Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Njema Kwa Watu wa Mataifa Yote

Habari Njema Kwa Watu wa Mataifa Yote

Habari Njema Kwa Watu wa Mataifa Yote

“Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—MATENDO 1:8.

1. Tunazingatia nini tukiwa walimu wa Biblia, na kwa nini?

WALIMU stadi hawazingatii tu mambo wanayowafundisha wanafunzi wao bali pia jinsi wanavyowafundisha. Tunafanya vivyo hivyo tukiwa walimu wa kweli ya Biblia. Tunazingatia ujumbe tunaohubiri na njia tunazotumia. Ujumbe wetu, yaani, habari njema ya Ufalme wa Mungu, haubadiliki, lakini sisi hubadili njia zetu kulingana na hali. Kwa nini? Ili tufikie watu wengi iwezekanavyo.

2. Tunamwiga nani tunapobadili njia zetu za kuhubiri?

2 Tunapobadili njia zetu za kuhubiri, tunawaiga watumishi wa zamani wa Mungu. Kwa mfano, fikiria mtume Paulo. Alisema hivi: “Kwa Wayahudi nilikuwa kama Myahudi . . . Kwa wale wasio na sheria nilikuwa kama asiye na sheria . . . Kwa walio dhaifu nilikuwa dhaifu, ili niwapate walio dhaifu. Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine.” (1 Wakorintho 9:19-23) Paulo alipata matokeo alipobadili njia zake za kuhubiri. Sisi pia tutapata matokeo tukibadili utangulizi wetu ili uwafae watu tunaozungumza nao.

Kufikia “Miisho ya Dunia”

3. (a) Tunakabili tatizo gani katika kazi yetu ya kuhubiri? (b) Maneno ya Isaya 45:22 yanatimizwaje leo?

3 Tatizo kubwa linalowakabili wale wanaohubiri habari njema ni ukubwa wa eneo, yaani, “dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Katika karne iliyopita, watumishi wengi wa Yehova walijitahidi sana kwenda katika nchi nyingine ili kueneza habari njema. Matokeo yalikuwa nini? Ongezeko kubwa ajabu ulimwenguni pote. Mwanzoni mwa karne ya 20, kazi ya kuhubiri ilifanywa katika nchi chache tu, lakini leo Mashahidi wa Yehova wanahubiri kwa bidii katika nchi 235! Kwa kweli, habari njema ya Ufalme inatangazwa hata kufikia “miisho ya dunia.”—Isaya 45:22.

4, 5. (a) Ni nani ambao wametimiza jukumu muhimu katika kueneza habari njema? (b) Baadhi ya ofisi za tawi zilisema nini kuhusu wageni wanaotumika katika maeneo yaliyo chini ya ofisi hizo?

4 Kwa nini kuna ongezeko kubwa hivyo? Sababu ni nyingi. Wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi na, hivi karibuni, wanafunzi zaidi ya 20,000 waliofuzu katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, wamechangia sehemu kubwa. Vilevile Mashahidi wengi ambao wamehamia nchi zenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme kwa gharama yao wamechangia pia ongezeko hilo. Wakristo hao wenye kujitolea, wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee, waseja na waliofunga ndoa, hutimiza sehemu muhimu sana katika kuhubiri ujumbe wa Ufalme duniani pote. (Zaburi 110:3; Waroma 10:18) Wanathaminiwa sana. Baadhi ya ofisi za tawi ziliandika hivi kuhusu wahubiri kutoka nchi nyingine waliojitolea kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa yaliyo chini ya ofisi hizo.

5 “Mashahidi hawa wapendwa huongoza katika kuhubiri maeneo ya mbali, husaidia kuanzisha makutaniko mapya, na huwasaidia ndugu na dada kukua kiroho.” (Ekuado) “Ikiwa mamia ya wageni wanaotumika huku wangeondoka, makutaniko hayangekuwa thabiti. Ni baraka kuwa nao.” (Jamhuri ya Dominika) “Katika mengi ya makutaniko yetu, kuna idadi kubwa ya akina dada, na hata katika makutaniko fulani asilimia 70 ya wahubiri ni akina dada. (Zaburi 68:11) Wengi wa dada hao ni wapya katika kweli, lakini dada waseja mapainia ambao wametoka nchi nyingine hutimiza jukumu muhimu sana la kuwazoeza. Dada hao kutoka nchi nyingine wanatusaidia sana!” (Nchi moja ya Ulaya Mashariki) Je, umewahi kufikiria kutumika katika nchi nyingine? *Matendo 16:9, 10.

“Watu Kumi Kutoka Katika Lugha Zote”

6. Andiko la Zekaria 8:23 linaonyeshaje kwamba tungekabili tatizo la lugha katika kazi yetu ya kuhubiri?

6 Tatizo lingine kubwa tunalokabili ni lugha nyingi ambazo zinazungumzwa duniani. Neno la Mungu lilitabiri hivi: “Itakuwa katika siku hizo kwamba watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zekaria 8:23) Katika utimizo wa leo wa unabii huo, wale watu kumi wanawakilisha umati mkubwa, uliotabiriwa katika Ufunuo 7:9. Hata hivyo, ona kwamba kulingana na unabii wa Zekaria, hao “watu kumi” hawangetoka tu katika mataifa yote bali pia wangetoka “katika lugha zote za mataifa.” Je, tumeona sehemu hiyo muhimu ya unabii huo ikitimizwa? Bila shaka.

7. Takwimu zinaonyeshaje kwamba watu “kutoka katika lugha zote” wanahubiriwa habari njema?

7 Fikiria takwimu zifuatazo. Miaka 50 iliyopita vichapo vyetu vilichapishwa katika lugha 90. Leo, vinachapishwa katika lugha zaidi ya 400. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amefanya yote awezayo kutayarisha vichapo hata katika lugha ambazo zinazungumzwa na watu wachache. (Mathayo 24:45) Kwa mfano, vichapo vya Biblia sasa vinapatikana katika lugha ya Greenland (inayozungumzwa na watu 47,000), lugha ya Palau (inayozungumzwa na watu 15,000), na Yapese (inayozungumzwa na watu wasiozidi 7,000).

“Mlango Mkubwa” Unaotokeza Nafasi Mpya

8, 9. Ni jambo gani limetufungulia “mlango mkubwa,” na maelfu ya Mashahidi wamekabilianaje na hali hiyo?

8 Siku hizi si lazima twende nchi nyingine ili tuwahubirie watu wa lugha zote habari njema. Katika miaka ya karibuni, mamilioni ya wakimbizi na wahamiaji wanaozungumza lugha mbalimbali wamehamia nchi zilizoendelea kiuchumi. Kwa mfano, huko Paris, Ufaransa, lugha 100 hivi zinazungumzwa. Huko Toronto, Kanada, kuna lugha 125; na London, Uingereza, lugha zaidi ya 300 za kigeni zinazungumzwa! Watu hao kutoka nchi nyingine wanaishi katika maeneo mengi ya makutaniko na hilo limefungua “mlango mkubwa” unaotokeza nafasi mpya za kuwahubiria habari njema watu kutoka katika mataifa yote.—1 Wakorintho 16:9.

9 Maelfu ya Mashahidi wanakabiliana na hali hiyo kwa kujifunza lugha nyingine. Si rahisi kwa wengi wao. Hata hivyo, jitihada zao si za bure kwani wanapata shangwe wanapowasaidia wakimbizi na wahamiaji kujifunza kweli ya Neno la Mungu. Katika mwaka mmoja wa hivi karibuni, asilimia 40 hivi ya wote waliobatizwa kwenye makusanyiko ya wilaya katika nchi moja ya Ulaya Magharibi walikuwa wahamiaji kutoka nchi nyingine.

10. Umekitumiaje kijitabu Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote? (Ona sanduku “Yaliyomo Katika Kijitabu Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote,” kwenye ukurasa wa 26.)

10 Ni kweli kwamba wengi wetu hatuwezi kujifunza lugha ya kigeni. Hata hivyo, tunaweza kuwasaidia wahamiaji kwa kutumia vizuri kijitabu kipya cha Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote (Kiingereza na Kifaransa), * ambacho kina ujumbe wa Biblia wenye kuvutia katika lugha mbalimbali. (Yohana 4:37) Je, unakitumia kijitabu hicho katika huduma?

Watu Wanapokataa Habari Njema

11. Ni tatizo gani lingine tunalokabili katika maeneo fulani?

11 Uvutano wa Shetani unapoongezeka duniani, mara nyingi tunakabili tatizo lingine—katika maeneo fulani watu wengi wanakataa habari njema. Bila shaka, hatushangazwi na hali hiyo kwa kuwa Yesu alitabiri kwamba ingekuwa hivyo. Alisema hivi kuhusu siku zetu: “Upendo wa walio wengi zaidi utapoa.” (Mathayo 24:12) Kwa kweli, imani ya wengi katika Mungu na heshima yao kuelekea Biblia imepungua. (2 Petro 3:3, 4) Ndiyo sababu katika sehemu fulani za ulimwengu ni watu wachache sana wanaokuwa wanafunzi wa Kristo. Lakini hilo halimaanishi kwamba jitihada za ndugu na dada zetu Wakristo wapendwa ambao wanahubiri kwa uaminifu katika maeneo kama hayo magumu ni za bure. (Waebrania 6:10) Kwa nini? Fikiria mambo yafuatayo.

12. Kazi yetu ya kuhubiri inatimiza makusudi gani mawili?

12 Injili ya Mathayo inakazia makusudi mawili makuu ya kazi yetu ya kuhubiri. Kusudi moja ni ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19) Kusudi la pili ni kwamba ujumbe wa Ufalme unatolewa kuwa “ushahidi.” (Mathayo 24:14) Makusudi yote mawili ni muhimu, lakini kusudi la pili ni la pekee. Kwa nini?

13, 14. (a) Ni sehemu gani kuu ya ishara ya kuwapo kwa Kristo? (b) Tunapaswa kukumbuka nini hasa tunapohubiri katika maeneo magumu?

13 Mwandishi wa Biblia, Mathayo, aliandika swali hili ambalo mitume walimuuliza Yesu: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Yesu aliwajibu kwamba kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ingekuwa sehemu kuu ya ishara hiyo. Je, alimaanisha kufanya wanafunzi? Hapana. Alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Kwa hiyo, Yesu alionyesha kwamba kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ingekuwa sehemu muhimu ya ishara hiyo.

14 Basi, tunapohubiri habari njema ya Ufalme, tunakumbuka kwamba hata ikiwa nyakati nyingine hatufaulu kufanya wanafunzi, tunafaulu kutoa “ushahidi.” Iwe watu wanakubali au la, wao wanajua kazi tunayofanya, hivyo tunashiriki kutimiza unabii wa Yesu. (Isaya 52:7; Ufunuo 14:6, 7) Shahidi mmoja kijana kutoka Ulaya Magharibi anayeitwa Jordy alisema hivi: “Mimi hufurahi sana kujua kwamba Yehova ananitumia kutimiza Mathayo 24:14.” (2 Wakorintho 2:15-17) Hapana shaka kwamba unahisi vivyo hivyo.

Ujumbe Wetu Unapopingwa

15. (a) Yesu aliwaonya wafuasi wake kimbele kuhusu nini? (b) Ni nini hutuwezesha kuhubiri licha ya upinzani?

15 Tatizo lingine ni upinzani mkali kuelekea kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Yesu aliwaonya kimbele wafuasi wake hivi: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mathayo 24:9) Kama Wakristo wa mapema, wafuasi wa Yesu leo wamechukiwa, wamepingwa, na kuteswa. (Matendo 5:17, 18, 40; 2 Timotheo 3:12; Ufunuo 12:12, 17) Katika nchi fulani, wamepigwa marufuku na serikali. Hata hivyo, Wakristo wa kweli katika nchi hizo wanaendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa sababu wanataka kumtii Mungu. (Amosi 3:8; Matendo 5:29; 1 Petro 2:21) Ni nini kinachowawezesha Wakristo hao na Mashahidi wengine ulimwenguni pote kuendelea kuhubiri? Yehova huwatia nguvu kwa roho yake takatifu.—Zekaria 4:6; Waefeso 3:16; 2 Timotheo 4:17.

16. Yesu alionyeshaje uhusiano uliopo kati ya kazi ya kuhubiri na roho ya Mungu?

16 Yesu alikazia uhusiano uliopo kati ya roho ya Mungu na kazi ya kuhubiri alipowaambia wafuasi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8; Ufunuo 22:17) Mfuatano wa matukio katika andiko hilo ni muhimu. Kwanza, wanafunzi walipokea roho takatifu, kisha wakaanza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Wangeweza tu kuvumilia katika kazi ya kutoa “ushahidi kwa mataifa yote” kwa msaada wa roho ya Mungu. (Mathayo 24:13, 14; Isaya 61:1, 2) Ndiyo sababu Yesu alisema kwamba roho takatifu ni “msaidizi.” (Yohana 15:26) Alisema kwamba roho ya Mungu ingewafundisha na kuwaongoza wanafunzi wake.—Yohana 14:16, 26; 16:13.

17. Roho takatifu hutusaidiaje tunapopingwa vikali?

17 Roho ya Mungu inatusaidiaje leo wakati kazi yetu ya kuhubiri habari njema inapopingwa vikali? Roho ya Mungu hutuimarisha, nayo huwapinga wale wanaotutesa. Ili kuelewa hilo, fikiria tukio moja katika maisha ya Mfalme Sauli.

Apingwa na Roho ya Mungu

18. (a) Sauli alibadilikaje akawa mbaya sana? (b) Sauli alimtesa Daudi katika njia zipi?

18 Sauli alianza vyema akiwa mfalme wa kwanza wa Israeli, lakini baadaye akamwasi Yehova. (1 Samweli 10:1, 24; 11:14, 15; 15:17-23) Kwa hiyo roho ya Mungu ikaacha kumtegemeza mfalme huyo. Sauli alimkasirikia sana Daudi, ambaye alitiwa mafuta kuwa mfalme anayefuata wa Israeli na aliyetegemezwa na roho ya Mungu. (1 Samweli 16:1, 13, 14) Daudi alionekana kuwa anaweza kushambuliwa kwa urahisi kwa sababu alikuwa na kinubi tu hali Sauli alikuwa na mkuki. Kwa hiyo, siku moja Daudi alipokuwa akipiga kinubi, ‘Sauli aliutupa mkuki na kusema: “Nitampigilia Daudi ukutani!” lakini Daudi akakwepa kutoka mbele yake, mara mbili.’ (1 Samweli 18:10, 11) Baadaye, Sauli alimsikiliza mwanaye Yonathani, rafiki ya Daudi, na kuapa hivi: “Kama Yehova anavyoishi, [Daudi] hatauawa.” Lakini Sauli ‘akatafuta tena kumpigilia Daudi ukutani kwa mkuki.’ Hata hivyo, Daudi “akakwepa kutoka mbele ya Sauli, hivi kwamba akaupigilia mkuki ule ndani ya ukuta.” Daudi alikimbia, lakini Sauli akamfuata. Wakati huo hatari, roho ya Mungu ilimpinga Sauli. Jinsi gani?—1 Samweli 19:6, 10.

19. Roho ya Mungu ilimlindaje Daudi?

19 Daudi alikimbia hadi kwa nabii Samweli, lakini Sauli akawatuma wajumbe wake wakamkamate Daudi. Hata hivyo, walipofika mahali ambapo alikuwa amejificha, ‘roho ya Mungu ikaja juu ya wajumbe hao wa Sauli, nao pia wakaanza kutenda kama manabii.’ Walilemewa sana na roho ya Mungu hivi kwamba walisahau kabisa sababu iliyowaleta hapo. Sauli aliwatuma wajumbe mara mbili zaidi ili wamlete Daudi, nao pia wakalemewa na roho ya Mungu. Mwishowe, Mfalme Sauli mwenyewe alienda kumtafuta Daudi, lakini Sauli pia akashindwa kustahimili roho ya Mungu. Kwa kweli, roho takatifu ilimfanya alale chini “mchana huo wote na usiku huo wote,” hivyo Daudi akawa na wakati wa kutosha wa kukimbia.—1 Samweli 19:20-24.

20. Tunajifunza nini kutokana na simulizi la jinsi Sauli alivyomtesa Daudi?

20 Simulizi hilo kuhusu Sauli na Daudi linatufundisha jambo lenye kutia moyo sana: Watu wanaowatesa watumishi wa Mungu hawawezi kufaulu wanapopingwa na roho ya Mungu. (Zaburi 46:11; 125:2) Yehova alikusudia Daudi awe mfalme wa Israeli. Hakuna mtu yeyote angeweza kubadili kusudi hilo. Katika siku zetu, Yehova amekusudia kwamba “habari njema ya ufalme itahubiriwa.” Hakuna mtu yeyote anayeweza kuzuia kazi hiyo.—Matendo 5:40, 42.

21. (a) Baadhi ya wapinzani leo hutendaje? (b) Tuna uhakika gani?

21 Viongozi fulani wa kidini na wa kisiasa hutumia uwongo na hata jeuri kujaribu kutuzuia kufanya kazi hiyo. Hata hivyo, Yehova atawalinda watu wake leo kama alivyomlinda Daudi kiroho. (Malaki 3:6) Kwa hiyo, tunasema hivi kwa uhakika kama Daudi: “Nimeweka tegemeo langu katika Mungu. Sitaogopa. Mtu wa udongo anaweza kunitenda nini?” (Zaburi 56:11; 121:1-8; Waroma 8:31) Kwa msaada wa Yehova, na tuendelee kukabiliana na matatizo yote tunapotekeleza kazi aliyotukabidhi ya kuwahubiria watu wa mataifa yote habari njema ya Ufalme.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona sanduku “Ninaridhika Sana,” kwenye ukurasa wa 22.

^ fu. 10 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini sisi hubadili njia zetu za kuhubiri ili zilingane na hali?

• “Mlango mkubwa” uliofunguliwa unatokeza nafasi gani mpya?

• Kazi yetu ya kuhubiri inatimiza nini, hata katika maeneo magumu?

• Kwa nini hakuna mpinzani yeyote anayeweza kuzuia kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

Ninaridhika Sana

“Wanafurahia kumtumikia Yehova kwa umoja.” Maelezo hayo yanahusu familia moja iliyohamia Bolivia kutoka Hispania. Mwana wa familia hiyo alikuwa ametangulia kwenda huko kusaidia kikundi kilichokuwa mbali. Shangwe yake iliwavutia wazazi wake sana hivi kwamba muda si muda familia yote, kutia ndani wavulana wanne walio kati ya umri wa miaka 14 na 25, ilienda kutumika huko. Sasa watatu kati ya wavulana hao ni mapainia, na yule aliyeenda huko kwanza alihudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma hivi karibuni.

Angelica, mwenye umri wa miaka 30, kutoka Kanada, ambaye anatumika huko Ulaya Mashariki, anasema: “Kuna matatizo mengi ya kukabiliana nayo lakini ninaridhika kuwasaidia watu katika huduma. Ninaguswa moyo pia na shukrani nyingi zinazotolewa na Mashahidi wa eneo hilo ambao hunishukuru mara nyingi kwa sababu ya kuja kuwasaidia.”

Dada wawili wa familia moja wenye umri wa karibu miaka 30, kutoka Marekani, ambao wanatumika katika Jamhuri ya Dominika, wanasema hivi: “Tulihitaji kuzoea desturi mbalimbali. Hata hivyo, tuliendelea na kazi yetu ya kuhubiri, na sasa saba kati ya wanafunzi wetu wa Biblia wanahudhuria mikutano.” Dada hao wawili walisaidia sana kuanzisha kikundi cha wahubiri wa Ufalme katika mji usio na kutaniko.

Laura, dada mwenye umri wa karibu miaka 30, amekuwa akitumika katika nchi ya kigeni kwa zaidi ya miaka minne. Anasema: “Nimeazimia kuishi maisha rahisi. Kufanya hivyo huwasaidia wahubiri kuona kwamba kuishi maisha yenye kiasi ni uamuzi wa kibinafsi na huonyesha kwamba mtu ana usawaziko wa kiakili, bali si kwamba ni maskini. Nimepata shangwe kubwa sana kwa kuwasaidia wengine, hasa vijana. Matatizo ya kutumika katika nchi ya kigeni hayawezi kulinganishwa na shangwe hiyo. Siwezi kuacha utumishi wangu ili nifanye jambo lingine maishani, na nitaendelea maadamu Yehova anaruhusu.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

Yaliyomo Katika Kijitabu Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote

Kijitabu Habari Njema kwa Watu wa Mataifa Yote (Kiingereza na Kifaransa) kina ujumbe wa kurasa moja katika lugha 92 hivi. Ujumbe huo umeelekezwa kwa mtu binafsi. Kwa hiyo mwenye-nyumba anaposoma ujumbe huo, ni kana kwamba unazungumza naye.

Kuna ramani ya ulimwengu katika sehemu ya ndani ya jalada. Tumia ramani hiyo kuanzisha mazungumzo na mwenye-nyumba. Labda unaweza kuonyesha nchi unamoishi na umuulize anakotoka. Kwa njia hiyo, unaweza kumstarehesha na kumchochea azungumze.

Utangulizi wa kijitabu hicho unaorodhesha hatua kadhaa ambazo tunapaswa kuchukua ili kuwasaidia ifaavyo wale wanaozungumza lugha ambayo hatuelewi. Tafadhali soma hatua hizo kwa uangalifu na uzitumie kwa makini sana.

Sehemu ya yaliyomo inaorodhesha lugha na pia alama ya kila lugha. Orodha hiyo itakusaidia kutambua alama ya lugha katika trakti zetu na vichapo vya lugha nyingine.

[Picha]

Je, unatumia kijitabu hiki katika huduma?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Sasa vichapo vyetu vya Biblia vinachapishwa katika lugha zaidi ya 400

GHANA

UFILIPINO

LAPLAND (SWEDEN)

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Je, unaweza kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme?

EKUADO

JAMHURI YA DOMINIKA