Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mambo Kwisha”

“Mambo Kwisha”

“Mambo Kwisha”

KATIKA mwaka wa 2002, Mashahidi wa Yehova walikuwa na kusanyiko la wilaya katika jiji la Mbandaka, kaskazini-magharibi mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Wakati Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilipotolewa katika Lingala kwenye kusanyiko hilo, waliokuwepo waliruka kwa shangwe, na baadhi yao wakatokwa na machozi. Baadaye, watu walikimbia jukwaani ili kuona Biblia hiyo mpya, huku wakipaaza sauti hivi: “Basuki, Basambwe,” maana yake: “Mambo kwisha! Makanisa yameaibishwa!”

Kwa nini walisisimuka sana hivyo, na kwa nini walisema maneno hayo? Katika sehemu fulani za Mbandaka, Mashahidi wa Yehova hawakuweza kupata Biblia za Lingala. Kwa nini? Kwa sababu makanisa yalikataa kuwauzia Mashahidi wa Yehova Biblia. Mashahidi walilazimika kuwaomba watu wengine wakawanunulie Biblia. Sasa walifurahi sana kwa sababu makanisa hayataweza tena kuwazuia wasipate Biblia.

Zaidi ya kuwafaidi Mashahidi wa Yehova, tafsiri hiyo mpya itawafaidi pia watu kwa jumla. Mtu mmoja aliyesikiliza programu hiyo ya kusanyiko akiwa nyumbani kwake kupitia vipaaza-sauti, aliiandikia hivi ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova: “Ninafurahi sana kwamba Biblia hii imetolewa. Itatufundisha mambo mengi. Mimi si Shahidi wa Yehova, lakini ninasubiri kwa hamu Biblia hiyo ambayo mmechapisha.”

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana sasa ikiwa nzima katika lugha 33, nayo tafsiri ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo inapatikana katika lugha nyingine 19, kutia ndani Lingala. Unaweza kumwomba Shahidi wa Yehova akueleze jinsi unavyoweza kupata Biblia hiyo bora.