Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kwanza cha Wafalme

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kwanza cha Wafalme

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Kwanza cha Wafalme

“WAADILIFU wanapokuwa wengi, watu hushangilia; lakini mtu yeyote mwovu anapotawala, watu huugua.” (Methali 29:2) Kitabu cha Kwanza cha Wafalme kinaonyesha wazi kwamba methali hiyo ni ya kweli. Kinasimulia maisha ya Sulemani, ambaye wakati wa utawala wake taifa la Israeli la kale linakuwa na usalama na mafanikio makubwa. Kitabu cha Kwanza cha Wafalme kina masimulizi yanayoonyesha jinsi taifa lilivyogawanyika baada ya kifo cha Sulemani na kuhusu wafalme 14 waliotawala baada yake. Baadhi yao walitawala Israeli na wengine walitawala Yuda. Ni wafalme wawili tu kati ya wafalme hao walioendelea kuwa waaminifu kwa Yehova. Zaidi ya hayo, kitabu hicho kinaelezea utendaji wa manabii sita, kutia ndani Eliya.

Kitabu hicho ambacho kiliandikwa na nabii Yeremia akiwa Yerusalemu na Yuda, kinazungumzia kipindi cha miaka 129 hivi, kuanzia mwaka wa 1040 K.W.K. hadi 911 K.W.K. Inaonekana kwamba Yeremia alipokuwa akiandika kitabu hicho alitumia maandishi ya kale, kama vile “kitabu cha mambo ya Sulemani.” Maandishi hayo ya kale hayapatikani tena.—1 Wafalme 11:41; 14:19; 15:7.

MFALME MWENYE HEKIMA ALETA AMANI NA MAFANIKIO

(1 Wafalme 1:1–11:43)

Kitabu cha Kwanza cha Wafalme kinaanza kwa kusimulia jinsi Adoniya, mwana wa Mfalme Daudi, anavyojaribu kunyakua ufalme kutoka kwa baba yake. Nabii Nathani anachukua hatua haraka na kuharibu njama hiyo, kisha Sulemani, mwana wa Daudi, anawekwa kuwa mfalme. Yehova anapendezwa na ombi la mfalme huyo mpya, naye anampa “moyo wenye hekima na wenye uelewaji” pamoja na “utajiri na utukufu.” (1 Wafalme 3:12, 13) Hekima ya mfalme huyo haina kifani, nao utajiri wake hauwezi kulinganishwa na wa mwingine yeyote. Taifa la Israeli linafurahia kipindi cha amani na mafanikio.

Sulemani anakamilisha miradi mbalimbali ya ujenzi, kutia ndani hekalu la Yehova na majengo ya serikali. Ikiwa Sulemani ataendelea kuwa mtiifu, Yehova anamhakikishia hivi: “Nitakifanya imara kiti cha ufalme wako juu ya Israeli mpaka wakati usio na kipimo.” (1 Wafalme 9:4, 5) Pia, Mungu wa kweli anamwonya kuhusu matokeo ya kutotii. Hata hivyo, Sulemani anaoa wake wengi wageni. Kwa sababu ya kushawishiwa nao, Sulemani anageukia ibada ya uwongo anapozeeka. Yehova anatabiri kwamba ufalme wake utagawanyika. Katika mwaka wa 997 K.W.K., Sulemani anakufa, baada ya kutawala kwa miaka 40. Rehoboamu, mwana wake, anakuwa mfalme.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:5—Kwa nini Adoniya alijaribu kunyakua utawala wakati Daudi alipokuwa hai? Biblia haisemi. Hata hivyo, tunaweza kukata kauli kwamba Adoniya alifikiri ana haki ya kuwa mfalme kwa sababu sasa yeye ndiye aliyekuwa mwana mkubwa zaidi kati ya wana wa Daudi waliosalia. Hiyo ni kwa sababu ndugu zake wakubwa Amnoni na Absalomu walikuwa wamekufa na huenda Kileabu aliyekuwa pia mwana wa Daudi alikuwa amekufa vilevile. (2 Samweli 3:2-4; 13:28, 29; 18:14-17) Kwa sababu alikuwa amemwomba Yoabu mkuu wa majeshi na Abiathari kuhani mkuu mwenye uvutano wamuunge mkono, inaelekea Adoniya alikuwa na uhakika kwamba atafaulu. Biblia haisemi ikiwa Adoniya alijua kwamba Daudi alikusudia Sulemani arithi ufalme. Hata hivyo, Adoniya alipofanya “dhabihu” fulani hakumkaribisha Sulemani na wengine waliokuwa waaminifu kwa Daudi. (1 Wafalme 1:9, 10) Jambo hilo linaonyesha kwamba alimwona Sulemani kuwa mpinzani wake.

1:49-53; 2:13-25—Kwa nini Sulemani alimuua Adoniya baada ya kumsamehe? Wakati Adoniya alipomwambia Bath-sheba amwombe mfalme kwa niaba yake ili apewe Abishagi kuwa mke wake, Bath-sheba hakutambua lengo la Adoniya lakini Sulemani alilitambua. Ingawa Daudi hakuwa amelala na Abishagi, msichana huyo mrembo alionwa kuwa suria wake. Kulingana na desturi za wakati huo, Abishagi alipaswa kuwa mali ya yule aliyekuwa na haki ya kumrithi Daudi. Huenda Adoniya alifikiri kwamba kwa kumfanya Abishagi kuwa mke wake, angeweza kujaribu tena kupata ufalme. Sulemani alipotambua kwamba ombi la Adoniya lilionyesha tamaa ya kunyakua ufalme, alibatilisha uamuzi wake wa kumsamehe.

6:37–8:2—Hekalu lilizinduliwa wakati gani? Hekalu lilikamilishwa katika mwezi wa nane wa mwaka wa 1027 K.W.K., ambao ulikuwa mwaka wa 11 wa utawala wa Sulemani. Inaonekana kwamba kazi ya kuleta vyombo na kufanya matayarisho mengine ilichukua miezi 11. Inaonekana uzinduzi ulifanywa katika mwezi wa saba wa mwaka wa 1026 K.W.K. Inaelekea masimulizi hayo yanataja miradi mingine ya ujenzi iliyofanywa baada ya hekalu kukamilika na kabla ya kuzinduliwa, ili kutoa habari kamili kuhusu kazi za ujenzi.—2 Mambo ya Nyakati 5:1-3.

9:10-13—Je, tendo la Sulemani la kumpa Mfalme Hiramu wa Tiro zawadi ya majiji 20 katika nchi ya Galilaya lilipatana na Sheria ya Musa? Huenda Sheria inayotajwa kwenye Mambo ya Walawi 25:23, 24 ilihusu maeneo yaliyokaliwa tu na Waisraeli. Inawezekana kwamba majiji ambayo Sulemani alimpa Hiramu yalikaliwa na watu wasio Waisraeli, ijapokuwa yalikuwa ndani ya Nchi ya Ahadi. (Kutoka 23:31) Huenda tendo hilo pia lilionyesha kwamba Sulemani hakufuata Sheria kikamili, kama ilivyokuwa wakati ambapo ‘aliongeza farasi kwa ajili yake’ na kuoa wanawake wengi. (Kumbukumbu la Torati 17:16, 17) Vyovyote vile, Hiramu hakuridhishwa na zawadi hiyo. Labda majiji hayo hayakutunzwa vizuri na wakaaji wake wapagani, au huenda hayakuwa mahali panapofaa.

11:4—Je, Sulemani alikosa uaminifu kwa sababu alivurugika akili alipozeeka? Haielekei ilikuwa hivyo. Sulemani alikuwa kijana alipoanza kutawala, na ijapokuwa alitawala kwa miaka 40, hakuwa mzee sana alipokufa. Isitoshe, hakuacha kabisa kumwabudu Yehova. Inaonekana alijaribu kuchanganya imani.

Mambo Tunayojifunza:

2:26, 27, 35. Mambo ambayo Yehova hutabiri hutimia sikuzote. Wakati Abiathari, aliyekuwa wa ukoo wa Eli, alipoondolewa kuwa kuhani, hilo lilitimiza “neno la Yehova alilokuwa amesema juu ya nyumba ya Eli.” Andiko la Hesabu 25:10-13 lilitimizwa wakati Sadoki, aliyekuwa wa ukoo wa Finehasi, alipowekwa mahali pa Abiathari.—Kutoka 6:25; 1 Samweli 2:31; 3:12; 1 Mambo ya Nyakati 24:3.

2:37, 41-46. Ni hatari sana kufikiri kwamba tunaweza kuepuka adhabu tunapovunja sheria! Wale wanaoacha kimakusudi ‘barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima’ watapata matokeo mabaya ya uamuzi wao usio wa hekima.—Mathayo 7:14.

3:9, 12-14. Yehova hujibu sala zinazotoka moyoni za watumishi wake wanaoomba hekima, uelewaji, na mwongozo ili waweze kumtumikia.—Yakobo 1:5.

8:22-53. Sulemani alionyesha kutoka moyoni uthamini wake kwa Yehova, Mungu wa fadhili zenye upendo, anayetimiza ahadi, na ambaye ni Msikiaji wa sala! Kutafakari maneno ya sala ya uzinduzi ya Sulemani kutatusaidia tuthamini zaidi mambo hayo na mengineyo kuhusu utu wa Mungu.

11:9-14, 23, 26. Sulemani alipokosa kutii katika miaka ya baadaye, Yehova alisimamisha wapinzani. Mtume Petro anasema: “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”—1 Petro 5:5.

11:30-40. Mfalme Sulemani alijaribu kumuua Yeroboamu kwa sababu ya yale ambayo Ahiya alikuwa ametabiri kumhusu Yeroboamu. Hiyo ilikuwa tofauti kabisa na jinsi ambavyo mfalme huyo alitenda miaka 40 hivi mapema, wakati alipokataa kulipiza kisasi juu ya Adoniya na waasi wengine! (1 Wafalme 1:50-53) Mtazamo wake ulibadilika kwa sababu alimwacha Yehova.

UFALME WAGAWANYIKA

(1 Wafalme 12:1–22:53)

Yeroboamu na watu wanamwendea Mfalme Rehoboamu ili kumwomba awapunguzie mzigo mzito waliowekewa na baba yake, Sulemani. Badala ya kukubali ombi lao, Rehoboamu anatisha kufanya mzigo wao kuwa mzito zaidi. Makabila kumi yanaasi na kumfanya Yeroboamu awe mfalme juu yao. Ufalme unagawanyika. Rehoboamu anatawala ufalme wa kusini wenye makabila mawili, yaani, Yuda na Benyamini, naye Yeroboamu anatawala ufalme wa kaskazini wa Israeli wenye makabila kumi.

Ili kuwazuia watu wasiende Yerusalemu kuabudu, Yeroboamu anasimamisha ndama wawili wa dhahabu, mmoja huko Dani na mwingine huko Betheli. Baadhi ya wafalme wanaotawala Israeli baada ya Yeroboamu ni Nadabu, Baasha, Ela, Zimri, Tibni, Omri, Ahabu, na Ahazia. Nao wafalme wanaotawala Yuda baada ya Rehoboamu ni Abiyamu, Asa, Yehoshafati, na Yehoramu. Manabii wanaotabiri katika siku za wafalme hao wanatia ndani Ahiya, Shemaya, na mtu mwingine wa Mungu asiyetajwa kwa jina, na vilevile Yehu, Eliya, na Mikaya.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

18:21—Kwa nini watu walinyamaza wakati Eliya alipowauliza kama watamfuata Yehova au Baali? Huenda walitambua kwamba walikuwa wameshindwa kumpa Yehova ujitoaji kamili ambao anadai na hivyo wakahisi wana hatia. Au huenda dhamiri zao zilikuwa zimekufa ganzi hivi kwamba hawakuona ni kosa kumwabudu Baali huku wakidai kuwa waabudu wa Yehova. Ni baada tu ya Yehova kuonyesha nguvu zake ndipo waliposema: “Yehova ndiye Mungu wa kweli! Yehova ndiye Mungu wa kweli!”—1 Wafalme 18:39.

20:34—Baada ya Yehova kumpa Ahabu ushindi dhidi ya Wasiria, kwa nini Ahabu hakumuua Ben-hadadi, mfalme wao? Badala ya kumuua Ben-hadadi, Ahabu alifanya agano pamoja naye ambalo lingemwezesha kupata barabara za Damasko, mji mkuu wa Siria. Inaonekana masoko yangeanzishwa kwenye barabara hizo. Mapema, baba ya Ben-hadadi alikuwa amejipatia barabara za Samaria kwa ajili ya biashara. Hivyo, Ben-hadadi aliachiliwa huru ili Ahabu aweze kuanzisha biashara huko Damasko.

Mambo Tunayojifunza:

12:13, 14. Tunapofanya maamuzi muhimu maishani, tunapaswa kuomba mashauri ya watu wenye hekima na waliokomaa ambao wanayajua Maandiko na kuheshimu sana kanuni za Mungu.

13:11-24. Shauri au dokezo linalotiliwa shaka linapaswa kuchunguzwa kwa kutumia mwongozo bora wa Neno la Mungu hata ikiwa limetoka kwa mwamini mwenzetu mwenye nia njema.—1 Yohana 4:1.

14:13. Yehova hutuchunguza ili kuona mema ndani yetu. Hata mema hayo yawe madogo kadiri gani, anaweza kuyakuza tunapojitahidi tuwezavyo kumtumikia.

15:10-13. Tunapaswa kukataa kwa ujasiri uasi-imani na badala yake tuendeleze ibada ya kweli.

17:10-16. Yule mjane wa Sarefathi alimtambua Eliya kuwa nabii na kumtendea kama nabii, naye Yehova akambariki kwa matendo yake ya imani. Leo, Yehova pia hutambua matendo yetu ya imani, naye huwapa thawabu wale wanaounga mkono kazi ya Ufalme kwa njia mbalimbali.—Mathayo 6:33; 10:41, 42; Waebrania 6:10.

19:1-8. Tunapopingwa vikali, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia.—2 Wakorintho 4:7-9.

19:10, 14, 18. Waabudu wa kweli hawako peke yao kamwe. Yehova na vilevile ndugu zao ulimwenguni pote wako pamoja nao.

19:11-13. Yehova hawakilishwi na nguvu za asili.

20:11. Ben-hadadi alipojigamba kwamba ataharibu Samaria, mfalme wa Israeli alimjibu hivi: “Mtu anayejifunga mshipi [wa mavazi yake ya vita anapojitayarishia vita] asijisifu kama yeye anayejifungua mshipi” wa mavazi yake ya vita baada ya kutoka vitani. Tunapopata daraka jipya, tunapaswa kuepuka kujiamini kupita kiasi kama vile mtu mwenye kujigamba.—Methali 27:1; Yakobo 4:13-16.

Kinatufaidi Sana

Musa aliporejelea wakati ambapo Sheria ilitolewa kwenye Mlima Sinai, aliwaambia wana wa Israeli hivi: “Tazama, ninaweka mbele yenu leo baraka na laana: baraka, ikiwa mtatii amri za Yehova Mungu wenu ninazowaamuru ninyi leo; na laana, ikiwa hamtatii amri za Yehova Mungu wenu nanyi mgeuke kutoka katika njia ambayo ninawaamuru ninyi juu yake leo.”—Kumbukumbu la Torati 11:26-28.

Kitabu cha Kwanza cha Wafalme kinatuonyesha waziwazi ukweli huo muhimu! Kama tulivyoona, kitabu hicho pia kinatufundisha mambo mengine muhimu. Bila shaka, ujumbe wake uko hai na una nguvu.—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Hekalu na majengo mengine yaliyojengwa na Sulemani

[Picha katika ukurasa wa 30, 31]

Baada ya Yehova kuonyesha nguvu zake, watu walipaaza sauti hivi: “Yehova ndiye Mungu wa kweli!”