maandiko ya Biblia, alifundisha kwamba Mungu hana jina? Kwa sababu alikuwa akifafanua, si Mungu halisi wa Biblia, bali mungu wa falsafa ya Kigiriki asiye na jina na asiyefikika.

Nafsi Ni Nini?

Philo alifundisha kwamba nafsi na mwili ni vitu viwili tofauti. Anazungumza kuhusu mtu kuwa “anafanyizwa na mwili na nafsi.” Je, nafsi inaweza kufa? Ona maelezo ya Philo: “Tunapokuwa hai, mwili wetu unaishi ingawa nafsi yetu imekufa na imezikwa ndani ya mwili wetu, kana kwamba katika kaburi fulani. Lakini [mwili] ukifa, nafsi yetu inaishi maisha yake yenyewe, na kuwekwa huru kutokana na uovu na mwili uliokufa ambamo ndani yake nafsi hufungwa.” Kulingana na Philo, kufa kwa nafsi ni kwa mfano tu. Kwa kweli, haifi kabisa. Haiwezi kufa.

Hata hivyo, Biblia inafundisha nini kuhusu nafsi? Andiko la Mwanzo 2:7 linasema hivi: “Yehova Mungu akamfanya mtu kutoka katika mavumbi ya nchi na kupuliza katika mianzi ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi hai.” Kulingana na Biblia, wanadamu hawana nafsi, bali wao wenyewe ni nafsi.

Pia Biblia inafundisha kwamba nafsi inakufa. Andiko la Ezekieli 18:4 linasema: “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” Kutokana na maandiko hayo tunaweza kwa kufaa kukata kauli hii: Mwanadamu ni nafsi. Hivyo, mwanadamu anapokufa, nafsi inakufa.—Mwanzo 19:19. *

Baada ya kifo cha Philo, Wayahudi hawakujali sana mafundisho yake. Hata hivyo, dini zinazojidai kuwa za Kikristo zilikubali mafundisho yake. Eusebius na viongozi wengine wa kanisa waliamini kwamba Philo aligeuka akawa Mkristo. Jerome alimtia kwenye orodha ya Mababa wa Kanisa. Wakristo walioasi imani, na si Wayahudi, ndio waliohifadhi maandishi ya Philo.

Maandishi ya Philo yalitokeza mapinduzi ya kidini. Uvutano wake uliongoza watu wanaojidai kuwa Wakristo kukubali fundisho la kutokufa kwa nafsi ambalo ni kinyume cha maandiko. Nalo fundisho la Philo kuhusu Logos (au, Neno) lilisaidia katika kuanzisha fundisho la Utatu, fundisho la Wakristo walioasi imani ambalo halipatani na Biblia.

Usidanganywe

Katika uchunguzi wake wa Maandiko ya Kiebrania, Philo alihakikisha kwamba “hakuondoa maana yoyote ya mifano ambayo huenda haikuelezwa waziwazi.” Hata hivyo, kama inavyoonyeshwa kwenye Kumbukumbu la Torati 4:2, Musa alisema hivi kuhusu Sheria ya Mungu: “Nanyi msiongeze kwenye neno ninalowaamuru ninyi, wala msiondoe lolote kutoka katika hilo, ili mzishike amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru ninyi.” Ingawa yaelekea alikuwa na nia nzuri, Philo aliongeza mambo ya kukisia-kisia ambayo, kama wingu zito, yalifunika mafundisho yaliyo wazi ya Neno la Mungu lililoongozwa na roho.

Mtume Petro alisema hivi: “Haikuwa kwa kufuata hadithi za uwongo zilizotungwa kwa ufundi kwamba tuliwafahamisha ninyi juu ya nguvu na kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 1:16) Tofauti na maandishi ya Philo, maagizo ya Petro kwa kutaniko la Kikristo la mapema yalitegemea mambo ya kweli na mwongozo wa roho ya Mungu, “roho ya ile kweli,” ambayo iliwaongoza katika kweli yote.—Yohana 16:13.

Ikiwa unapendezwa kumwabudu Mungu wa Biblia, unahitaji mwongozo wa kweli, si maelezo yanayotegemea kufikiri kwa wanadamu. Unahitaji ujuzi sahihi kumhusu Yehova na mapenzi yake, na unahitaji sifa ya unyenyekevu ili kuwa mwanafunzi mnyoofu. Ukijifunza Biblia ukiwa na mtazamo huo unaofaa, utajua “maandishi matakatifu, ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” Utaona kwamba Neno la Mungu linaweza kukufanya uwe na ‘uwezo kamili, na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—2 Timotheo 3:15-17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kuhusu nafsi, kichapo The Jewish Encyclopedia cha mwaka wa 1910 kinasema hivi: “Imani ya kwamba nafsi inaendelea kuishi baada ya mwili kuoza ni fundisho la kifalsafa au makisio ya kidini bali si imani ya msingi, na hakuna mahali linapofundishwa katika Maandiko Matakatifu.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

JIJI ALILOISHI PHILO

Philo aliishi na kufanya kazi huko Aleksandria ya Misri. Kwa karne nyingi, Aleksandria lilikuwa ndilo jiji kuu la ulimwengu wa vitabu na mijadala ya wasomi.

Wanafunzi walielimishwa na wasomi mashuhuri ambao walifundisha katika shule za jiji hilo. Maktaba ya Aleksandria ilijulikana sana ulimwenguni pote. Mamia ya maelfu ya vitu viliongezwa katika maktaba hiyo kwa kuwa watunzaji wa maktaba walijitahidi juu chini kupata nakala za hati zote zilizoandikwa.

Baadaye, heshima ya ulimwengu kuelekea Aleksandria na ujuzi wake ilianza kupungua hatua kwa hatua. Watawala wa Roma walilipa jiji la Roma umashuhuri, na hivyo kitovu cha utamaduni kikahamishwa hadi Ulaya. Kuporomoka kwa Aleksandria kulifikia kilele chake katika karne ya saba W.K., wakati wavamizi walipoliteka jiji hilo. Hadi leo, wanahistoria wanasikitika kuhusu kutoweka kwa maktaba hiyo mashuhuri, baadhi yao wakidai kwamba maendeleo ya ustaarabu yalicheleweshwa kwa muda wa miaka 1,000.

[Hisani]

L. Chapons/Illustrirte Familien-Bibel nach der deutschen Uebersetzung Dr. Martin Luthers

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

KUFASIRI MIFANO LEO

Sitiari kwa kawaida ni ‘usemi wa mfano wenye maana ya kuhusianisha kitu kimoja na kingine chenye sifa sawa.’ Inasemekana kwamba maandishi yanayotumia sitiari huwa na mifano inayowakilisha mambo muhimu zaidi ambayo maana yake imefichwa. Kama Philo wa Aleksandria, baadhi ya walimu wa dini wa siku hizi hutumia mifano ili kuifafanua Biblia.

Fikiria masimulizi ya Mwanzo sura ya 1-11, ambayo yanaeleza historia ya wanadamu tangu uumbaji hadi kutawanywa kwa watu kwenye mnara wa Babeli. Tafsiri ya Kikatoliki ya The New American Bible inasema hivi kuhusu sehemu hiyo ya Biblia: “Ili kufanya ukweli ulio katika sura hizo ueleweke na Waisraeli ambao wangezihifadhi, zilihitaji kuelezwa kwa kutumia mambo yaliyojulikana na watu wa wakati huo. Kwa sababu hiyo, ukweli wenyewe unapaswa kutofautishwa wazi na hadithi zinazoficha maana yake.” Hiyo inamaanisha kwamba maneno ya kitabu cha Mwanzo sura ya 1-11 hayapaswi kuchukuliwa kihalisi. Badala yake, kama vile vazi linavyofunika mwili, ndivyo maneno hayo yanavyofunika maana nzito.

Hata hivyo, Yesu alifundisha kwamba sura hizo za kwanza za kitabu cha Mwanzo zilikuwa za kweli. (Mathayo 19:4-6; 24:37-39) Mitume Paulo na Petro walifundisha vivyo hivyo. (Matendo 17:24-26; 2 Petro 2:5; 3:6, 7) Wanafunzi wanyoofu wa Biblia wanakataa maelezo ambayo hayapatani na Neno lote la Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mnara Mkubwa wa Taa wa Aleksandria

[Hisani]

Archives Charmet/Bridgeman Art Library