Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Kuleta Habari Njema za Jambo Bora’

‘Kuleta Habari Njema za Jambo Bora’

‘Kuleta Habari Njema za Jambo Bora’

“Jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye . . . anayeleta habari njema za jambo bora.”—ISAYA 52:7.

1, 2. (a) Ni mambo gani yenye kutisha yanayotukia kila siku? (b) Watu wengi huhisije wanapopata habari mbaya kila siku?

LEO watu wanapokea habari nyingi mbaya ulimwenguni pote. Wanapowasha redio, wanasikia habari zenye kutisha kuhusu magonjwa hatari yanayoikumba dunia. Wanapotazama habari kwenye televisheni wanaona picha zenye kusikitisha sana za watoto wenye njaa wakiomba msaada. Wanasoma katika magazeti kuhusu mabomu yanayolipua majengo na kuwaua watu wengi wasio na hatia.

2 Naam, mambo yenye kutisha yanatukia kila siku. Tamasha ya ulimwengu huu kwa hakika inabadilika na kuwa mbaya zaidi. (1 Wakorintho 7:31) Gazeti moja huko Ulaya Magharibi lilisema, nyakati nyingine ni kama ulimwengu wote “unakaribia kuteketea.” Si ajabu kwamba watu wengi wanafadhaika! Mtu mmoja aliyenukuliwa katika uchunguzi wa habari za televisheni nchini Marekani alitoa maoni ambayo bila shaka ni sawa na ya mamilioni ya watu wengine aliposema hivi: ‘Baada ya kutazama habari, mimi hushuka moyo sana. Zote ni habari mbaya. Zinanihuzunisha sana.’

Habari Ambazo Kila Mtu Anahitaji Kusikia

3. (a) Biblia inatangaza habari gani njema? (b) Kwa nini unathamini habari njema za Ufalme?

3 Je, habari njema zinaweza kupatikana katika ulimwengu huu wenye kuhuzunisha? Bila shaka zinaweza kupatikana! Inafariji kujua kwamba Biblia inatangaza habari njema. Hizo ni habari za kwamba Ufalme wa Mungu utakomesha magonjwa, njaa, uhalifu, vita, na kila namna ya ukandamizaji. (Zaburi 46:9; 72:12) Je, hizo si habari ambazo kila mtu anahitaji kusikia? Mashahidi wa Yehova wanaamini hivyo. Kwa hiyo, wanajulikana kila mahali kwa sababu wanajitahidi daima kuwahubiria watu wa mataifa yote habari njema za Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.

4. Ni mambo gani kuhusu huduma yetu tutakayozungumzia katika makala hii na katika ile inayofuata?

4 Basi, tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuhubiri habari njema kwa bidii na kuridhika tunapofanya hivyo—hata katika maeneo ambayo watu wengi hawataki ujumbe wetu? (Luka 8:15) Bila shaka tutafaidika tukipitia kifupi mambo matatu muhimu kuhusu kazi yetu ya kuhubiri. Tunaweza kuchunguza (1) nia yetu, au kwa nini tunahubiri; (2) ujumbe wetu, au kile tunachohubiri; na (3) njia zetu, au jinsi tunavyohubiri. Tunapokuwa na nia inayofaa, ujumbe ulio wazi, na kutumia njia zenye matokeo, tutawapa watu wa kila namna nafasi ya kusikia habari bora kabisa—habari njema za Ufalme wa Mungu. *

Kwa Nini Tunahubiri Habari Njema?

5. (a) Ni sababu gani kuu inayotuchochea kuhubiri? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba kutii amri ya Biblia ya kuhubiri huonyesha kwamba tunampenda Mungu?

5 Hebu tuzungumzie jambo la kwanza, yaani, nia yetu. Kwa nini tunahubiri habari njema? Sababu yetu ni kama ya Yesu. Alisema: “Ninampenda Baba.” (Yohana 14:31; Zaburi 40:8) Kwa hiyo, kumpenda Mungu ndiyo sababu kuu inayotuchochea kuhubiri. (Mathayo 22:37, 38) Biblia inahusianisha kumpenda Mungu na huduma, kwa kuwa inasema hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.” (1 Yohana 5:3; Yohana 14:21) Je, amri za Mungu zinatia ndani ile amri ya ‘kwenda kufanya wanafunzi’? (Mathayo 28:19) Ndiyo. Ingawa maneno hayo yalisemwa na Yesu, kwa kweli yalitoka kwa Yehova. Jinsi gani? Yesu alieleza hivi: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yohana 8:28; Mathayo 17:5) Kwa hiyo, tunapotii amri ya kuhubiri, tunamwonyesha Yehova kwamba tunampenda.

6. Kumpenda Mungu hutuchochea katika njia zipi kuhubiri?

6 Pia, kumpenda Yehova hutuchochea kuhubiri kwa sababu tunataka kupinga uwongo ambao Shetani anaeneza kumhusu. (2 Wakorintho 4:4) Shetani ametilia shaka uadilifu wa utawala wa Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunatamani sana kushiriki katika kufunua uchongezi wa Shetani na kulitakasa jina la Mungu mbele ya wanadamu. (Isaya 43:10-12) Isitoshe, tunashiriki katika huduma kwa sababu tumejua sifa za Yehova na njia zake. Tunahisi tukiwa karibu naye na tunatamani sana kuwaeleza wengine kumhusu Mungu wetu. Kwa kweli, wema wa Yehova na njia zake za uadilifu hutuletea shangwe kubwa sana hivi kwamba hatuwezi kuacha kuongea juu yake. (Zaburi 145:7-12) Moyo wetu unatusukuma kumsifu na kutangaza ‘sifa zake bora’ kwa wale ambao watasikiliza.—1 Petro 2:9; Isaya 43:21.

7. Mbali na kumpenda Mungu, ni sababu gani nyingine muhimu inayotufanya tuhubiri?

7 Kuna sababu nyingine muhimu inayotufanya tuendelee kuhubiri: Tunataka kwa moyo wote kuwafariji wale wanaofadhaishwa na habari nyingi mbaya na wale wanaoteseka kwa sababu mbalimbali. Tunajitahidi kumwiga Yesu tunapowafariji wengine. Kwa mfano, angalia simulizi la Marko sura ya 6.

8. Simulizi la Marko sura ya 6 linaonyesha nini kuhusu hisia za Yesu kuwaelekea watu?

8 Mitume wametoka kuhubiri na wanamsimulia Yesu mambo yote ambayo wamefanya na kufundisha. Yesu anaona kwamba mitume wamechoka, kwa hiyo anawaambia waende pamoja naye ili ‘wapumzike kidogo.’ Kwa hiyo wanapanda mashua na kwenda mahali patulivu. Watu wanawafuata, wakikimbia kando ya bahari, na muda si muda wanawafikia. Yesu anafanya nini? Biblia inasema hivi: “Akaona umati mkubwa, lakini akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:31-34) Kwa sababu anawasikitikia watu, Yesu anaendelea kuhubiri habari njema ajapokuwa mchovu. Ni wazi kwamba Yesu anawasikitikia sana watu hao. Anawahurumia.

9. Simulizi la Marko sura ya 6 linatufunza nini kuhusu nia inayofaa ya kuhubiri?

9 Tunajifunza nini kutokana na simulizi hilo? Tukiwa Wakristo tunahisi tuna wajibu wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Tunatambua jukumu letu la kutangaza habari njema, kwa kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe.” (1 Timotheo 2:4) Hata hivyo, hatuhubiri ili kutimiza wajibu tu, bali pia tunahubiri kwa sababu ya huruma. Ikiwa kama Yesu tunawahurumia watu sana, moyo wetu utatuchochea kufanya yote tuwezayo kuwahubiria habari njema. (Mathayo 22:39) Kuwa na nia nzuri ya kushiriki katika huduma kutatuchochea tuhubiri habari njema bila kuacha.

Ujumbe Wetu Ni Habari Njema za Ufalme wa Mungu

10, 11. (a) Isaya anaelezaje ujumbe ambao tunahubiri? (b) Yesu aliletaje habari njema za jambo bora, na watumishi wa Mungu katika nyakati zetu wameigaje kielelezo cha Yesu?

10 Tuchunguze jambo la pili kuhusu huduma yetu, yaani, ujumbe wetu. Tunahubiri nini? Nabii Isaya alitoa maelezo haya mazuri sana kuhusu ujumbe ambao tunatangaza: “Jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye anayeleta habari njema, yeye anayetangaza amani, yeye anayeleta habari njema za jambo bora, yeye anayetangaza wokovu, yeye anayeuambia Sayuni: ‘Mungu wako amekuwa mfalme!’”—Isaya 52:7.

11 Maneno makuu katika andiko hilo, “Mungu wako amekuwa mfalme,” yanatukumbusha ujumbe ambao tunapaswa kutangaza, yaani, habari njema za Ufalme wa Mungu. (Marko 13:10) Ona pia kwamba mstari huo unakazia ubora wa ujumbe wetu. Isaya anatumia maneno kama vile “wokovu,” “habari njema,” “amani,” na “jambo bora.” Katika karne ya kwanza W.K., miaka mingi baada ya siku za Isaya, Yesu Kristo alitimiza unabii huo kwa njia ya pekee alipoweka kielelezo katika kutangaza kwa bidii habari njema za jambo bora, yaani, kuja kwa Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Katika nyakati zetu, hasa tangu mwaka wa 1919, Mashahidi wa Yehova wameiga kielelezo cha Yesu kwa kutangaza kwa bidii habari njema za Ufalme wa Mungu uliosimamishwa na baraka ambazo utaleta.

12. Habari njema za Ufalme zina matokeo gani kwa wale wanaozikubali?

12 Habari njema za Ufalme zina matokeo gani kwa wale wanaozikubali? Leo habari njema zinawafariji watu na kuwapa tumaini kama ilivyokuwa katika siku za Yesu. (Waroma 12:12; 15:4) Zinawapa watu wanyoofu tumaini kwa sababu wanajifunza kwamba kuna sababu nzuri za kutarajia hali bora wakati ujao. (Mathayo 6:9, 10; 2 Petro 3:13) Tumaini hilo huwasaidia sana watu wanaomwogopa Mungu waendelee kuwa na mtazamo mzuri. Mtunga-zaburi anasema kwamba ‘hawataogopa hata habari mbaya.’—Zaburi 112:1, 7.

Ujumbe “Unaofunga Majeraha ya Waliovunjika Moyo”

13. Nabii Isaya anataja baraka gani ambazo wale wanaokubali habari njema wanapata sasa?

13 Zaidi ya hayo, wale wanaokubali habari njema tunazohubiri hupata kitulizo na baraka sasa. Jinsi gani? Nabii Isaya alitaja baadhi ya baraka hizo alipotabiri hivi: “Roho ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova iko juu yangu, kwa sababu Yehova amenitia mafuta niwatangazie wapole habari njema. Amenituma kufunga majeraha ya waliovunjika moyo, kutangaza uhuru kwa wale waliochukuliwa mateka na kufunguliwa kabisa kwa macho hata kwa walio wafungwa; kutangaza mwaka wa nia njema upande wa Yehova na siku ya kisasi upande wa Mungu wetu; kuwafariji wote wanaoomboleza.”—Isaya 61:1, 2; Luka 4:16-21.

14. (a) Maneno “kufunga majeraha ya waliovunjika moyo” yanaonyesha nini kuhusu ujumbe wa Ufalme? (b) Tunamwigaje Yehova katika kuwajali waliovunjika moyo?

14 Unabii huo unaonyesha kwamba kwa kuhubiri habari njema, Yesu ‘angefunga majeraha ya waliovunjika moyo.’ Isaya anatumia mfano mzuri kama nini! Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘funga majeraha’ “mara nyingi linatumiwa kuhusu ‘kufunga’ bendeji, na hivyo kutibu au kuponya waliojeruhiwa.” Muuguzi mwenye kujali anaweza kufunga bendeji au kitambaa kwenye kiungo cha mwili kilichojeruhiwa ili kukitegemeza. Vivyo hivyo, wahubiri wenye kujali wanapohubiri ujumbe wa Ufalme, wanawategemeza wale wote wanaokubali ujumbe huo ambao wanateseka kwa njia fulani. Na wanapowategemeza wenye uhitaji, wanamwiga Yehova katika kuwajali watu wengine. (Ezekieli 34:15, 16) Mtunga-zaburi anasema hivi kumhusu Mungu: “Anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”—Zaburi 147:3.

Jinsi Ujumbe wa Ufalme Unavyobadili Maisha ya Watu

15, 16. Simulia mambo yaliyoonwa yanayoonyesha jinsi ujumbe wa Ufalme unavyowategemeza na kuwaimarisha wenye uhitaji.

15 Mambo mengi yaliyoonwa yanaonyesha jinsi ujumbe wa Ufalme unavyowategemeza na kuwaimarisha wale waliovunjika moyo. Fikiria kisa cha Oreanna, mwanamke mzee kutoka Amerika Kusini ambaye alikuwa amepoteza kabisa hamu ya kuishi. Shahidi mmoja wa Yehova alianza kumtembelea Oreanna na kumsomea Biblia na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. * Mwanzoni, mwanamke huyo aliyeshuka moyo alisikiliza usomaji huo akiwa amelala kitandani huku akiwa amefumba macho yake, naye alikuwa akishusha pumzi kwa nguvu mara kwa mara. Hata hivyo, baada ya muda alianza kujitahidi kuketi kitandani wakati wa usomaji huo. Baadaye, alianza kuketi kwenye kiti sebuleni na kumngoja mwalimu wake wa Biblia. Halafu, mwanamke huyo akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Jumba la Ufalme. Alitiwa moyo na yale aliyojifunza kwenye mikutano hiyo, naye akaanza kuwapa vichapo vya Biblia watu wote waliopita karibu na nyumba yake. Kisha, Oreanna akabatizwa akiwa na umri wa miaka 93 na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ujumbe wa Ufalme ulimsaidia kupata tena na hamu ya kuishi.—Methali 15:30; 16:24.

16 Ujumbe wa Ufalme unawategemeza sana hata wale ambao wanajua kwamba maisha yao yatakatishwa na ugonjwa. Kwa mfano, fikiria kisa cha Maria kutoka Ulaya Magharibi. Alikuwa na ugonjwa unaosababisha kifo na hakuwa na matumaini yoyote. Alikuwa ameshuka moyo kabisa alipotembelewa na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, alipojifunza kuhusu makusudi ya Mungu, maisha yake yakawa na maana tena. Alibatizwa na akawa mwenye bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Katika miaka miwili ya mwisho ya maisha yake, alikuwa mwenye shangwe nyingi na tumaini. Maria alikufa akiwa na tumaini thabiti la ufufuo.—Waroma 8:38, 39.

17. (a) Ujumbe wa Ufalme unabadilije maisha ya wale wanaoukubali? (b) Wewe binafsi umejionea kwa njia gani kwamba Yehova “anawainua wote ambao wameinama chini”?

17 Mambo hayo yanathibitisha kwamba ujumbe wa Ufalme unaweza kubadili maisha ya watu ambao wanataka kujua kweli za Biblia. Watu ambao wanaomboleza kifo cha mpendwa hupata nguvu tena wanapojifunza kuhusu tumaini la ufufuo. (1 Wathesalonike 4:13) Watu maskini ambao hujitahidi sana kulisha familia zao hupata tena heshima na ujasiri wanapojifunza kwamba Yehova hatawaacha kamwe ikiwa watakuwa washikamanifu kwake. (Zaburi 37:28) Kwa msaada wa Yehova, watu wengi walioshuka moyo hupata nguvu hatua kwa hatua ili kukabiliana na ugonjwa huo na hata baadhi yao hupona. (Zaburi 40:1, 2) Kwa kweli, hivi sasa Yehova anatumia nguvu za Neno lake ‘kuwainua wote ambao wameinama chini.’ (Zaburi 145:14) Tunapoona jinsi habari njema za Ufalme zinavyowafariji waliovunjika moyo katika eneo letu na katika kutaniko la Kikristo, jambo hilo hutukumbusha tena na tena kwamba tuna habari bora zaidi leo!—Zaburi 51:17.

“Dua Yangu kwa Mungu kwa Ajili Yao”

18. Paulo alihisije Wayahudi walipokataa habari njema, na kwa nini?

18 Watu wengi hukataa ujumbe wetu licha ya kwamba una habari bora zaidi. Itikio lao linaweza kutufanya tuhisije? Tunaweza kuhisi kama mtume Paulo. Aliwahubiria Wayahudi mara nyingi, lakini wengi wao wakakataa ujumbe wa wokovu. Paulo aliumia sana moyoni walipokataa. Alikiri hivi: “Nina huzuni kubwa na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu.” (Waroma 9:2) Paulo aliwahurumia Wayahudi ambao aliwahubiria. Alihuzunika sana kuona wakikataa habari njema.

19. (a) Kwa nini ni jambo linaloeleweka kwamba nyakati nyingine tunaweza kuhisi tumevunjika moyo? (b) Ni nini kilichomsaidia Paulo kuendelea na kazi yake ya kuhubiri?

19 Sisi pia tunahubiri habari njema kwa sababu ya huruma. Kwa hiyo, ni jambo linaloeleweka kwamba tunaweza kuvunjika moyo watu wengi wanapokataa ujumbe wa Ufalme. Tunahisi hivyo kwa sababu tunahangaikia kikweli hali ya kiroho ya wale tunaowahubiria. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka mfano wa mtume Paulo. Ni nini kilichomsaidia kuendelea na kazi yake ya kuhubiri? Ingawa alihuzunika na kuumia moyoni Wayahudi walipokataa habari njema, Paulo hakukata tamaa na kufikiri kwamba Wayahudi wote hawangeweza kusaidiwa. Alitumaini kwamba baadhi yao wangemkubali Kristo. Kwa hiyo, Paulo alieleza hisia zake kuhusu Myahudi mmoja-mmoja aliposema hivi: “Nia njema ya moyo wangu na dua yangu kwa Mungu kwa ajili yao, kwa kweli, ni kwa ajili ya wokovu wao.”—Waroma 10:1.

20, 21. (a) Tunawezaje kumwiga Paulo katika huduma yetu? (b) Makala inayofuata itazungumzia jambo gani kuhusu huduma yetu?

20 Ona mambo mawili ambayo Paulo alikazia. Nia ya moyo wake ilikuwa kwamba watu fulani wapate wokovu, naye alimwomba Mungu kwa ajili yao. Leo tunamwiga Paulo. Tunadumisha nia ya moyoni ya kumtafuta mtu yeyote ambaye huenda akawa na mwelekeo unaofaa kuelekea habari njema. Tunasali daima kwa Yehova tupate watu wa aina hiyo ili tuweze kuwasaidia wafuate njia ya wokovu.—Methali 11:30; Ezekieli 33:11; Yohana 6:44.

21 Hata hivyo, ili kuwapelekea watu wengi iwezekanavyo ujumbe wa Ufalme, hatupaswi kukazia tu uangalifu kwa nini tunahubiri na kile tunachohubiri, bali pia jinsi tunavyohubiri. Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Makala hii itazungumzia mambo mawili ya kwanza. Makala ya pili itazungumzia jambo la tatu.

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Umejifunza Nini?

• Tunashiriki katika huduma kwa sababu zipi?

• Tunahubiri ujumbe gani mkuu?

• Wale wanaokubali ujumbe wa Ufalme wanapata baraka zipi?

• Ni nini kitakachotusaidia kuendelea na huduma yetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ujumbe wa Ufalme huwaimarisha waliovunjika moyo

[Picha katika ukurasa wa 20]

Sala hutusaidia kuvumilia katika huduma yetu