Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanajitoa kwa Hiari

Wanajitoa kwa Hiari

Wanajitoa kwa Hiari

“WATU wako watajitoa kwa hiari.” (Zaburi 110:3) Maneno hayo yana umuhimu wa pekee kwa wanafunzi 46 wa darasa la 118 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Walijitayarishaje kuhudhuria shule hiyo ambayo huwafundisha watakaokuwa wamishonari kushughulikia hali ya kiroho ya watu katika nchi za kigeni? Mike na Stacie, ambao walihudhuria darasa la 118, walieleza hivi: “Uamuzi wetu wa kuishi maisha rahisi ulitusaidia kuzingatia mambo ya kiroho na kuepuka vitu ambavyo vingetukengeusha. Tuliazimia kutoruhusu mafanikio ya kibiashara yatuzuie kufikia miradi ya kiroho.” Sawa na Mike na Stacie, wanafunzi wengine wa darasa hilo walijitoa kwa hiari na sasa wanatumika wakiwa watangazaji wa Ufalme katika mabara manne tofauti.

Siku ya Jumamosi, Machi 12, 2005, wahudhuriaji 6,843 walifurahi kusikiliza programu ya kuhitimu. Mwenyekiti alikuwa ndugu Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuwakaribisha kwa uchangamfu wageni waliohudhuria kutoka nchi 28, alikazia uangalifu ubora wa elimu ya Biblia. Akimnukuu mwalimu Mmarekani William Lyon Phelps, Ndugu Jaracz alisema: “Kila mtu ambaye anaijua Biblia kabisa aweza kwa kweli kuitwa mtu aliyeelimika.” Ingawa elimu ya kilimwengu ina faida elimu ya Biblia ni bora zaidi. Inawasaidia watu kupata ujuzi juu ya Mungu, ambao huongoza kwenye uzima wa milele. (Yohana 17:3) Ndugu Jaracz aliwapongeza wahitimu kwa kujitolea kwa hiari ili kushiriki kwa njia kubwa zaidi katika programu ya elimu ya Biblia inayofanywa katika makutaniko zaidi ya 98,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.

Wahitimu Watiwa Moyo

Baada ya utangulizi wa mwenyekiti, William Samuelson alizungumzia kichwa hiki kinachotegemea Zaburi 52:8, “Jinsi Unavyoweza Kuwa Kama Mzeituni Wenye Majani Mengi Katika Nyumba ya Mungu.” Alisema kwamba mzeituni hutumiwa kwa njia ya mfano katika Biblia kuwakilisha uwezo wa kuzaa kwa wingi, umaridadi, na heshima. (Yeremia 11:16) Akiwalinganisha wanafunzi na mizeituni, msemaji alisema: “Yehova atawaona kuwa maridadi na wenye heshima mnapoendelea kwa uaminifu kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme katika maeneo mtakayotumwa.” Kama vile mzeituni unavyohitaji mizizi iliyoenea ili kustahimili majira ya kiangazi, ndivyo wanafunzi wanavyohitaji kuimarisha mizizi yao ya kiroho ili waweze kuvumilia ubaridi, upinzani, au majaribu mengine ambayo huenda wakayakabili wanapotumika katika nchi za kigeni.—Mathayo 13:21; Wakolosai 2:6, 7.

John E. Barr, mmoja kati ya washiriki watatu wa Baraza Linaloongoza ambao walikuwa na sehemu katika programu hiyo, alizungumzia kichwa, “Ninyi Ndio Chumvi ya Dunia.” (Mathayo 5:13) Alionyesha kwamba kama vile chumvi inavyohifadhi chakula ili kisioze, ndivyo na kazi ya wamishonari ya kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu itakavyowaokoa wale wanaosikiliza, ikiwalinda wasioze kiadili na kiroho. Kisha kwa fadhili, Ndugu Barr aliwasihi wahitimu waendelee ‘kudumisha amani’ na wengine. (Marko 9:50) Msemaji huyo alisema: “Kuzeni matunda ya roho, na kuhakikisha kwamba sikuzote mnasema na kutenda kwa neema huku mkiwajali wengine.”

Wallace Liverance, ambaye ni mwalimu wa Gileadi, alizungumzia kichwa “Baki Kwenye Meli Katika Maji Yenye Kina Kirefu.” Kama vile meli iliyo ndani ya maji yenye kina kirefu inavyoweza kuelekea upande unaofaa, ndivyo na kuelewa “mambo mazito ya Mungu,” yaani, kweli kuhusu kusudi la Mungu na jinsi litakavyotimizwa, kunavyoweza kumsaidia mtu kufanya maendeleo ya kiroho. (1 Wakorintho 2:10) Kukaa ndani ya maji ya kiroho yasiyo na kina kwa kutosheka na “mambo ya msingi ya maneno matakatifu ya Mungu” hutuzuia kufanya maendeleo na huenda hata kukafanya ‘imani yetu ivunjike.’ (Waebrania 5:12, 13; 1 Timotheo 1:19) “Acheni ‘kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi’ viwategemeze katika migawo yenu ya umishonari,” akamalizia Ndugu Liverance.—Waroma 11:33.

Mark Noumair ambaye pia ni mwalimu wa Gileadi, alizungumzia kichwa “Je, Mtahifadhi Urithi Wenu?” Kwa zaidi ya miaka 60, Shule ya Gileadi imetumainiwa na imepata sifa bora kwa sababu ya ‘rundo la ushahidi mzuri’ unaotolewa na wahitimu wa shule hiyo. (Mwanzo 31:48) Wanafunzi wa darasa la 118 wameupokea urithi huo wa Gileadi. Ndugu Noumair aliwatia moyo wanafunzi wawaige Watekoa wa siku za Nehemia na washirikiane kwa unyenyekevu na kutaniko pamoja na wamishonari wenzao. Wanafunzi walitiwa moyo waepuke mtazamo wenye kiburi wa ‘watu mashuhuri’ waliotajwa na Nehemia na badala yake wawe tayari kufanya kazi kwa utulivu na bila kujipendekeza.—Nehemia 3:5.

Mambo Yaliyoonwa na Mahojiano Yenye Kujenga

Sehemu nyingine ya programu ilikuwa na kichwa “Neno la Mungu Likaendelea Kukua.” (Matendo 6:7) Wakielekezwa na Lawrence Bowen, mwalimu wa Gileadi, wanafunzi waliigiza mambo yaliyoonwa ambayo walifurahia katika utumishi wa shambani walipokuwa wakihudhuria shule. Mambo hayo yalionyesha kwamba wanafunzi walikuwa wametangaza Neno la Mungu kwa bidii na kwamba Yehova alikuwa amebariki sana jitihada zao.

Richard Ashe aliwahoji Wanabetheli ambao hufanya kazi pamoja na wanafunzi wa Gileadi. Maelezo yao yalionyesha jinsi ambavyo familia ya Betheli huwasaidia wanafunzi wa Gileadi ili wafaidike sana na shule hiyo. Kisha, Geoffrey Jackson akawahoji baadhi ya wanafunzi wa zamani waliohitimu Shule ya Gileadi. Walikazia kwamba wamishonari wana nafasi nyingi za kumsifu na kumtukuza Yehova. Mmoja wao alisema: “Watu huchunguza kila kitu unachofanya ukiwa mmishonari. Wanasikiliza, wanatazama, na wanakumbuka.” Hivyo, wanafunzi walitiwa moyo sikuzote wawe kielelezo kizuri. Bila shaka, shauri hilo zuri litakuwa lenye thamani siku zijazo.

Stephen Lett, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya kumalizia yenye kichwa, “Nendeni Mkiwa Wachukuzi wa ‘Maji Yaliyo Hai.’” (Yohana 7:38) Alisema kwamba kwa miezi mitano, wanafunzi wamefaidika sana kwa kunywa sana kutokana na Neno la Mungu la kweli. Lakini wamishonari wapya watatumiaje habari ambazo wamejifunza? Ndugu Lett aliwasihi wahitimu wawape wengine maji hayo ya kiroho bila ubinafsi ili wapate “chemchemi ya maji . . . inayobubujika ili kutokeza uzima wa milele.” (Yohana 4:14) Msemaji aliongezea: “Msikose kamwe kumpa Yehova, ambaye ndiye ‘chemchemi ya maji yaliyo hai,’ heshima na utukufu anaostahili. Mwe na subira mnapofundisha wale ambao wametoka katika Babiloni Mkubwa lililokumbwa na ukame.” (Yeremia 2:13) Ndugu Lett alimalizia kwa kuwatia moyo wahitimu kuiga kwa uchangamfu roho na bibi-arusi na kuendelea kusema: “‘Njoo!’ Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17.

Ndugu Jaracz alimalizia programu kwa kuwapa wasikilizaji salamu kutoka nchi mbalimbali. Kisha mmoja wa wahitimu wa darasa hilo akasoma barua ya shukrani.

Je, unaweza kujitolea kutumikia mahali penye uhitaji zaidi? Ikiwa ndivyo, fuatia miradi ya kiroho kama wahitimu hao. Pata shangwe na uradhi ambao mtu hupata anapojitolea kwa hiari kumtumikia Mungu—uwe utatumika ukiwa mmishonari katika nchi ya kigeni au ukiwa mhudumu karibu na nyumbani.

[Picha katika ukurasa wa 13]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 8

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 19

Idadi ya wanafunzi: 46

Wastani wa umri: 33.0

Wastani wa miaka katika kweli: 16.5

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 12.9

[Picha katika ukurasa wa 15]

Darasa la 118 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Brockmeyer, A.; Moloney, S.; Symonds, N.; Lopez, Y.; Howard, C. (2) Jastrzebski, T.; Brown, D.; Hernandez, H.; Malagón, I.; Jones, A.; Connell, L. (3) Howard, J.; Lareau, E.; Shams, B.; Hayes, S.; Brown, O. (4) Burrell, J.; Hammer, M.; Mayer, A.; Kim, K.; Stanley, R.; Rainey, R. (5) Jastrzebski, P.; Zilavetz, K.; Ferris, S.; Torres, B.; Torres, F. (6) Connell, J.; Hernandez, R.; Moloney, M.; Malagón, J.; Shams, R.; Hayes, J. (7) Ferris, A.; Hammer, J.; Stanley, G.; Kim, C.; Symonds, S.; Lopez, D.; Burrell, D. (8) Brockmeyer, D.; Mayer, J.; Rainey, S.; Zilavetz, S.; Jones, R.; Lareau, J.