Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nafurahia Sehemu Yangu ya Kufundisha Biblia Duniani Kote

Nafurahia Sehemu Yangu ya Kufundisha Biblia Duniani Kote

Simulizi la Maisha

Nafurahia Sehemu Yangu ya Kufundisha Biblia Duniani Kote

LIMESIMULIWA NA ANNA MATHEAKIS

Meli ilikuwa inaungua. Kama ingezama, ningekufa maji ndani ya meli hiyo iliyokuwa na urefu wa meta 171. Nilijitahidi kufa na kupona nisife maji, huku nikikabiliana na mawimbi makali. Ili nisizame, ilinibidi kushikilia jaketi ya kujiokolea iliyokuwa imevaliwa na mwanamke mwingine. Nilimwomba Mungu anipe nguvu na ujasiri. Sikuwa na lingine la kufanya.

MKASA huo ulitokea mwaka wa 1971, nilipokuwa nikirudi Italia, nchi ya tatu ambako nilikuwa nimetumwa kutumika nikiwa mmishonari. Nilipoteza karibu kila kitu katika mkasa huo. Lakini sikupoteza mambo yaliyo muhimu zaidi, yaani, uhai, ndugu Wakristo wenye upendo, na pendeleo la kumtumikia Yehova. Nilikuwa nimemtumikia Yehova katika mabara matatu, na mkasa huo ulikuwa tukio moja tu katika maisha yangu yenye mambo mengi.

Nilizaliwa mwaka wa 1922. Familia yetu iliishi Rām Allāh, kilometa 16 hivi kaskazini ya Jerusalem. Wazazi wangu walizaliwa katika kisiwa cha Krete, lakini baba yangu alilelewa Nazareti. Mimi ndiye niliyekuwa mtoto wa mwisho kati ya wavulana watatu na wasichana wawili. Tulifadhaishwa sana na kifo cha kaka yangu wa pili, aliyekufa maji kwenye Mto Yordani akiwa kwenye matembezi ya shule. Baada ya msiba huo, mama yangu alikataa kuishi Rām Allāh, hivyo tukahamia Athens, Ugiriki, nikiwa na umri wa miaka mitatu.

Familia Yetu Yapata Kweli ya Biblia

Muda mfupi baada ya kuhamia Ugiriki, kaka yangu mkubwa Nikos, aliyekuwa na umri wa miaka 22, alihubiriwa na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Alifurahia sana kujifunza Biblia, naye alihubiri kwa bidii sana. Jambo hilo lilimkasirisha baba yangu sana, hivyo akamfukuza Nikos nyumbani. Hata hivyo, wakati baba yangu aliposafiri kwenda Palestina, mimi, mama yangu, na dada yangu tulikuwa tukiandamana na Nikos kwenda kwenye mikutano ya Kikristo. Bado ninakumbuka vizuri jinsi mama yangu alivyozungumza kwa shauku kuhusu mambo aliyojifunza kwenye mikutano hiyo. Lakini muda mfupi baadaye, alikufa kwa kansa akiwa na umri wa miaka 42. Katika kipindi hicho kigumu, dada yangu Ariadne alijitwika jukumu la kuitunza familia, naye alifanya hivyo kwa upendo. Ingawa alikuwa na umri mdogo, kwa miaka mingi yeye alikuwa kama mama kwangu.

Baba yangu alikuwa akinipeleka katika Kanisa Othodoksi alipokuwa Athens, na baada ya kifo chake, niliendelea kwenda kanisani, ingawa si kwa ukawaida. Baadaye niliacha kanisa hilo kwa kuwa waumini wake hawakuishi kupatana na mapenzi ya Mungu.

Baada ya baba yangu kufa, nilipata kazi ya kudumu katika wizara ya fedha. Lakini ndugu yangu alikuwa ameamua kutumia maisha yake kuhubiri kuhusu Ufalme, naye alihubiri kwa miaka mingi huko Ugiriki. Alihamia Cyprus mwaka wa 1934. Wakati huo hakukuwa Mashahidi wengine wa Yehova waliobatizwa katika kisiwa hicho, kwa hiyo akawa na pendeleo la kuendeleza kazi ya kuhubiri huko. Alimwoa Galatia, ambaye pia alianza utumishi wa wakati wote na kuendelea kwa miaka mingi. * Mara nyingi Nikos alitutumia magazeti na vitabu vinavyoifafanua Biblia, lakini hatukuvisoma. Alikaa Cyprus hadi kifo chake.

Kuifanya Kweli ya Biblia Iwe Mali Yangu

George Douras, rafiki ya Nikos ambaye alikuwa Shahidi mwenye bidii huko Athens, alitutembelea mwaka wa 1940 na kutualika kujiunga na kikundi kidogo kilichokuwa kikijifunzia Biblia nyumbani kwake. Tulikubali mwaliko huo kwa furaha, na muda si muda tukaanza kuwaeleza wengine mambo tuliyokuwa tukijifunza. Mimi na dada yangu tulichochewa na yale tuliyojifunza katika Biblia na kujiweka wakfu kwa Yehova. Ariadne alibatizwa mwaka wa 1942, nami nikabatizwa mwaka wa 1943.

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoisha, Nikos alitualika Cyprus, kwa hiyo tukahamia Nicosia mwaka wa 1945. Kazi ya kuhubiri haikuwa imezuiwa huko Cyprus kama ilivyokuwa nchini Ugiriki. Tulihubiri nyumba kwa nyumba na pia barabarani.

Miaka miwili baadaye, Ariadne alilazimika kurudi Ugiriki. Akiwa huko alikutana na ndugu ambaye angekuwa mume wake baadaye, hivyo akabaki Athens. Punde si punde, dada yangu na mume wake walinitia moyo nirudi Ugiriki na kuanza utumishi wa wakati wote katika jiji la Athens. Kwa kuwa nilikuwa na mradi wa kuwa painia, nilirudi Athens, ambako uhitaji ulikuwa mkubwa zaidi.

Milango Mipya ya Utendaji Yafunguliwa

Nilianza utumishi wa upainia Novemba 1, 1947, na nilihubiri muda wa saa 150 kila mwezi. Kutaniko letu lilikuwa na eneo kubwa la kuhubiri, na ilinibidi kutembea sana. Hata hivyo, nilipata baraka nyingi. Mara nyingi polisi walimkamata Shahidi yeyote waliyempata akihubiri au akihudhuria mikutano ya Kikristo, kwa hiyo nilikamatwa baada ya muda mfupi.

Nilishtakiwa kwa kosa la kushawishi watu wageuze imani yao. Hilo lilikuwa kosa baya sana wakati huo. Nilifungwa kifungo cha miezi miwili kwenye Gereza la Wanawake la Averof, huko Athens. Huko nilikutana na Shahidi mwingine mwanamke na ingawa tulikuwa gerezani, tulifurahia ushirika wa Kikristo wenye kujenga. Baada ya kumaliza kifungo changu, niliendelea na utumishi wa upainia kwa furaha. Wengi kati ya wale niliojifunza Biblia nao wanaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu na jambo hilo huniletea shangwe nyingi.

Katika mwaka wa 1949, nilialikwa kuhudhuria darasa la 16 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) huko Marekani, ambako watumishi wa wakati wote huzoezwa kwa ajili ya kazi ya umishonari. Mimi na watu wa familia yetu tulifurahi sana. Niliamua kuhudhuria kusanyiko la kimataifa huko New York City mwaka wa 1950, kisha kujiunga na Shule ya Gileadi.

Nilipofika Marekani, kwa miezi michache nilipata pendeleo la kutunza vyumba kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova huko New York City. Hali kwenye makao makuu ilikuwa safi, yenye kupendeza, na yenye kujenga, nao ndugu na dada walikuwa wenye furaha. Sitasahau miezi sita niliyokaa huko. Kisha wakati ukafika wa kujiunga na Shule ya Gileadi. Tulijifunza mambo mengi sana kwa muda wa miezi mitano ambayo ilipita upesi. Sisi wanafunzi tulitambua ubora na manufaa ya kujua Maandiko, furaha yetu ikaongezeka, nasi tukawa na hamu nyingi ya kuwafundisha wengine kweli ambayo itawawezesha kupata uhai.

Nilikotumwa Kwanza Nikiwa Mmishonari

Kwenye Shule ya Gileadi, tuliruhusiwa kuchagua wale ambao tungetumika pamoja nao katika kazi ya umishonari kabla ya kutumwa. Nilitumwa pamoja na Ruth Hemmig (sasa anaitwa Bosshard), dada mwenye sifa bora. Mimi na Ruth tulifurahi sana tulipotumwa Istanbul, Uturuki, nchi iliyo katikati ya Asia na Ulaya! Tulijua kwamba kazi ya kuhubiri haikuruhusiwa kisheria katika nchi hiyo, lakini tulikuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatutegemeza.

Istanbul ni jiji maridadi la kimataifa. Huko tulipata masoko yaliyojaa watu, aina bora zaidi za mapishi ulimwenguni, majumba ya ukumbusho yenye vitu vyenye kuvutia, majengo na mwambao wenye kupendeza. Lakini jambo muhimu zaidi ni kwamba tulipata watu wanyoofu waliotaka kujifunza kumhusu Mungu. Kulikuwa Mashahidi wachache jijini Istanbul na wengi wao walikuwa Waarmenia, Wagiriki, na Wayahudi. Lakini kulikuwa watu wa mataifa mengine, na ilifaa kujifunza lugha mbalimbali, kutia ndani Kituruki. Tulifurahia sana kukutana na watu wa mataifa mbalimbali waliokuwa na hamu ya kuijua ile kweli. Wengi wao wanaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.

Kwa kusikitisha, Ruth hakukubaliwa kuendelea kukaa Uturuki, hivyo akalazimika kuondoka. Anaendelea na utumishi wa wakati wote huko Uswisi. Ingawa miaka mingi imepita, ningali ninamkosa sana kwa urafiki wake wenye kupendeza na wenye kujenga.

Nahamia Bara Lingine

Katika mwaka wa 1963, sikukubaliwa kuendelea kukaa Uturuki. Ilikuwa vigumu kuwaacha Wakristo wenzangu ambao niliwaona wakifanya maendeleo ya kiroho huku wakipambana na matatizo mengi. Ili kunitia moyo, watu wa familia yetu walinilipia nauli ya kwenda New York City ili nihudhurie kusanyiko huko. Wakati huo sikujua nchi ambako ningetumwa.

Baada ya kusanyiko nilitumwa Lima, Peru. Nilitumwa pamoja na dada mwingine kijana, na tulisafiri moja kwa moja kutoka New York hadi Lima. Nilijifunza Kihispania na niliishi kwenye makao ya wamishonari yaliyokuwa juu ya ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia sana kuhubiri huko na kuwajua ndugu na dada katika eneo hilo.

Natumwa Nchi Nyingine na Kujifunza Lugha Nyingine

Baada ya muda, watu wa familia yetu huko Ugiriki walianza kuathiriwa na uzee na afya mbaya. Lakini hawakuniomba niache utumishi wa wakati wote na kurudia yale yanayoonwa kuwa maisha ya kawaida ili niweze kuwasaidia. Hata hivyo, baada ya kutafakari na kusali sana, niliona inafaa nitumike karibu na familia yetu. Kwa upendo, ndugu kwenye ofisi ya tawi walikubaliana na maoni yangu, nao wakanituma Italia. Familia yetu ilijitolea kulipia gharama za kuhama. Kwa kweli, kulikuwa na uhitaji mkubwa wa waeneza-injili nchini Italia.

Kwa mara nyingine, ilinibidi kujifunza lugha mpya, yaani, Kiitaliano. Mwanzoni nilitumwa katika jiji la Foggia na baadaye nikatumwa Naples, ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa zaidi. Nilipaswa kuhubiri katika eneo linaloitwa Posilipo, mojawapo ya maeneo yenye kuvutia zaidi huko Naples. Ingawa eneo hilo lilikuwa kubwa sana, kulikuwa na mhubiri mmoja tu wa Ufalme. Nilifurahia sana kuhubiri, naye Yehova alinisaidia kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia. Baada ya muda, kulikuwa na kutaniko kubwa katika eneo hilo.

Watu wa kwanza kabisa ambao nilijifunza Biblia pamoja nao huko Posilipo ni mama mmoja na watoto wake wanne. Mama huyo na binti zake wawili bado ni Mashahidi wa Yehova. Pia, nilijifunza na mume na mke ambao walikuwa na msichana mdogo. Wote walifanya maendeleo ya kiroho na kuonyesha wakfu wao kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji. Sasa binti yao ameolewa na mtumishi mwaminifu wa Yehova, na wote wawili wanamtumikia Mungu kwa bidii. Nilipokuwa nikijifunza Biblia na familia moja kubwa, nilivutiwa sana na nguvu za Neno la Mungu. Tuliposoma maandiko kadhaa yanayoonyesha kwamba Mungu hakubali kuabudiwa kupitia sanamu, mama hata hakungoja tumalize kujifunza. Aliharibu papo hapo sanamu zote zilizokuwa nyumbani kwake!

Katika Hatari za Baharini

Sikuzote nilisafiri kwa meli kati ya Italia na Ugiriki. Kwa kawaida nilifurahia safari hizo. Lakini mwaka wa 1971, mambo yalikuwa tofauti. Nilikuwa nikirudi Italia kwa meli iliyoitwa Heleanna. Asubuhi na mapema Agosti 28, moto ulizuka kwenye jiko la meli hiyo. Moto huo ulienea, nao abiria wakawa na wasiwasi. Wanawake walianza kupoteza fahamu, watoto walikuwa wakilia, nao wanaume walikuwa wakiteta vikali na kutoa vitisho. Watu walikimbilia mashua za kuokolea maisha zilizokuwa kwenye sitaha. Lakini jaketi za kujiokolea zilikuwa chache sana, nao mtambo wa kushusha mashua za kuokolea maisha haukufanya kazi vizuri. Sikuwa na jaketi ya kujiokolea, nao moto ulikuwa unazidi kuwa mkubwa, kwa hiyo nikaona jambo la busara kufanya ni kujitosa baharini.

Punde baada ya kujitosa baharini, nilimwona mwanamke ambaye alikuwa amevaa jaketi ya kujiokolea akielea karibu nami. Ilionekana kama hawezi kuogelea, kwa hiyo nikamshika mkono ili kumburuta kutoka kwenye meli iliyokuwa ikizama. Kwa kuwa mawimbi yalizidi kuwa makali, nilipambana nayo ili nisizame, nami nikachoka sana. Sikuwa na matumaini yoyote kamwe, lakini niliendelea kumwomba Yehova anipe ujasiri, na jambo hilo likanitia nguvu. Hali hiyo ilinikumbusha wakati Paulo alipoharibikiwa na meli.—Matendo, sura ya 27.

Huku nikiwa nimemshika yule mwanamke, niliendelea kupambana na mawimbi kwa muda wa saa nne, huku nikiogelea tu nilipokuwa na nguvu za kufanya hivyo na kumwomba Yehova anisaidie. Mwishowe niliona mashua ndogo ikitukaribia. Niliokolewa lakini mwenzangu alikuwa tayari amekufa. Tulipofika mjini Bari, Italia, nilipelekwa hospitalini, ambako nilipewa huduma ya kwanza. Nililazwa hospitalini kwa muda wa siku kadhaa. Mashahidi wengi walinitembelea na kwa fadhili wakashughulikia mahitaji yangu yote. Upendo wa Kikristo walioonyesha uliwavutia sana wagonjwa wengine waliokuwa wamelazwa pia. *

Baada ya kupona kabisa, nilitumwa Roma. Niliombwa nihubiri kwenye eneo la biashara la katikati mwa jiji, na kwa msaada wa Yehova nilihubiri kwa miaka mitano. Nilifurahia utumishi nchini Italia kwa miaka 20, na niliwapenda Waitaliano sana.

Narudi Athens

Afya ya Ariadne na mume wake ilidhoofika sana. Niliona kwamba nikikaa karibu nao, ninaweza kulipia kwa kadiri fulani mema ambayo walinitendea kwa upendo. Nilihuzunika sana kuondoka Italia. Hata hivyo, ndugu kwenye ofisi ya tawi waliniruhusu kuondoka, na tangu mwaka wa 1985, nimekuwa nikifanya utumishi wa upainia jijini Athens, ambako nilianza utumishi wa wakati wote mwaka wa 1947.

Nilihubiri katika eneo la kutaniko letu, na niliwauliza ndugu katika ofisi ya tawi kama ningeweza pia kuhubiri katika eneo la biashara la katikati mwa jiji. Nilihubiri katika eneo hilo kwa miaka mitatu pamoja na painia mwingine. Tuliwahubiria kikamili watu ambao kwa kawaida hawapatikani nyumbani.

Kadiri wakati unavyosonga ndivyo tamaa yangu ya kutumika inavyozidi kuongezeka, lakini nguvu zinaendelea kwisha. Sasa mume wa dada yangu amekufa, naye Ariadne, ambaye amekuwa kama mama kwangu, amekuwa kipofu. Afya yangu ilikuwa nzuri nilipokuwa mtumishi wa wakati wote. Hivi karibuni nilianguka kwenye ngazi ya marumaru na kuvunjika mkono wangu wa kuume. Kisha nikaanguka tena na kuvunjika nyonga. Nilifanyiwa upasuaji na kulazimika kukaa kitandani kwa muda mrefu. Sasa siwezi kutembea vizuri. Mimi hutumia mkongojo na hutoka nje tu ikiwa nimeandamana na mtu mwingine. Hata hivyo, mimi hufanya yote niwezayo nikitumaini kwamba afya yangu itaboreka. Kushiriki katika kazi ya kufundisha Biblia, hata kwa kiwango kidogo, bado ndilo jambo ambalo huniletea furaha na uradhi mkubwa zaidi.

Ninapokumbuka miaka yenye furaha nilipokuwa mtumishi wa wakati wote, mimi humshukuru Yehova sana. Yehova pamoja na washiriki wa sehemu ya duniani ya tengenezo lake wamenipa mwongozo na msaada ufaao na kuniwezesha kutumia uwezo wangu kikamili. Hivyo nimetumia maisha yangu kumtumikia Yehova. Ninamwomba Yehova sana ili anitie nguvu niendelee kumtumikia. Ninafurahi kwamba nimeweza kushiriki kwa kiwango kidogo katika kazi ya kufundisha Biblia duniani kote ambayo anaongoza.—Malaki 3:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona ukurasa wa 73-89 wa Kitabu cha Mwaka cha 1995 cha Mashahidi wa Yehova, cha Kiingereza, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 34 Unaweza kupata habari zaidi katika gazeti la Amkeni! la Kiingereza la Februari 8, 1972, ukurasa wa 12-16.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Nikiwa na dada yangu Ariadne na mume wake Michalis, nilipokuwa nikiondoka kwenda Shule ya Gileadi

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mimi na Ruth Hemmig tulitumwa Istanbul, Uturuki

[Picha katika ukurasa wa 11]

Nikiwa Italia, mapema katika miaka ya 1970

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nikiwa na dada yangu Ariadne leo