Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi, Waandalieni Mahitaji Watu wa Familia Zenu

Wazazi, Waandalieni Mahitaji Watu wa Familia Zenu

Wazazi, Waandalieni Mahitaji Watu wa Familia Zenu

“Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, . . . ameikana imani.”—1 TIMOTHEO 5:8.

1, 2. (a) Kwa nini inatia moyo kuona familia zikihudhuria mikutano ya Kikristo pamoja? (b) Familia hukabili hali gani ngumu ili kufika kwenye mikutano kwa wakati?

UNAPOTAZAMA huku na huku katika kutaniko la Kikristo kabla ya mkutano kuanza, unaweza kuona watoto safi na nadhifu wakiketi karibu na wazazi wao. Je, haifurahishi kuona jinsi watu wa familia hizo wanavyopendana na wanavyompenda Yehova? Lakini ni rahisi kusahau kwamba jitihada nyingi zinahitajiwa ili familia iweze kufika mkutanoni kwa wakati.

2 Kwa kawaida, wazazi huwa na shughuli nyingi mchana kutwa, lakini siku za mkutano, familia huwa na shughuli nyingi hata zaidi. Chakula kinahitaji kutayarishwa, kazi nyingine za nyumbani zinahitaji kufanywa, na vilevile kazi za shule zinapaswa kumalizwa. Wazazi ndio huwa na kazi nyingi zaidi ya kuhakikisha kwamba kila mtu ni safi, amekula, na yuko tayari kwa wakati. Bila shaka, watoto wanaweza kufanya jambo lisilotazamiwa wakati usiofaa kabisa. Mtoto mkubwa anaweza kurarua nguo yake akicheza, naye yule mdogo amwage chakula chake. Au wanaweza kuanza kuzozana. (Methali 22:15) Matokeo huwa nini? Mambo yanaweza kwenda kombo licha ya wazazi kupanga mambo kwa uangalifu. Hata hivyo, karibu sikuzote familia hizo hufika kwenye Jumba la Ufalme kabla ya mkutano kuanza. Inatia moyo kama nini kuwaona mkutanoni juma baada ya juma, mwaka baada ya mwaka, huku watoto wakikua na kuwa watumishi wa Yehova!

3. Tunajuaje kwamba Yehova huthamini sana familia?

3 Ingawa nyakati nyingine kazi yako ukiwa mzazi ni ngumu na hata yenye kuchosha sana, uwe na hakika kwamba Yehova huthamini sana jitihada zako. Yehova ndiye Mwanzilishi wa familia. Hivyo, Neno lake linasema kwamba kila familia “hupata jina,” yaani, imekuwepo, kwa sababu ya Yehova. (Waefeso 3:14, 15) Kwa hiyo, wakati ninyi wazazi mnapojitahidi kutimiza majukumu yenu kwa njia ifaayo, mnamwonyesha heshima Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. (1 Wakorintho 10:31) Je, hilo si pendeleo kubwa? Basi, inafaa tuchunguze daraka ambalo Yehova amewapa wazazi. Katika makala hii, tutafikiria jambo hilo kuhusiana na kuandaa mahitaji ya familia. Na tuchunguze njia tatu ambazo Mungu hutarajia wazazi waandae mahitaji ya familia zao.

Kuandaa Mahitaji ya Kimwili

4. Yehova ameandaa mipango gani katika familia ili kutosheleza mahitaji ya watoto?

4 Mtume Paulo aliandika: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Paulo alikuwa akimfikiria nani alipotaja “yeyote”? Alikuwa akimfikiria kichwa cha familia ambaye kwa kawaida ni baba. Mungu pia amempa mwanamke daraka lenye heshima la kuwa msaidizi wa mume wake. (Mwanzo 2:18) Nyakati za Biblia, mara nyingi wanawake waliwasaidia waume zao kuandaa mahitaji ya familia. (Methali 31:13, 14, 16) Leo, kuna familia nyingi zenye mzazi mmoja. * Wazazi wengi Wakristo wasio na wenzi wanafanya kazi nzuri ya kuandaa mahitaji ya familia zao. Kwa kweli, inafaa familia kuwa na wazazi wote wawili, huku baba akiongoza mambo.

5, 6. (a) Wale wanaojitahidi kuandaa mahitaji ya kimwili ya familia zao hukabili matatizo gani? (b) Wazazi wataweza kuvumilia kwa kudumisha maoni gani kuhusu kazi?

5 Kwenye 1 Timotheo 5:8, Paulo alikuwa akizungumzia kuandaa mahitaji gani? Muktadha unaonyesha kwamba alikuwa akizungumza waziwazi kuhusu mahitaji ya kimwili ya familia. Leo kuna matatizo mengi ambayo huenda kichwa cha familia akakabili anapoandaa mahitaji ya kimwili ya familia. Kwa mfano, matatizo ya kiuchumi yameenea ulimwenguni pote, na ndivyo na ongezeko la ukosefu wa kazi, kuachishwa kazi, na kupanda kwa gharama ya maisha. Ni nini kinachoweza kumsaidia yule anayeandaa mahitaji ya familia avumilie matatizo hayo?

6 Yule anayeandaa mahitaji ya familia anapaswa kukumbuka kwamba anatimiza mgawo kutoka kwa Yehova. Maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaonyesha kwamba mwanamume aliye na uwezo wa kuandaa mahitaji ya familia lakini anakataa kufanya hivyo, ni kama mtu ambaye “ameikana imani.” Mkristo atajitahidi kabisa kuepuka kuonwa hivyo na Mungu. Lakini inasikitisha kwamba leo watu wengi hawana “upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:1, 3) Baba wengi huepa daraka lao na kuacha familia katika shida. Waume Wakristo huepuka kuwa na mtazamo huo wa kukosa hisia na kutojali kuhusu kuandaa mahitaji ya familia zao. Tofauti na wafanyakazi wenzao, wazazi Wakristo huiona hata kazi ya hali ya chini kuwa yenye heshima na muhimu, na pia kuwa njia ya kumpendeza Yehova Mungu, kwa kuwa inawawezesha kuandaa mahitaji ya wapendwa wao.

7. Kwa nini inafaa kwamba wazazi watafakari mfano wa Yesu?

7 Vichwa vya familia wanaweza pia kunufaika kwa kutafakari mfano mkamilifu wa Yesu. Kumbuka kwamba unabii wa Biblia unamtaja Yesu kuwa ‘Baba yetu wa Milele.’ (Isaya 9:6, 7) Akiwa “Adamu wa mwisho,” Yesu anachukua mahali pa “mtu wa kwanza Adamu” kwa ukamili akiwa baba ya wanadamu wenye imani. (1 Wakorintho 15:45) Yesu ni baba anayefaa, tofauti na Adamu aliyekuwa mwenye ubinafsi. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Kwa hili tumeujua upendo, kwa sababu huyo aliitoa nafsi yake kwa ajili yetu.” (1 Yohana 3:16) Naam, kwa hiari Yesu alitoa uhai wake kwa ajili ya wengine. Hata hivyo, kila siku alitanguliza mahitaji ya wengine hata katika mambo madogo. Enyi wazazi, inafaa kuiga roho hiyo isiyo na ubinafsi.

8, 9. (a) Wazazi wanaweza kujifunza nini kutoka kwa ndege kuhusu kuandaa mahitaji ya watoto wao bila ubinafsi? (b) Wazazi wengi Wakristo wanaonyeshaje roho ya kujitolea?

8 Wazazi wanaweza kujifunza mengi kuhusu upendo usio na ubinafsi kutokana na maneno haya ambayo Yesu aliwaambia watu wa Mungu waliokuwa wamepotoka: “Ni mara ngapi nilitaka kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake!” (Mathayo 23:37) Hapa Yesu anatumia mfano mzuri wa kuku anayetumia mabawa yake kukinga vifaranga vyake. Kwa kweli, wazazi wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa ndege anayeongozwa na silika, ambaye atakuwa tayari kujihatarisha ili kuwalinda makinda yake yasipatwe na madhara. Hata hivyo, inastaajabisha kuona yale ambayo ndege wenye makinda hufanya kila siku. Wao huruka huku na huku wakitafuta chakula. Hata wakati ambapo wamechoka, wao huweka chakula kwenye midomo ya makinda yao ambayo hukimeza na kwa kawaida hupiga kelele kudai chakula zaidi. Viumbe wengi wa Yehova huonyesha “hekima ya kisilika” kwa jinsi ambavyo wao hushughulikia mahitaji ya watoto wao.—Methali 30:24.

9 Vivyo hivyo, wazazi Wakristo ulimwenguni pote wanaonyesha roho nzuri ya kujinyima. Ni afadhali wewe upatwe na madhara lakini watoto wako wawe salama. Isitoshe, unajitolea kwa hiari kila siku ili kuandaa mahitaji ya familia yako. Wengi wenu huamka mapema ili kufanya kazi zenye kuchosha sana. Mnajitahidi sana ili kuziandalia familia zenu chakula bora. Mnajikakamua kuhakikisha kwamba watoto wenu wana nguo safi, makao mazuri, na elimu ya kutosha. Nanyi hufanya hivyo siku baada ya siku, mwaka baada ya mwaka. Bila shaka, kujitolea na kuvumilia kwenu humpendeza Yehova! (Waebrania 13:16) Lakini licha ya hayo, mnakumbuka kwamba kuna mahitaji mengine muhimu zaidi mnayopaswa kuandalia familia zenu.

Kuandaa Mahitaji ya Kiroho

10, 11. Ni mahitaji gani yaliyo muhimu zaidi kati ya mahitaji ya mwanadamu, na wazazi Wakristo wanapaswa kufanya nini kwanza ili kuwatimizia watoto wao mahitaji hayo?

10 Ni muhimu zaidi kuandaa mahitaji ya kiroho kuliko ya kimwili. Yesu alisema: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4; 5:3) Wazazi mnaweza kufanya nini ili kuandaa mahitaji ya kiroho ya watoto wenu?

11 Kuhusu jambo hilo, labda andiko ambalo hunukuliwa mara nyingi zaidi ni Kumbukumbu la Torati 6:5-7. Tafadhali fungua Biblia yako na usome mistari hiyo. Ona kwamba wazazi wanaambiwa waboreshe kwanza uhusiano wao na Mungu, kwa kusitawisha upendo kwa Yehova na kuyaweka maneno yake moyoni. Naam, unahitaji kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, kuisoma Biblia kwa ukawaida na kutafakari ili uweze kuzielewa vizuri na pia kuzipenda njia, kanuni, na sheria za Yehova. Kwa kufanya hivyo, moyo wako utajaa kweli nzuri za Biblia ambazo zitafanya uwe na shangwe na pia kumheshimu na kumpenda Yehova. Utakuwa na mambo mengi mazuri ya kuwafundisha watoto wako.—Luka 6:45.

12. Wazazi wanawezaje kumwiga Yesu katika kukazia kweli za Biblia kwa watoto wao?

12 Wazazi wenye nguvu kiroho huwa tayari kufuata shauri kwenye Kumbukumbu la Torati 6:7, la ‘kukazia’ maneno ya Yehova kwa watoto wao kila wakati. ‘Kukazia’ humaanisha kufundisha na kusisitiza kwa kurudia-rudia. Yehova anajua vizuri kwamba sote, na hasa watoto, tunahitaji kurudia-rudia mambo ili kujifunza. Hivyo, katika huduma yake, Yesu alifundisha kwa kurudia-rudia mambo. Kwa mfano, alipowafundisha wanafunzi wake wawe wanyenyekevu badala ya kuwa wenye kiburi na mashindano, alitafuta njia mbalimbali za kurudia kanuni hiyo. Alifundisha kwa kutoa hoja, kwa mifano, na kwa kuonyesha mambo kwa vitendo. (Mathayo 18:1-4; 20:25-27; Yohana 13:12-15) Hata hivyo, inapendeza kwamba Yesu hakukosa subira kamwe. Vivyo hivyo, wazazi wanahitaji kutafuta njia za kuwafundisha watoto wao kweli za msingi na kurudia-rudia kanuni za Yehova kwa subira hadi watoto wazielewe na kuzifuata.

13, 14. Ni pindi gani ambapo wazazi wanaweza kukazia kweli za Biblia kwa watoto wao, nao watatumia nini wanapofanya hivyo?

13 Wakati wa funzo la familia ni kipindi kinachofaa cha kufundisha mambo hayo. Kwa kweli, ili hali ya kiroho ya familia iwe bora, ni muhimu kuwa na funzo la Biblia la familia lenye kujenga, lenye furaha, na linalofanywa kwa ukawaida. Familia za Kikristo ulimwenguni hufurahia funzo hilo, nazo hutumia vichapo vinavyoandaliwa na tengenezo la Yehova kutayarisha funzo kulingana na mahitaji ya watoto. Kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu na kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, * ni zawadi za pekee katika kufundisha watoto. Hata hivyo, kuna pindi nyingine za kuwafundisha watoto mbali na wakati wa funzo la familia.

14 Kama andiko la Kumbukumbu la Torati 6:7 linavyoonyesha, kuna pindi nyingi ambapo ninyi wazazi mnaweza kuzungumzia mambo ya kiroho pamoja na watoto wenu. Mnaweza kupata nafasi za kuandaa mahitaji ya kiroho ya watoto wenu mnaposafiri pamoja, mnapofanya kazi za nyumbani, au kustarehe pamoja. Bila shaka, hamhitaji kuzungumza mfululizo na watoto wenu kuhusu kweli za Biblia. Badala yake, jaribuni kuwa na mazungumzo ya kiroho na yenye kujenga katika familia. Kwa mfano, gazeti la Amkeni! huwa na makala nyingi kuhusu mambo mbalimbali. Makala hizo zinaweza kutumiwa ili kuzungumza kuhusu wanyama, maeneo ya asili yenye kuvutia ulimwenguni, na maisha na utamaduni mbalimbali wenye kuvutia. Mazungumzo hayo yanaweza kuwachochea watoto wasome vichapo zaidi vinavyoandaliwa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.—Mathayo 24:45-47.

15. Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao waione kazi ya Kikristo ya kuhubiri kuwa yenye kupendeza na kufurahisha?

15 Kuzungumzia mambo yenye kujenga pamoja na watoto wako kutakusaidia kutimiza uhitaji mwingine wa kiroho. Watoto Wakristo wanahitaji kujifunza kuwaeleza wengine imani yao kwa matokeo. Unapozungumzia habari fulani yenye kuvutia katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni!, unaweza kutafuta njia za kuonyesha jinsi habari hiyo inavyohusiana na kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, huenda ukamuuliza mtoto hivi: “Je, haingekuwa vizuri kama watu wengi zaidi wangejua habari hii kumhusu Yehova? Unafikiri tunawezaje kumsaidia mtu apendezwe na habari hii?” Mazungumzo kama hayo yanaweza kuwasaidia watoto wapendezwe zaidi kuwaeleza wengine mambo wanayojifunza. Halafu, unapoenda kuhubiri pamoja na watoto wako, wanaona mfano halisi wa kutenda kupatana na mazungumzo hayo. Pia, wanaweza kujifunza kwamba kazi ya kuhubiri inapendeza na kufurahisha, na inaleta uradhi na shangwe nyingi.—Matendo 20:35.

16. Watoto wanaweza kujifunza nini kwa kusikiliza sala za wazazi wao?

16 Wazazi pia huandaa mahitaji ya kiroho ya watoto wao kupitia sala. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kusali, naye alisali pamoja nao pindi nyingi. (Luka 11:1-13) Hebu wazia jinsi walivyojifunza mambo mengi waliposali pamoja na Mwana wa Yehova! Vivyo hivyo, watoto wako wanaweza kujifunza mengi kutokana na sala zako. Kwa mfano, wanaweza kujifunza kwamba Yehova hutaka tuzungumze naye kwa uhuru kutoka moyoni na kumweleza tatizo lolote tunaloweza kuwa nalo. Naam, sala zako zinaweza kuwasaidia watoto wako wajifunze ukweli huu muhimu: Wanaweza kuwa na uhusiano na Baba yao wa mbinguni.—1 Petro 5:7.

Kuandaa Mahitaji ya Kihisia

17, 18. (a) Biblia huonyeshaje umuhimu wa kuwaonyesha watoto upendo? (b) Akina baba wanapaswa kumwigaje Yehova katika kuwaonyesha watoto wao upendo?

17 Bila shaka, watoto pia wana mahitaji muhimu ya kihisia. Neno la Mungu linawaeleza wazazi kwamba ni muhimu kutosheleza mahitaji hayo. Kwa mfano, wanawake vijana wanahimizwa “wawapende watoto wao.” Kufanya hivyo kunahusiana na kuamsha akili za akina mama vijana, au kuwa na akili timamu. (Tito 2:4) Ni jambo la akili kumwonyesha mtoto upendo kwa kuwa hilo humfundisha kuwapenda wengine na huleta manufaa ya kudumu. Kwa upande mwingine, ni upumbavu kutomwonyesha mtoto upendo. Hilo humuumiza sana na huonyesha kwamba mzazi ameshindwa kumwiga Yehova ambaye, licha ya kasoro zetu, hutuonyesha upendo mwingi sana.—Zaburi 103:8-14.

18 Yehova hata huchukua hatua ya kwanza kuwaonyesha upendo watoto wake walio duniani. Kama andiko la 1 Yohana 4:19 linavyosema, “yeye alitupenda sisi kwanza.” Ninyi akina baba hasa mnapaswa kumwiga Yehova, kwa kuchukua hatua ya kwanza kujenga uhusiano wenye upendo na watoto wenu. Biblia huwatia moyo akina baba waepuke kuwakasirisha watoto wao “ili wasivunjike moyo.” (Wakolosai 3:21) Ni mambo machache yanayowakasirisha watoto zaidi kuliko kuona kwamba mzazi hawapendi wala hawathamini. Akina baba ambao husita kuonyesha hisia zao wanapaswa kukumbuka mfano wa Yehova. Hata alizungumza kutoka mbinguni ili kuonyesha kuwa anamkubali na kumpenda Mwana wake. (Mathayo 3:17; 17:5) Jambo hilo lilimtia Yesu moyo sana! Vivyo hivyo, watoto hupata nguvu na ujasiri mwingi wazazi wanapoonyesha wazi kuwa wanawapenda na kuwakubali.

19. Kwa nini nidhamu ni muhimu, nao wazazi Wakristo hujitahidi kuwa na usawaziko gani?

19 Bila shaka, upendo wa mzazi hauonyeshwi kwa maneno tu. Upendo huonyeshwa hasa kwa matendo. Mzazi anaweza kudhihirisha upendo wake kwa kuandaa mahitaji ya kimwili na ya kiroho, hasa anapofanya hivyo kwa njia inayoonyesha anachochewa na upendo. Pia, nidhamu ni njia muhimu ya kuonyesha upendo wa mzazi. Naam, “yeye ambaye Yehova anampenda, humtia nidhamu.” (Waebrania 12:6) Kwa upande mwingine, mzazi asiyewatia watoto wake nidhamu anawachukia! (Methali 13:24) Sikuzote Yehova hutoa nidhamu kwa usawaziko na “kwa kiwango kinachofaa.” (Yeremia 46:28) Si rahisi sikuzote kwa wazazi wasio wakamilifu kuwa na usawaziko huo. Lakini, inafaa wajitahidi kadiri wawezavyo. Nidhamu inayotolewa kwa upendo na kwa uthabiti humsaidia mtoto kukua na kuwa na furaha na mafanikio maishani. (Methali 22:6) Kila mzazi Mkristo angependa maisha ya mtoto wake yawe hivyo, sivyo?

20. Wazazi wanawezaje kuwapa watoto wao nafasi bora ya ‘kuchagua uzima?’

20 Enyi wazazi, mnapofanya kazi muhimu ambayo Yehova amewapa, yaani, kuandaa mahitaji ya kimwili, ya kiroho, na ya kihisia ya watoto wenu, kunakuwa na faida nyingi. Kwa kufanya hivyo, mnawapa watoto wenu nafasi bora ya ‘kuchagua uzima’ na baadaye ‘kuendelea kuwa hai.’ (Kumbukumbu la Torati 30:19) Watoto wanaochagua kumtumikia Yehova na kubaki katika njia ya uzima wanapoendelea kukomaa huwaletea wazazi wao shangwe kubwa. (Zaburi 127:3-5) Shangwe hiyo itadumu milele! Lakini vijana wanawezaje kumsifu Yehova sasa? Makala inayofuata itazungumzia habari hiyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika mazungumzo haya, tutamrejelea baba kuwa ndiye anayeandaa mahitaji ya familia. Hata hivyo, kanuni zinazotajwa zinawahusu pia wanawake Wakristo ambao wanategemewa kuandaa mahitaji ya familia.

^ fu. 13 Vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Ungejibuje?

Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwaandalia watoto wao

• kimwili?

• kiroho?

• kihisia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ndege wengi hujitahidi juu chini kulisha makinda yao

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wazazi wanapaswa kuboresha kwanza uhusiano wao na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Wazazi wanaweza kupata pindi nyingi za kuwafundisha watoto wao kumhusu Muumba

[Picha katika ukurasa wa 22]

Watoto hupata nguvu na ujasiri wazazi wanapoonyesha kuwa wanawakubali